Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tuadhimishe Mlo wa Jioni wa Bwana?

Kwa Nini Tuadhimishe Mlo wa Jioni wa Bwana?

Kwa Nini Tuadhimishe Mlo wa Jioni wa Bwana?

“Nilipokea kutoka kwa Bwana kile nilichowapa nyinyi pia.” —1 WAKORINTHO 11:23.

1, 2. Yesu alifanya nini usiku wa Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 33 W.K.?

MWANA mzaliwa-pekee wa Yehova alikuwepo pamoja na wale wanaume 11 ‘waliokuwa wameshikamana naye katika majaribu yake.’ (Luka 22:28) Ilikuwa Alhamisi jioni, Machi 31, mwaka wa 33 W.K., na yaelekea mwezi mpevu ulikuwa uking’aa kwenye anga la Yerusalemu. Yesu Kristo na mitume wake walikuwa wamemaliza tu kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa. Yuda Iskariote aliyekuwa msaliti alikuwa amefukuzwa, lakini wale wengine walibaki. Kwa nini? Kwa sababu Yesu alitaka kufanya jambo fulani muhimu sana. Jambo gani?

2 Hebu mwandishi wa Injili Mathayo atueleze kilichotukia kwa sababu alikuwepo. Aliandika hivi: “Yesu alichukua mkate na, baada ya kusema baraka, akaumega na, akiwapa wanafunzi, akasema: ‘Chukueni, kuleni. Huu wamaanisha mwili wangu.’ Pia, alichukua kikombe na, akiisha kushukuru, akawapa hicho, akisema: ‘Nyweni kutoka hicho, nyinyi nyote; kwa maana hii yamaanisha “damu yangu ya agano,” inayopaswa kumwagwa kwa niaba ya wengi kwa msamaha wa dhambi.’” (Mathayo 26:26-28) Je, tukio hilo lingekomea hapo? Lilikuwa na umuhimu gani? Je, lina maana yoyote kwetu leo?

“Fulizeni Kufanya Hili”

3. Kwa nini mambo aliyofanya Yesu usiku wa Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., yalikuwa muhimu sana?

3 Yesu Kristo alifanya jambo muhimu sana maishani mwake usiku wa Nisani 14, mwaka wa 33 W.K. Mtume Paulo alieleza tukio hilo alipowaandikia Wakristo watiwa-mafuta huko Korintho, ambako bado watu walikuwa wakisherehekea mwadhimisho huo zaidi ya miaka 20 baadaye. Ingawa Paulo hakuwa pamoja na Yesu na wale mitume 11 mwaka wa 33 W.K., ni wazi kwamba baadhi yao walimwambia mambo yaliyotukia usiku huo. Zaidi ya hayo, hapana shaka kwamba Mungu alimfunulia Paulo mambo yaliyotukia wakati huo. Paulo alisema hivi: “Nilipokea kutoka kwa Bwana kile nilichowapa nyinyi pia, kwamba Bwana Yesu katika usiku aliokuwa akielekea kukabidhiwa alitwaa mkate na, baada ya kutoa shukrani, akaumega na kusema: ‘Huu wamaanisha mwili wangu ulio kwa ajili yenu. Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.’ Akafanya hivyohivyo kwa habari ya kikombe pia, baada ya yeye kula mlo wa jioni, akisema: ‘Kikombe hiki chamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu. Fulizeni kufanya hili, mara nyingi kadiri mkinywavyo, katika ukumbuko wangu.’”—1 Wakorintho 11:23-25.

4. Kwa nini Wakristo wanapaswa kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana?

4 Mwandishi wa Injili Luka anathibitisha kwamba Yesu aliamuru hivi: “Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.” (Luka 22:19) Maneno hayo yametafsiriwa hivi pia: “Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu” (Union Version) na “Fanyeni hivi kwa kunikumbuka.” (Biblia Habari Njema) Mara nyingi mwadhimisho huo huitwa Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Paulo anauita pia Mlo wa Jioni wa Bwana, na jina hilo linafaa kwa sababu ulianzishwa wakati wa jioni. (1 Wakorintho 11:20) Wakristo wanaamriwa waadhimishe Mlo wa Jioni wa Bwana. Lakini kwa nini mwadhimisho huo ulianzishwa?

Kwa Nini Ukumbusho Ulianzishwa?

5, 6. (a) Taja sababu moja iliyomfanya Yesu aanzishe Ukumbusho. (b) Taja sababu nyingine iliyofanya Mlo wa Jioni wa Bwana uanzishwe.

