Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wanasikia” Ujumbe wa Ufalme Nchini Brazili

“Wanasikia” Ujumbe wa Ufalme Nchini Brazili

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

“Wanasikia” Ujumbe wa Ufalme Nchini Brazili

ILI kuwatangazia Viziwi habari njema za Ufalme, Mashahidi wa Yehova wengi nchini Brazili wamekubali ugumu wa kujifunza Lugha ya Ishara ya Kibrazili. Jitihada zao zina matokeo mazuri, kama mambo yaliyoonwa yafuatayo yanavyoonyesha.

Eva, * mwanamke kiziwi huko São Paulo, alianza kujifunza lugha ya ishara wakati yeye na watoto wake walipoanza kuishi na mwanamume kiziwi. Akiwa kwenye jengo kubwa lenye maduka mengi, Eva na huyo mpenzi wake wa kiume walikutana na Mashahidi viziwi nao wakaalikwa kuhudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme. Walikubali, wakifikiri kwamba walikuwa wamealikwa kwenye tafrija tu.

Kwa sababu Eva hakujua lugha ya ishara vizuri, hakuelewa sana yaliyosemwa mkutanoni. Baadaye, Mashahidi kadhaa walimwalika nyumbani kwao ili wale chakula chepesi. Mashahidi hao walitumia picha kwenye broshua Furahia Milele Maisha Duniani!, kumweleza kuhusu ahadi ya Mungu ya kuwa na paradiso duniani wakati ujao. Eva alipendezwa na mambo aliyojifunza na akaanza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida.

Punde baada ya hapo, Eva alimwacha mpenzi wake wa kiume ili aishi kulingana na viwango vya Biblia. Ajapopatwa na upinzani mkali kutoka kwa familia yake, Eva aliendelea kufanya maendeleo ya kiroho na akabatizwa mwaka wa 1995. Miezi sita baadaye, Eva alijiandikisha kuwa painia, au mtangazaji wa Ufalme wa wakati wote. Tangu wakati huo amesaidia watu wanne viziwi kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa.

Carlos alizaliwa akiwa kiziwi. Tangu utotoni alianza kutumia dawa za kulevya, ukosefu wa adili, na wizi. Alipotishwa na genge fulani lililopingana nao, Carlos alitorokea São Paulo na kukaa na João kwa muda fulani. João, kama vile Carlos, alikuwa kiziwi na aliishi maisha yasiyo na adili.

Baada ya miaka kadhaa, Carlos alijifunza ujumbe wa Ufalme, kisha akabadili maisha yake na kuhalalisha ndoa yake. Baada ya kutimiza matakwa ya Kimaandiko, Carlos alionyesha wakfu wake kwa Yehova kwa kubatizwa. Wakati huohuo, bila Carlos kujua, João pia alipata habari njema, naye pia akafanya mabadiliko makubwa maishani mwake. Alipojifunza kwamba Yehova hapendi matumizi ya sanamu, João alitupa sanamu zake zote za “watakatifu” alizokuwa amekusanya. Baada ya kuacha njia yake ya zamani ya maisha, João pia alibatizwa.

Carlos na João walifurahi kama nini walipokutana kwenye Jumba la Ufalme na kuona mabadiliko ambayo kila mmoja wao alikuwa amefanya! Sasa wote ni vichwa vya familia wanaochukua madaraka yao kwa uzito na ni watangazaji wa Ufalme wenye bidii.

Nchini Brazili, kuna makutaniko ya lugha ya ishara 30 kwa sasa na kuna vikundi 154, na wahubiri 2,500, ambao kati yao 1,500 ni viziwi. Kwenye Makusanyiko ya Wilaya kwa ajili ya viziwi ya “Walimu wa Neno la Mungu” ya 2001 huko Brazili, watu zaidi ya 3,000 walihudhuria na 36 wakabatizwa. Tunatumaini kwamba kwa baraka za Yehova, viziwi wengine wengi watakubali ujumbe wa Ufalme.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Majina yamebadilishwa.