Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Kaeni Katika Neno Langu’

‘Kaeni Katika Neno Langu’

‘Kaeni Katika Neno Langu’

“Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, nyinyi kwa kweli ni wanafunzi wangu.”—YOHANA 8:31.

1. (a) Yesu aliporudi mbinguni, aliacha nini duniani? (b) Tutazungumzia maswali gani?

YESU KRISTO, yule Mwanzilishi wa Ukristo, hakuacha ameandika vitabu vyovyote, wala kujenga minara yoyote ya ukumbusho, wala kuacha amelundika mali hapa duniani aliporudi mbinguni. Hata hivyo, aliacha wanafunzi na vilevile matakwa hususa ya kuwa mwanafunzi. Kwa kweli, katika Injili ya Yohana, tunaona kwamba Yesu alitaja matakwa matatu muhimu ambayo mtu yeyote anayetaka kuwa mwanafunzi wake anapaswa kuyatimiza. Hayo ni matakwa gani? Tunaweza kufanya nini ili kuyatimiza? Nasi tunaweza kuhakikishaje kwamba tuna sifa zinazotustahilisha kuwa wanafunzi wa Kristo leo? *

2. Kama lilivyoandikwa katika Injili ya Yohana, ni lipi takwa muhimu la kuwa mwanafunzi?

2 Miezi sita hivi kabla ya kifo chake, Yesu alienda Yerusalemu na kuhubiria umati wa watu waliokuwa wamekusanyika huko kwa ajili ya Sherehe ya Vibanda iliyosherehekewa kwa muda wa juma moja. Sherehe hiyo ilipokuwa katikati, “wengi wa umati waliweka imani katika yeye” kwa sababu ya mahubiri yake. Yesu aliendelea kuhubiri hivi kwamba siku ya mwisho ya sherehe hiyo, “wengi waliweka imani katika yeye.” (Yohana 7:10, 14, 31, 37; 8:30) Wakati huo, Yesu alielekeza fikira zake kwa waamini wapya na kutaja takwa moja muhimu la kuwa mwanafunzi ambalo liliandikwa na mtume Yohana: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, nyinyi kwa kweli ni wanafunzi wangu.”—Yohana 8:31.

3. Ni sifa gani inayohitajiwa ili mtu ‘akae katika neno la Yesu’?

3 Yesu hakusema maneno hayo ili kuonyesha kwamba waamini wapya hawakuwa na imani. Badala yake, alikuwa akisema kwamba walikuwa na fursa ya kuwa wanafunzi wake wa kweli—mradi wangekaa katika neno lake na kuwa wavumilivu. Walikuwa wamekubali neno lake, lakini sasa walipaswa kukaa katika neno hilo. (Yohana 4:34; Waebrania 3:14) Kwa kweli, Yesu aliona uvumilivu kuwa sifa muhimu kwa wafuasi wake hivi kwamba alipozungumza na mitume wake mara ya mwisho, kama tusomavyo katika Injili ya Yohana, Yesu aliwasihi mara mbili hivi: ‘Endeleeni kunifuata mimi.’ (Yohana 21:19, 22) Wakristo wengi wa mapema walifanya hivyo. (2 Yohana 4) Ni nini kilichowasaidia kuvumilia?

4. Ni nini kilichowawezesha Wakristo wa mapema kuvumilia?

4 Mtume Yohana, aliyekuwa mwanafunzi mwaminifu wa Kristo kwa miaka 70 hivi, alitaja jambo fulani muhimu. Aliwapongeza Wakristo waaminifu kwa kusema: “Nyinyi ni wenye nguvu na neno la Mungu hukaa katika nyinyi na mmemshinda mwovu.” Wanafunzi hao wa Kristo walivumilia, au walikaa katika neno la Mungu, kwa sababu neno la Mungu lilikaa ndani yao. Walilithamini sana. (1 Yohana 2:14, 24) Vivyo hivyo leo, ili ‘kuvumilia hadi mwisho,’ tunahitaji kuhakikisha kwamba neno la Mungu linakaa ndani yetu. (Mathayo 24:13) Tunawezaje kufanya hivyo? Tunapata jibu katika kielezi kimoja cha Yesu.