5 Sababu moja iliyofanya Ukumbusho uanzishwe ilihusiana na kusudi la kifo cha Yesu. Alikufa akiwa mtetezi wa enzi kuu ya Baba yake wa mbinguni. Hivyo, Kristo alithibitisha kwamba Shetani Ibilisi, aliyedai kwa uwongo kwamba wanadamu wanamtumikia Mungu kwa sababu za kichoyo, ni mwongo. (Ayubu 2:1-5) Yesu alikufa akiwa mwaminifu na hivyo akathibitisha dai hilo kuwa la uwongo na kuufurahisha moyo wa Yehova.—Mithali 27:11.

6 Mlo wa Jioni wa Bwana ulianzishwa pia ili kutukumbusha kwamba Yesu ‘alitoa nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi’ alipokufa akiwa mwanadamu mkamilifu asiye na dhambi. (Mathayo 20:28) Mwanadamu wa kwanza alipomwasi Mungu, alipoteza uhai mkamilifu wa kibinadamu na mataraja yake yote. Hata hivyo, Yesu alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Yohana 3:16) Kwa kweli, “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uhai udumuo milele kwa njia ya Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana hutukumbusha upendo mwingi sana ulioonyeshwa na Yehova na Mwanaye kuhusiana na kifo cha Yesu cha kidhabihu. Tunapaswa kuwashukuru sana kwa sababu ya upendo wao.

Uadhimishwe Lini?

7. Wakristo watiwa-mafuta hula mifano ya Ukumbusho “mara nyingi” kwa njia gani?

7 Paulo alisema hivi kuhusu Mlo wa Jioni wa Bwana: “Mara nyingi kwa kadiri mlavyo mkate huu na kunywa kikombe hiki, mwafuliza kutangaza kifo cha Bwana, mpaka awasilipo.” (1 Wakorintho 11:26) Wakristo wote watiwa-mafuta huendelea kula mifano ya Ukumbusho hadi kifo chao. Na hivyo wanaendelea kutangaza mbele za Yehova Mungu na ulimwengu kwamba wana imani katika dhabihu ya Yesu ya fidia iliyoandaliwa na Mungu.

8. Jamii ya watiwa-mafuta ingeendelea kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana mpaka lini?

8 Jamii ya Wakristo watiwa-mafuta ingeendelea kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo mpaka lini? Paulo alisema, “mpaka awasilipo.” Hilo lamaanisha kwamba mwadhimisho huo ungeendelea mpaka Yesu aje na kuwapokea wafuasi wake watiwa-mafuta mbinguni kupitia ufufuo wakati wa “kuwapo” kwake. (1 Wathesalonike 4:14-17) Hilo linapatana na maneno ambayo Yesu aliwaambia mitume wake 11 waliokuwa waaminifu: “Nikishika njia yangu kwenda na kuwatayarishia nyinyi mahali, mimi ninakuja tena na hakika nitawapokea nyinyi nyumbani kwangu mwenyewe, ili mahali nilipo nyinyi pia mpate kuwa.”—Yohana 14:3.

9. Maneno ya Yesu katika Marko 14:25 yanamaanisha nini?

9 Yesu alipoanzisha Ukumbusho, aliwaambia hivi mitume wake waaminifu kuhusu kikombe cha divai: “Sitakunywa tena kamwe kutokana na zao la mzabibu hadi siku ile nitakapolinywa likiwa jipya katika ufalme wa Mungu.” (Marko 14:25) Kwa kuwa Yesu hangekunywa divai halisi huko mbinguni, ni wazi kwamba alikuwa akifikiria pindi zenye shangwe ambazo nyakati nyingine huwakilishwa na divai. (Zaburi 104:15; Mhubiri 10:19) Yesu na wafuasi wake walitarajia kwa hamu sana wakati ambapo wangefurahia kuwa pamoja katika Ufalme.—Waroma 8:23; 2 Wakorintho 5:2.

10. Ukumbusho unapaswa kuadhimishwa mara ngapi?

10 Je, kifo cha Yesu chapaswa kuadhimishwa kila mwezi, kila juma, au hata kila siku? La. Yesu alianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana kisha akauawa wakati wa sikukuu ya Kupitwa, siku ambayo Wayahudi waliadhimisha “ukumbusho” wa kukombolewa kwa Waisraeli kutoka utumwani Misri mwaka wa 1513 K.W.K. (Kutoka 12:14) Sikukuu ya Kupitwa ilifanywa mara moja kila mwaka, siku ya 14 ya mwezi wa Nisani kwenye kalenda ya Wayahudi. (Kutoka 12:1-6; Mambo ya Walawi 23:5) Hilo lamaanisha kwamba kifo cha Yesu chapasa kuadhimishwa mara moja tu kila mwaka kama Sikukuu ya Kupitwa—si kila mwezi, kila juma, au kila siku.

