Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutafuta Ufalme Kwanza Huridhisha na Huleta Furaha Maishani

Kutafuta Ufalme Kwanza Huridhisha na Huleta Furaha Maishani

Simulizi la Maisha

Kutafuta Ufalme Kwanza Huridhisha na Huleta Furaha Maishani

LIMESIMULIWA NA JETHA SUNAL

Baada ya kiamsha-kinywa tulisikia tangazo lifuatalo kwenye redio: “Kazi ya Mashahidi wa Yehova imepigwa marufuku.”

MNAMO 1950, tukiwa wanawake wanne wenye umri wa miaka 20 na kitu, tulikuwa tukitumikia kama mishonari wa Mashahidi wa Yehova katika Jamhuri ya Dominika. Mwaka mmoja ulikuwa umepita tangu tulipowasili.

Utumishi wa mishonari haukuwa mradi wangu wa maisha awali. Ni kweli kwamba nilikwenda kanisani nilipokuwa mtoto. Hata hivyo, baba yangu aliacha kwenda kanisani wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu. Nilipopewa kipaimara katika Kanisa la Kianglikana mwaka wa 1933, askofu alisoma mstari mmoja tu katika Biblia, kisha akaanza kuongea kuhusu siasa. Mama yangu aliudhika sana hivi kwamba hakurudi kanisani tena kamwe.

Maisha Yetu Yalibadilika

Wazazi wangu, William Karl na Mary Adams, walikuwa na watoto watano. Wana wao waliitwa Don, Joel, na Karl. Dada yangu Joy alikuwa kitinda-mimba na mimi nilikuwa mkubwa. Nadhani nilikuwa na umri wa miaka 13 nilipomkuta Mama akisoma kijitabu kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova nilipotoka shuleni siku moja. Kilikuwa na kichwa The Kingdom, the Hope of the World (Ufalme, Tumaini la Ulimwengu). “Hii ndiyo kweli,” aliniambia.

Mama alizungumza nasi juu ya mambo aliyojifunza katika Biblia. Alionyesha kwa maneno na matendo umuhimu wa shauri hili la Yesu: ‘Tafuta kwanza ufalme na uadilifu wake.’—Mathayo 6:33.

Mara nyingi sikutaka kumsikiliza. Siku moja nilisema: “Mama, acha kunihubiria ama sitakupangusia vyombo tena.” Hata hivyo, aliendelea kusema nasi kwa busara. Sisi sote tuliambatana naye kwa ukawaida kwenye masomo ya Biblia yaliyofanywa katika nyumba ya Clara Ryan, aliyeishi karibu nasi huko Elmhurst, Illinois, Marekani.

Pia Clara alifundisha masomo ya kupiga piano. Wanafunzi wake walipofanya maonyesho ya muziki ya kila mwaka, alitumia nafasi hiyo kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu na tumaini la ufufuo. Nilipendezwa na muziki, kwa kuwa tangu nilipokuwa na umri wa miaka saba nilikuwa nimejifunza kupiga fidla, kwa hiyo nilimsikiliza Clara.

Punde sisi watoto tulianza kuhudhuria mikutano ya kutaniko pamoja na Mama magharibi mwa Chicago. Hiyo ilikuwa safari ndefu kwa basi na gari-moshi la mjini, lakini jambo hilo lilituzoeza mapema maishani kuelewa maana ya kutafuta Ufalme kwanza. Miaka mitatu baada ya Mama kubatizwa, niliambatana naye kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Chicago mwaka wa 1938. Jiji hilo lilikuwa mojawapo ya majiji 50 ambapo watu waliweza kusikiliza programu ya kusanyiko hilo kwenye redio. Mambo niliyosikia yalinigusa moyoni.

Lakini, nilipenda muziki pia. Nilihitimu shule ya upili mwaka wa 1938, na Baba alipanga nijifunze muziki kwenye Shule ya Muziki ya Marekani huko Chicago. Kwa hiyo miaka miwili iliyofuata nilijifunza muziki, nilicheza katika makundi mawili ya wanamuziki, na nilitaka kuwa mwanamuziki.

Mwalimu wangu wa fidla, Herbert Butler, alikuwa amehamia Marekani kutoka Ulaya. Kwa hiyo nikampa kijitabu Refugees, * (Wakimbizi) nikitumaini atakisoma. Alikisoma, na baada ya somo langu juma lililofuata, akasema hivi: “Jetha, unacheza vizuri, na ukiendelea na masomo yako, ungeweza kupata kazi ya kufunza muziki, au kujiunga na kundi fulani la wanamuziki wanaocheza kwenye redio.” Aliongezea hivi, akigusagusa kijitabu nilichompa: “Lakini nadhani kwamba unapenda ujumbe huu zaidi. Mbona usichague kufanya kazi ya kueneza ujumbe huu?”

Nilifikiria jambo hilo kwa uzito. Badala ya kuendelea na masomo ya muziki nilikubali kuandamana na Mama kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Detroit, Michigan, mnamo Julai 1940. Tulilala kwenye mahema katika kambi maalumu. Nilibeba fidla yangu, na nilijiunga na wanamuziki waliocheza kwenye kusanyiko. Na pia nilikutana na mapainia wengi kambini, yaani, wahubiri wa wakati wote. Wote walikuwa wenye furaha sana. Niliamua kubatizwa na nikajaza ombi la upainia. Nilisali kwa Yehova anisaidie kuendelea na huduma ya wakati wote bila kuacha.

Nilianza utumishi wa painia katika mji wa kwetu. Baadaye, nilitumikia huko Chicago. Nilihamia Kentucky mwaka wa 1943. Kabla tu ya kusanyiko la wilaya mwaka huo, nilialikwa kuhudhuria darasa la pili la Shule ya Gileadi, ambapo ningezoezwa kufanya kazi ya mishonari. Darasa hilo lingeanza mnamo Septemba 1943.

Wakati wa kusanyiko hilo, nilikaa kwa Shahidi aliyeniruhusu kuchagua nguo zozote za binti yake nilizozitaka. Binti yake alikuwa amejiunga na jeshi, na alikuwa amemwambia mama yake awapatie wengine vitu vyake vyote. Niliona jambo hilo kuwa utimizo wa ahadi hii ya Yesu: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.” (Mathayo 6:33) Miezi mitano tuliyokuwa Gileadi ilienda haraka sana, na baada ya kuhitimu Januari 31, 1944, nilitazamia kwa hamu kuanza utumishi wa mishonari.

Wao Pia Walichagua Utumishi wa Wakati Wote

Mama alikuwa ameanza utumishi wa painia mwaka wa 1942. Wakati huo, ndugu zangu watatu na dada yangu walikuwa bado shuleni. Mara nyingi Mama aliwachukua baada ya shule na kuambatana nao katika huduma ya shambani. Aliwafundisha pia kusaidia kufanya kazi za nyumbani. Mara nyingi yeye mwenyewe alilala kwa kuchelewa kwani alikuwa akipiga pasi na kufanya kazi nyingine za lazima ili aweze kuhubiri mchana.

Mnamo Januari 1943, nilipokuwa nikifanya upainia huko Kentucky, ndugu yangu Don alianza pia kupainia. Jambo hilo lilimvunja Baba moyo kwa sababu alitumaini kwamba watoto wake wote wangepata elimu ya chuo, kama yeye na Mama. Baada ya kuwa painia kwa miaka miwili hivi, Don alialikwa kuendelea na huduma ya wakati wote akiwa mfanyakazi katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York.

Joel alianza kupainia Juni 1943 akiwa bado anaishi nyumbani. Wakati huo alijaribu kumsadikisha Baba ahudhurie kusanyiko fulani lakini hakufaulu. Hata hivyo, baada ya Joel kujaribu kuanzisha funzo la Biblia la nyumbani katika eneo bila kufanikiwa, Baba alikubali Joel amfunze kitabu “The Truth Shall Make You Free.” Alijibu maswali kwa urahisi, lakini alimkaza Joel athibitishe kwa Maandiko mambo ambayo kitabu kilisema. Jambo hilo lilimsaidia Joel kuthamini hata zaidi kweli za Biblia kutoka moyoni.

Joel alitumaini kwamba Kamati ya Kuamua Wahudumu wa Kidini iliyomruhusu Don asijiandikishe jeshini, ingemruhusu yeye pia asijiandikishe. Lakini kamati ilipoona kwamba Joel alikuwa kijana, ilikataa kumhesabu kuwa mhudumu na ikamtumia barua ya kujiandikisha jeshini. Alipokataa kujiandikisha, hati ya kumkamata ilitolewa. Baada ya Shirika la Upelelezi la Marekani kumkamata, alikaa katika gereza la Cook County kwa siku tatu.

Baba alitumia nyumba yetu kama dhamana ili aachiliwe. Baadaye akafanya vivyo hivyo kuwasaidia vijana wengine Mashahidi waliokuwa katika hali hiyo. Ukosefu huo wa haki ulimkera sana baba yangu hivi kwamba alienda na Joel kujaribu kukata rufani huko Washington, D. C. Hatimaye, Joel alihesabiwa kuwa mhudumu, na kesi ikafutwa. Baba yangu alisema hivi katika barua aliyoniandikia nikiwa katika utumishi wa mishonari: “Nafikiri Yehova ndiye anayestahili kusifiwa kwa sababu ya ushindi huo!” Mwishoni mwa Agosti 1946, Joel pia alialikwa kuwa mfanyakazi katika makao makuu huko Brooklyn.

Karl alipainia mara kadhaa wakati wa likizo kabla ya kumaliza shule ya upili mapema mwaka wa 1947 kisha akaanza upainia wa kawaida mwaka huohuo. Baba alikuwa mgonjwa-mgonjwa, kwa hiyo Karl alimsaidia katika biashara yake kwa muda kabla ya kwenda kupainia mahali pengine. Mwishoni mwa mwaka wa 1947, Karl alianza kufanya kazi pamoja na Don na Joel kwenye makao makuu huko Brooklyn akiwa Mwanabetheli.

Joy alipomaliza shule ya upili, alianza kupainia. Kisha akajiunga na ndugu zake huko Betheli mwaka wa 1951. Alifanya kazi ya usafi na pia katika Idara ya Maandikisho. Mwaka wa 1955 aliolewa na Roger Morgan ambaye pia alikuwa Mwanabetheli. Baada ya miaka saba, waliamua kuondoka Betheli kwa sababu walitaka kuwa na watoto. Muda si muda walipata na kulea watoto wawili, ambao pia wanamtumikia Yehova.

Baada ya watoto wote kuanza utumishi wa wakati wote, Mama alimtia Baba moyo, na hivyo Baba pia akajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa mwaka wa 1952. Kwa miaka 15 kabla ya kifo chake, aliongea na wengine kwa ustadi kuhusu kweli ya Ufalme ijapokuwa ugonjwa ulimtatiza.

Baada ya kuacha upainia kwa muda kwa sababu ya ugonjwa wa Baba, Mama aliendelea na upainia hadi kifo chake. Hakutumia gari wala baiskeli. Alikuwa mfupi, na alitembea kila mahali, mara nyingi akienda sehemu za mbali mashambani ili kuongoza mafunzo ya Biblia.

Kuanza Utumishi wa Mishonari

Baada ya kuhitimu Shule ya Gileadi, baadhi yetu tulipainia kaskazini ya New York City kwa mwaka mmoja tukingoja kupata hati za kusafiri tulizohitaji. Mwishowe, tuliondoka ili kwenda Kuba mwaka wa 1945 ambako tulizoea maisha mapya pole kwa pole. Wengi walisikiliza mahubiri yetu, na punde sote tulikuwa tukiongoza mafunzo mengi ya Biblia. Tulitumika huko kwa miaka kadhaa. Kisha tukatumwa Jamhuri ya Dominika. Siku moja nilikutana na mwanamke mmoja aliyenisihi nimtembelee mteja wake Suzanne Enfroy, mwanamke kutoka Ufaransa, aliyetaka kuelewa Biblia.

Suzanne alikuwa Myahudi, na Hitler alipovamia Ufaransa, mume wake alimhamisha pamoja na watoto wao wawili hadi nchi nyingine. Suzanne alianza mara moja kuzungumza na wengine kuhusu mambo ambayo alikuwa akijifunza. Kwanza alizungumza na yule mwanamke aliyeniomba nimtembelee, kisha akazungumza na rafiki yake kutoka Ufaransa anayeitwa Blanche. Wote wawili walifanya maendeleo, wakabatizwa.

Suzanne aliniuliza hivi: “Ninawezaje kuwasaidia watoto wangu?” Mwanawe alikuwa akisomea udaktari, na binti yake alikuwa akijifunza kucheza dansi aina ya bale, akitumaini kucheza dansi kwenye jumba la Radio City Music Hall huko New York. Suzanne aliwaandikishia magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kwa hiyo, mwana wa Suzanne na mke wake, na dada pacha wa mke wake wakawa Mashahidi. Mume wa Suzanne, Louis, alikuwa na wasiwasi kwa sababu mke wake alipendezwa na Mashahidi wa Yehova hali serikali ya Jamhuri ya Dominika ilikuwa imepiga kazi yetu marufuku. Lakini baada ya familia nzima kuhamia Marekani yeye pia akawa Shahidi.

Waliendelea Kutumikia Licha ya Marufuku

Ijapokuwa kazi ya Mashahidi ya Yehova ilipigwa marufuku huko Jamhuri ya Dominika muda mfupi baada ya sisi kutumwa huko mwaka wa 1949, tuliazimia kumtii Mungu kuwa Mtawala kuliko wanadamu. (Matendo 5:29) Tuliendelea kutafuta kwanza Ufalme wa Mungu kwa kuhubiri habari njema kama Yesu alivyowaagiza wafuasi wake. (Mathayo 24:14) Hata hivyo, tulijifunza “kuwa wenye hadhari kama nyoka na bado kuwa wasio na hatia kama njiwa” tulipokuwa tukihubiri. (Mathayo 10:16) Fidla yangu ilinisaidia sana katika jambo hilo. Niliibeba kila nilipoenda kuongoza mafunzo ya Biblia. Wanafunzi wangu hawakujifunza kucheza fidla, lakini familia kadhaa wakawa watumishi wa Yehova.

Baada ya kupigwa marufuku, sisi wasichana wanne, yaani, mimi, Mary Aniol, Sophia Soviak, na Edith Morgan, tulihamishwa kutoka makao ya mishonari huko San Francisco de Macorís hadi makao ya mishonari yaliyokuwa katika ofisi ya tawi katika mji mkuu, Santo Domingo. Lakini kila mwezi, nilisafiri hadi mahali tulipotumikia awali ili kuwafundisha watu muziki. Hivyo niliweza kuwabebea ndugu zetu Wakristo chakula cha kiroho ndani ya mfuko wa fidla yangu na kurudi na ripoti zao za utumishi.

Wakati ndugu kutoka San Francisco de Macorís walipofungwa huko Santiago kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutojiunga na upande wowote katika siasa, niliombwa kuwapelekea pesa na hata Biblia ikiwezekana, na kurudi na habari kwa familia zao. Walinzi wa gereza la Santiago walipoona mfuko wa fidla mkononi mwangu waliuliza hivi: “Mfuko huo ni wa nini?” Nikajibu: “Ni wa kuwatumbuiza.”

Wimbo mmoja kati ya zile nilizocheza ulitungwa na Shahidi aliyekuwa amefungwa katika kambi ya mateso ya Nazi. Wimbo huo sasa ni namba 29 katika kitabu cha nyimbo cha Mashahidi wa Yehova. Niliucheza ili ndugu zetu waliofungwa wajifunze kuimba wimbo huo.

Nilipata habari kwamba Mashahidi wengi walikuwa wamehamishwa hadi kwenye shamba la mkuu wa serikali, Trujillo. Niliambiwa kwamba shamba hilo lilikuwa karibu na barabara iliyotumiwa na basi. Karibu  adhuhuri nilishuka kutoka katika basi na kuulizia njia ya kufika kwenye shamba hilo. Mwenye-duka mmoja aliniashiria kwa kidole milima kadhaa na kunipa farasi wake na mvulana wa kuniongoza mradi niache fidla yangu kama dhamana.

Baada ya milima hiyo, ilitubidi sote wawili kuvuka mto tukiwa tumepanda farasi. Huko, tuliwaona kasuku wengi wenye manyoya yenye rangi ya samawati na kijani-kibichi iliyometameta kwenye jua. Walikuwa maridadi wee! Nikasali hivi: “Asante Yehova, kwa kuwaumba wakiwa maridadi hivyo.” Hatimaye, tukafika kwenye shamba hilo saa kumi jioni. Askari mkuu aliniruhusu kwa upole kuongea na ndugu, na akanipa ruhusa ya kuwapa vitu vyote nilivyowaletea, hata Biblia ndogo.

Nilisali muda wote tulipokuwa tukirudi kwa sababu giza lilikuwa limeingia. Tulirudi dukani tukiwa tumelowa kabisa kwa sababu ya mvua. Kwa kuwa basi la mwisho lilikuwa limeondoka, nilimwomba mwenye-duka anisimamishie lori lililokuwa linapita. Je, ingekuwa hatari kusafiri na wanaume wawili waliokuwa katika lori hilo? Mmoja wao aliniuliza: “Je, unamjua Sophie? Yeye alimfunza dada yangu.” Niliona kwamba Yehova amejibu sala yangu! Nilisafiri nao salama hadi Santo Domingo.

Nilikuwa baadhi ya wale waliotoka Jamhuri ya Dominika waliohudhuria kusanyiko la kimataifa la Mashahidi wa Yehova katika Uwanja wa Yankee huko New York mwaka wa 1953. Familia yetu yote, kutia ndani baba yangu, ilihudhuria kusanyiko hilo. Baada ya ripoti kutolewa kuhusu kazi ya kuhubiri huko Jamhuri ya Dominika, mimi na Mary Aniol, mishonari mwenzangu, tulipewa mgawo kwenye kusanyiko wa kuonyesha jinsi tulivyohubiri wakati wa marufuku.

Furaha ya Pekee Katika Kazi ya Kuzunguka

Mwaka huo nilikutana na Rudolph Sunal, aliyenioa mwaka uliofuata. Watu wa familia yake walikuwa wamekuwa Mashahidi huko Allegheny, Pennsylvania, muda mfupi baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu. Baada ya kufungwa gerezani kwa sababu ya msimamo wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu, alianza kutumikia katika Betheli huko Brooklyn, New York. Muda mfupi baada ya kufunga ndoa, aliombwa kutembelea makutaniko akiwa mwangalizi asafiriye. Kwa miaka 18 iliyofuata, niliambatana naye katika kazi hiyo.

Tulitembelea makutaniko huko Pennsylvania, West Virginia, New Hampshire, Massachusetts, na sehemu nyinginezo. Tulikaa na ndugu zetu Wakristo nyumbani kwao. Tulifurahi sana kuwajua vizuri na kumtumikia Yehova pamoja nao. Walituonyesha upendo wa moyoni na walitukaribisha kwa uchangamfu. Baada ya Joel kumwoa Mary Aniol, aliyekuwa mishonari mwenzangu, walitembelea makutaniko huko Pennsylvania na Michigan kwa miaka mitatu. Baadaye Joel alialikwa tena kuwa Mwanabetheli pamoja na Mary mwaka wa 1958.

Karl alikuwa ametumikia Betheli kwa miaka saba alipotumwa kutembelea makutaniko kwa miezi michache ili apate mazoezi zaidi. Baadaye akawa mwalimu wa Shule ya Gileadi. Mwaka wa 1963, alimwoa Bobbie aliyetumikia Betheli kwa uaminifu hadi kifo chake Oktoba 2002.

Don ametumikia Betheli kwa miaka mingi, na mara kwa mara ametumwa nchi nyingine kuwasaidia wale wanaofanya kazi kwenye ofisi za tawi na vilevile mishonari. Amesafiri hadi nchi za Mashariki, Afrika, Ulaya, na sehemu mbalimbali za Amerika. Dolores, mke wake mwaminifu husafiri naye mara nyingi.

Hali Zetu Zilibadilika

Baba yangu alikufa baada ya kuugua kwa muda mrefu, lakini kabla afe aliniambia alifurahi sana kwamba sote tulikuwa tumeamua kumtumikia Yehova Mungu. Alisema kwamba tulikuwa tumebarikiwa zaidi kuliko kama tungalipata elimu ya chuo ambayo alinuia tupate. Baada ya kumsaidia Mama kufunga virago ili ahamie karibu na dada yangu Joy, mimi na mume wangu tulikubali kuwa mapainia huko New England ili tuwe karibu na mama yake aliyehitaji msaada wetu. Baada ya mama yake kufa, mama yangu aliishi nasi kwa miaka 13. Kisha, Mama aliyekuwa na tumaini la kimbingu akafa Januari 18, 1987, akiwa na umri wa miaka 93.

Mara nyingi marafiki walipomsifu kwa kuwazoeza watoto wake kumpenda na kumtumikia Yehova, Mama alijibu kwa unyenyekevu: “Ni kwamba tu watoto wangu walikuwa ‘udongo’ mzuri.” (Mathayo 13:23) Ilikuwa baraka iliyoje kuwa na wazazi waliomhofu Mungu ambao walituonyesha mfano mzuri kwa kuwa na bidii na unyenyekevu!

Bado Tunaweka Ufalme Kwanza

Tumeendelea kuweka Ufalme wa Mungu kwanza maishani mwetu na tumejaribu pia kufuata shauri la Yesu kuhusu kutoa. (Luka 6:38; 14:12-14) Yehova naye ametuandalia kwa ukarimu mahitaji yetu. Maisha yetu yamekuwa yenye kuridhisha na yenye furaha.

Mimi na Rudy tungali tunapenda muziki. Inafurahisha sana wengine wanaopenda muziki wanapotutembelea nyumbani jioni na tunapiga pamoja ala zetu za muziki. Lakini muziki si jambo kuu maishani mwangu, bali hunistarehesha tu. Sasa mimi na mume wangu tunafurahia kuona matokeo ya huduma yetu ya upainia, yaani, watu ambao tumewasaidia katika miaka iliyopita.

Licha ya matatizo ya afya niliyo nayo sasa, naweza kusema kwamba tumekuwa na maisha yenye kuridhisha na yenye furaha sana kwa zaidi ya miaka 60 katika utumishi wa wakati wote. Kila asubuhi ninapoamka, mimi humshukuru Yehova kwa kujibu sala niliyotoa nilipoanza huduma ya wakati wote miaka mingi iliyopita, nami hujiuliza, ‘Nawezaje kutafuta Ufalme kwanza leo?’

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, lakini hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Familia yetu mwaka wa 1948 (kushoto hadi kulia): Joy, Don, Mama, Joel, Karl, mimi, na Baba

[Picha katika ukurasa wa 25]

Mama alionyesha mfano mzuri kwa kuwa na bidii katika huduma

[Picha katika ukurasa wa 26]

Karl, Don, Joel, Joy, na mimi leo baada ya miaka 50 hivi kupita

[Picha katika ukurasa wa 27]

Kushoto hadi kulia: Mimi, Mary Aniol, Sophia Soviak, na Edith Morgan tulipokuwa mishonari huko Jamhuri ya Dominika

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nikiwa na Mary (kushoto) kwenye Uwanja wa Yankee, 1953

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikiwa na mume wangu alipokuwa mwangalizi wa mzunguko