Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mlo wa Jioni wa Bwana Una Maana Gani Kwako?

Mlo wa Jioni wa Bwana Una Maana Gani Kwako?

Mlo wa Jioni wa Bwana Una Maana Gani Kwako?

“Yeyote yule aulaye mkate au akinywaye kikombe cha Bwana isivyostahili atakuwa mwenye hatia kwa habari ya mwili na damu ya Bwana.”—1 WAKORINTHO 11:27.

1. Ni tukio gani muhimu zaidi litakalofanywa mwaka wa 2003, nalo lilianzaje?

TUKIO muhimu zaidi katika mwaka wa 2003 litafanywa Aprili 16 baada ya jua kutua. Mashahidi wa Yehova watakusanyika ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo. Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, Yesu alianzisha mwadhimisho huo, unaoitwa pia Mlo wa Jioni wa Bwana, baada ya yeye na mitume wake kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa mnamo Nisani 14, mwaka wa 33 W.K. Mifano ya Ukumbusho, yaani, mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu huwakilisha mwili wa Kristo usiokuwa na dhambi na damu yake iliyomwagwa ambayo ndiyo dhabihu pekee inayoweza kuwakomboa wanadamu kutokana na dhambi waliyorithi na kifo.—Waroma 5:12; 6:23.

2. Ni onyo gani linalotolewa kwenye 1 Wakorintho 11:27?

2 Wale wanaoshiriki kula mifano ya Ukumbusho wanapaswa kufanya hivyo kwa njia inayostahili. Mtume Paulo alieleza hilo waziwazi alipowaandikia Wakristo katika Korintho la kale, ambako Mlo wa Jioni wa Bwana haukuwa ukiadhimishwa kwa njia inayofaa. (1 Wakorintho 11:20-22) Paulo aliandika: “Yeyote yule aulaye mkate au akinywaye kikombe cha Bwana isivyostahili atakuwa mwenye hatia kwa habari ya mwili na damu ya Bwana.” (1 Wakorintho 11:27) Maneno hayo yanamaanisha nini?

Wengine Waliadhimisha Ukumbusho Isivyostahili

3. Wakristo wengi Wakorintho walitendaje kwenye miadhimisho ya Mlo wa Jioni wa Bwana?

3 Wakristo wengi Wakorintho walishiriki Ukumbusho isivyostahili. Kulikuwa na migawanyiko kati yao, na kwa muda fulani, baadhi yao walibeba na kula chakula chao cha jioni kabla au wakati wa mwadhimisho huo, na mara nyingi walikula na kunywa kupita kiasi. Hawakuwa chonjo kiakili wala kiroho, na hivyo wakawa ‘wenye hatia kwa habari ya mwili na damu ya Bwana.’ Wale ambao hawakubeba chakula walihisi njaa na kukengeushwa fikira. Naam, wengi wao walikula bila kuheshimu wala kutambua umuhimu wa tukio hilo. Si ajabu kwamba walijiletea hukumu wao wenyewe!—1 Wakorintho 11:27-34.

4, 5. Kwa nini ni muhimu wale wanaoshiriki mifano ya Ukumbusho kwa ukawaida wajichunguze?

4 Ukumbusho unapokaribia kila mwaka, ni muhimu wale wanaoshiriki mifano kwa ukawaida wajichunguze. Ili kushiriki mlo huo wa ushirika ifaavyo, ni lazima wawe katika hali nzuri ya kiroho. Mtu yeyote asiyeheshimu, au hata anayedharau dhabihu ya Yesu anaweza ‘kukatiliwa mbali na watu wa Mungu,’ kama Mwisraeli aliyeshiriki mlo wa ushirika akiwa najisi.—Mambo ya Walawi 7:20; Waebrania 10:28-31.

