Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Fulizeni Kuzaa Matunda Mengi’

‘Fulizeni Kuzaa Matunda Mengi’

‘Fulizeni Kuzaa Matunda Mengi’

“Mfulize kuzaa matunda mengi na kujithibitisha wenyewe kuwa wanafunzi wangu.”—YOHANA 15:8.

1. (a) Yesu aliwatajia mitume wake takwa gani la kuwa mwanafunzi? (b) Tunapaswa kujiuliza swali gani?

ULIKUWA usiku wa kuamkia kifo chake. Yesu alikuwa ametumia muda wa kutosha kuwatia moyo mitume wake kwa kuzungumza nao waziwazi. Kufikia sasa, yaonekana ilikuwa baada ya saa sita usiku, lakini Yesu aliendelea kuzungumza na hao rafiki zake wa karibu kwa sababu aliwapenda. Kisha, alipokuwa akizungumza nao, aliwakumbusha takwa jingine walilopaswa kutimiza ili kuendelea kuwa wanafunzi wake. Alisema: “Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mfulize kuzaa matunda mengi na kujithibitisha wenyewe kuwa wanafunzi wangu.” (Yohana 15:8) Je, leo sisi tunatimiza sifa hiyo ya kuwa wanafunzi? Inamaanisha nini kuwa wenye “kuzaa matunda mengi”? Ili kupata jibu, na tuchunguze mazungumzo ya Yesu jioni hiyo.

2. Yesu asimulia kielezi gani kuhusu matunda jioni kabla ya kifo chake?

2 Shauri la kuzaa matunda limetajwa katika kielezi kimoja ambacho Yesu alisimulia mitume wake. Alisema: “Mimi ndio mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mlimaji. Kila tawi katika mimi lisilozaa matunda yeye huliondolea mbali, na kila linalozaa matunda yeye hulisafisha, lipate kuzaa matunda zaidi. Tayari nyinyi ni safi kwa sababu ya neno ambalo nimewaambia. Kaeni katika muungano nami, na mimi katika muungano nanyi. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa matunda likiwa pekee isipokuwa likae katika mzabibu, katika njia hiyohiyo wala nyinyi hamwezi, isipokuwa mkae katika muungano nami. Mimi ndio mzabibu, nyinyi ndiyo matawi. . . . Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mfulize kuzaa matunda mengi na kujithibitisha wenyewe kuwa wanafunzi wangu. Kama vile Baba amenipenda mimi nami nimewapenda nyinyi, kaeni katika upendo wangu. Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu.”—Yohana 15:1-10.

3. Wafuasi wa Yesu wanapaswa kufanya nini ili kuzaa matunda?

3 Katika kielezi hicho, Yehova ndiye Mlimaji, Yesu ndiye mzabibu, nao mitume ambao Yesu alikuwa akizungumza nao ndio matawi. Mitume wangezaa matunda maadamu wangejitahidi ‘kukaa katika muungano’ na Yesu. Kisha Yesu alieleza jinsi ambavyo mitume hao wangefaulu kudumisha muungano huo muhimu: “Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu.” Baadaye, mtume Yohana aliandika maneno kama hayo kwa Wakristo wenzake: “Yeye ambaye hushika amri [za Kristo] hukaa katika muungano na yeye.” * (1 Yohana 2:24; 3:24) Kwa hiyo, kwa kushika amri za Kristo, wafuasi wake hukaa katika muungano naye, na muungano huo huwawezesha kuzaa matunda. Tunapaswa kuzaa matunda ya aina gani?

Fursa ya Kukua

4. Tunaweza kujifunza nini kutokana na uhakika wa kwamba Yehova “huliondolea mbali” kila tawi lisilozaa matunda?

4 Katika kielezi cha mzabibu, Yehova “huliondolea mbali,” tawi lisipozaa matunda. Jambo hilo linatufunza nini? Linatufunza kwamba wanafunzi wote wanatakiwa wazae matunda kwa kuwa wanaweza kufanya hivyo licha ya hali zao na udhaifu wao. Kwa kweli, ingekuwa kinyume cha njia za upendo za Yehova ‘kuondolea mbali,’ mwanafunzi wa Kristo kwa sababu ya kushindwa kutimiza jambo linalozidi uwezo wake.—Zaburi 103:14; Wakolosai 3:23; 1 Yohana 5:3.

