Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Madhabahu Itumiwe Katika Ibada?

Je, Madhabahu Itumiwe Katika Ibada?

Je, Madhabahu Itumiwe Katika Ibada?

JE, MADHABAHU hutumiwa sana katika dini yako? Waabudu wengi katika makanisa yanayosemekana kuwa ya Kikristo huona madhabahu kuwa muhimu sana katika ibada yao. Biblia inasema nini kuhusu matumizi ya madhabahu katika ibada?

Madhabahu ya kwanza inayotajwa katika Biblia ni ile iliyojengwa na Nuhu kwa ajili ya kutoa dhabihu za wanyama, alipotoka katika safina baada ya Gharika. *Mwanzo 8:20.

Baada ya Mungu kuvuruga lugha huko Babeli, wanadamu walitawanyika kotekote duniani. (Mwanzo 11:1-9) Kwa kuwa wanadamu wana mwelekeo wa kiasili wa kuabudu, walijitahidi kumkaribia Mungu ambaye hawakumjua. Walimtafuta kwa “kupapasa-papasa” kana kwamba walikuwa vipofu. (Matendo 17:27; Waroma 2:14, 15) Tangu siku za Nuhu, watu wa makabila na mataifa mengi wameijengea miungu yao madhabahu. Watu fulani wa dini na tamaduni mbalimbali wametumia madhabahu katika ibada isiyo ya kweli. Madhabahu zilitumiwa mara nyingi na watu wasiomjua Mungu wa kweli katika ibada iliyochukiza ya kutolewa kwa dhabihu za wanadamu na hata watoto. Baadhi ya wafalme wa Israeli waliomwacha Yehova walijengea miungu ya kipagani, kama vile Baali, madhabahu. (1 Wafalme 16:29-32) Lakini vipi matumizi ya madhabahu katika ibada ya kweli?

Matumizi ya Madhabahu Katika Ibada ya Kweli Nchini Israeli

Baada ya Nuhu, wanadamu wengine waaminifu walijenga madhabahu ili kumwabudu Yehova, Mungu wa kweli. Abrahamu alijenga madhabahu huko Shekemu, karibu na Betheli, Hebroni, na kwenye Mlima Moria, ambako alimtoa dhabihu kondoo-dume aliyeandaliwa na Mungu badala ya Isaka. Baadaye Isaka, Yakobo, na Musa walisukumwa na mioyo yao kujenga madhabahu ili wamwabudu Mungu.—Mwanzo 12:6-8; 13:3, 18; 22:9-13; 26:23-25; 33:18-20; 35:1, 3, 7; Kutoka 17:15, 16; 24:4-8.

Mungu alipowapa Waisraeli Sheria yake, aliwaamuru wajenge “maskani ya hema la kukutania,” lililoweza kuhamishwa, ambalo lingetumiwa sana katika ibada yao. (Kutoka 39:32, 40) Hema hilo la kukutania lilikuwa na madhabahu mbili. Madhabahu ya matoleo ya kuteketezwa iliyotengenezwa kwa mbao ya mshita na kufunikwa kwa shaba, iliwekwa mbele ya mlango wa maskani ya hema la kukutania, nayo ilitumiwa kuteketeza dhabihu za wanyama. (Kutoka 27:1-8; 39:39; 40:6, 29) Madhabahu ya kufukizia uvumba ilitengenezwa pia kwa mbao ya mshita lakini hiyo ilifunikwa kwa dhahabu, nayo ilikuwa ndani ya maskani ya hema la kukutania, mbele ya pazia la mahali patakatifu sana. (Kutoka 30:1-6; 39:38; 40:5, 26, 27) Uvumba wa pekee ulifukizwa juu yake mara mbili kwa siku, asubuhi na jioni. (Kutoka 30:7-9) Hekalu lililojengwa na Mfalme Sulemani lilikuwa na madhabahu mbili pia kama vile maskani ya hema la kukutania.

