Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilipata Majaribu Makali Sana

Nilipata Majaribu Makali Sana

Simulizi la Maisha

Nilipata Majaribu Makali Sana

Limesimuliwa na Pericles Yannouris

Chumba cha gereza kilikuwa chenye unyevu mwingi nami nilisikia baridi sana. Nilipoketi humo peke yangu nikiwa nimejifunika kwa blanketi nyembamba tu, nilikumbuka uso wenye ubaridi wa mke wangu mchanga nilipokamatwa na wanamgambo siku mbili mapema na kumwacha yeye na watoto wetu wawili wadogo waliokuwa wagonjwa. Baadaye mke wangu ambaye hakukubali imani yangu, alinitumia mikate miwili na barua fupi iliyosema hivi: “Nakutumia mikate hii, na ninatumaini kwamba utakuwa mgonjwa kama watoto wako.” Je, ningerudi tena na kumwona mke wangu na watoto wangu?

TUKIO hilo lilikuwa moja tu kati ya matukio mengi katika mapambano yangu magumu na ya muda mrefu ya kupigania imani ya Kikristo. Mapambano hayo yalitia ndani upinzani wa jamaa, kutengwa na jamii, kushtakiwa mahakamani, na mateso makali. Lakini kwa nini mimi, mtu mpole na mwenye kumwamini Mungu nilijikuta katika mahali pabaya hivyo? Acha nieleze.

Kijana Maskini Mwenye Mradi wa Fahari

Nilipozaliwa mwaka wa 1909 huko Stavromeno, Krete, kulikuwa na vita, umaskini, na njaa nchini mwetu. Baadaye mimi na ndugu na dada zangu wadogo wanne tuliponea chupuchupu kuambukizwa Homa ya Hispania. Nakumbuka kwamba, mara kwa mara, wazazi wetu walitufungia ndani ya nyumba kwa majuma kadhaa ili tusiambukizwe ugonjwa huo.

Baba alikuwa mkulima maskini aliyeshikilia dini sana, lakini hakupinga mawazo mapya. Alikuwa ameishi Ufaransa na Madagaska, kwa hiyo alikuwa amejua maoni mapya kuhusu dini. Hata hivyo, watu wa familia yetu waliendelea kufuata dini ya Kanisa Othodoksi la Ugiriki. Tulihudhuria Misa kila Jumapili na tulimkaribisha nyumbani askofu wa eneo letu alipokuja kwa ajili ya ziara yake ya kila mwaka. Nilikuwa mwana-kwaya na nilitaka kuwa kasisi.

Nilijiunga na kikosi cha polisi mwaka wa 1929. Baba alikufa nilipokuwa kazini Thessalonica, kaskazini mwa Ugiriki. Kwa sababu nilitafuta faraja na nuru ya kiroho, niliomba nihamishwe kufanya kazi katika kituo cha polisi kwenye Mlima Athos, eneo la watawa ambalo ni “mlima mtakatifu” * kwa wafuasi wa Kanisa Othodoksi. Nilifanya kazi huko kwa miaka minne na niliweza kuchunguza maisha ya watawa kwa ukaribu. Badala ya kumkaribia Mungu, nilichukizwa kuona ukosefu wa maadili na ufisadi wa watawa uliokuwa wazi kabisa. Nilichukizwa pia wakati kasisi mmoja ambaye nilikuwa nimemheshimu aliponijia na kutaka kulala nami. Ijapokuwa mambo kama hayo yalinivunja moyo, bado nilitaka sana kumtumikia Mungu na kuwa kasisi. Hata nilivalia vazi la kasisi na kupigwa picha kama kumbukumbu. Hatimaye nilirudi Krete tena.

“Yeye Ni Ibilisi!”

Mwaka wa 1942 nilimwoa Frosini, msichana mrembo aliyekuwa wa familia iliyoheshimika. Azimio langu la kuwa kasisi lilitiwa nguvu nilipooa kwa kuwa watu wa familia ya mke wangu walikuwa watu wa dini. * Niliazimia kwenda Athens nikajifunze kwenye vyuo vya dini huko. Mwishoni mwa mwaka 1943 niliwasili kwenye bandari ya Iráklion, Krete, ili nisafiri hadi Athens, lakini meli ikaniacha. Huenda nilikosa kwenda Athens kwa sababu nilikuwa nimepata chanzo kingine cha faraja ya kiroho. Ni nini kilichokuwa kimetukia?