11, 12. Historia inaonyesha nini kuhusu miadhimisho ya kale ya Ukumbusho?

11 Kwa hiyo basi, Ukumbusho unapaswa kuadhimishwa Nisani 14 kila mwaka. Ensaiklopedia moja ya kidini inasema: ‘Wakristo wa Asia Ndogo walijulikana kuwa waadhimishaji wa tarehe 14 kwa sababu ya desturi yao ya kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana mnamo Nisani 14 bila kubadili-badili tarehe . . . Tarehe hiyo inaweza kuangukia siku ya Ijumaa au siku nyingine yoyote.’—The New Schaff-Herzog Encyclopedia of Religious Knowledge, Buku la 4, ukurasa wa 44.

12 Akitoa maelezo kuhusu zoea hilo la karne ya pili W.K., mwanahistoria J. L. von Mosheim anasema kwamba waadhimishaji wa tarehe 14 walifanya Ukumbusho Nisani 14 kwa sababu “walijihisi wakiwa na wajibu wa kufuata mfano wa Kristo kama walivyofuata sheria.” Mwanahistoria mwingine anasema: “Makanisa ya waadhimishaji wa tarehe 14 huko Asia yalifuata kielelezo cha kanisa la Yerusalemu. Katika karne ya pili makanisa hayo yaliadhimisha ukombozi uliotokana na kifo cha Kristo sambamba na Sikukuu yao ya Pasaka iliyofanywa Nisani 14.”—Studia Patristica, Buku la 5, 1962, ukurasa wa 8.

Mkate Unawakilisha Nini?

13. Yesu alitumia mkate wa aina gani alipoanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana?

13 Yesu alipoanzisha Ukumbusho, ‘aliuchukua mkate, akasema baraka, akaumega na kuwapa mitume.’ (Marko 14:22) Walitumia mkate uleule uliokuwa umetumiwa kwenye Sikukuu ya Kupitwa. (Kutoka 13:6-10) Mkate huo ulikuwa mwembamba na mkavu kwa sababu uliokwa bila chachu na hivyo ulihitaji kumegwa ili ugawanywe. Mikate ambayo Yesu alitokeza kimuujiza na kuwalisha maelfu ya watu ilikuwa pia mikavu, kwa sababu aliimega ili iweze kugawanywa. (Mathayo 14:19; 15:36) Hivyo basi tendo la kuumega mkate wa Ukumbusho halina maana yoyote ya kiroho.

14. (a) Kwa nini mkate wa Ukumbusho haupaswi kuwa na chachu? (b) Ni mkate wa aina gani unaoweza kutumiwa au kuokwa kwa ajili ya Mlo wa Jioni wa Bwana?

14 Yesu alisema hivi kuhusu mkate aliotumia alipoanzisha Ukumbusho: “Huu wamaanisha mwili wangu ulio kwa ajili yenu.” (1 Wakorintho 11:24; Marko 14:22) Mkate huo usiotiwa chachu ulifaa kabisa. Kwa nini? Kwa sababu chachu inaweza kufananisha ubaya, uovu, au dhambi. (1 Wakorintho 5:6-8) Mkate huo uliwakilisha mwili wa Yesu wa kibinadamu uliokuwa mkamilifu na usio na dhambi, ambao kwa kufaa ulikuwa umetolewa kuwa dhabihu ya fidia. (Waebrania 7:26; 10:5-10) Mashahidi wa Yehova hukumbuka jambo hilo na hivyo hutumia mkate usiotiwa chachu kwenye miadhimisho ya Ukumbusho kama Yesu alivyofanya. Nyakati nyingine, wao hutumia mkate maalumu unaotumiwa na Wayahudi wakati wa Pasaka kwa sababu hauna chachu wala vitu vingine kama vile vitunguu au mayai. La sivyo, mkate usiotiwa chachu unaweza kutayarishwa kwa kuchanganya kiasi kidogo cha maji na unga wa nafaka zilizosagwa pamoja na maganda yake (ngano ikiwezekana). Unga wapaswa kusukumwa uwe mwembamba na kuokwa kwenye kikaango chenye mafuta kidogo sana hadi mkate ukauke kabisa.