5. (a) Kielezi cha Yesu kinaonyeshaje kwamba tunaweza kufanya maendeleo katika kuzaa matunda? (b) Tutazungumzia aina gani mbili za matunda?

5 Pia kielezi cha Yesu cha mzabibu kinaonyesha kwamba chini ya hali zetu, tunapaswa kutafuta fursa za kufanya maendeleo katika utendaji wetu tukiwa wanafunzi. Ona jinsi Yesu anavyosema: “Kila tawi katika mimi lisilozaa matunda yeye huliondolea mbali, na kila linalozaa matunda yeye hulisafisha, lipate kuzaa matunda zaidi.” (Yohana 15:2) Akimalizia kielezi hicho, Yesu aliwahimiza wafuasi wake wazae “matunda mengi.” (Mstari wa 8) Hilo linamaanisha nini? Tukiwa wanafunzi, hatupaswi kuridhika tu na yale ambayo tumetimiza. (Ufunuo 3:14, 15, 19) Badala yake, tunapaswa kutafuta njia za kuendelea kuzaa matunda. Tunapaswa kujitahidi kuzaa kwa wingi matunda ya aina gani? Kuna aina mbili (1) “matunda ya roho” na (2) matunda ya Ufalme.—Wagalatia 5:22, 23; Mathayo 24:14.

Matunda ya Sifa za Kikristo

6. Yesu Kristo alikaziaje umuhimu wa kuonyesha tunda la kwanza la roho?

6 Sifa ya kwanza inayotajwa kati ya “matunda ya roho” ni upendo. Roho takatifu ya Mungu huwawezesha Wakristo waonyeshe upendo kwa kuwa wanatii amri ambayo Yesu alitoa muda mfupi kabla ya kusimulia kielezi cha mzabibu unaozaa matunda. Aliwaambia mitume wake hivi: “Ninawapa nyinyi amri mpya, kwamba mpendane.” (Yohana 13:34) Kwa kweli, alipokuwa akizungumza na mitume wake usiku huo wa mwisho duniani, Yesu aliwakumbusha tena na tena kuhusu uhitaji wa kuonyesha upendo.—Yohana 14:15, 21, 23, 24; 15:12, 13, 17.

7. Mtume Petro alionyeshaje kwamba kuzaa matunda kunahusiana na kuonyesha sifa kama za Kristo?

7 Petro aliyekuwako usiku huo, alifahamu kwamba wanafunzi wa kweli wa Kristo wanapaswa kuonyesha upendo kama wa Kristo na sifa nyingine zinazohusiana na upendo. Miaka kadhaa baadaye, Petro aliwatia moyo Wakristo wasitawishe sifa kama vile kujidhibiti, shauku ya kidugu, na upendo. Aliongeza kusema kwamba kufanya hivyo hutuzuia “kuwa ama wasiotenda ama wasiozaa matunda.” (2 Petro 1:5-8) Hata hali zetu ziweje, tunaweza kuonyesha matunda ya roho. Hivyo basi, na tujitahidi kuonyesha upendo, fadhili, upole, na sifa nyingine za Kikristo kwa kiwango kikubwa zaidi kwa kuwa “dhidi ya mambo ya namna hiyo hakuna sheria,” wala kikomo. (Wagalatia 5:23) Naam, na tuzae “matunda zaidi.”

Kuzaa Matunda ya Ufalme

8. (a) Kuna uhusiano gani kati ya matunda ya roho na matunda ya Ufalme? (b) Tunapaswa kufikiria swali gani?