Kwa miaka kadhaa, Emmanuel Lionoudakis, mhubiri kijana mwenye bidii aliyekuwa akishiriki pamoja na Mashahidi wa Yehova alikuwa amefundisha kweli za Biblia zenye nuru ya kiroho kotekote kisiwani Krete. * Watu fulani walivutiwa na jinsi Mashahidi walivyoeleza Neno la Mungu kinaganaga nao wakaacha dini za uwongo. Katika mji jirani wa Sitía, kikundi cha Mashahidi wenye bidii kilianzishwa. Jambo hili lilimwudhi askofu wa hapo. Yeye alikuwa ameishi Marekani na alijua kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa na matokeo sana katika kazi yao ya kuhubiri. Hivyo akaazimia kumaliza “uasi-imani” huo katika eneo lake. Mara kwa mara aliwachochea polisi kuwakamata Mashahidi na kuwafunga gerezani na kuwapeleka mahakamani kwa mashtaka mbalimbali ya uwongo.

Mmoja wa Mashahidi hao alijaribu kunieleza kweli za Biblia, lakini akakata kauli kwamba sipendezwi. Kwa hiyo akamtuma mhudumu aliyekuwa na ujuzi zaidi aongee nami. Kwa kuwa nilijibu kwa ukali, huyo Shahidi wa pili alirudi kwa wale wengine katika kikundi kile kidogo na kuwaambia hivi: “Pericles hatakuwa Shahidi kamwe. Yeye ni Ibilisi!”

Upinzani Waanza

Nashukuru kwamba Mungu hakuniona kuwa mwovu. Mnamo Februari 1945 ndugu yangu Demosthenes aliyesadiki kwamba Mashahidi wa Yehova wanafundisha kweli, alinipa kijitabu Comfort All That Mourn (Faraja kwa Wote Wanaoomboleza). * Nilivutiwa na kijitabu hicho. Tuliacha kwenda Kanisa Othodoksi mara moja, tukajiunga na kikundi kile kidogo huko Sitía, na kuwahubiria ndugu na dada zetu juu ya imani yetu mpya. Wote walikubali kweli ya Biblia. Kama nilivyotarajia, uamuzi wangu wa kuacha dini ya uwongo ulileta uhasama kutoka kwa mke wangu na familia yao, nao wakanitenga. Baba mkwe wangu alikataa kuongea nami kwa muda fulani. Kulikuwa na ugomvi na mgogoro sikuzote nyumbani. Hata hivyo, Mei 21, 1945, mimi na Demosthenes tulibatizwa na Ndugu Minos Kokkinakis. *

Mwishowe niliweza kutimiza mradi wa maisha yangu na kutumikia kama mhudumu wa kweli wa Mungu! Bado nakumbuka siku yangu ya kwanza katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Nilisafiri peke yangu hadi kijiji fulani nikiwa na vijitabu 35 mkobani. Nilianza kwenda nyumba kwa nyumba kwa woga. Lakini kadiri nilivyosonga mbele ndivyo nilivyopata ujasiri zaidi. Wakati kasisi mmoja mwenye hasira kali alipowasili, nilisimama imara kwa ujasiri, na kukataa kwenda naye kwenye kituo cha polisi, ijapokuwa alisisitiza niende. Nilimwambia kwamba singeondoka kabla ya kumaliza kuwahubiria watu wote kijijini humo, na ndivyo nilivyofanya. Nilikuwa na furaha nyingi hivi kwamba hata sikungojea basi bali nilitembea kwa miguu hadi nyumbani, umbali wa kilometa 15.

Mkononi mwa Majambazi Wakatili

Mnamo Septemba 1945, nilikabidhiwa madaraka zaidi katika kutaniko letu jipya huko Sitía. Punde vita ya wenyewe kwa wenyewe ikaanza Ugiriki. Vikundi vya wanamgambo walishambuliana kwa ukatili na chuki nyingi. Askofu wa eneo letu alichochea kikundi kimoja cha wanamgambo wa hapo wamalize Mashahidi kwa njia yoyote ile ambayo wangeweza. (Yohana 16:2) Wanamgambo hao waliposafiri kuelekea kijiji chetu, mwanamke mmoja mwenye fadhili aliyesafiri kwa basi lilelile alisikia jinsi walivyopanga njama hiyo ya “kimungu,” naye akatuonya. Tulijificha na mtu mmoja wa ukoo alichukua hatua ya kutusaidia. Hatukuuawa.