Divai Inawakilisha Nini?

15. Kikombe kilichotumiwa na Yesu alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake kilikuwa na nini?

15 Baada ya kupitisha mkate usiotiwa chachu, Yesu alichukua kikombe, “akashukuru akawapa [mitume], nao wote wakanywa kutoka hicho.” Kisha Yesu akaeleza: “Hii yamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ inayopaswa kumwagwa kwa ajili ya wengi.” (Marko 14:23, 24) Kikombe hicho kilikuwa na nini? Kilikuwa na divai iliyochacha, wala si maji ya zabibu yasiyochacha. Maandiko yanapotaja divai, hayamaanishi maji ya zabibu yasiyochacha. Kwa mfano, Yesu alisema kwamba divai iliyochacha ndiyo ingepasua ‘viriba vikuukuu vya divai’ wala si maji ya zabibu. Na maadui wa Kristo walidai kwamba alikuwa na ‘tabia ya kunywa divai.’ Dai lao halingekuwa na maana yoyote endapo divai ilikuwa maji ya zabibu tu. (Mathayo 9:17; 11:19) Watu walikunywa divai kwenye Sikukuu ya Kupitwa, na Kristo aliitumia alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake.

16, 17. Ni divai ya aina gani inayofaa kutumiwa kwenye miadhimisho ya Ukumbusho, na kwa nini?

16 Ni divai nyekundu tu inayoweza kuwakilisha ifaavyo damu ya Yesu iliyomwagwa. Yeye mwenyewe alisema hivi: “Hii yamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ inayopaswa kumwagwa kwa ajili ya wengi.” Naye mtume Petro aliandika: “Mwajua [Wakristo watiwa-mafuta] kwamba haikuwa kwa vitu vyenye kuharibika, kwa fedha au dhahabu, kwamba mlikombolewa kutoka kwenye namna ya mwenendo usio na matunda uliopokewa kupitia pokeo kutoka kwa baba zenu wa zamani. Bali ilikuwa kwa damu yenye bei, kama ile ya mwana-kondoo asiye na waa na asiye na doa, naam, ya Kristo.”—1 Petro 1:18, 19.

17 Hapana shaka kwamba Yesu alitumia divai nyekundu ya zabibu alipoanzisha Ukumbusho. Hata hivyo, divai fulani nyekundu zilizopo leo hazifai kwa sababu zimechanganywa na pombe kali au brandi au zimeongezwa vikolezo na mitishamba. Damu ya Yesu ilitosha kabisa, haikuhitaji kuongezwa vitu vingine. Kwa hiyo, divai zenye vikolezo kama vile port, sherry, na vermouth hazingefaa. Kikombe cha Ukumbusho chapaswa kuwa na divai nyekundu isiyotiwa vikolezo wala sukari. Divai nyekundu ya zabibu isiyo na sukari, inayotengenezewa nyumbani inaweza kutumiwa. Divai nyingine kama vile red burgundy na claret zinaweza pia kutumiwa.

18. Kwa nini Yesu hakubadili kimuujiza mkate na divai ya Ukumbusho?

18 Alipokuwa akianzisha mlo huo, Yesu hakubadili kimuujiza mifano hiyo iwe nyama na damu yake halisi. Kula nyama ya binadamu na kunywa damu yake kungekuwa kinyume cha sheria ya Mungu. (Mwanzo 9:3, 4; Mambo ya Walawi 17:10) Bado Yesu alikuwa na mwili wake wenye nyama na damu yake yote jioni hiyo. Mwili wake ulitolewa ukiwa dhabihu kamilifu, na damu yake ilimwagwa alasiri iliyofuata ya siku hiyohiyo ya Kiyahudi ya Nisani 14. Kwa hiyo, mkate na divai ya Ukumbusho ni mifano  tu inayowakilisha nyama na damu ya Kristo. *