8 Matunda yenye kupendeza na yenye ladha nzuri huupamba mti. Hata hivyo, matunda hayo yana manufaa zaidi ya kupamba mti. Pia matunda ni muhimu kwa kuwa hueneza mbegu na kuzidisha idadi ya miti. Vivyo hivyo, matunda ya roho hufanya mengi zaidi ya kupamba utu wetu wa Kikristo. Sifa kama vile upendo na imani hutuchochea kueneza ujumbe wa Ufalme ulio kama mbegu ambayo hupatikana katika Neno la Mungu. Ona jinsi mtume Paulo anavyokazia uhusiano muhimu uliopo kati ya matunda ya roho na matunda ya Ufalme. Anasema: “Sisi pia hudhihirisha imani [sehemu ya matunda ya roho] na kwa hiyo twasema.” (2 Wakorintho 4:13) Kwa kufanya hivyo, Paulo anazidi kueleza kwamba ‘tunamtolea Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo’—tunda la pili tunalohitaji kuonyesha. (Waebrania 13:15) Je, tuna fursa maishani mwetu za kuzaa “matunda zaidi,” tukiwa watangazaji wa Ufalme wa Mungu?

9. Je, kuzaa matunda ni kufanya wanafunzi? Eleza.

9 Ili tujibu kwa usahihi, kwanza tunahitaji kuelewa kinachomaanishwa na matunda ya Ufalme. Je, ni sahihi kusema kwamba kuzaa matunda kunamaanisha kufanya wanafunzi? (Mathayo 28:19) Je, matunda tunayozaa ni watu tunaowasaidia kuwa waabudu waliobatizwa wa Yehova? La. Ikiwa ingekuwa hivyo, jambo hilo lingewavunja moyo sana Mashahidi wenzetu wapendwa ambao kwa miaka mingi wametangaza ujumbe wa Ufalme kwa uaminifu katika maeneo yasiyo na matokeo sana. Naam, ikiwa matunda ya Ufalme tunayozaa yanawakilishwa tu na wanafunzi wapya, Mashahidi hao wanaofanya kazi kwa bidii wangekuwa kama matawi yasiyozaa katika kielezi cha Yesu! Bila shaka, hivyo sivyo ilivyo. Hivyo, basi matunda ya Ufalme ya huduma yetu ni nini hasa?

Kuzaa Matunda kwa Kueneza Mbegu ya Ufalme

10. Kielezi cha Yesu cha mpanzi na aina mbalimbali za udongo kinaonyeshaje matunda ya Ufalme?

10 Tunapata jibu katika kielezi cha Yesu cha mpanzi na aina mbalimbali za udongo. Jibu hilo linawatia moyo Mashahidi wanaohubiri maeneo yasiyo na matokeo sana. Yesu alisema kwamba mbegu ni ujumbe wa Ufalme unaopatikana katika Neno la Mungu, na kwamba udongo ni moyo wa mfano. Baadhi ya mbegu ‘zilianguka juu ya udongo mzuri, na, baada ya kuota, zikatokeza matunda.’ (Luka 8:8) Matunda gani? Baada ya bua la ngano kuota na kukomaa, linazaa matunda, yaani mbegu mpya, wala halizai mabua madogo ya ngano. Vivyo hivyo, matunda ambayo Mkristo hutokeza si lazima yawe ni wanafunzi wapya, bali ni mbegu mpya ya Ufalme.

11. Matunda ya Ufalme yanaweza kufasiriwaje?

11 Kwa hiyo, matunda si wanafunzi wapya wala sifa nzuri za Kikristo. Kwa kuwa mbegu inayopandwa ni neno la Ufalme, basi matunda ni mbegu zaidi za ufalme. Kwa habari hii, kuzaa matunda kunamaanisha kuzungumza juu ya Ufalme huo. (Mathayo 24:14) Je, sote tunaweza kuzaa matunda hayo ya Ufalme, yaani, kutangaza habari njema ya Ufalme hata hali zetu ziweje? Ndiyo! Katika kielezi hichohicho, Yesu anaeleza sababu.