Tukio hilo lilikuwa mwanzo wa mateso yetu. Kupigwa na kutishwa kukawa mambo ya kawaida. Wapinzani wetu walijaribu kutulazimisha turudi kanisani, tubatize watoto wetu, na tufanye ishara ya msalaba. Wakati mmoja walimpiga ndugu yangu hadi wakafikiri wamemwua. Nilihuzunika kuwaona dada zangu wawili wakipigwa baada ya mavazi yao kuraruliwa. Katika pindi hiyo, watu wa kanisa walibatiza watoto wanane wa Mashahidi wa Yehova kwa nguvu.

Mama yangu alikufa mwaka wa 1949. Kasisi alianza kutusaka tena, akitushtaki kwa kukiuka matakwa ya sheria yanayohusu ruhusa ya mazishi. Nilishtakiwa mahakamani lakini nikaachiliwa. Kesi hiyo ilikuwa ushahidi mkubwa kwa kuwa jina la Yehova lilitajwa katika maneno ya utangulizi ya kesi hiyo. Adui zetu hawakuwa na njia nyingine ya, eti, “kufanya tutambue ukweli,” ila kutukamata na kutupeleka uhamishoni. Walifanya hivyo Aprili 1949.

Mateso Makali Yaanza

Mimi na ndugu wengine wawili tulikamatwa. Mke wangu hata hakunitembelea kwenye kituo cha polisi. Kwanza tulipelekwa hadi gereza moja huko Iráklion. Kama nilivyoeleza mwanzoni, nilihisi upweke na nilikuwa nimevunjika moyo. Nilikuwa nimemwacha mke mchanga asiyekubali imani yangu na watoto wawili wachanga. Nilimwomba Yehova msaada kwa bidii. Nikakumbuka maneno haya ya Mungu katika Waebrania 13:5: “Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.” Nilitambua kwamba jambo la hekima ni kumtegemea Yehova kabisa.—Mithali 3:5.

Tuliambiwa kwamba tungepelekwa hadi Makrónisos, kisiwa kame karibu na pwani ya Athens, Ugiriki. Hata kusikia jina Makrónisos kulifanya watu waogope kwa kuwa wafungwa waliokuwa katika gereza hilo waliteswa na walilazimishwa kufanya kazi ngumu sana. Tulipitia Piraeus tulipokuwa njiani kwenda huko. Ijapokuwa tulikuwa tumefungwa pingu, tulitiwa moyo wakati baadhi ya waamini wenzetu walipoingia melini na kutukumbatia.—Matendo 28:14, 15.

Maisha huko Makrónisos yalikuwa yenye kutisha. Wanajeshi waliwatesa wafungwa tangu asubuhi mpaka usiku. Wafungwa wengi wasiokuwa Mashahidi walirukwa na akili, wengine wakafa, na wengi wakatoka wakiwa walemavu. Usiku tulisikia kilio cha wale waliokuwa wakiteswa. Blanketi yangu nyembamba haikunikinga na baridi usiku.

Muda si muda, Mashahidi wa Yehova walikuja kujulikana kambini kwa kuwa jina hilo lilitajwa kila asubuhi wafungwa walipoitwa majina kulingana na orodha. Kwa hiyo, tulikuwa na fursa nyingi za kutoa ushuhuda. Hata nilikuwa na pendeleo la kubatiza mfungwa mmoja wa kisiasa aliyekuwa amefanya maendeleo na kujiweka wakfu kwa Yehova.

Nilipokuwa uhamishoni niliendelea kumwandikia mke wangu mpendwa, lakini yeye hakuniandikia hata barua moja. Hata hivyo, niliendelea kumwandikia kwa upendo ili kumfariji na kumhakikishia kwamba hali hiyo ilikuwa ya muda tu na hatimaye tungeishi kwa furaha tena.

Idadi ya Mashahidi iliongezeka ndugu wengine walipowasili. Kwa kuwa nilifanya kazi ofisini, nilianzisha urafiki na kanali msimamizi wa kambi hiyo. Alistahi Mashahidi, kwa hiyo sikuogopa kumwomba aruhusu tutumiwe vichapo vya Biblia kutoka katika ofisi yetu huko Athens. “Jambo hilo haliwezekani,” akasema, “lakini watu wenu huko Athens wanaweza kuvifunga, kuandika jina langu juu yake, na kuvituma kwangu.” Nilipigwa na butwaa! Siku chache baadaye tulipokuwa tukiteremsha mizigo kutoka katika meli iliyokuwa imeingia, polisi mmoja alimsalimu kanali na kumwambia hivi: “Bwana, mzigo wako umefika.” “Mzigo upi?” akauliza. Kwa kuwa nilikuwa karibu na nikasikia mazungumzo hayo nikamnong’onezea hivi: “Yaonekana huo ni ule mzigo wetu ambao ulitumwa kwa jina lako kama ulivyosema.” Hiyo ilikuwa njia moja ambayo Yehova alitumia kutulisha kiroho.

Baraka Isiyotarajiwa, Kisha Mateso Mengine

Mwishoni mwa mwaka 1950 niliachiliwa. Nilirudi nyumbani nikiwa mgonjwa na nimekonda sana, na sikujua kama ningekaribishwa. Nilifurahi sana kumwona mke wangu na watoto wangu tena! Na nilishangaa kuona kwamba uhasama wa Frosini ulikuwa umepunguka. Barua nilizoandika nikiwa gerezani zilikuwa na matokeo. Frosini alikuwa ameguswa na uvumilivu na ustahimilivu wangu. Muda mfupi baadaye nilikuwa na mazungumzo marefu pamoja naye yaliyotupatanisha. Alikubali kujifunza Biblia na kumwamini Yehova na ahadi zake. Mojawapo ya siku zenye furaha zaidi maishani mwangu ilikuwa siku moja mwaka wa 1952 nilipombatiza Forsini aliyekuwa amejiweka wakfu kwa Yehova!

Mwaka wa 1955 tulianzisha kampeni ya kuwagawia makasisi wote kijitabu kinachoitwa Christendom or Christianity—Which One Is “the Light of the World”? Nilikamatwa na kufikishwa mahakamani, pamoja na Mashahidi wengine kadhaa. Kesi dhidi ya Mashahidi wa Yehova zilikuwa nyingi sana hivi kwamba mahakama ilipanga pindi ya pekee ili kesi zote zishughulikiwe. Katika siku hiyo, watu wote walioshughulikia mambo ya kisheria katika mkoa huo walikuwapo, na chumba kilijaa makasisi. Askofu alitembeatembea kwenye vijia katikati ya viti. Kasisi mmoja alinishtaki kwa kugeuza imani ya watu. Hakimu alimwuliza: “Je, imani yako ni dhaifu hivi kwamba ungeweza kugeuzwa imani kwa kusoma kijitabu kimoja?” Kasisi hakuwa na la kusema. Niliachiliwa, lakini ndugu wengine walihukumiwa vifungo vya miezi sita.

Katika miaka iliyofuata, tulikamatwa tena na tena, na kesi za mahakamani zilikuwa nyingi sana. Mawakili wetu walikuwa na kazi nyingi sana. Nilifikishwa mahakamani mara 17. Licha ya upinzani huo, tulifanya kazi ya kuhubiri kwa ukawaida. Tulikabili magumu hayo kwa furaha, na mateso yaliboresha imani yetu.—Yakobo 1:2, 3.

Mapendeleo na Magumu Mapya

Tulihamia Athens mwaka wa 1957. Punde niliteuliwa kutumikia katika kutaniko jipya. Kwa kuwa mke wangu aliniunga mkono kwa moyo wote tuliishi maisha rahisi, na tulikaza fikira juu ya utendaji wa kiroho. Kwa hiyo tuliweza kutumia wakati mwingi katika kazi ya kuhubiri. Mara kwa mara tuliombwa kuhamia makutaniko mbalimbali yenye uhitaji.