Ukumbusho Ni Mlo wa Ushirika

19. Kwa nini sahani na vikombe kadhaa vinaweza kutumiwa kwenye mwadhimisho wa Mlo wa Jioni wa Bwana?

19 Yesu alipoanzisha Ukumbusho, aliwaalika mitume wake waaminifu 11 wanywe kwa kikombe kilekile. Injili ya Mathayo inasema: “[Yesu] alichukua kikombe na, akiisha kushukuru, akawapa hicho, akisema: ‘Nyweni kutoka hicho, nyinyi nyote.’” (Mathayo 26:27) Wakati huo, ilikuwa rahisi kutumia “kikombe” kimoja tu badala ya vikombe kadhaa kwa sababu kulikuwa na washiriki 11 tu walioketi kwenye meza moja, na hivyo wangeweza kupokezana kikombe hicho. Mwaka huu, mamilioni ya watu watakusanyika kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana katika makutaniko zaidi ya 94,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Huenda kikombe kimoja kisiweze kutumiwa kwa ajili ya umati huo utakaokusanyika kuadhimisha mlo huo usiku huohuo. Ingawa makutaniko makubwa hutumia vikombe kadhaa ambavyo vinaweza kupitishwa miongoni mwa wasikilizaji kwa muda mfupi, bado vikombe hivyo vyenye divai huwakilisha damu ya Yesu ya dhabihu. Vivyo hivyo, sahani kadhaa zinaweza kutumiwa kupitisha mkate. Hakuna Andiko linalosema kwamba kikombe au gilasi inapaswa kuwa na umbo fulani hususa. Hata hivyo, tunapaswa kutumia kikombe na sahani itakayoonyesha kwamba tunaheshimu mwadhimisho huo. Ni hekima kutojaza kikombe pomoni ili divai isimwagike inapopitishwa.

20, 21. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Ukumbusho ni mlo wa ushirika?

20 Ukumbusho ni mlo wa ushirika hata ingawa sahani kadhaa za mkate na vikombe kadhaa vya divai vinaweza kutumiwa. Katika Israeli la kale, mtu angeweza kuandaa mlo wa ushirika kwa kumpeleka mnyama katika patakatifu pa Mungu, ambapo alichinjwa. Sehemu fulani ya mnyama huyo iliteketezwa kwenye madhabahu, sehemu nyingine ilichukuliwa na kuhani aliyekuwa akimtumikia na nyingine ilichukuliwa na wana wa Aroni waliokuwa makuhani. Mtoaji wa dhabihu hiyo na watu wa nyumbani mwake walishiriki mlo huo. (Mambo ya Walawi 3:1-16; 7:28-36) Ukumbusho pia ni mlo wa ushirika kwa sababu unahusisha watu kadhaa.

21 Yehova anahusika katika mlo huu wa ushirika kwa sababu yeye ndiye Mwanzilishi wa mpango huo. Yesu ndiye dhabihu, na Wakristo watiwa-mafuta hula mifano hiyo wakiwa washirika wa Kristo. Kula kwenye meza ya Yehova huonyesha kwamba washirika wana uhusiano wa amani pamoja naye. Kwa sababu hiyo, Paulo aliandika hivi: “Kikombe cha baraka ambacho sisi twabariki, je, hicho si ushirika katika damu ya Kristo? Ule mkate ambao sisi twamega, je, huo si ushirika katika mwili wa Kristo? Kwa sababu kuna mkate mmoja, sisi, tujapokuwa wengi, tuko mwili mmoja, kwa maana sisi sote tunashiriki mkate mmoja huo.”—1 Wakorintho 10:16, 17.

22. Tutajibu maswali gani kuhusu Ukumbusho?

22 Mlo wa Jioni wa Bwana ndio mwadhimisho pekee wa kidini unaofanywa na Mashahidi wa Yehova kila mwaka. Wanafanya hivyo kwa sababu Yesu aliwaamuru hivi wafuasi wake: “Fulizeni kufanya hili kwa ukumbuko wangu.” Wakati wa Ukumbusho, tunaadhimisha kifo cha Yesu ambacho kilikweza enzi kuu ya Yehova. Kama tulivyoona, mkate unaotumiwa kwenye mlo huo wa ushirika unawakilisha mwili wa kibinadamu wa Kristo uliotolewa dhabihu, na divai inawakilisha damu yake iliyomwagwa. Hata hivyo, ni watu wachache sana wanaokula mkate na wanaokunywa divai hiyo ya mfano. Kwa nini? Je, Ukumbusho una maana yoyote kwa mamilioni ya watu wasiokula mifano hiyo? Mlo wa Jioni wa Bwana unapaswa kuwa na maana gani kwako?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Ona Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 271, kinachochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Ungejibuje?

• Kwa nini Yesu alianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana?

• Ukumbusho unapaswa kuadhimishwa mara ngapi?

• Mkate usiotiwa chachu unaotumiwa kwenye Ukumbusho unawakilisha nini?

• Divai inayotumiwa kwenye Ukumbusho inawakilisha nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yesu alianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana