Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kusitawisha Maoni Yanayofaa Kuhusu Kazi

Jinsi ya Kusitawisha Maoni Yanayofaa Kuhusu Kazi

Jinsi ya Kusitawisha Maoni Yanayofaa Kuhusu Kazi

KWA sababu ya ushindani mkali sana katika masoko ya dunia na uzalishaji wa bidhaa kwa wingi, leo watu wengi hawana hamu ya kwenda kazini kila siku. Hata hivyo, tunapaswa kufurahia kazi yetu. Kwa nini? Kwa sababu tuliumbwa kwa mfano wa Mungu, naye hufurahia kazi yake. Kwa mfano, alipotazama kazi aliyokuwa amefanya mwishoni mwa “siku” sita za uumbaji, au vipindi virefu sana, kitabu cha Mwanzo 1:31 chasema: ‘Mungu aliona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.’

Sababu moja inayofanya Yehova aitwe “Mungu mwenye furaha” ni kuwa yeye anapenda kazi. (1 Timotheo 1:11) Basi, kadiri tunavyomwiga Mungu ndivyo tunavyokuwa wenye furaha zaidi. Mfalme Sulemani wa taifa la Israeli la kale, aliyekuwa mjenzi na msimamizi stadi, aliandika hivi kuhusu kazi: “Ni karama ya Mungu kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote.”—Mhubiri 3:13.

Inaweza kuwa vigumu kusitawisha maoni yanayofaa kuhusu kazi kwa kuwa leo mambo yanabadilika upesi kazini. Lakini Yehova Mungu huwabariki wale wanaofuata mwongozo wake wa upendo. (Zaburi 119:99, 100) Watu hao wanakuwa wafanyakazi wanaothaminiwa na wanaoaminika, kwa hiyo haielekei watafutwa kazi. Wanajizoeza kuwa na maoni ya kiroho wala si ya kimwili kuhusu maisha na kazi yao. Hilo huwawezesha kufanya maamuzi yanayofaa maishani na kutambua kwamba furaha yao na usalama wao hazitegemei tu kazi ya kuajiriwa au fursa za kupata kazi ambazo mara nyingi ni haba. (Mathayo 6:31-33; 1 Wakorintho 2:14, 15) Hiyo huwasaidia pia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu kazi.

Sitawisha Maoni Yanayompendeza Mungu Kuhusu Kazi

Watu wengine hufanya kazi nyingi kupita kiasi, nao huiona kazi yao kuwa muhimu kuliko kitu kingine chochote. Nao wengine hungojea tu saa za kazi ziishe ili waweze kurudi nyumbani. Ni maoni gani yanayofaa kuhusu kazi? Biblia inajibu: “Heri konzi moja pamoja na utulivu, kuliko konzi mbili pamoja na taabu.” (Mhubiri 4:6) Kufanya kazi nyingi kupita kiasi au kwa muda mrefu sana kunaleta madhara, ni kama “kufukuza upepo.” Kwa nini? Kwa sababu huenda tukaharibu mambo ambayo hutuletea furaha zaidi: uhusiano wetu pamoja na familia na marafiki, hali yetu ya kiroho, afya yetu, na hata maisha marefu. (1 Timotheo 6:9, 10) Badala ya kulemewa na konzi mbili za kazi pamoja na ugomvi na huzuni, ni heri kutosheka na vitu vichache vya kimwili na amani ya kadiri fulani.

Ingawa Biblia inatutia moyo tuwe na maoni hayo yanayofaa, haiungi mkono uvivu. (Mithali 20:4) Uvivu hufanya tusijiheshimu na huenda ukafanya wengine wasituheshimu. Lakini jambo lililo baya zaidi ni kwamba uvivu unaharibu uhusiano wetu na Mungu. Biblia husema waziwazi kwamba mtu anayekataa kufanya kazi hastahili kula kutokana na jasho la wengine. (2 Wathesalonike 3:10) Badala yake, anapaswa kubadili njia zake na kufanya kazi kwa bidii, na hivyo kujiruzuku na kuwaruzuku kwa njia inayofaa watu wanaomtegemea. Kwa kufanya kazi kwa bidii, anaweza hata kuwasaidia wale ambao kwa kweli wanahitaji msaada—jambo ambalo Neno la Mungu hututia moyo tufanye.—Mithali 21:25, 26; Waefeso 4:28.

