Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Iweni na Upendo Miongoni Mwenu Wenyewe’

‘Iweni na Upendo Miongoni Mwenu Wenyewe’

‘Iweni na Upendo Miongoni Mwenu Wenyewe’

“Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.”—YOHANA 13:35.

1. Yesu alikazia sifa gani muda mfupi tu kabla ya kifo chake?

“WATOTO wadogo.” (Yohana 13:33) Kwa kutumia maneno hayo ya upendo, Yesu alizungumza na mitume wake usiku wa kuamkia kifo chake. Masimulizi ya Injili hayaonyeshi kwamba Yesu alikuwa amewahi kutumia maneno hayo ya upendo kuzungumza na mitume wake. Hata hivyo, usiku huo wa pekee, alichochewa kuzungumza nao kwa upendo ili kuwaonyesha wafuasi wake kwamba aliwapenda sana. Kwa kweli, Yesu alizungumza kuhusu upendo mara 30 hivi usiku huo. Kwa nini alikazia sana sifa hiyo?

2. Kwa nini ni muhimu sana kwa Wakristo kuonyesha upendo?

2 Yesu alieleza ni kwa nini upendo ni muhimu sana. “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe,” akasema. (Yohana 13:35; 15:12, 17) Kuwa mfuasi wa Kristo huambatana sana na kuonyesha upendo wa kidugu. Wakristo wa kweli hutambuliwa kwa upendo mchangamfu wanaoonyeshana wala si mavazi ya aina fulani, au desturi fulani zisizo za kawaida. Upendo huo wa pekee ndio takwa la pili kati ya matakwa matatu ya kuwa mwanafunzi wa Kristo yaliyotajwa mwanzoni mwa makala iliyotangulia. Ni nini kitakachotusaidia tuendelee kutimiza takwa hili?

“Kufanya Hilo kwa Kipimo Chenye Kujaa Zaidi”

3. Mtume Paulo alitoa onyo gani kuhusu upendo?

3 Wanafunzi wa kweli wa Kristo leo huonyesha upendo huo wa pekee kama wafuasi wa Kristo wa karne ya kwanza. Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wa karne ya kwanza hivi: “Kuhusu upendo wa kidugu, hamhitaji sisi tuwe tukiwaandikia nyinyi, kwa maana nyinyi wenyewe hufundishwa na Mungu kupendana; na, kwa kweli, nyinyi mnafanya hilo kwa ndugu wote.” Hata hivyo, Paulo aliongeza kusema hivi: “Mwendelee kufanya hilo kwa kipimo chenye kujaa zaidi.” (1 Wathesalonike 3:12; 4:9, 10) Sisi pia tunahitaji kutii onyo la Paulo na kujitahidi kuonyeshana upendo “kwa kipimo chenye kujaa zaidi.”

4. Kulingana na Paulo na Yesu, tunapaswa kuwafikiria nani hasa?

4 Katika barua hiyohiyo iliyoongozwa na roho ya Mungu, Paulo aliwatia moyo waamini wenzake ‘waseme kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo,’ na ‘kutegemeza walio dhaifu.’ (1 Wathesalonike 5:14) Pindi nyingine, aliwakumbusha Wakristo kwamba ‘wale walio na nguvu, wanapaswa kuchukua udhaifu wa wale wasio na nguvu.’ (Waroma 15:1) Yesu pia alitoa maagizo kuhusu kuwasaidia walio dhaifu. Yesu alimwambia Petro hivi baada ya kutabiri kwamba Petro angemwacha usiku ambao angekamatwa: “Mara uwapo umerudi, watie nguvu ndugu zako.” Kwa nini? Kwa sababu wao pia wangekuwa wamemwacha Yesu na hivyo wangehitaji msaada. (Luka 22:32; Yohana 21:15-17) Kwa hiyo, Neno la Mungu hutuambia tuwaonyeshe upendo wale ambao ni dhaifu kiroho na ambao huenda hawashirikiani tena na kutaniko la Kikristo. (Waebrania 12:12) Kwa nini tufanye hivyo? Tunapata jibu kutokana na vielezi viwili dhahiri vilivyotolewa na Yesu.