Kutoa Yaliyo Bora ili Kumtukuza Mungu

12. Je, Wakristo wote wanaweza kuzaa matunda ya Ufalme? Eleza.

12 ‘Kwa habari ya yule aliyepandwa juu ya udongo ulio bora, hutokeza, huyu mara mia, yule sitini, yule mwingine thelathini.’ (Mathayo 13:23) Huenda nafaka zilizopandwa shambani zisitokeze kiasi kilekile cha mazao ikitegemea hali. Vivyo hivyo, kwa sababu ya hali huenda yale tunayoweza kutimiza katika kutangaza habari njema yasilingane na ya wengine, na Yesu alionyesha kwamba anatambua jambo hilo. Huenda wengine wakawa na fursa zaidi, wengine wakawa na afya bora na nguvu zaidi. Hivyo, huenda tukafanya mengi au machache kuliko wengine. Hata hivyo, Yehova anafurahi iwapo tunatoa yaliyo bora zaidi. (Wagalatia 6:4) Hata ikiwa uzee au ugonjwa unaodhoofisha unatuzuia tusishiriki sana kazi ya kuhubiri, Yehova, Baba yetu mwenye huruma hutuhesabu miongoni mwa wale ‘wanaofuliza kuzaa matunda mengi.’ Kwa nini? Kwa sababu tunampa ‘vyote tulivyo navyo’—utumishi wa nafsi yote. *Marko 12:43, 44; Luka 10:27.

13. (a) Ni sababu gani kuu zaidi inayofanya ‘tuendelee na kufuliza’ kuzaa matunda ya Ufalme? (b) Ni nini kitakachotusaidia tuendelee kuzaa matunda katika maeneo yasiyo na matokeo sana? (Ona sanduku katika ukurasa wa 21.)

13 Hata tuwe tunazaa matunda ya Ufalme kadiri gani, tutachochewa ‘tuendelee na kufuliza kuzaa matunda’ tunapokumbuka sababu ya kufanya hivyo. (Yohana 15:16) Yesu alitaja sababu kuu zaidi: “Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mfulize kuzaa matunda mengi.” (Yohana 15:8) Naam, kazi yetu ya kuhubiri hulitukuza jina la Yehova mbele ya watu wote. (Zaburi 109:30) Honor, Shahidi mwaminifu mwenye umri wa miaka 70 na kitu anasema: “Ni pendeleo kumwakilisha Aliye Juu Zaidi Sana, hata katika maeneo yasiyo na matokeo sana.” Wakati Claudio, Shahidi mwenye bidii tangu 1974, alipoulizwa kwa nini anaendelea kuhubiri hata ingawa ni wachache wanaoitikia katika eneo lao, alinukuu Yohana 4:34, ambapo tunasoma maneno haya ya Yesu: “Chakula changu ni kwamba mimi nifanye mapenzi yake aliyenituma na kumaliza kazi yake.” Claudio aliongeza kusema: “Kama Yesu, ningependa kuanza na pia kumaliza kazi yangu ya kutangaza Ufalme.” (Yohana 17:4) Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanakubaliana naye.—Ona sanduku “Jinsi ya ‘Kuzaa Matunda kwa Uvumilivu,’” katika ukurasa wa 21.

Kuhubiri na Kufundisha

14. (a) Kazi ya Yohana Mbatizaji na ya Yesu ilikuwa na makusudi gani mawili? (b) Ungeelezaje utendaji wa Kikristo leo?

14 Yohana Mbatizaji ndiye mtangazaji wa kwanza wa Ufalme anayetajwa katika vitabu vya Injili. (Mathayo 3:1, 2; Luka 3:18) Kusudi lake kuu lilikuwa ‘kutoa ushahidi,’ naye alifanya hivyo kwa imani kubwa na kwa tumaini kwamba “watu wa namna zote wapate kuamini.” (Yohana 1:6, 7) Kwa kweli, baadhi ya watu waliohubiriwa na Yohana walikuja kuwa wanafunzi wa Kristo. (Yohana 1:35-37) Kwa hiyo, Yohana alihubiri na vilevile kufanya wanafunzi. Yesu pia alikuwa mhubiri na mwalimu. (Mathayo 4:23; 11:1) Kwa hiyo haishangazi kwamba Yesu aliwaamuru wafuasi wake wahubiri ujumbe wa Ufalme na pia wawasaidie watu wanaokubali ujumbe huo kuwa wanafunzi wake. (Mathayo 28:19, 20) Kwa hiyo kazi yetu leo inatia ndani kuhubiri na kufundisha.