“Hema la Kweli” na Madhabahu ya Mfano

Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli ilikuwa na mambo mengi mbali na sheria zilizowaongoza katika maisha yao na katika kutoa dhabihu na sala. Paulo alisema kwamba mambo mengi yaliyoamriwa katika Sheria yalikuwa “kiwakilishi cha mfano,” “kielezi” au “kivuli cha vitu vya kimbingu.” (Waebrania 8:3-5; 9:9; 10:1; Wakolosai 2:17) Kwa hiyo, mbali na kuwaongoza Waisraeli hadi Kristo alipokuja, Sheria ilionyesha kimbele makusudi ya Mungu ambayo yangetimizwa kupitia Yesu Kristo. (Wagalatia 3:24) Jambo hilo linamaanisha kwamba sehemu fulani za Sheria zilikuwa za kiunabii. Kwa mfano, kondoo wa Pasaka, ambaye damu yake ilikuwa ishara ya wokovu kwa Waisraeli, alikuwa mfano wa Yesu Kristo. Yeye ndiye “Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu,” na ambaye damu yake ilimwagwa ili kutuondolea dhambi.—Yohana 1:29; Waefeso 1:7.

Mambo mengi yaliyohusu maskani ya hema la kukutania na hekalu yalikuwa mfano wa mambo halisi ya kiroho. (Waebrania 8:5; 9:23) Hivyo, Paulo anaandika kuhusu “hema la kweli, ambalo Yehova alisimamisha, wala si mwanadamu.” Anaongeza: ‘Kristo alikuja akiwa kuhani wa cheo cha juu wa mambo mema ambayo yamekuwa, kupitia hema kubwa zaidi na kamilifu zaidi ambalo halikufanywa kwa mikono, yaani, si la uumbaji huu.’ (Waebrania 8:2; 9:11) “Hema kubwa zaidi na kamilifu zaidi” ni hekalu kubwa la kiroho la Yehova, yaani, mpango wa ibada. Maandiko yanaonyesha kwamba hekalu kubwa la kiroho ni mpango ambao unawawezesha wanadamu kumkaribia Yehova kwa msingi wa dhabihu ya upatanisho ya Yesu Kristo.—Waebrania 9:2-10, 23-28.

Bila shaka imani yetu kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Mungu inaimarishwa tunapotambua kwamba mipango na kanuni mbalimbali za Sheria ni mifano ya mambo makuu na muhimu zaidi ya kiroho. Pia tunathamini zaidi hekima ya Mungu ambayo inaonekana wazi katika Maandiko.—Waroma 11:33; 2 Timotheo 3:16.

Madhabahu ya matoleo ya kuteketeza pia ilikuwa mfano wa mambo ambayo yangekuja. Yaelekea hiyo inawakilisha “mapenzi” ya Mungu, au utayari wake wa kukubali dhabihu kamilifu ya kibinadamu ambayo Yesu alitoa.—Waebrania 10:1-10.

Baadaye katika kitabu cha Waebrania, Paulo anasema jambo la kupendeza: “Sisi tuna madhabahu ambayo kutoka hiyo wale wafanyao utumishi mtakatifu kwenye hema hawana mamlaka ya kula.” (Waebrania 13:10) Alikuwa akizungumzia madhabahu gani?

Wafasiri wengi Wakatoliki husema kwamba madhabahu inayotajwa katika Waebrania 13:10 inamaanisha madhabahu inayotumiwa wakati wa Karamu ya Bwana. Inasemekana kwamba katika sherehe hiyo dhabihu ya Kristo hutolewa upya kila kipindi cha Misa. Lakini mambo mengine katika mazungumzo ya Paulo yanaonyesha kwamba madhabahu ambayo Paulo alizungumzia ilikuwa ya mfano. Wasomi kadhaa wanaamini kwamba neno “madhabahu” linalotajwa katika andiko hilo linatumiwa katika njia ya mfano. Mjesuti Giuseppe Bonsirven, anasema kwamba jambo hilo “linapatana vizuri sana na mifano mingine yote ya barua hiyo [kwa Waebrania].” Anasema hivi: “Hapo awali Wakristo walitumia neno ‘madhabahu’ katika maana ya kiroho na lilianza tu kutumiwa kuhusiana na Karamu ya Bwana, na hasa kuhusu madhabahu inayotumiwa wakati wa karamu hiyo baada kifo cha Irenaeus, na hasa baada ya kifo cha Tertullian na Mtakatifu Cyprian.”