5 Paulo alilinganisha Ukumbusho na mlo wa ushirika katika Israeli la kale. Alitaja kwamba wale wanaokula huwa washirika katika Kristo halafu akasema: “Hamwezi kuwa mkinywa kikombe cha Yehova na kikombe cha roho waovu; hamwezi kuwa mkishiriki ‘meza ya Yehova’ na meza ya roho waovu.” (1 Wakorintho 10:16-21) Endapo mtu anayeshiriki kwa ukawaida mifano ya Ukumbusho anatenda dhambi nzito, anapaswa kuungama dhambi hiyo kwa Yehova na kuomba msaada wa kiroho kutoka kwa wanaume wazee kutanikoni. (Mithali 28:13; Yakobo 5:13-16) Akitubu kikweli na kuonyesha matunda yafaayo toba, hatakuwa akila isivyostahili.—Luka 3:8.

Wahudhuria Wakiwa Watazamaji Wenye Heshima

6. Mungu amewapa nani pendeleo la kushiriki Mlo wa Jioni wa Bwana?

6 Je, wale wanaowafanyia mema mabaki ya ndugu za Kristo 144,000 wanapaswa kushiriki kula Mlo wa Jioni wa Bwana? (Mathayo 25:31-40; Ufunuo 14:1) La. Mungu amewapa pendeleo hilo watu ambao amewatia mafuta kwa roho takatifu ili wawe “warithi-washirika pamoja na Kristo.” (Waroma 8:14-18; 1 Yohana 2:20) Basi wale wanaotumaini kuishi milele katika paradiso duniani chini ya utawala wa Ufalme wana pendeleo gani? (Luka 23:43; Ufunuo 21:3, 4) Wao huhudhuria Ukumbusho wakiwa watazamaji wenye heshima kwa kuwa wao si warithi-washirika pamoja na Yesu wenye tumaini la kwenda mbinguni.—Waroma 6:3-5.

7. Wakristo wa karne ya kwanza walijuaje kwamba wanastahili kushiriki mifano ya Ukumbusho?

7 Wakristo wa kweli katika karne ya kwanza walitiwa mafuta kwa roho takatifu. Wengi wao walikuwa na zawadi moja au zaidi za kimuujiza za roho, kama vile kuongea kwa lugha mbalimbali. Kwa hiyo, haingekuwa vigumu kwao kujua kwamba walikuwa wametiwa mafuta kwa roho na hivyo walistahili kushiriki mifano ya Ukumbusho. Hata hivyo, nyakati zetu, maneno haya yaliyoandikwa kwa mwongozo wa Mungu yanaweza kumsaidia mtu kujua ikiwa yeye ni mmoja wa wale waliotiwa mafuta kwa roho: “Wote wenye kuongozwa na roho ya Mungu, hao ndio wana wa Mungu. Kwa maana hamkupokea roho ya utumwa inayosababisha hofu tena, bali mlipokea roho ya tendo la kufanywa kuwa wana, roho ambayo kwayo twapaaza kilio: ‘Abba, Baba!’”—Waroma 8:14, 15.

8. Ni nani wanaofananishwa na “ngano” na “magugu” kwenye Mathayo sura ya 13?

8 Tangu kutaniko la kwanza la Kikristo lilipoanzishwa, watiwa-mafuta halisi waliendelea kukua kama “ngano” katika shamba lenye “magugu,” au Wakristo wasio wa kweli. (Mathayo 13:24-30, 36-43) Tangu miaka ya 1870, “ngano” ilianza kuonekana waziwazi, na miaka 100 hivi baadaye, waangalizi Wakristo watiwa-mafuta waliambiwa hivi: “Wazee . . . wanapaswa kuwapa masharti haya wale wanaokusanyika [kwa ajili ya Ukumbusho],—(1) wanapaswa kuwa na imani katika damu [ya Kristo]; na (2) wajitoe kwa Bwana na utumishi wake, hadi kifo. Kisha wanapaswa kuwaalika wale wanaotimiza masharti hayo na waliojitoa kwa Bwana washiriki kuadhimisha kifo cha Bwana.”—Studies in the Scriptures, Buku la 6, The New Creation, ukurasa wa 473. *

Kuwatafuta “Kondoo Wengine”

9. Maoni kuhusu “umati mkubwa” yalirekebishwaje mwaka wa 1935, na hilo liliwaathirije baadhi ya watu waliokuwa wakishiriki mifano ya Ukumbusho hapo awali?