15. Kuna ufanani gani kati ya namna watu wanavyoitikia habari njema sasa na walivyoitikia katika karne ya kwanza W.K.?

15 Kati ya watu waliomsikia Paulo akihubiri na kufundisha katika karne ya kwanza W.K., ‘wengine walianza kuamini mambo yaliyosemwa na wengine wakawa hawaamini.’ (Matendo 28:24) Leo, watu wanaitikia vivyo hivyo. Kwa kusikitisha, mbegu nyingi za Ufalme huanguka katika udongo usiofaa. Hata hivyo, mbegu nyingine bado huanguka kwenye udongo mzuri, hutoa mizizi, na kuota, kama Yesu alivyotabiri. Kwa kweli, ulimwenguni pote, kwa wastani watu zaidi ya 5,000 huwa wanafunzi wa kweli wa Kristo kila juma! Wanafunzi hao wapya ‘huamini mambo yaliyosemwa,’ ijapokuwa watu wengine wengi hawaamini. Ni nini kilichofanya mioyo yao ipokee ujumbe wa Ufalme? Mara nyingi ni upendezi walioonyeshwa na Mashahidi. Mashahidi walipata matokeo mazuri kwa kutia maji mbegu mpya kwa njia ya mfano. (1 Wakorintho 3:6) Fikiria mifano miwili tu kati ya mifano mingi.

Kupendezwa Kibinafsi na Watu Huwa na Matokeo Mazuri

16, 17. Kwa nini ni muhimu tupendezwe na watu tunaokutana nao katika huduma?

16 Karolien, Shahidi mchanga anayeishi Ubelgiji, alimtembelea mwanamke mzee ambaye hakupendezwa na ujumbe wa Ufalme. Kwa kuwa mwanamke huyo alikuwa amefungwa bendeji mkononi, Karolien na mwenzake walitaka kumsaidia, lakini mwanamke huyo akakataa. Siku mbili baadaye Mashahidi hao walirudi nyumbani kwa mwanamke huyo ili kumjulia hali. “Kukawa na matokeo mazuri,” akasema Karolien. “Alishangaa kuona kwamba tulipendezwa naye kikweli. Alitualika nyumbani kwake, na tukaanza kujifunza Biblia pamoja naye.”

17 Sandi, Shahidi anayeishi Marekani, pia hupendezwa na watu anaowahubiria. Yeye hutazama matangazo ya kuzaliwa kwa watoto katika gazeti moja la kwao na kuwatembelea wazazi waliojifungua hivi karibuni akiwa na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. * Kwa kuwa akina mama waliojifungua huwa nyumbani na hupenda kuwaonyesha wageni mtoto wao mchanga, mara nyingi mazungumzo huanzia hapo. “Mimi huzungumza na wazazi kuhusu umuhimu wa kuwa na uhusiano wa karibu na mtoto wao mchanga kupitia kusoma,” asema Sandi. “Baadaye ninazungumzia magumu ya kulea watoto katika ulimwengu wa sasa.” Hivi karibuni, baada ya kumtembelea mama mmoja, yeye na watoto wake sita walianza kumtumikia Yehova. Tunaweza kufurahia matokeo mazuri katika huduma yetu kwa kuchukua hatua ya kwanza na kupendezwa kibinafsi na watu.

18. (a) Kwa nini sisi sote tunaweza kutimiza takwa la “kuzaa matunda mengi”? (b) Ni matakwa gani matatu ya kuwa mwanafunzi yanayotajwa katika Injili ya Yohana ambayo umeazimia kutimiza?

18 Inatia moyo kama nini kujua kwamba tunaweza kutimiza takwa la ‘kufuliza kuzaa matunda mengi’! Iwe tu wachanga au wazee, tuna afya nzuri au mbaya, tunahubiri maeneo yenye matokeo au yasiyo na matokeo sana, sote tunaweza kuzaa matunda mengi. Jinsi gani? Kwa kuonyesha matunda ya roho kwa kadiri kubwa zaidi na kwa kueneza ujumbe wa Ufalme wa Mungu kwa kadiri tuwezavyo. Wakati huohuo, tunajitahidi ‘kukaa katika neno la Yesu’ na ‘kuwa na upendo miongoni mwetu.’ Naam, kwa kutimiza matakwa hayo matatu muhimu ya kuwa mwanafunzi ambayo yametajwa katika Injili ya Yohana, tunathibitisha kwamba sisi ‘kwa kweli sisi ni wanafunzi wa Kristo.’—Yohana 8:31; 13:35.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ingawa matawi ya mzabibu katika kielezi hicho yanawakilisha mitume wa Yesu na Wakristo wengine watakaorithi Ufalme wa kimbingu wa Mungu, kielezi hicho kina kweli zinazoweza kuwanufaisha wafuasi wa Kristo leo.—Yohana 3:16; 10:16.