Kuzoezwa Tangu Utotoni Kuwa na Maoni Yafaayo Kuhusu Kazi

Ni vigumu mtu kuzoea kufanya kazi kwa bidii asipozoezwa tangu utotoni. Hivyo, Biblia huwashauri wazazi hivi: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) Wazazi wenye hekima huweka kielelezo kizuri kwa kufanya kazi kwa bidii, nao huanza kuwazoeza watoto wao kwa kuwapa kazi nyumbani kulingana na umri wao. Ingawa huenda watoto wasifurahie kufanya kazi fulani, baadaye watajiona kuwa washiriki wa familia wanaothaminiwa—hasa Baba na Mama wanapowapongeza kwa kazi yao nzuri. Inasikitisha kwamba wazazi fulani huwafanyia watoto wao kila kitu, wakifikiria kimakosa kwamba hiyo ni fadhili. Ingefaa wazazi kama hao watafakari andiko la Mithali 29:21, NW, linalosema: “Mtu akimbembeleza mtumishi [mtoto] wake tangu ujanani, atakuwa mtu asiye na shukrani katika maisha yake ya baadaye.”

Wazazi wanaojali daraka lao pia hufuatia kwa makini maendeleo ya watoto wao shuleni, wakiwatia moyo wajifunze na kusoma kwa bidii shuleni. Jambo hilo linaweza kuwasaidia watoto baadaye watakapoajiriwa.

Chagua Kazi kwa Hekima

Biblia haitaji ni kazi ya aina gani tunayopaswa kufanya, hata hivyo inatupatia mwongozo mzuri ili kazi tunayochagua kufanya isiathiri maendeleo yetu ya kiroho, utumishi wetu kwa Mungu, na majukumu mengine. Kwa mfano, mtume Paulo aliandika: “Wakati ubakio umepunguzwa. Tangu sasa acheni wale . . . wanaoutumia ulimwengu [wawe] kama wale wasioutumia kwa ukamili; kwa maana mandhari ya ulimwengu huu inabadilika.” (1 Wakorintho 7:29-31) Hakuna kitu chenye kudumu au imara kabisa katika mfumo huu wa mambo. Kutumia wakati wetu wote na nguvu zetu zote kutumikia ulimwengu huu ni kama kutumia akiba yetu yote kujenga nyumba katika eneo ambalo kwa kawaida hukumbwa na mafuriko. Ni jambo la upumbavu kama nini kufanya hivyo!

Katika tafsiri nyingine za Biblia maneno “wasioutumia kwa ukamili” yametafsiriwa kuwa “wasiojiingiza sana” na “wasiojishughulisha sana nao.” (The Jerusalem Bible; Today’s English Version) Watu wenye hekima hukumbuka daima kwamba wakati uliobaki wa mfumo huu wa mambo “umepunguzwa” na kwamba ‘kujiingiza’ au ‘kujishughulisha sana’ na mfumo huu hukatisha tamaa na huleta majuto.—1 Yohana 2:15-17.

‘Mungu Hatatuachilia Mbali kwa Vyovyote’

Yehova anajua mahitaji yetu vema kuliko vile sisi wenyewe tuyajuavyo. Pia anajua tunaishi wakati gani kuhusiana na kutimizwa kwa kusudi lake. Hivyo anatukumbusha hivi: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa fedha, huku nyinyi mkiridhika na vitu vilivyopo. Kwa maana [Mungu] amesema: ‘Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.’” (Waebrania 13:5) Maneno hayo yanafariji kama nini! Kwa kumwiga Mungu anayewajali watu wake kwa upendo, Yesu alizungumzia kirefu maoni yanayofaa kuhusu kazi na vitu vya kimwili alipowafundisha wanafunzi wake katika yale Mahubiri maarufu ya Mlimani.—Mathayo 6:19-33.

Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufuata mafundisho hayo. Kwa mfano, Shahidi mmoja, aliye fundi wa umeme, alikataa ombi la mwajiri wake la kufanya kazi ya ziada kwa ukawaida. Kwa nini? Kwa sababu hakutaka kazi yake ya kuajiriwa ipunguze wakati ambao alitumia pamoja na familia yake na kufanya mambo ya kiroho. Mwajiri wake alikubaliana naye kwa kuwa alikuwa mfanyakazi mzuri, aliyeaminika. Bila shaka, si sikuzote mambo yanakuwa hivyo, na huenda mtu akalazimika kutafuta kazi nyingine ili kuwa na maisha mazuri. Hata hivyo, kwa kawaida wale wanaomtumaini Yehova kabisa hutambua kwamba mwenendo wao mzuri na kufanya kazi kwao kwa bidii huvutia waajiri wao.—Mithali 3:5, 6.

Wakati Kazi Zote Zitakapofurahisha

Katika mfumo huu wa mambo usio mkamilifu, hapana shaka kwamba sikuzote kutakuwako matatizo na wasiwasi kuhusiana na kazi ya kuajiriwa au matazamio ya kuipata. Huenda hata mambo yakawa mabaya zaidi kadiri hali katika ulimwengu zinavyozidi kuyumbayumba na uchumi kubadilika-badilika au hata kuharibika. Lakini hali hiyo ni ya muda tu. Karibuni kila mtu atakuwa na kazi. Na zaidi, kazi zote zitakuwa nzuri na zenye kufurahisha. Itawezekanaje? Ni nini kitakacholeta mabadiliko hayo?

Kupitia nabii wake Isaya, Yehova alitaja wakati ambapo kila mtu atakuwa na kazi. Yehova alisema, “Mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” (Isaya 65:17) Alikuwa akizungumza juu ya serikali yake mpya ambayo itatawala jamii mpya kabisa ya wanadamu, iliyo tofauti na ya sasa.—Danieli 2:44.

Unabii huo unasema hivi kuhusu jinsi watu watakavyoishi na kufanya kazi: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu; kwa sababu wao ni wazao wa hao waliobarikiwa na BWANA, na watoto wao pamoja nao.”—Isaya 65:21-23.

Hali zitakuwa tofauti kama nini katika ulimwengu huo mpya ambao Mungu anakusudia kuuleta! Je, ungependa kuishi katika ulimwengu kama huo, ambapo ‘hautajitaabisha kwa kazi bure’ badala yake utafurahia kabisa “matunda” ya kazi yako? Hata hivyo, ona ni nani watakaofurahia baraka hizo: “Wao ni wazao wa hao waliobarikiwa na BWANA.” Unaweza kuwa mmoja wa “hao waliobarikiwa” kwa kujifunza kumhusu Yehova na kutimiza matakwa yake. Yesu alisema: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Mashahidi wa Yehova watafurahia kukusaidia upate ujuzi huo unaotoa uhai kwa kujifunza pamoja nawe kwa ukawaida Neno la Mungu, Biblia.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

“WANAHITAJIKA SANA”

“Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kwa wanadamu,” Biblia inasema. (Wakolosai 3:23) Bila shaka, mfanyakazi anayeongozwa na kanuni hiyo anapofanya kazi atapendwa sana. Kwa sababu hiyo, J. J. Luna katika kitabu chake How to Be Invisible, anawashauri waajiri wanaotaka wafanyakazi watafute washiriki wenye bidii wa dini mbalimbali. Lakini anaendelea kusema: ‘Ukweli ni kwamba sisi kwa kawaida huajiri Mashahidi [wa Yehova].’ Sababu moja anayotoa ni kwamba Mashahidi wanajulikana sana kuwa watu wanyofu, jambo linalofanya ‘wahitajike sana’ katika kazi za aina mbalimbali.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Unakuwa mwenye furaha unapofanya kazi na vilevile kutenga wakati kwa mambo ya kiroho na starehe