“Anayelisikia Neno”

5. (a) Yesu anataja aina gani tofauti za udongo katika mojawapo ya vielezi vyake? (b) Katika kielezi cha Yesu mbegu na udongo zinawakilisha nini?

5 Yesu alitaja kielezi cha mpanzi anayepanda mbegu, ambacho kinapatikana katika Injili ya Mathayo, Marko, na Luka. (Mathayo 13:1-9, 18-23; Marko 4:1-9, 14-20; Luka 8:4-8, 11-15) Unaposoma masimulizi hayo, utaona kwamba jambo kuu katika kielezi hicho ni kwamba mbegu ileile inaanguka kwenye udongo mbalimbali na matokeo yakawa tofauti. Udongo wa kwanza ni mgumu, wa pili hauna kina, nao wa tatu umejaa miiba. Udongo wa nne ni “bora” na “mzuri,” tofauti na aina hizo tatu. Kulingana na ufafanuzi wa Yesu, mbegu ni ujumbe wa Ufalme unaopatikana katika Neno la Mungu, nao udongo unawakilisha watu wenye hali mbalimbali za moyoni. Ingawa kuna mambo yanayofanana kuhusu watu wanaowakilishwa na aina hizo tofauti-tofauti za udongo, wale wanaowakilishwa na udongo ulio bora wana sifa fulani inayowatofautisha na wengine.

6. (a) Aina ya nne ya udongo unaotajwa katika kielezi cha Yesu unatofautianaje na zile aina nyingine tatu, na hilo linamaanisha nini? (b) Ni nini kilicho muhimu ili kuonyesha uvumilivu tukiwa wanafunzi wa Kristo?

6 Simulizi linalopatikana katika andiko la Luka 8:12-15 linaonyesha kwamba katika hali zote nne, watu ‘husikia neno.’ Hata hivyo, wale wenye “moyo ulio bora na mwema” huchukua hatua zaidi baada ya “kusikia lile neno.” ‘Wanalihifadhi na kuzaa matunda kwa uvumilivu.’ Kwa kuwa udongo ulio bora na mzuri ni wenye kina na si mgumu, mizizi ya mbegu hupenya ndani na kwa hiyo mbegu huota na kuzaa matunda. (Luka 8:8) Vivyo hivyo, wale wenye mioyo iliyo bora huelewa, huthamini, na kuvama katika neno la Mungu. (Waroma 10:10; 2 Timotheo 2:7) Neno la Mungu hukaa ndani yao. Kwa hiyo, wao huzaa matunda kwa uvumilivu. Hivyo basi, ni muhimu kulithamini sana Neno la Mungu ili tuweze kuonyesha uvumilivu tukiwa wanafunzi wa Kristo. (1 Timotheo 4:15) Hata hivyo, tunawezaje kusitawisha uthamini huo wa Neno la Mungu?

Hali ya Moyoni na Kutafakari kwa Makini

7. Ni jambo gani linalohusianishwa sana na moyo mzuri?

7 Ona jambo ambalo Biblia inahusianisha na moyo ulio bora na mzuri. “Moyo wa mwenye haki hufikiri [“hutafakari,” NW] jinsi atakavyojibu.” (Mithali 15:28) “Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya [“kutafakari kwa,” NW] moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee BWANA.” (Zaburi 19:14) “Kinywa changu kitanena hekima, na fikira za [“kutafakari kwa” NW] moyo wangu zitakuwa na busara.”—Zaburi 49:3.

8. (a) Tunapaswa kuepuka nini tunaposoma Biblia, na tunapaswa kufanya nini? (b) Tunapata manufaa gani kwa kutafakari Neno la Mungu kwa sala? (Tia ndani sanduku “Mmewekwa Imara Katika Kweli.”)

