Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Iweni Hodari na Wenye Moyo wa Ushujaa!’

‘Iweni Hodari na Wenye Moyo wa Ushujaa!’

‘Iweni Hodari na Wenye Moyo wa Ushujaa!’

“Jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.”—YOHANA 16:33.

1. Waisraeli walitiwaje moyo kwa kufikiria mambo ambayo wangekabili Kanaani?

WAISRAELI walipokaribia kuvuka Mto Yordani na kuingia katika Nchi ya Ahadi, Musa aliwaambia hivi: “Iweni hodari na moyo wa ushujaa, msiogope wala msiwahofu; kwa maana BWANA, Mungu wako, yeye ndiye anayekwenda pamoja nawe.” Kisha Musa akamwita Yoshua aliyekuwa amechaguliwa kuwaongoza Waisraeli hadi Kanaani, na kumwambia tena awe na moyo mkuu. (Kumbukumbu la Torati 31:6, 7) Baadaye, Yehova alimtia moyo Yoshua, akimwambia: “Uwe hodari na moyo wa ushujaa . . . Uwe hodari tu na ushujaa mwingi.” (Yoshua 1:6, 7, 9) Maneno hayo yalifaa wakati huo. Waisraeli wangehitaji kuwa na ujasiri ili kukabiliana na maadui wenye nguvu ng’ambo ya Yordani.

2. Ni hali gani inayotukabili leo na tunahitaji nini?

2 Karibuni, Wakristo wa kweli wataingia katika ulimwengu mpya ulioahidiwa, na kwa sababu hiyo wanahitaji kuwa jasiri kama Yoshua. (2 Petro 3:13; Ufunuo 7:14) Hata hivyo, tunakabili hali tofauti na Yoshua. Yoshua alipigana kwa mikuki na panga. Sisi hupigana vita ya kiroho na hatutumii silaha halisi. (Isaya 2:2-4; Waefeso 6:11-17) Isitoshe, Yoshua alipigana vita vingi vikali hata baada ya kuingia Nchi ya Ahadi. Lakini sasa tunakabili vita vikali hata zaidi kabla ya kuingia katika ulimwengu mpya. Na tuchunguze hali fulani ambazo hutaka tuwe na ujasiri.

Kwa Nini Tunahitaji Kujitahidi?

3. Biblia husema nini kuhusu mpinzani wetu mkuu?

3 Mtume Yohana aliandika hivi: “Sisi twajua twatokana na Mungu, lakini ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Maneno hayo yanaonyesha sababu hasa ya Wakristo kujitahidi ili kudumisha imani yao. Mkristo anapodumisha uaminifu, anamshinda Shetani Ibilisi kwa kadiri fulani. Kwa hiyo, Shetani huzunguka huku na huku “kama simba anayenguruma” akijaribu kuwatisha na kuwameza Wakristo waaminifu. (1 Petro 5:8) Kwa kweli, anawashambulia Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao. (Ufunuo 12:17) Yeye huwashambulia kwa kutumia wanadamu ambao kwa kujua au kutojua wanamtumikia. Tunahitaji kuwa jasiri ili kusimama imara dhidi ya Shetani na wote wanaomwakilisha.

4. Yesu alitoa onyo gani, lakini Wakristo wa kweli wameonyesha sifa gani?

4 Kwa kuwa Yesu alijua kwamba Shetani na wale wanaomwakilisha wangepinga vikali habari njema, aliwaonya wafuasi wake hivi: ‘Watu watawakabidhi nyinyi kwenye dhiki na watawaua nyinyi, nanyi mtakuwa vitu vya kuchukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.’ (Mathayo 24:9) Maneno hayo yalitimizwa katika karne ya kwanza, na yanatimizwa leo. Kwa kweli, baadhi ya Mashahidi wa Yehova leo wameteswa vikali kama watumishi wengine wa Mungu walioishi zamani. Hata hivyo, Wakristo wa kweli huonyesha ujasiri wanapokabili mateso. Wanatambua kwamba “kuwaogopa wanadamu huleta mtego,” na hawataki kunaswa katika mtego.—Mithali 29:25.

5, 6. (a) Ni hali zipi hutaka tuwe jasiri? (b) Wakristo waaminifu hutendaje ujasiri wao unapojaribiwa?

5 Mbali na mateso, kuna magumu mengine ambayo hutaka tuwe jasiri. Wengine huona ugumu kuhubiria watu wasiowajua habari njema. Ujasiri wa baadhi ya watoto wa shule hujaribiwa wanapoambiwa wakariri kiapo cha uaminifu kwa nchi na bendera. Kwa kuwa kiapo hicho ni cha kidini, watoto Wakristo wameazimia kwa ujasiri kutenda kwa njia inayompendeza Mungu, na mwenendo wao mzuri unatia moyo.

6 Tunahitaji kuwa jasiri wapinzani wanapotumia vyombo vya habari kueneza habari zisizofaa kuhusu watumishi wa Mungu au wanapojaribu kupinga ibada ya kweli kwa kutunga “madhara kwa njia ya sheria.” (Zaburi 94:20) Kwa mfano, tuhisije wakati magazeti, redio au televisheni zinaposambaza habari zenye kupotosha au uwongo wa waziwazi kuhusu Mashahidi wa Yehova? Je, tunapaswa kushangaa? La. Tunatarajia mambo hayo. (Zaburi 109:2) Na hatushangai watu fulani wanapoamini habari hizo za uwongo na zilizopotoshwa kwa kuwa “mjinga huamini kila neno.” (Mithali 14:15) Hata hivyo, Wakristo waaminifu hawaamini kamwe kila jambo linalosemwa kuhusu ndugu zao. Bila shaka, hawakosi kuhudhuria mikutano ya Kikristo, hawapunguzi bidii yao katika huduma ya shambani, wala imani yao haidhoofishwi na habari hizo za uwongo. Kinyume na hilo, “[wana]jipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu . . . kupitia utukufu na fedheha, kupitia ripoti mbaya na ripoti njema; kama wadanganyi [kwa maoni ya wapinzani] na bado [kwa hakika] wanasema kweli.”—2 Wakorintho 6:4, 8.

7. Tunaweza kujiuliza maswali gani ya kujichunguza?

7 Paulo alisema hivi alipomwandikia Timotheo: “Mungu alitupa sisi si roho ya woga, bali ile ya nguvu . . . Kwa hiyo usiwe mwenye kuaibikia ushahidi juu ya Bwana wetu.” (2 Timotheo 1:7, 8; Marko 8:38) Baada ya kusoma maneno hayo, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninaaibikia imani yangu, au je, mimi ni jasiri? Mahali ninapofanya kazi (au shuleni), je, ninawajulisha wengine kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova, au je, ninaogopa kujitambulisha? Je, ninaaibika kuwa tofauti na wengine, au ninafurahi kuwa tofauti na wengine kwa sababu ya uhusiano wangu na Yehova?’ Ikiwa yeyote anaogopa kuhubiri habari njema au kuwa na imani isiyowapendeza wengi, basi na akumbuke shauri ambalo Yehova alimpa Yoshua: “Uwe hodari na moyo wa ushujaa.” Usisahau kamwe kwamba jambo lililo muhimu si jinsi wafanyakazi au wanafunzi wenzako wanavyokuona bali ni jinsi Yehova na Yesu Kristo wanavyokuona.—Wagalatia 1:10.

Jinsi ya Kusitawisha Ujasiri

8, 9. (a) Pindi fulani, ujasiri wa Wakristo wa mapema ulijaribiwaje? (b) Petro na Yohana walitendaje walipotishwa, na ikawaje kwao na kwa ndugu zao?