9 Muda si muda, tengenezo la Yehova lilianza kukazia fikira jamii nyingine mbali na wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo. Jambo muhimu sana kuhusiana na jamii hiyo lilitukia katikati ya miaka ya 1930. Hapo awali, watu wa Mungu walifikiri kwamba “umati mkubwa” unaotajwa kwenye Ufunuo 7:9 ni jamii ya pili ya kiroho ambayo ingeungana na watiwa-mafuta 144,000 waliofufuliwa na kwenda mbinguni—wakiwa waandamani wa bibi-arusi wa Kristo. (Zaburi 45:14, 15; Ufunuo 7:4; 21:2, 9) Lakini hotuba iliyotolewa kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Washington, D.C., Marekani mnamo Mei 31, 1935, ilieleza kupitia Maandiko kwamba “umati mkubwa” (“mkutano mkubwa,” Union Version) ni “kondoo wengine” wanaoishi katika nyakati za mwisho. (Yohana 10:16) Baada ya kusanyiko hilo, baadhi ya watu walioshiriki mifano ya Ukumbusho hapo awali waliacha kula kwa sababu waligundua kwamba walikuwa na tumaini la kuishi duniani, si mbinguni.

10. “Kondoo wengine” leo wana wajibu na tumaini gani?

10 “Kondoo wengine” wenye imani katika fidia, waliojiweka wakfu kwa Mungu, na ambao wanaunga mkono “kundi dogo” la watiwa-mafuta katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme wamekuwa wakikusanywa hasa tangu mwaka wa 1935. (Luka 12:32) Kondoo hawa wengine wana tumaini la kuishi milele duniani, lakini wako sawa na mabaki ya warithi wa Ufalme katika mambo mengine yote. Kama wakazi wageni katika Israeli la kale ambao walimwabudu Yehova na kuitii Sheria, kondoo wengine leo hukubali wajibu wa Kikristo, kama vile kuhubiri habari njema pamoja na washiriki wa Israeli la kiroho. (Wagalatia 6:16) Hakuna mkazi yeyote mgeni angeweza kuwa mfalme au kuhani wa Israeli. Vivyo hivyo, hakuna mshiriki yeyote wa kondoo wengine anayeweza kutawala au kuwa kuhani katika Ufalme wa mbinguni.—Kumbukumbu la Torati 17:15.

11. Tarehe ambayo mtu alijiweka wakfu inawezaje kuonyesha iwapo anaweza kuwa mmoja wa watiwa-mafuta?

11 Katika miaka ya 1930, ilianza kuwa wazi kwamba kwa ujumla, jamii ya kimbingu ilikuwa imechaguliwa. Sasa, kondoo wengine wenye tumaini la kuishi duniani wamekuwa wakikusanywa kwa miaka 70 hivi. Mtiwa-mafuta akiasi, yaelekea sana kwamba mshiriki wa kondoo wengine ambaye amekuwa akimtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka mingi, ndiye anayeweza kuitwa achukue nafasi ya yule aliyeasi kati ya wale 144,000.

Kwa Nini Wengine Hufikiri Kimakosa Kwamba Wana Tumaini la Kwenda Mbinguni?