8 Kama waandikaji hao wa Biblia, sisi pia tunahitaji kutafakari Neno la Mungu na utendaji wake kwa njia inayofaa na kwa sala. Tunaposoma Biblia au vitabu vinavyozungumzia Biblia, hatupaswi kuwa kama watalii wenye haraka-haraka ambao hutoka kwenye mandhari moja yenye kuvutia huku wakipiga picha bila hata kufurahia mandhari hizo. Badala yake, tunapojifunza Biblia tungependa kutenga wakati wa kutosha kufurahia usomaji wetu. * Neno la Mungu huathiri moyo wetu tunapotafakari mambo tunayosoma. Neno la Mungu hugusa hisia zetu na kuelekeza fikira zetu. Pia hutuchochea kumweleza Mungu mawazo yetu ya ndani katika sala. Kwa hiyo, tunampenda Yehova zaidi, na upendo wetu kwake hutuchochea tuendelee kumfuata Yesu hata chini ya hali ngumu. (Mathayo 10:22) Bila shaka, ni muhimu kutafakari yale ambayo Mungu anasema iwapo tunataka kudumu tukiwa waaminifu hadi mwisho.—Luka 21:19.

9. Tunawezaje kuhakikisha kwamba moyo wetu unaendelea kupokea neno la Mungu?

9 Pia kielezi cha Yesu kinaonyesha kwamba kuna mambo yanayozuia mbegu ya neno la Mungu isikue. Kwa hiyo, ili tudumu tukiwa wanafunzi waaminifu, tunapaswa (1) kutambua vizuizi vinavyowakilishwa na hali mbalimbali zisizofaa za udongo katika kielezi hicho na (2) kuchukua hatua ya kurekebisha au kuepuka vizuizi hivyo. Kwa kufanya hivyo, tutahakikisha kwamba mioyo yetu inaendelea kupokea mbegu ya Ufalme na kuzaa matunda.

“Kando ya Barabara” Yamaanisha Wale Wanaokengeushwa

10. Fafanua aina ya kwanza ya udongo katika kielezi cha Yesu na ueleze udongo huo unamaanisha nini.

10 Mbegu inaanguka kwanza kwenye udongo ulio “kando ya barabara,” ambapo mbegu hiyo ‘inakanyagwakanyagwa.’ (Luka 8:5) Udongo ulio kando ya barabara inayopita katikati ya shamba la nafaka ni mgumu kwa sababu ya kukanyagwa-kanyagwa na watu. (Marko 2:23) Vivyo hivyo, wale ambao huruhusu hekaheka za ulimwengu ziwakoseshe wakati na nguvu huenda wakajikuta wamekengeushwa na hivyo kukosa kulithamini neno la Mungu. Wanasikia neno hilo, lakini hawalitafakari. Kwa hiyo, mioyo yao inashindwa kulipokea. Kabla hawajaanza kulipenda, “Ibilisi huja na kuliondoa lile neno kutoka mioyoni mwao ili wasipate kuamini waokolewe.” (Luka 8:12) Je, jambo hilo linaweza kuepukwa?

11. Tunaweza kuzuiaje hali yetu ya moyoni isiwe kama udongo mgumu?

11 Kuna mengi yanayoweza kufanywa ili kuzuia moyo usiwe kama udongo ulio kando ya barabara ambao hautokezi mazao. Udongo ambao umekanyagwa-kanyagwa na kuwa mgumu unaweza kuwa laini ukilimwa na watu wakiacha kuukanyaga. Vivyo hivyo, kutafuta wakati wa kujifunza na kutafakari Neno la Mungu kunaweza kufanya moyo uwe kama udongo mzuri unaotokeza mazao. Siri ni kutokengeushwa na mambo ya kawaida maishani. (Luka 12:13-15) Badala yake, hakikisha kwamba unatenga wakati wa kutafakari “mambo yaliyo ya maana zaidi” maishani.—Wafilipi 1:9-11.