8 Tunawezaje kusitawisha ujasiri utakaotuwezesha kudumisha uaminifu wakati huu wenye magumu? Wakristo wa mapema walisitawishaje ujasiri? Fikiria kilichotukia wakati makuhani wakuu na wazee huko Yerusalemu walipowaambia Petro na Yohana wakome kuhubiri katika jina la Yesu. Wanafunzi hao walikataa, wakatishwa, kisha wakaachiliwa. Mara tu baada ya hapo, walijiunga tena na ndugu zao, na wote wakasali pamoja wakisema: “Yehova, yaangalie matisho yao, na kuwaruhusu watumwa wako kufuliza kusema neno lako kwa ujasiri wote.” (Matendo 4:13-29) Yehova alijibu sala yao kwa kuwaimarisha kwa roho takatifu, na kama viongozi Wayahudi walivyosema baadaye, ‘wakajaza Yerusalemu’ kwa mafundisho yao.—Matendo 5:28.

9 Na tuchunguze mambo yaliyotokea wakati huo. Wanafunzi walipotishwa na viongozi Wayahudi, hawakuacha kuhubiri kwa sababu ya mateso. Badala yake, wanafunzi hao waliomba wapewe ujasiri ili waendelee kuhubiri. Kisha wakatenda kulingana na sala yao, naye Yehova akawaimarisha kwa roho yake. Jambo lililowapata linaonyesha kwamba maneno ambayo Paulo aliandika miaka kadhaa baadaye yanahusu Wakristo wanapokabili mateso. Paulo alisema: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.”—Wafilipi 4:13.

10. Kisa cha Yeremia kinaweza kuwasaidiaje wenye haya?

10 Je, mtu mwenye haya anaweza kumtumikia Yehova kwa ujasiri licha ya upinzani? Bila shaka! Kumbuka jinsi Yeremia alivyohisi Yehova alipomchagua kuwa nabii. Mvulana huyo alisema: “Mimi ni mtoto.” Ni wazi kwamba alihisi kuwa hafai. Hata hivyo, Yehova alimtia moyo kwa maneno haya: “Usiseme, mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru. Usiogope kwa sababu ya hao maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe.” (Yeremia 1:6-10) Yeremia alimtumaini Yehova, na kwa nguvu za Yehova akashinda woga na kuendelea kuhubiri kwa ujasiri katika Israeli.

11. Ni nini ambacho huwasaidia Wakristo leo wawe kama Yeremia?

11 Leo, Wakristo watiwa-mafuta wana kazi kama ya Yeremia, na wakiungwa mkono na “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” wanaendelea kutangaza makusudi ya Yehova, licha ya ubaridi, dhihaka, na mateso. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Wanapata kitia-moyo kutokana na maneno ambayo Yehova alimwambia Yeremia: “Usiogope.” Hawasahau kamwe kwamba Mungu amewapa kazi ya kuhubiri ujumbe wake.—2 Wakorintho 2:17.

Vielelezo vya Ujasiri Tunavyopaswa Kuiga

12. Yesu aliweka kielelezo gani bora cha kuwa jasiri, naye aliwatiaje moyo wafuasi wake?

12 Tunaweza kupata msaada wa kusitawisha ujasiri tukizingatia vielelezo vya wengine ambao wametenda kwa ujasiri kama Yeremia. (Zaburi 77:12) Kwa mfano, tunapochunguza huduma ya Yesu, tunavutiwa na ujasiri alioonyesha aliposhawishiwa na Shetani na alipopingwa vikali na viongozi Wayahudi. (Luka 4:1-13; 20:19-47) Kwa nguvu za Yehova, Yesu alikuwa thabiti sana, na muda mfupi kabla ya kifo chake aliwaambia wanafunzi wake: “Ulimwenguni mnakuwa na dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33; 17:16) Ikiwa wanafunzi wa Yesu wangefuata kielelezo chake, wao pia wangeshinda. (1 Yohana 2:6; Ufunuo 2:7, 11, 17, 26) Lakini wangehitaji ‘kujipa moyo.’