Kondoo Aliyepotea na Sarafu Iliyopotea

5, 6. (a) Yesu alisimulia vielezi gani viwili vifupi? (b) Vielezi hivyo vinaonyesha nini kuhusu Yehova?

5 Ili kuwafundisha wasikilizaji wake jinsi Yehova anavyowaona wale ambao wamepoteza mwelekeo, Yesu alisimulia vielezi viwili vifupi. Kielezi kimoja kilihusu mchungaji. Yesu alisema: “Ni mtu gani kati yenu mwenye kondoo mia, apotezapo mmoja wao, hataacha nyuma wale tisini na tisa nyikani na kwenda kumtafuta aliyepotea mpaka ampate? Na akiisha kumpata humweka juu ya mabega yake na kushangilia. Naye afikapo nyumbani huita marafiki wake na majirani wake pamoja, akiwaambia, ‘Shangilieni pamoja nami, kwa sababu nimempata kondoo wangu aliyekuwa amepotea.’ Mimi nawaambia nyinyi kwamba ndivyo kutakuwa na shangwe zaidi mbinguni juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye kuliko juu ya waadilifu tisini na tisa wasio na uhitaji wa toba.”—Luka 15:4-7.

6 Kielezi cha pili kilihusu mwanamke fulani. Yesu alisema: “Ni mwanamke gani mwenye sarafu za drakma kumi, ikiwa apoteza sarafu moja ya drakma, asiyewasha taa na kufagia nyumba yake na kutafuta kwa uangalifu mpaka aipate? Naye akiisha kuipata huwaita wanawake walio marafiki wake na majirani pamoja, akisema, ‘Shangilieni pamoja nami, kwa sababu nimeipata sarafu ya drakma niliyoipoteza.’ Hivyo, mimi nawaambia nyinyi, ndivyo shangwe hutokea miongoni mwa malaika za Mungu juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye.”—Luka 15:8-10.

7. Tunaweza kujifunza mambo gani mawili kutokana na kielezi cha kondoo aliyepotea na sarafu iliyopotea?

7 Tunaweza kujifunza nini kutokana na vielezi hivyo vifupi? Vinatuonyesha (1) tunavyopaswa kuhisi kuelekea wale walio dhaifu na (2) mambo tunayopaswa kufanya ili kuwasaidia. Na tuchunguze mambo hayo.

Kilipotea Lakini Kilithaminiwa

8. (a) Mchungaji na mwanamke walihisije vitu vyao vilipopotea? (b) Tunajifunza nini kutokana na jinsi walivyohisi kuhusu vitu vilivyopotea?

8 Katika vielezi vyote viwili, kitu fulani kilipotea, lakini ona jinsi wenye vitu hivyo walivyohisi. Mchungaji hakusema: ‘Kondoo mmoja ana faida gani, je, sina kondoo 99? Simhitaji kondoo huyo.’ Mwanamke huyo hakusema: ‘Kwa nini nihangaikie sarafu moja? Zile tisa nilizo nazo zanitosha.’ Badala ya kusema hivyo, mchungaji alimtafuta kondoo aliyepotea kana kwamba alikuwa na kondoo huyo mmoja tu. Naye mwanamke huyo aliona kwamba amepata hasara kwa kupoteza sarafu moja kana kwamba hakuwa na sarafu nyingine. Katika visa vyote viwili, wenye vitu hivyo vilivyopotea waliviona kuwa vyenye thamani. Tunajifunza nini?

9. Ni nini kinachoonyeshwa na hangaiko la mchungaji na mwanamke?

9 Ona jinsi Yesu alivyomalizia vielezi vyote viwili: “Ndivyo kutakuwa na shangwe zaidi mbinguni juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye” na “ndivyo shangwe hutokea miongoni mwa malaika za Mungu juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye.” Kwa hiyo, hangaiko lililoonyeshwa na mchungaji na mwanamke huyo linatufundisha kwa kiwango kidogo jinsi Yehova na viumbe wake walio mbinguni wanavyohisi. Kwa hiyo, wale ambao wamepoteza mwelekeo na kuacha kushirikiana na watu wa Mungu ni wenye thamani machoni pa Yehova kama vile vitu vilivyopotea vilivyokuwa na thamani kwa mchungaji na mwanamke. (Yeremia 31:3) Huenda watu hao wakawa dhaifu kiroho, lakini huenda wasiwe waasi. Licha ya udhaifu wao, huenda kwa kadiri fulani wakawa wanajitahidi kutimiza matakwa ya Yehova. (Zaburi 119:176; Matendo 15:29) Kwa hiyo, kama ilivyokuwa zamani, Yehova hafanyi haraka ‘kuwatupa usoni pake.’—2 Wafalme 13:23.

10, 11. (a) Tungependa kuwaonaje wale ambao wameacha kushirikiana na kutaniko? (b) Kulingana na vielezi viwili vya Yesu, tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawajali?

10 Kama Yehova na Yesu, sisi pia tunawajali sana wale walio dhaifu na ambao hawashirikiani na kutaniko la Kikristo. (Ezekieli 34:16; Luka 19:10) Tunamwona mtu aliye dhaifu kiroho kama kondoo aliyepotea—si mtu asiyeweza kusaidiwa. Hatusemi: ‘Kwa nini tujishughulishe na mtu aliye dhaifu? Kutaniko linaendelea vizuri bila yeye.’ Badala yake, tunawaona wale ambao wameacha njia na wanaotaka kurudi kama Yehova anavyowaona—kuwa wenye thamani.

11 Hata hivyo, tunawezaje kuonyesha kwamba tunawajali? Vielezi viwili vya Yesu vinaonyesha kwamba tunaweza kufanya hivyo (1) kwa kuonyesha kwamba tunapendezwa nao, (2) kwa kuwa wenye fadhili, na (3) kuwa wenye bidii. Na tuchunguze mambo hayo moja baada ya jingine.

Pendezwa Nao

12. Maneno ‘kwenda kumtafuta aliyepotea’ yanaonyesha nini kuhusu mtazamo wa mchungaji?

12 Katika kielezi cha kwanza kati ya vielezi hivyo viwili, Yesu anasema kwamba mchungaji ‘atakwenda kumtafuta aliyepotea.’ Mchungaji anaonyesha upendezi na kujitahidi kutafuta kondoo aliyepotea. Mchungaji huyo hazuiwi na magumu, hatari, wala umbali. Badala yake anaendelea na jitihada yake “mpaka ampate.”—Luka 15:4.

13. Wanaume wa kale wenye imani walichukua hatua gani kuelekea walio dhaifu, nasi tunawezaje kuiga mifano hiyo ya Biblia?

13 Vivyo hivyo, ili kusaidia mtu anayehitaji kutiwa moyo mara nyingi mwenye nguvu anapaswa kuonyesha upendezi. Wanaume waaminifu wa kale walifahamu jambo hilo. Kwa mfano, Yonathani, mwana wa Mfalme Sauli alipotambua kwamba rafiki yake wa chanda na pete, Daudi, alihitaji kutiwa moyo, Yonathani “akainuka akamwendea Daudi huko Horeshi, akamtia nguvu mkono wake katika Mungu.” (1 Samweli 23:15, 16) Karne kadhaa baadaye, Gavana Nehemia alipoona kwamba baadhi ya ndugu zake Wayahudi walikuwa wamevunjika moyo, yeye pia ‘mara moja alisimama’ na kuwatia moyo ‘wamkumbuke Yehova.’ (Nehemia 4:14, NW) Leo, sisi pia tungependa ‘kusimama—kuonyesha upendezi—kuimarisha walio dhaifu. Lakini ni nani wanaopaswa kufanya hivyo kutanikoni?

14. Ni nani anayepaswa kusaidia walio dhaifu katika kutaniko la Kikristo?

14 Wazee Wakristo hasa wana daraka la ‘kutia nguvu mikono iliyo dhaifu na kufanya imara magoti yaliyolegea’ na ‘kuwaambia walio na moyo wa hofu, Jipeni moyo, msiogope.’ (Isaya 35:3, 4; 1 Petro 5:1, 2) Hata hivyo, shauri la Paulo juu ya ‘kusema kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo’ na ‘kutegemeza walio dhaifu’ halikutolewa kwa wazee peke yao. Badala yake, maneno ya Paulo yalihusu ‘kutaniko lote la Wathesalonike.’ (1 Wathesalonike 1:1; 5:14) Kwa hiyo Wakristo wote wana daraka la kusaidia walio dhaifu. Kama yule mchungaji katika kielezi cha Yesu, kila Mkristo anapaswa kuchochewa “kwenda kumtafuta aliyepotea.” Bila shaka, tunaweza kutoa msaada huo kwa njia inayofaa kwa kushirikiana na wazee. Je, unaweza kufanya jambo fulani kusaidia mtu aliye dhaifu katika kutaniko lenu?

Uwe Mwenye Fadhili

15. Ni nini ambacho huenda kilifanya mchungaji atende jinsi alivyotenda?

15 Mchungaji anafanya nini hatimaye anapompata kondoo aliyepotea? “Humweka juu ya mabega yake.” (Luka 15:5) Hiyo ni hatua muhimu na yenye kugusa hisia kama nini! Huenda kondoo huyo alitangatanga siku nyingi, usiku na mchana, katika eneo asilolijua, na labda akakabili hatari ya kunyemelewa na simba. (Ayubu 38:39, 40) Bila shaka kondoo huyo amedhoofika kwa sababu ya kukosa chakula. Kondoo huyo ni dhaifu sana hivi kwamba hawezi kushinda vikwazo mbalimbali anapokuwa njiani kurudi zizini. Kwa hiyo, mchungaji anainama, anamwinua kondoo kwa wororo, anambeba na kumrudisha zizini. Tunawezaje kuonyesha hangaiko kama la mchungaji huyo?

16. Kwa nini tuwe na fadhili kama yule mchungaji mwenye kondoo aliyepotea?

16 Huenda mtu ambaye ameacha kushirikiana na kutaniko akawa amechoka kiroho. Kama kondoo aliyetenganishwa na mchungaji, huenda mtu huyo alirandaranda bila kusudi katika ulimwengu huu wenye uadui. Bila ulinzi kutoka katika kundi, kutaniko la Kikristo, anakabili hatari kubwa sana ya kushambuliwa na Ibilisi, ambaye “hutembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.” (1 Petro 5:8) Isitoshe, amedhoofika kwa kukosa chakula cha kiroho. Kwa hiyo, bila kusaidiwa yaelekea yeye ni dhaifu sana hivi kwamba hawezi kushinda vikwazo mbalimbali akiwa safarini kurudi kutanikoni. Kwa hiyo, tunapaswa kuinama kwa njia ya mfano, kumwinua aliye dhaifu, na kumbeba hadi kutanikoni. (Wagalatia 6:2) Tunawezaje kufanya hivyo?

17. Tunawezaje kumwiga mtume Paulo tunapomtembelea mtu aliye dhaifu?

17 Mtume Paulo alisema: “Kama mtu yeyote ni dhaifu, nami pia ni dhaifu.” (2 Wakorintho 11:29, Biblia Habari Njema; 1 Wakorintho 9:22) Paulo aliwahurumia watu, kutia ndani walio dhaifu. Sisi pia tungependa kuwahurumia wale walio dhaifu. Unapomtembelea Mkristo aliye dhaifu kiroho, mhakikishie kwamba ana thamani machoni pa Yehova na kwamba Mashahidi wenzake wanamkosa sana. (1 Wathesalonike 2:17) Mjulishe kwamba Mashahidi wangependa kumtia moyo na wako tayari kuwa ‘ndugu aliyezaliwa siku ya taabu.’ (Mithali 17:17; Zaburi 34:18) Mazungumzo yetu machangamfu yanaweza kumtia moyo hatua kwa hatua na anaweza kurudi tena kwenye kundi. Tunapaswa kufanya nini baada ya hapo? Tunapata mwongozo kutokana na kielezi cha mwanamke na sarafu iliyopotea.

Uwe Mwenye Bidii

18. (a) Kwa nini mwanamke anayesimuliwa katika kielezi hakukata tamaa? (b) Mwanamke huyo alionyesha jitihada gani yenye bidii, na matokeo yakawaje?

18 Mwanamke aliyepoteza sarafu anajua kwamba anakabili hali ngumu lakini hakati tamaa. Iwapo sarafu hiyo ingeanguka kichakani au kutumbukia ndani ya ziwa lenye tope, labda mwanamke huyo angekata tamaa kabisa. Hata hivyo, kwa kuwa anajua kwamba sarafu hiyo iko mahali fulani nyumbani mwake, ambapo anaweza kuipata, anaitafuta kwa makini na kwa bidii. (Luka 15:8) Kwanza, anawasha taa ili kuangaza nyumba. Kisha anafagia sakafu kwa ufagio akitumaini kusikia mlio fulani. Hatimaye, anapekua kwa bidii kila pembe na nyufa za nyumba hadi anapoona kitu chenye kumetameta. Mwanamke huyo anathawabishwa kwa sababu ya jitihada yake yenye bidii!

19. Hatua zilizochukuliwa na mwanamke katika kielezi cha sarafu iliyopotea zinaweza kutufunza nini kuhusu kuwasaidia walio dhaifu?

19 Habari hiyo inayohusu kielezi hicho, inatukumbusha kwamba sote tunaweza kutimiza daraka la Kimaandiko la kusaidia Mkristo aliye dhaifu. Wakati huohuo, tunatambua kwamba jitihada inahitajiwa. Kwa kweli, mtume Paulo aliwaambia wazee wa Efeso hivi: “Kwa kufanya kazi ya jasho hivyo ni lazima msaidie wale walio dhaifu.” (Matendo 20:35a) Kumbuka kwamba mwanamke huyo hatafuti sarafu hiyo nyumbani mwake pasipo mpango. La, anafaulu kwa sababu anaitafuta kwa makini “mpaka aipate.” Vivyo hivyo, tunapojitahidi kumsaidia mtu aliye dhaifu kiroho, tunahitaji tuwe na bidii na kusudi. Tunaweza kufanya nini?

20. Walio dhaifu wanaweza kusaidiwaje?

20 Tunawezaje kumsaidia mtu aliye dhaifu awe na imani na shukrani? Huenda ikatubidi kujifunza Biblia pamoja naye tukitumia kichapo kinachofaa cha Kikristo. Kwa kweli, kujifunza Biblia pamoja na mtu aliye dhaifu hutuwezesha kumsaidia hatua kwa hatua na kikamilifu. Huenda mwangalizi wa utumishi akaamua ni nani anayeweza kutoa msaada unaohitajiwa. Anaweza kupendekeza habari ambazo mtu huyo anaweza kujifunza na ni kichapo gani kinachofaa zaidi. Kama yule mwanamke anayetajwa katika kielezi anavyotumia vifaa vinavyofaa ili kutimiza kazi yake, sisi leo tuna vifaa vinavyotusaidia kutimiza kazi tuliyopewa na Mungu ya kusaidia walio dhaifu. Vichapo vipya tulivyopata hivi karibuni vitatusaidia sana kutimiza kazi hiyo. Vitabu hivyo ni, Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli na Mkaribie Yehova. *

21. Kusaidia walio dhaifu huletaje baraka kwa wote?

21 Kusaidia walio dhaifu huleta baraka kwa wote. Mtu anayesaidiwa hupata furaha ya kuungana tena na marafiki wa kweli. Tunapata furaha ya kweli ambayo hutokana tu na kutoa. (Luka 15:6, 9; Matendo 20:35b) Kutaniko lote huwa na uchangamfu kila mshiriki anapopendezwa na wengine. Zaidi ya yote, Wachungaji wetu wanaojali, Yehova na Yesu, hupata sifa watumishi wao walio duniani wanapoiga nia ya kusaidia walio dhaifu. (Zaburi 72:12-14; Mathayo 11:28-30; 1 Wakorintho 11:1; Waefeso 5:1) Kwa hiyo, tuna sababu nzuri kama nini ya kuendelea ‘kuwa na upendo miongoni mwetu’!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini sote tunahitaji kuonyeshana upendo?

• Kwa nini tuwaonyeshe upendo walio dhaifu?

• Tunajifunza nini kutokana na kielezi cha kondoo aliyepotea na sarafu iliyopotea?

• Tunaweza kuchukua hatua gani hususa kusaidia mtu aliye dhaifu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Katika kuwasaidia walio dhaifu, tunaonyesha upendezi, tunakuwa wenye fadhili na bidii

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kusaidia walio dhaifu huleta baraka kwa wote