Gazeti moja la Kikatoliki, linasema kwamba matumizi ya madhabahu yalienea katika “enzi ya Constantine” wakati “makanisa yalipoanza kujengwa.” Gazeti la Rivista di Archeologia Cristiana (Uchunguzi wa Akiolojia ya Wakristo) lilisema: “Ni kweli kwamba katika karne mbili za kwanza, hakukuwa na mahali maalumu pa ibada, bali Wakristo walikutanika katika nyumba za watu . . . , na baada ya ibada zilitumiwa tena kama nyumba za kawaida.”

Matumizi ya Madhabahu Katika Dini Zinazoitwa za Kikristo

Gazeti la Kanisa Katoliki La Civiltà Cattolica linasema kwamba “madhabahu si jambo la maana katika jengo la kanisa tu bali pia katika Kanisa lililo hai.” Hata hivyo, Yesu Kristo hakuanzisha sherehe yoyote ile ya ibada iliyohusisha madhabahu; wala hakuwaagiza wanafunzi wake watumie madhabahu katika ibada. Yesu alipotaja madhabahu katika Mathayo 5:23, 24 na katika maandiko mengineyo, alizungumzia desturi za kawaida katika dini ya Wayahudi, lakini hakusema kamwe kwamba wafuasi wake walipaswa kumwabudu Mungu kwa kutumia madhabahu.

Mwanahistoria Mmarekani, George Foot Moore (1851-1931), aliandika hivi: “Mambo makuu katika ibada ya Wakristo hayajabadilika, lakini ile ibada sahili inayofafanuliwa na Justin katikati ya karne ya pili hatimaye ikaongezwa desturi zenye madoido mengi.” Desturi na sherehe za ibada katika Kanisa Katoliki ni nyingi na tata sana hivi kwamba zinafundishwa katika vyuo vya dini vya kanisa hilo. Moore aliongeza: “Mwelekeo wa kufanya desturi za ibada za Wakristo ziwe za fahari zaidi ulichochewa wakati makasisi Wakristo walipokuja kuonwa kuwa waandamani wa makuhani waliowekwa na Mungu katika Agano la Kale. Mavazi ya fahari ya kuhani mkuu, mavazi rasmi ya wale makuhani wengine, maandamano ya sherehe, Walawi walioimba zaburi, na moshi wa uvumba uliotoka katika chetezo zilizoning’inia, yote yalikuwa yameagizwa na Mungu. Kwa hiyo, wakuu wa kanisa waliyaona hayo yote kuwa mfano wa kuiga, na udhuru wa kuwa na sherehe za fahari kama dini za kipagani au hata kuzipita.”

Huenda ukashangaa kujua kwamba mapokeo mengi, sherehe, mavazi, na vitu vinginevyo vya ibada katika makanisa mbalimbali hayatokani na mafundisho ya Kristo katika Injili, bali yanatokana na mapokeo na sherehe za Wayahudi na wapagani. Kitabu Enciclopedia Cattolica kinasema hivi kuhusu Kanisa Katoliki: “Kwa habari ya matumizi ya madhabahu, kanisa hilo limeiga dini ya Wayahudi na kwa kiwango fulani dini za kipagani.” Minucius Felix, mtetea-imani aliyeishi katika karne ya tatu W.K., aliandika kwamba Wakristo hawakuwa na ‘wala hekalu wala madhabahu.’ Kamusi Religioni e Miti (Dini na Hekaya) inasema hivi vilevile: “Wakristo wa mapema walikataa kutumia madhabahu ili wawe tofauti na Wayahudi na waabudu wapagani.”

Kwa kuwa Ukristo hasa ulihusisha kanuni zinazopaswa kukubaliwa na kufuatwa maishani na watu katika kila nchi, hakukuwa tena na uhitaji wa jiji takatifu duniani, au hekalu halisi lenye madhabahu wala makuhani wa kibinadamu wenye cheo waliovalia mavazi ya kipekee. Yesu alisema hivi: ‘Saa inakuja wakati ambapo wala si katika mlima huu wala katika Yerusalemu nyinyi watu mtamwabudu Baba. Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli.’ (Yohana 4:21, 23) Makanisa mengi hupuuza maagizo ya Yesu kuhusu jinsi ya kumwabudu Mungu wa kweli kwa kusisitiza kufuata sherehe zao tata na kwa kutumia madhabahu katika ibada.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Huenda Kaini na Habili walimtolea Yehova dhabihu zao kwenye madhabahu.—Mwanzo 4:3, 4.