13. Paulo aliwapa Wafilipi kitia-moyo gani?

13 Miaka kadhaa baada ya kifo cha Yesu, Paulo na Sila walifungwa gerezani katika jiji la Filipi. Baadaye, Paulo alitia moyo kutaniko la Filipi liendelee ‘kusimama imara katika roho moja, kwa nafsi moja likipigana sambamba kwa ajili ya imani ya habari njema, na bila kuogopeshwa sana katika jambo lolote na wapinzani wao.’ Ili kuwatia moyo waendelee kusimama imara, Paulo alisema: “Jambo hilihili [kuteswa kwa Wakristo] ni ithibati kwao ya uangamizo [kwa wanaowatesa], lakini ya wokovu kwenu; na wonyesho huu ni kutoka kwa Mungu, kwa sababu nyinyi mlipewa pendeleo kwa ajili ya Kristo, si kuweka tu imani yenu katika yeye, bali pia kuteseka kwa ajili yake.”—Wafilipi 1:27-29.

14. Ujasiri wa Paulo huko Roma ulikuwa na matokeo gani?

14 Paulo alipoandikia kutaniko la Filipi, alikuwa gerezani tena, wakati huo alikuwa amefungwa huko Roma. Hata hivyo, aliendelea kuwahubiria wengine kwa ujasiri. Matokeo yakawaje? Aliandika: “Vifungo vyangu vimejulikana kwa watu wote kwa kushirikiana na Kristo miongoni mwa Walindaji wa Praetori wote na wale wengine wote; na walio wengi zaidi kati ya akina ndugu katika Bwana, wakihisi uhakika kwa sababu ya vifungo vyangu vya gereza, wanaonyesha moyo mkuu hata zaidi kulisema neno la Mungu bila hofu.”—Wafilipi 1:13, 14.

15. Tunaweza kupata wapi vielelezo vizuri vya imani vinavyoweza kuimarisha azimio letu la kuwa jasiri?

15 Kielelezo cha Paulo kinatutia moyo. Tunatiwa moyo pia na vielelezo vizuri vya Wakristo ambao wamevumilia mateso leo katika nchi zinazotawaliwa na makasisi au watawala wa kimabavu. Masimulizi mengi ya Wakristo hao yameandikwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na pia katika vitabu Yearbook of Jehovah’s Witnesses. Unaposoma masimulizi hayo, kumbuka kwamba wahusika ni watu wa kawaida kama sisi; lakini Yehova aliwapa nguvu zisizo za kawaida wakavumilia hali ngumu sana. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatupa nguvu tukikabili hali ngumu.

Ujasiri Wetu Humpendeza Yehova na Kumletea Sifa

16, 17. Tunawezaje kusitawisha ujasiri leo?

16 Mkristo huonyesha ujasiri anapotetea kweli na uadilifu kwa uthabiti. Naye huonyesha ujasiri mkubwa hata zaidi anapokuwa thabiti licha ya woga. Kwa kweli, Mkristo yeyote anaweza kuwa jasiri ikiwa anataka kufanya mapenzi ya Yehova, ameazimia kudumu akiwa mwaminifu, anamtegemea Mungu daima, na ikiwa sikuzote anakumbuka kwamba wakati uliopita, Yehova aliwaimarisha watu wengine wengi. Isitoshe, tunapotambua kwamba ujasiri wetu humpendeza Yehova na kumletea sifa, tunaazimia kuwa thabiti hata zaidi. Tumeazimia kuvumilia dhihaka au hali mbaya zaidi kwa sababu tunampenda sana Yehova.—1 Yohana 2:5; 4:18.

17 Tunapoteseka kwa ajili ya imani yetu, hatupaswi kufikiri kamwe kwamba mateso hayo yanatupata kwa sababu tumetenda dhambi. (1 Petro 3:17) Tunateseka kwa sababu ya kutetea enzi kuu ya Yehova, kutenda mema, na kutokuwa sehemu ya ulimwengu. Mtume Petro alisema hivi kuhusiana na habari hiyo: “Ikiwa, mnapotenda mema na kuteseka, mwalivumilia, hili ni jambo lenye kukubalika kwa Mungu.” Pia Petro alisema: “Acheni wale wanaoteseka kwa kupatana na mapenzi ya Mungu wafulize kukabidhi nafsi zao kwa Muumba mwaminifu wanapotenda mema.” (1 Petro 2:20; 4:19) Naam, imani yetu humpendeza Yehova Mungu wetu mwenye upendo, na kumletea sifa. Tuna sababu nzuri kama nini ya kuwa jasiri!

Kuzungumza na Wenye Mamlaka

18, 19. Ni ujumbe gani tunaotoa tunapoonyesha ujasiri mbele ya hakimu?

18 Yesu alipowaambia wafuasi wake kwamba wangeteswa, pia alisema: “[Watu] watawakabidhi nyinyi kwenye mahakama za mtaa, nao watawapiga nyinyi mijeledi katika masinagogi yao. Naam, mtaburutwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.” (Mathayo 10:17, 18) Tunahitaji kuwa jasiri tunapofikishwa mbele ya hakimu au mtawala kwa sababu ya mashtaka ya uwongo. Hata hivyo, tunapotumia fursa hizo kuwahubiria watu hao kwa ujasiri tunatumia pindi hiyo ngumu kutimiza jambo muhimu. Kwa kufanya hivyo, ni kana kwamba tunawatolea mahakimu ujumbe wa Yehova unaopatikana katika Zaburi ya 2: “Na sasa, enyi wafalme, fanyeni akili, enyi waamuzi wa dunia, mwadibiwe. Mtumikieni BWANA kwa kicho.” (Zaburi 2:10, 11) Mara nyingi, Mashahidi wa Yehova wanaposhtakiwa kwa uwongo mahakamani, mahakimu hutetea uhuru wa ibada nasi tunathamini jambo hilo. Hata hivyo, baadhi ya mahakimu wamefuata maoni ya wapinzani. Andiko husema hivi kuhusu mahakimu hao: “Mwadibiwe.”

19 Mahakimu wanapaswa kutambua kwamba sheria ya Yehova Mungu ndiyo kuu zaidi. Wanapaswa kukumbuka kwamba wanadamu wote, kutia ndani mahakimu, wanawajibika kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Waroma 14:10) Tuhukumiwe kwa haki au la, tuna kila sababu ya kuwa jasiri kwa sababu Yehova anatutegemeza. Biblia husema: “Heri wote wanaomkimbilia.”—Zaburi 2:12.

20. Kwa nini tutakuwa na furaha ikiwa tutavumilia mateso na habari za uwongo?

20 Yesu alisema hivi katika Mahubiri ya Mlimani: “Wenye furaha ni nyinyi watu wawashutumupo na kuwanyanyasa nyinyi na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo ovu dhidi yenu kwa ajili yangu. Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa katika mbingu; kwa maana katika njia hiyo waliwanyanyasa manabii waliokuwa kabla yenu.” (Mathayo 5:11, 12) Kwa kweli, mateso hayapendezi, lakini tunafurahi tunaposimama imara licha ya mateso na habari za uwongo zinazoenezwa na vyombo vya habari. Kusimama imara huonyesha kwamba tunampendeza Yehova, na tutapata thawabu. Ujasiri wetu huonyesha kwamba tuna imani ya kweli na hutuhakikishia kwamba tuna kibali cha Mungu. Naam, unaonyesha kwamba tunamtumaini Yehova kabisa. Tumaini hilo ni muhimu kwa Mkristo kama tutakavyoona katika makala inayofuata.

Umejifunza Nini?

• Ni hali zipi leo ambazo hutaka tuwe jasiri?

• Tunawezaje kusitawisha ujasiri?

• Ni akina nani wanaotuwekea kielelezo kizuri cha kuwa jasiri?

• Kwa nini tunataka kuwa jasiri?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Simone Arnold (sasa ni Liebster) wa Ujerumani, Widdas Madona wa Malawi, na Lydia na Oleksii Kurdas wa Ukrainia walionyesha ujasiri kutoka kwa Yehova na kumpinga mwovu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Hatuaibikii habari njema

[Picha katika ukurasa wa 11]

Ujasiri wa Paulo akiwa gerezani ulisaidia kueneza habari njema

[Picha katika ukurasa wa 12]

Tunatoa ujumbe muhimu tunapomweleza hakimu msimamo wetu wa Kimaandiko kwa ujasiri