12. Mtu anapaswa kukoma kula mifano ya Ukumbusho katika hali zipi, na kwa nini?

12 Wakristo watiwa-mafuta hawana shaka yoyote kwamba wana mwito wa kimbingu. Lakini vipi ikiwa watu fulani ambao si watiwa-mafuta wamekuwa wakila mifano ya Ukumbusho? Baada ya kujua kwamba hawana tumaini la kwenda mbinguni, bila shaka dhamiri yao itawachochea waache kula mifano hiyo. Mungu hatamkubali mtu yeyote anayejifanya ana mwito wa kuwa mfalme na kuhani mbinguni huku akijua kwamba hajapokea kamwe mwito huo wa kimbingu. (Waroma 9:16; Ufunuo 20:6) Yehova alimwangamiza Mlawi aitwaye Kora kwa sababu alitaka kunyakua kwa kimbelembele ukuhani wa Haruni. (Kutoka 28:1; Hesabu 16:4-11, 31-35) Mkristo yeyote akigundua kwamba amekula kimakosa mifano ya Ukumbusho, anapaswa kukoma kisha amwombe Yehova msamaha kwa unyenyekevu.—Zaburi 19:13.

13, 14. Kwa nini huenda watu wengine wakafikiri kimakosa kwamba wana mwito wa kimbingu?

13 Kwa nini huenda watu wengine wakafikiri kimakosa kwamba wana mwito wa kimbingu? Wanaweza kukata tamaa ya kuishi duniani baada ya kufiwa na mwenzi wa ndoa au kupata msiba mwingine. Au huenda wakatamani kuwa na tumaini la kwenda mbinguni kama rafiki yao wa karibu anayedai kuwa Mkristo mtiwa-mafuta. Ni wazi kwamba Mungu hajampa mtu yeyote kazi ya kuwachagua wengine kwa ajili ya pendeleo hili. Naye hawatii mafuta warithi wa Ufalme kwa kufanya wasikie sauti zinazowajulisha kwamba wamechaguliwa.

14 Huenda wengine wakadhani kwamba wana mwito wa kimbingu kwa sababu ya fundisho la dini za uwongo kwamba watu wote wazuri huenda mbinguni. Kwa hiyo, tunahitaji kujihadhari ili tusipotoshwe na maoni yenye kosa tuliyokuwa nayo zamani au na mambo mengine. Kwa mfano, huenda wengine wakajiuliza hivi: ‘Je, mimi hutumia dawa zinazoathiri hisia zangu? Je, mimi huwa na hisia nyingi mno zinazoweza kunifanya nifikirie kimakosa kuwa nimetiwa mafuta?’

15, 16. Kwa nini watu wengine wanaweza kufikiri kimakosa kwamba wao ni watiwa-mafuta?

15 Wengine wanaweza kujiuliza: ‘Je, ninataka kuwa mashuhuri? Je, ninajitakia makuu sasa au nina tamaa ya kuwa mrithi-mshirika wa Kristo wakati ujao?’ Warithi wa Ufalme walipoteuliwa katika karne ya kwanza, si wote walikuwa wasimamizi kutanikoni. Na wale wenye mwito wa kimbingu hawajitafutii umashuhuri wala kujigamba kwamba wametiwa mafuta. Wana sifa ya unyenyekevu tunayotarajia ionyeshwe na wale ‘walio na akili ya Kristo.’—1 Wakorintho 2:16.

16 Huenda wengine wakafikiri kwamba wana mwito wa kimbingu kwa sababu ya kuwa na ujuzi mwingi mno wa Biblia. Lakini kutiwa mafuta kwa roho hakumfanyi mtu awe na ujuzi wa kipekee, ndiyo sababu Paulo alihitaji kuwafundisha na kuwashauri watiwa-mafuta fulani. (1 Wakorintho 3:1-3; Waebrania 5:11-14) Mungu ana mpango wa kuwapa watu wake wote chakula cha kiroho. (Mathayo 24:45-47) Kwa hiyo hakuna mtu anayepaswa kufikiri kwamba ana hekima nyingi kuliko wale wenye tumaini la kuishi duniani eti kwa sababu yeye ni Mkristo mtiwa-mafuta. Kuwa stadi katika kujibu maswali ya Kimaandiko, katika kuhubiri, au kutoa hotuba zinazotegemea Biblia hakuonyeshi kwamba mtu ametiwa mafuta kwa roho. Wakristo wenye tumaini la kuishi duniani wana ustadi huo pia.