“Juu ya Tungamo-Mwamba” Yamaanisha Kuwa Mwoga

12. Sababu halisi ni ipi ambayo inafanya mche katika aina ya pili ya udongo unaotajwa kwenye kielezi cha Yesu unyauke?

12 Mbegu inapoanguka kwenye aina ya pili ya udongo, haibaki hapo, kama ilivyokuwa katika aina ya kwanza ya udongo. Inaota mizizi na kuchipuka. Lakini jua linapotokea, mche huo unachomwa na joto la jua na kunyauka. Hata hivyo, ona jambo hili muhimu. Mche huo haunyauki hasa kwa sababu ya joto. Kwani, mmea unaomea katika udongo mzuri unapigwa na jua pia, lakini haunyauki—unasitawi. Mbona kuwe na tofauti hiyo? Yesu anasema, mmea huo unanyauka “kwa sababu ya kutokuwa na kina cha udongo” na “kutokuwa na unyevunyevu.” (Mathayo 13:5, 6; Luka 8:6) “Tungamo-mwamba,” lililo chini ya udongo wa juu, linazuia mbegu hiyo isipenyeze mizizi vya kutosha na kupata unyevu na kuimarika. Mche huo unanyauka kwa sababu udongo huo hauna kina.

13. Ni watu gani walio kama udongo usio na kina, na ni nini hasa ambacho hufanya waogope?

13 Sehemu hii ya kielezi inahusu watu ambao “hulipokea lile neno kwa shangwe” na kumfuata Yesu kwa bidii “kwa majira.” (Luka 8:13) Wanapokabili “dhiki au mnyanyaso” mkali, wanaogopa sana hivi kwamba wanapoteza shangwe na nguvu na kuacha kumfuata Kristo. (Mathayo 13:21) Hata hivyo, sababu hasa inayofanya waogope si upinzani. Kwa kuwa kuna mamilioni ya wanafunzi wa Kristo wanaovumilia dhiki mbalimbali na bado wanadumu wakiwa waaminifu. (2 Wakorintho 2:4; 7:5) Sababu halisi inayofanya wengine waogope na kuacha kweli ni kwamba hali yao ya moyoni iliyo kama mwamba huwazuia wasitafakari vya kutosha mambo yanayofaa ya kiroho. Kwa hiyo, hawapendezwi kikweli na Yehova na neno lake na hivyo hawana nguvu za kuvumilia mnyanyaso. Mtu anawezaje kuepuka hali hiyo?

14. Mtu anapaswa kuchukua hatua gani ili kuzuia hali ya moyo wake isiwe kama udongo usio na kina?

14 Mtu anapaswa kuhakikisha kwamba moyo wake hauna vizuizi vilivyo kama mwamba, kama vile kuweka kinyongo kwa muda mrefu, hali ya ubinafsi isiyo dhahiri, au hisia fulani zisizofaa. Ikiwa kuna vizuizi kama hivyo, nguvu za neno la Mungu zinaweza kuvivunja. (Yeremia 23:29; Waefeso 4:22; Waebrania 4:12) Baada ya hapo, kutafakari kwa sala kutachochea “kupandwa kwa neno” ndani kabisa ya moyo wa mtu. (Yakobo 1:21) Kufanya hivyo kutatokeza nguvu za kukabiliana na nyakati zenye kuvunja moyo na kutokeza ujasiri wa kudumisha uaminifu licha ya majaribu.

“Katikati ya Miiba” Yamaanisha Kuwa na Moyo Nusu-nusu

15. (a) Kwa nini tuzingatie aina ya tatu ya udongo iliyotajwa na Yesu? (b) Ni nini kinachotokea hatimaye kuhusiana na udongo wa aina ya tatu, na kwa nini?

15 Tunapaswa kuzingatia aina ya tatu ya udongo, yaani udongo wenye miiba, kwa sababu unafanana kwa njia fulani na udongo mzuri. Mbegu iliyoanguka kwenye udongo wenye miiba inatoa mizizi na kuota sawa na ile inayoanguka kwenye udongo mzuri. Mwanzoni, hakuna tofauti katika ukuzi wa mmea mpya katika aina hizi mbili za udongo. Hata hivyo, baada ya muda hali fulani inatokea ambayo hatimaye inasonga mmea. Tofauti na udongo mzuri, udongo huu umejaa miiba. Mmea mchanga unapochipuka kutoka udongoni, unasongwa na ‘miiba inayokua pamoja nao.’ Kwa muda fulani mimea hiyo inapigania lishe, nuru, na nafasi, lakini hatimaye miiba inashinda mmea huo na ‘kuusonga.’—Luka 8:7.

16. (a) Ni watu gani wanaofanana na udongo wenye miiba? (b) Kulingana na masimulizi ya vitabu vitatu vya Injili, miiba huwakilisha nini?—Ona kielezi-chini.

16 Ni watu gani wanaofanana na udongo wenye miiba? Yesu anaeleza hivi: “Hawa ndio ambao wamesikia, lakini, kwa kuchukuliwa na mahangaiko na mali na raha za maisha haya, wao husongwa kabisa na hawakamilishi kitu.” (Luka 8:14) Kama vile mbegu za mpanzi na miiba inavyokua katika udongo kwa wakati uleule, ndivyo watu fulani hujaribu kujifunza neno la Mungu na wakati uleule kufuatia “raha za maisha haya.” Ukweli wa neno la Mungu hupandwa katika mioyo yao, lakini unakabili ushindani kutoka kwa mambo mengine wanayohitaji kuyashughulikia. Moyo wao wa mfano umegawanyika. (Luka 9:57-62) Hilo huwazuia wasiwe na wakati wa kutosha kutafakari neno la Mungu kwa sala na kwa njia inayofaa. Wanashindwa kuvama katika neno la Mungu na hivyo wanakosa kuonyesha uthamini unaohitajiwa ili kuvumilia. Hatua kwa hatua, ufuatiaji wa mambo ya kimwili huzuia na hata ‘husonga kabisa’ mambo ya kiroho. * Wale wasiompenda Yehova kwa moyo wote wanapatwa na matokeo ya kuhuzunisha kama nini!—Mathayo 6:24; 22:37.

17. Tunapaswa kufanya maamuzi gani maishani ili tusisongwe na miiba ya mfano inayotajwa katika kielezi cha Yesu?

17 Kwa kutanguliza mambo ya kiroho badala ya mambo ya kimwili, tunaepuka kusongwa na matatizo na raha za ulimwengu huu. (Mathayo 6:31-33; Luka 21:34-36) Hatupaswi kupuuza kusoma na kutafakari yale tunayosoma katika Biblia. Tutapata wakati zaidi wa kutafakari kwa makini na kwa sala tukifanya maisha yetu yawe sahili kadiri tuwezavyo. (1 Timotheo 6:6-8) Watumishi wa Mungu ambao kwa njia ya mfano wameng’oa miiba kutoka kwenye udongo ili mmea unaozaa matunda upate lishe, nuru na nafasi zaidi, wanabarikiwa na Yehova. Sandra mwenye umri wa miaka 26 anasema hivi: “Ninapotafakari baraka ambazo nimepata kwa kujifunza kweli, ninaona kwamba ulimwengu hauwezi kutoa kitu chochote kinacholingana na kweli!”—Zaburi 84:11.

18. Tunawezaje kukaa katika neno la Mungu na kuvumilia tukiwa Wakristo?

18 Bila shaka, sisi sote, wakubwa kwa wadogo, tutakaa katika neno la Mungu na kuvumilia tukiwa wanafunzi wa Kristo mradi tu neno la Mungu linakaa ndani yetu. Kwa hiyo, na tuhakikishe kwamba udongo wa moyo wetu wa mfano hautakuwa mgumu, usio na kina, au wenye miiba, bali utabaki ukiwa mwepesi na wenye kina. Kwa kufanya hivyo, tutaweza kuvama katika neno la Mungu na “kuzaa matunda kwa uvumilivu.”—Luka 8:15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Katika makala hii, tutazungumzia takwa la kwanza. Matakwa yale mengine mawili yatazungumziwa katika makala zinazofuata.

^ fu. 8 Kwa mfano, ili kutafakari kwa sala sehemu fulani uliyosoma katika Biblia, unaweza kujiuliza hivi: ‘Je, sehemu hii inafunua sifa moja au sifa zaidi za Yehova? Inahusianaje na kichwa cha Biblia? Ninawezaje kuitumia maishani mwangu au kuitumia kuwasaidia wengine?’

^ fu. 16 Kulingana na masimulizi ya mfano wa Yesu katika vitabu vitatu vya Injili, mbegu inasongwa na matatizo na raha za ulimwengu huu: “Mahangaiko ya mfumo huu wa mambo,” “nguvu za udanganyifu wa mali,” “tamaa za mambo yale mengine,” na “raha za maisha haya.”—Marko 4:19; Mathayo 13:22; Luka 8:14; Yeremia 4:3, 4.

Ungejibuje?

• Kwa nini tunahitaji ‘kukaa katika neno la Yesu’?

• Tunawezaje kuruhusu neno la Mungu likae katika moyo wetu?

• Ni watu wa aina gani wanaowakilishwa na aina nne za udongo zinazotajwa na Yesu?

• Unawezaje kupata wakati wa kutafakari neno la Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

MMEWEKWA IMARA KATIKA KWELI”

MWAKA baada ya mwaka, watu wengi ambao wamekuwa wanafunzi wa Kristo kwa muda mrefu huthibitisha kwamba ‘wamewekwa imara katika kweli.’ (2 Petro 1:12) Ni nini huwasaidia kuvumilia? Ona baadhi ya maelezo wanayotoa.

“Mimi husoma kifungu fulani cha Biblia na kusali kabla sijalala. Kisha ninatafakari mambo niliyosoma.”—Jean, aliyebatizwa mwaka wa 1939.

“Ninapotafakari jinsi Yehova aliye juu sana anavyotupenda kwelikweli ninahisi nikiwa salama na mwenye nguvu za kuendelea nikiwa mwaminifu.”—Patricia, aliyebatizwa mwaka wa 1946.

“Kuwa na mazoea mazuri ya kusoma Biblia na kutafakari ‘mambo yenye kina kirefu ya Mungu,’ kumeniwezesha niendelee kumtumikia Yehova.”—1 Wakorintho 2:10; Anna, aliyebatizwa mwaka wa 1939.

“Mimi husoma Biblia pamoja na vitabu vyetu vinavyozungumzia Biblia nikiwa na kusudi la kuchunguza moyo wangu na nia yangu.”—Zelda, aliyebatizwa mwaka wa 1943.

“Mimi hufurahia sana pindi ninapotembea na kuzungumza na Yehova kwa sala na kumweleza jinsi ninavyohisi.”—Ralph, aliyebatizwa mwaka wa 1947.

“Mimi huanza siku kwa kusoma andiko la siku na kifungu fulani cha Biblia. Ninapata jambo jipya la kutafakari siku nzima.”—Marie, aliyebatizwa mwaka wa 1935.

“Mimi huchochewa sana na vitabu vinavyozungumzia vitabu vya Biblia mstari kwa mstari.”—Daniel, aliyebatizwa mwaka wa 1946.

Wewe hutafakari neno la Mungu kwa sala wakati gani?—Danieli 6:10b; Marko 1:35; Matendo 10:9.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Tunaweza “kuzaa matunda kwa uvumilivu” kwa kutanguliza mambo ya kiroho