Mnamo mwaka wa 1963 mwana wangu alifikia umri wa miaka 21, ambao ni umri wa kujiandikisha jeshini. Kwa sababu Mashahidi walikataa kujiandikisha, wote walioitwa kujiandikisha walipigwa, wakadhihakiwa, na kufedheheshwa. Mwana wangu alipitia magumu hayo pia. Nilimpatia blanketi langu kutoka Makrónisos ili kumtia moyo afuate mfano wa wengine waliokuwa waaminifu. Kwa kawaida ndugu walioitwa kujiandikisha jeshini walihukumiwa kifungo cha miaka miwili hadi minne katika mahakama ya jeshi. Baada ya kuachiliwa waliitwa tena na kuhukumiwa tena. Kwa sababu nilikuwa mhudumu wa dini, niliweza kutembelea magereza mbalimbali na kuwasiliana kidogo na mwana wangu na Mashahidi wengine waaminifu. Mwana wangu alifungwa kwa zaidi ya miaka sita.

Yehova Alitusaidia Kuvumilia

Baada ya uhuru wa dini kurudishwa Ugiriki, nilikuwa na pendeleo la kutumikia kama painia wa pekee wa muda katika kisiwa cha Rhodes. Kisha, mwaka wa 1986, niliombwa niende kusaidia kutaniko la Sitía, Krete. Nilifurahi kukubali kwenda kutumikia tena katika kutaniko nilipoanza utumishi langu wa Kikristo, na kutumikia pamoja na waamini wenzangu wapendwa ambao nimewajua tangu ujana wangu.

Mimi ni mzee wa jamaa yetu, na ninafurahi sana kuwaona karibu watu 70 wa jamaa yangu wakimtumikia Yehova, na idadi hiyo inazidi kuongezeka.  Wengine wa jamaa yetu wametumikia kama wazee katika kutaniko, watumishi wa huduma, mapainia, Wanabetheli, na waangalizi wasafirio. Kwa zaidi ya miaka 58, imani yangu imejaribiwa kwa mateso makali sana. Sasa mimi nina umri wa miaka 93, na ninapofikiria yaliyopita maishani mwangu, sijuti kwamba nimemtumikia Mungu. Yeye ndiye amenipa nguvu ya kuitikia mwaliko huu wa upendo: “Mwanangu, nipe moyo wako; macho yako yapendezwe na njia zangu.”—Mithali 23:26.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Desemba 1, 1999, ukurasa wa 30-31.

^ fu. 11 Makasisi wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki huruhusiwa kuoa.

^ fu. 12 Simulizi la maisha ya Emmanuel Lionoudakis limo katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1999, ukurasa wa 25-29.

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini hakipigwi chapa tena.

^ fu. 15 Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1993, ukurasa 27-31, linazungumzia ushindi wa kesi ya mahakamani iliyomhusu Minos Kokkinakis.

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

Makrónisos ni Kisiwa cha Kutisha

Kwa muda wa miaka kumi, kuanzia 1947 hadi 1957, wafungwa 100,000 walipelekwa kwenye kisiwa kame cha Makrónisos. Miongoni mwao walikuwa Mashahidi waaminifu wengi sana waliopelekwa huko kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote katika vita. Mara nyingi wale waliochochea wahamishwe walikuwa makasisi wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki ambao waliwashtaki Mashahidi kwa uwongo kuwa Wakomunisti.

Kuhusu mbinu za eti “kuwarekebisha wakosaji” zilizotumiwa huko Makrónisos, kitabu cha marejezo cha Kigiriki kinachoitwa Papyros Larousse Britannica kinasema hivi: “Mbinu katili za mateso, . . . hali ya makao, ambayo haipaswi kuonekana katika nchi iliyostaarabika, na jinsi walinzi walivyowavunjia wafungwa heshima . . . hayo yote ni aibu kubwa kwa nchi ya Ugiriki.”

Baadhi ya Mashahidi waliambiwa kwamba hawangeachiliwa kamwe kama hawangekana imani yao. Hata hivyo, Mashahidi walikuwa waaminifu. Isitoshe, baadhi ya wafungwa wa kisiasa walikuja kukubali kweli ya Biblia kwa sababu walifungwa pamoja na Mashahidi.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Minos Kokkinakis (wa tatu kutoka kulia) na mimi (wa nne kutoka kushoto), tukiwa kwenye kisiwa cha Makrónisos

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikihubiri pamoja na Shahidi mwenzangu huko Sitía, Krete, nilikotumikia nikiwa kijana