17. Kutiwa mafuta kwa roho hutegemea nini na nani?

17 Mzee au Mkristo mwingine mkomavu anaweza kuzungumza na mwamini mwenzake ambaye angependa kujua mengi kuhusu mwito wa kimbingu. Hata hivyo, hakuna mtu anayeweza kumfanyia mwingine uamuzi huo. Mtu aliye na mwito huo kikweli hahitaji kuwauliza wengine ikiwa ana tumaini la kwenda mbinguni. Watiwa-mafuta ‘wamepewa uzaliwa mpya, si kupitia mbegu ya uzazi yenye kufisidika, bali kupitia isiyofisidika, kupitia neno la Mungu aliye hai na anayedumu daima.’ (1 Petro 1:23) Kupitia roho yake na Neno lake, Mungu hupanda “mbegu” inayomfanya mtu awe “kiumbe kipya,” mwenye tumaini la kwenda mbinguni. (2 Wakorintho 5:17) Yehova ndiye anayewachagua. Kutiwa mafuta ‘kwategemea, si yeye anayetaka wala yeye anayekimbia, bali Mungu.’ (Waroma 9:16) Basi mtu anawezaje kuwa na uhakika kwamba ana mwito wa kimbingu?

Kinachowahakikishia Watiwa-Mafuta

18. Roho ya Mungu hutoaje ushahidi pamoja na roho ya watiwa-mafuta?

18 Ushuhuda wa roho ya Mungu huwahakikishia Wakristo watiwa-mafuta kwamba wana tumaini la kwenda mbinguni. Paulo aliandika hivi: “Mlipokea roho ya tendo la kufanywa kuwa wana, roho ambayo kwayo twapaaza kilio: ‘Abba, Baba!’ Hiyo roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu. Basi, ikiwa sisi ni watoto, sisi pia ni warithi: warithi wa Mungu kwelikweli, lakini warithi-washirika pamoja na Kristo, mradi twateseka pamoja ili tupate pia kutukuzwa pamoja.” (Waroma 8:15-17) Chini ya mwelekezo wa roho takatifu, roho, au nia yenye nguvu ya watiwa-mafuta huwashurutisha kufuata yale ambayo Maandiko husema kuhusu wana wa kiroho wa Yehova. (1 Yohana 3:2) Roho ya Mungu huwafanya wahisi kwamba wao ni wana wa Mungu na hutia ndani yao tumaini la pekee. (Wagalatia 4:6, 7) Bila shaka wangefurahia sana kuishi milele duniani wakiwa wanadamu wakamilifu pamoja na washiriki wao wa familia na rafiki zao, lakini Mungu hajawapa tumaini hilo. Kupitia roho yake, Mungu amewapa tumaini lenye nguvu sana la kwenda mbinguni hivi kwamba wako tayari kudhabihu mahusiano yote duniani na mataraja yoyote waliyokuwa nayo.—2 Wakorintho 5:1-5, 8; 2 Petro 1:13, 14.

19. Agano jipya hutimiza kusudi gani katika maisha ya Mkristo mtiwa-mafuta?

19 Wakristo watiwa-mafuta wana hakika kwamba wana tumaini la kwenda mbinguni na wameingizwa katika agano jipya. Yesu alitaja jambo hilo alipoanzisha Ukumbusho na kusema: “Kikombe hiki chamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu, ambayo inapaswa kumwagwa kwa ajili yenu.” (Luka 22:20) Washiriki wa agano jipya ni Mungu na watiwa-mafuta. (Yeremia 31:31-34; Waebrania 12:22-24) Yesu ndiye mpatanishi. Agano jipya ambalo lilianzishwa kupitia damu ya Kristo iliyomwagwa, lilikusanya Wayahudi na vilevile watu wa mataifa ili watetee jina la Yehova na kuwa sehemu ya “mbegu” ya Abrahamu. (Wagalatia 3:26-29; Matendo 15:14) ‘Agano hilo linalodumu milele’ huwawezesha Waisraeli wa kiroho kufufuliwa na kupewa uhai usioweza kufa huko mbinguni.—Waebrania 13:20.