^ fu. 12 Wale ambao hawawezi kutoka nyumbani mwao kwa sababu ya uzee au ugonjwa wanaweza kutoa ushahidi kwa kuandika barua, au inapowezekana wanaweza kutumia simu, au labda kuwahubiria watu wanaokuja kuwatembelea.

^ fu. 17 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maswali ya Kurudia

• Tunapaswa kuzaa matunda ya aina gani kwa wingi?

• Kwa nini tunaweza kutimiza mradi wa “kuzaa matunda mengi”?

• Ni matakwa gani matatu muhimu ya kuwa mwanafunzi yanayotajwa katika Injili ya Yohana ambayo tumezungumzia?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

JINSI YA “KUZAA MATUNDA KWA UVUMILIVU”

NI NINI hukusaidia kuendelea kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa uaminifu katika maeneo yasiyo na matokeo sana? Hapa pana majibu mazuri kwa swali hilo.

“Kujua kwamba Yesu anatutegemeza kabisa hunitia moyo niwe na mtazamo mzuri na kuvumilia, hata hali iweje katika eneo.”—Harry, mwenye umri wa miaka 72; aliyebatizwa mwaka wa 1946.

“Mimi hutiwa moyo na andiko la 2 Wakorintho 2:17. Andiko hilo linasema kwamba tunashiriki huduma ‘mbele ya Mungu, kwa ushirika na Kristo.’ Ninapokuwa shambani, ninafurahia kushirikiana na marafiki wangu bora zaidi.”—Claudio, mwenye umri wa miaka 43: aliyebatizwa mwaka wa 1974.

“Kusema kweli, mimi huona ugumu sana kuhubiri. Hata hivyo, nimeona kwamba maneno haya yanayopatikana katika andiko la Zaburi 18:29 ni ya kweli: ‘Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta.’”—Gerard, mwenye umri wa miaka 79; aliyebatizwa mwaka wa 1955.

“Nikisoma andiko moja tu shambani, ninaridhika kuona kwamba mtu fulani alikubali moyo wake uchunguzwe na Biblia.”—Eleanor, mwenye umri wa miaka 26; aliyebatizwa mwaka wa 1989.

“Mimi hujaribu kutumia tangulizi mbalimbali. Kuna tangulizi nyingi sana hivi kwamba siwezi kutumia zote katika miaka inayobaki ya maisha yangu.”—Paul, mwenye umri wa miaka 79; aliyebatizwa mwaka wa 1940.

“Mimi sikasiriki watu wanapokataa kusikiliza. Mimi hujaribu kuwa mwenye urafiki, kuzungumza na watu na kusikiliza maoni yao.”—Daniel, mwenye umri wa miaka 75; aliyebatizwa mwaka wa 1946.

“Nimekutana na watu waliobatizwa hivi karibuni ambao waliniambia kwamba kazi yangu ya kuhubiri iliwasaidia kwa kadiri fulani wawe Mashahidi. Sikujua kwamba mtu mwingine alijifunza Biblia pamoja nao na kuwasaidia wafanye maendeleo. Ninafurahi kujua kwamba tunafanya kazi ya kuhubiri kwa kushirikiana.”—Joan, mwenye umri wa miaka 66; aliyebatizwa mwaka wa 1954.

Ni nini hukusaidia “kuzaa matunda kwa uvumilivu”?—Luka 8:15.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Tunazaa matunda mengi kwa kuonyesha matunda ya roho na kutangaza ujumbe wa Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yesu alimaanisha nini alipowaambia mitume wake hivi: “Mfulize kuzaa matunda mengi”?