Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Weupe wa Moyo Pekee Unatosha Kumpendeza Mungu?

Je, Weupe wa Moyo Pekee Unatosha Kumpendeza Mungu?

Je, Weupe wa Moyo Pekee Unatosha Kumpendeza Mungu?

JE, KWA kweli weupe wa moyo ni sifa nzuri katika maisha yetu ya kila siku? Weupe wa moyo ni hali ya kuwa bila unafiki au kujifanya, bali kuwa mnyofu na mwenye kusema kweli. Kwa wazi, sifa hii ni yenye faida katika kusitawisha uhusiano mzuri pamoja na wengine. Mtume Paulo alisihi hivi: “Iweni watiifu katika kila jambo kwa wale ambao ni mabwana-wakubwa wenu katika maana ya kimwili, si kwa matendo ya utumishi wa macho, kama wapendeza-wanadamu, bali kwa weupe wa moyo, kwa kumhofu Yehova.” (Wakolosai 3:22) Ni nani ambaye hangependa mfanyakazi kama huyo mwenye weupe wa moyo? Leo, watu walio na weupe wa moyo wanaweza kupata kazi kwa urahisi na kudumisha kazi hizo.

Hata hivyo, kile ambacho hufanya weupe wa moyo kuwa sifa nzuri zaidi ni jinsi sifa hiyo inavyohusu uhusiano wetu pamoja na Mungu. Waisraeli wa kale walifurahia baraka za Mungu walipofuata kwa makini sheria za Mungu na sherehe mbalimbali. Paulo akizungumza kuhusu usafi wa kutaniko, alisihi hivi Wakristo: “Acheni tushike msherehekeo, si kwa chachu ya zamani, wala si kwa chachu ya ubaya na uovu, bali kwa keki zisizotiwa chachu za weupe wa moyo na kweli.” (1 Wakorintho 5:8) Ili ibada yetu ikubaliwe na Mungu, ni muhimu kuwa na sifa nzuri ya weupe wa moyo. Lakini, ona kwamba weupe wa moyo peke yake hautoshi. Ni lazima uambatane na kweli.

Huenda watengenezaji wa meli ya Titanic wakawa waliamini kwa moyo mweupe kwamba meli hiyo haingeweza kamwe kuzama. Hata hivyo, katika safari yake ya kwanza mwaka wa 1912, iligonga mwamba wa barafu na watu 1,517 wakafa. Huenda ikawa Wayahudi fulani wa karne ya kwanza waliamini kwa unyofu njia yao ya kumwabudu Mungu, lakini bidii yao haikuwa “kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Ili tukubaliwe na Mungu, lazima imani yetu ya moyo mweupe ipatane na habari iliyo sahihi. Mashahidi wa Yehova wanaoishi karibu nawe watafurahi kukusaidia uchunguze yale yanayohusika katika kumtumikia Mungu kwa weupe wa moyo na kweli.