20. Watiwa-mafuta wanaingizwa katika agano gani pamoja na Kristo?

20 Watiwa-mafuta wana uhakika kuhusu tumaini lao. Wanaingizwa pia katika agano jingine, agano la Ufalme. Yesu alisema hivi kuhusu ushirika wao pamoja naye: “Nyinyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami nafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu amefanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme.” (Luka 22:28-30) Agano hili kati ya Kristo na wafalme watakaotawala naye linafanya kazi milele.—Ufunuo 22:5.

Wakati wa Ukumbusho Huthawabisha Sana

21. Tunawezaje kufaidika kabisa wakati wa Ukumbusho?

21 Wakati wa Ukumbusho ni pindi yenye kuthawabisha sana. Tunaweza kufaidika kwa kufuata ratiba ya usomaji wa Biblia iliyopangwa kwa ajili ya pindi hiyo. Ni wakati ufaao sana wa kusali, kutafakari kuhusu maisha ya Yesu duniani na kifo chake, na kushiriki katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. (Zaburi 77:12; Wafilipi 4:6, 7) Mwadhimisho huo hutukumbusha upendo wa Mungu na Kristo kuhusiana na dhabihu ya fidia ya Yesu. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16) Fidia hiyo hutupatia tumaini na faraja na inapaswa kuimarisha azimio letu la kufuata hatua za Kristo. (Kutoka 34:6; Waebrania 12:3) Ukumbusho unapaswa pia kutuchochea kutimiza wakfu wetu tukiwa watumishi wa Mungu na kuwa wafuasi waaminifu wa Mwanaye mpendwa.

22. Mungu amewapatia wanadamu zawadi gani kubwa zaidi, na tunawezaje kuonyesha shukrani zetu?

22 Yehova hutupatia zawadi nzuri ajabu! (Yakobo 1:17) Tuna mwongozo wa Neno lake, msaada wa roho yake, na tumaini la kuishi milele. Dhabihu ya Yesu ndiyo zawadi kubwa zaidi ambayo Mungu ametoa kwa ajili ya dhambi za watiwa-mafuta na wengine wote walio na imani. (1 Yohana 2:1, 2) Basi, kifo cha Yesu kina maana gani kwako? Je, utakuwa miongoni mwa wale watakaokusanyika kuonyesha shukrani zao kwa kifo hicho Aprili 16, 2003 baada ya jua kutua, ili kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Vilichapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa havichapishwi tena.

Ungejibuje?

• Ni nani wanaostahili kushiriki mifano ya Ukumbusho?

• Kwa nini “kondoo wengine” huhudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana wakiwa watazamaji wenye heshima?

• Wakristo watiwa-mafuta hujuaje kwamba wanastahili kushiriki kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo?

• Wakati wa Ukumbusho ni pindi inayofaa ya kufanya nini?

[Maswali ya Funzo]

[Grafu/Picha katika ukurasa wa 18]

 

Hudhurio la Ukumbusho

MILIONI

15,597,746

15

14

13,147,201

13

12

11

10

 9

 8

 7

 6

 5

4,925,643

 4

 3

 2

 1

878,303

63,146

1935 1955 1975 1995 2002

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, utahudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana mwaka huu?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wakati wa Ukumbusho ni pindi inayofaa ya kusoma Biblia zaidi na kushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme