Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Watu Huteswa kwa Sababu ya Dini?

Kwa Nini Watu Huteswa kwa Sababu ya Dini?

Kwa Nini Watu Huteswa kwa Sababu ya Dini?

JE, UNAAMINI kwamba watu wanapaswa kuteswa kwa sababu ya dini yao? Wengi wangejibu la, mradi hawaingilii haki za wengine. Hata hivyo, watu wameteswa kwa sababu ya dini tangu zamani na bado wanaendelea kuteswa. Kwa mfano, Mashahidi wengi wa Yehova katika Ulaya na nchi nyinginezo ulimwenguni walinyimwa haki zao na kuteswa vikali mara nyingi katika kipindi chote cha karne ya 20.

Wakati huo, serikali mbili kuu za kimabavu huko Ulaya zilipanga njama ya kuwatesa Mashahidi wa Yehova kikatili kwa muda mrefu. Mambo waliyopitia yanatufundisha nini kuhusu mateso ya kidini? Na tunaweza kujifunza nini kutokana na namna walivyotenda walipoteswa?

“Si Sehemu ya Ulimwengu”

Mashahidi wa Yehova wanajitahidi sana kutii sheria, kuwa wenye amani, na wanyofu. Hawapingi serikali au kutaka mapambano nazo, wala hawachochei serikali ziwatese kwa sababu wanataka kufa ajili ya imani yao. Wakristo hao hawaungi mkono upande wowote katika mambo ya siasa. Jambo hilo lapatana na maneno ya Yesu: “[Wafuasi wangu] si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16) Serikali nyingi hutambua msimamo wa Mashahidi wa kutounga mkono upande wowote katika mambo ya siasa. Lakini watawala wa kimabavu hawaheshimu takwa la Biblia kwamba Wakristo hawapaswi kuwa sehemu ya ulimwengu.

Sababu ya jambo hilo ilielezwa kwenye mkutano uliofanywa kwenye Chuo Kikuu cha Heidelberg, Ujerumani, mnamo Novemba 2000. Mkutano huo ulikuwa na kichwa: “Kuonewa na Kujitetea kwa Mashahidi wa Yehova Chini ya Utawala wa Kimabavu wa Nazi na Ukomunisti.” Dakt. Clemens Vollnhals wa Taasisi ya Hannah-Arendt ya Utafiti Kuhusu Utawala wa Kimabavu alisema hivi: “Watawala wa kimabavu hawaridhiki na siasa tu bali wanadai mtu ajitiishe kwao kabisa.”

Wakristo wa kweli hawawezi ‘kujitiisha kabisa’ kwa serikali za wanadamu, kwa kuwa wameazimia kuwa waaminifu kwa Yehova Mungu pekee. Mashahidi wanaoishi chini ya tawala za kimabavu wameona kwamba nyakati nyingine madai ya Serikali na matakwa ya imani yao yanapingana. Wamefanya nini nyakati kama hizo? Tangu zamani, Mashahidi wa Yehova wamefuata kanuni hii ambayo wanafunzi wa Yesu Kristo walitaja: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.

Maelfu ya Mashahidi wamekuwa waaminifu kwa imani yao na hawajajihusisha na mambo ya kisiasa ijapokuwa wameteswa kikatili sana. Walivumiliaje? Walipataje nguvu ya kufanya hivyo? Acha wao wenyewe wajibu. Mashahidi na wasio Mashahidi wanaweza kujifunza nini kutokana na mambo waliyopitia?

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Mashahidi wa Yehova huko Ujerumani waliteswa kikatili na kwa muda mrefu chini ya serikali mbili kuu za kimabavu katika karne ya 20

[Blabu katika ukurasa wa 4]

“Watawala wa kimabavu hawaridhiki na siasa tu bali wanadai mtu ajitiishe kwao kabisa.”Dakt. Clemens Vollnhals

[Picha katika ukurasa wa 4]

Familia ya Kusserow walinyimwa uhuru wao kwa sababu walikataa kukana imani yao

[Picha katika ukurasa wa 4]

Johannes Harms aliuawa katika gereza la Nazi kwa sababu ya imani yake