Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtumaini Yehova kwa Moyo Wako Wote

Mtumaini Yehova kwa Moyo Wako Wote

Mtumaini Yehova kwa Moyo Wako Wote

“Wakujuao jina lako wakutumaini Wewe.”—ZABURI 9:10.

1, 2. Ni mambo gani yasiyofaa ambayo watu hutumaini ili kupata usalama?

KWA sababu kuna mambo mengi yanayohatarisha hali yetu leo, ni kawaida kutafuta mtu anayeweza kutulinda au kitu kinachoweza kutulinda. Watu wengine hufikiri kwamba wakati wao ujao utakuwa salama wakiwa na pesa nyingi, lakini kwa kweli, pesa hazitegemeki. Biblia husema: “Azitegemeaye mali zake ataanguka.” (Mithali 11:28) Wengine huwategemea viongozi wa kibinadamu, lakini hata viongozi bora hukosea na hatimaye, wote hufa. Kwa hekima, Biblia husema: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.” (Zaburi 146:3) Maneno hayo yaliyoandikwa kwa mwongozo wa Mungu yanatuonya tusitumaini jitihada zetu wenyewe. Sisi pia ni “binadamu.”

2 Nabii Isaya aliwashutumu viongozi wa taifa la Israeli wa wakati wake kwa sababu walitumaini “maneno ya uongo kuwa kimbilio.” (Isaya 28:15-17) Walitafuta usalama kwa kushirikiana kisiasa na mataifa jirani. Ushirikiano huo haukutegemeka—ulikuwa wa uongo. Vivyo hivyo, viongozi wengi wa kidini leo hushirikiana na viongozi wa kisiasa. Ushirikiano huo pia utakuwa wa “uongo.” (Ufunuo 17:16, 17) Hautaleta usalama wa kudumu.

Yoshua na Kalebu Walikuwa Vielelezo Bora

3, 4. Habari iliyoletwa na Yoshua na Kalebu ilitofautianaje na ya wale wapelelezi wengine kumi?

3 Basi tumtegemee nani ili kupata usalama? Tumtegemee yule ambaye Yoshua na Kalebu walimtegemea siku za Musa. Baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka Misri, walikuwa tayari kuingia Kanaani, Nchi ya Ahadi. Watu 12 walitumwa kuipeleleza nchi hiyo na baada ya siku 40, walileta habari. Ni Yoshua na Kalebu tu walioleta habari nzuri kuhusu nchi ya Kanaani ambayo Waisraeli walitarajia kumiliki. Wengine walikubali kwamba nchi hiyo ilikuwa yenye kupendeza lakini wakasema: “Watu wanaokaa katika nchi ile ni hodari, na miji yao ina maboma, nayo ni makubwa sana . . . Hatuwezi kupanda tupigane na watu hawa; kwa maana wana nguvu kuliko sisi.”—Hesabu 13:27, 28, 31.

4 Waisraeli waliwasikiliza wale wapelelezi kumi wakaogopa, na kuanza kumnung’unikia Musa. Hatimaye, Yoshua na Kalebu wakasema hivi kwa hisia nyingi: “Nchi ile tuliyopita kati yake ili kuipeleleza, ni nchi njema mno ya ajabu. Ikiwa BWANA anatufurahia, atatuingiza katika nchi hii atupe iwe yetu, nayo ni nchi yenye wingi wa maziwa na asali. Lakini msimwasi BWANA, wala msiwaogope wale wenyeji wa nchi.” (Hesabu 14:6-9) Hata hivyo, Waisraeli hawakusikiliza na hivyo hawakuruhusiwa kuingia katika Nchi ya Ahadi wakati huo.

5. Kwa nini Yoshua na Kalebu walileta habari nzuri?

5 Kwa nini Yoshua na Kalebu walileta habari nzuri, huku wapelelezi wengine kumi wakileta habari mbaya? Wapelelezi wote 12 waliona miji ileile yenye maboma na mataifa yaleyale. Wale wapelelezi kumi hawakukosea waliposema kwamba Waisraeli hawakuwa na nguvu za kutosha kuwashinda wakazi wa nchi hiyo. Yoshua na Kalebu walijua hivyo pia. Hata hivyo, wale kumi waliona mambo kwa maoni ya kibinadamu. Kwa upande mwingine, Yoshua na Kalebu walimtumaini Yehova. Walikuwa wameona matendo yake yenye nguvu huko Misri, kwenye Bahari Nyekundu, na chini ya Mlima Sinai. Miaka mingi baadaye habari za matendo hayo zilimchochea Rahabu aliyeishi Yeriko kuhatarisha maisha yake kwa ajili ya watu wa Yehova! (Yoshua 2:1-24; 6:22-25) Yoshua na Kalebu, walioshuhudia matendo hayo ya Yehova, walikuwa na uhakika kabisa kwamba Mungu angeendelea kuwapigania watu wake. Miaka 40 baadaye, tumaini lao lilitimizwa wakati kizazi kipya cha Waisraeli, chini ya uongozi wa Yoshua, kilipoingia Kanaani na kuwashinda wakazi wa nchi hiyo.

Kwa Nini Tumtumaini Yehova Kabisa?

6. Kwa nini Wakristo wanakabili majaribu leo, na wanapaswa kumtumaini nani?

6 Kama Waisraeli tunakabili maadui wenye nguvu kuliko sisi, katika ‘nyakati hizi hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.’ (2 Timotheo 3:1) Tunajaribiwa kimaadili, kiroho, na nyakati nyingine hata kimwili. Hatuwezi kushinda majaribu hayo kwa uwezo wetu, kwa kuwa yanasababishwa na Shetani Ibilisi ambaye ana nguvu zinazozidi za wanadamu. (Waefeso 6:12; 1 Yohana 5:19) Basi, tumtumaini nani? Mtu mwaminifu wa kale alisali hivi kwa Yehova: “Wakujuao jina lako wakutumaini Wewe.” (Zaburi 9:10) Tukimjua Yehova kikweli na kuelewa maana ya jina lake, tutamtumaini kabisa kama Yoshua na Kalebu.—Yohana 17:3.

7, 8. (a) Uumbaji hutusaidiaje kumtumaini Yehova? (b) Biblia hutupa sababu gani za kumtumaini Yehova?

7 Kwa nini tumtumaini Yehova? Yoshua na Kalebu walimtumaini kwa sababu waliona matendo yake yenye nguvu. Sisi pia tumeyaona. Kwa mfano, fikiria uumbaji wa Yehova, kutia ndani ulimwengu, na mabilioni ya magalaksi ya nyota. Nguvu nyingi sana za asili ambazo Yehova anadhibiti zinaonyesha kwamba yeye ni Mweza-Yote. Tunapotafakari maajabu ya uumbaji, hatuna budi kukubaliana na Ayubu aliyesema hivi kumhusu Yehova: “Ni nani awezaye kumzuia? Ni nani awezaye kumwuliza, Wafanya nini?” (Ayubu 9:12) Kwa kweli, ikiwa Yehova yuko upande wetu, hatuhitaji kumwogopa yeyote ulimwenguni.—Waroma 8:31.

8 Fikiria pia Neno la Yehova, Biblia. Kitabu hiki chenye hekima isiyo na kikomo kina nguvu za kutusaidia kushinda mazoea mabaya na kuishi kupatana na mapenzi ya Yehova. (Waebrania 4:12) Biblia hutusaidia kujua jina la Yehova na maana yake. (Kutoka 3:14) Tunatambua kwamba Yehova akipenda anaweza kuwa Baba mwenye upendo, Hakimu mwadilifu, Shujaa mshindi, ili kutimiza makusudi yake. Tunaona jinsi neno lake hutimia. Tunapojifunza Neno la Mungu, tunachochewa kusema kama mtunga-zaburi: “Nalitumainia neno lako.”—Zaburi 119:42; Isaya 40:8.

9. Fidia na ufufuo wa Yesu huimarishaje tumaini letu katika Yehova?

9 Sababu nyingine inayotufanya tumtumaini Yehova ni fidia. (Mathayo 20:28) Ni jambo lenye kupendeza sana kwamba Mungu alimtuma Mwanawe ili afe akiwa fidia kwa ajili yetu. Ama kweli fidia hutimiza mengi. Hufunika dhambi za wanadamu wote wanaotubu na kumgeukia Yehova kwa moyo mnyoofu. (Yohana 3:16; Waebrania 6:10; 1 Yohana 4:16, 19) Ilimbidi Yesu afe na kufufuliwa ili kulipia fidia. Muujiza huo ulioshuhudiwa na mamia ya watu hufanya pia tumtumaini Yehova. Hutuhakikishia kwamba matumaini yetu yatatimizwa.—Matendo 17:31; Waroma 5:5; 1 Wakorintho 15:3-8.

10. Tuna sababu zipi za kibinafsi za kumtumaini Yehova?

10 Hizo ni baadhi ya sababu zinazofanya tumtumaini Yehova kabisa. Kuna sababu nyingine nyingi, hata za kibinafsi. Kwa mfano, mara kwa mara sote hukabili hali ngumu maishani. Tunapojitahidi kuzitatua kwa mwongozo wa Yehova, tunapata faida za kufuata mwongozo huo. (Yakobo 1:5-8) Kadiri tunavyomtegemea Yehova kila siku maishani na kuona manufaa ya kufanya hivyo, ndivyo tumaini letu litakavyoimarika zaidi.

Daudi Alimtumaini Yehova

11. Daudi alimtumaini Yehova chini ya hali gani?

11 Daudi wa Israeli la kale alimtumaini Yehova. Daudi alitishwa na Mfalme Sauli aliyetaka kumuua, na alikabili pia jeshi lenye nguvu la Wafilisti waliojaribu kushinda Israeli. Na bado aliokoka na hata akashinda. Kwa nini? Daudi aeleza: “BWANA ni nuru yangu na wokovu wangu, nimwogope nani? BWANA ni ngome ya uzima wangu, nimhofu nani?” (Zaburi 27:1) Sisi pia tutafanikiwa tukimtumaini Yehova.

12, 13. Daudi alionyeshaje kwamba tunapaswa kumtumaini Yehova hata wapinzani wakitumia ndimi zao kama silaha dhidi yetu?

12 Pindi moja Daudi alisali: “Mungu, uisikie sauti yangu katika malalamiko yangu; unilinde uhai wangu na hofu ya adui. Utanificha mbali na shauri la siri la watenda mabaya, mbali na ghasia ya watu wafanyao maovu; waliounoa ulimi wao kama upanga, wameielekeza mishale yao, maneno ya uchungu, wapate kumpiga mkamilifu faraghani.” (Zaburi 64:1-4) Hatujui kwa uhakika kilichomfanya Daudi aandike maneno hayo. Lakini tunajua kwamba leo, wapinzani ‘huunoa ulimi wao,’ wakitumia maneno kama silaha. ‘Wanawapiga’ Wakristo wakamilifu wakitumia maneno au vichapo kama “mishale” na kufanya watu watuelewe vibaya. Tukimtumaini Yehova bila kuyumba-yumba, matokeo yatakuwa nini?

13 Daudi aendelea kusema: “Mungu atawapiga shabaha, kwa mshale mara watapigwa. Ndivyo watakavyokwazwa, ulimi wao wenyewe ukishindana nao. . . . Mwenye haki atamfurahia BWANA na kumkimbilia.” (Zaburi 64:7-10) Naam, maadui wajaponoa ulimi wao dhidi yetu, mwishowe, ‘ulimi wao wenyewe utashindana nao.’ Hatimaye Yehova hubadili mambo ili wanaomtumaini wamfurahie.

Tumaini la Hezekia Lilitimizwa

14. (a) Hezekia alimtumaini Yehova alipokabili hatari gani? (b) Hezekia alionyeshaje kwamba hakuamini uongo wa Ashuru?

14 Vilevile, tumaini la Mfalme Hezekia kwa Yehova lilitimizwa. Wakati wa utawala wa Hezekia, jeshi lenye nguvu la Ashuru lilitisha Yerusalemu. Jeshi hilo lilishinda mataifa mengi. Hata lilikuwa limeshinda miji ya Yuda isipokuwa Yerusalemu. Senakeribu alijigamba kwamba angeshinda jiji hilo pia. Kupitia Rabshake, alisema kwa usahihi kwamba ingekuwa kazi bure kutumaini Misri ili kupata msaada. Hata hivyo, alisema: “Asikudanganye Mungu wako unayemtumaini, akisema, Yerusalemu hautatiwa katika mikono ya mfalme wa Ashuru.” (Isaya 37:10) Hata hivyo, Hezekia alijua kwamba Yehova si mdanganyifu. Kwa hiyo alisali hivi: “BWANA, Mungu wetu, utuokoe na mkono wake [Ashuru], falme zote za dunia zipate kujua ya kuwa wewe ndiwe BWANA, wewe peke yako.” (Isaya 37:20) Yehova alisikiliza sala ya Hezekia. Malaika mmoja aliua wanajeshi 185,000 wa Ashuru usiku mmoja. Jiji la Yerusalemu halikuharibiwa, naye Senakeribu hakurudi tena nchini Yuda. Wote waliosikia tukio hilo walitambua ukuu wa Yehova.

15. Ni nini tu kinachoweza kutusaidia kukabiliana na hali yoyote ngumu inayoweza kutokea katika ulimwengu huu wenye msukosuko?

15 Leo pia tunakabili hali ya kivita kama Hezekia. Vita vyetu ni vya kiroho. Tukiwa wapiganaji wa kiroho, tunahitaji kujifunza mbinu za kujilinda. Tunapaswa kutarajia mashambulizi na kuwa tayari kukabiliana nayo. (Waefeso 6:11, 12, 17) Mambo yanaweza kubadilika ghafula katika ulimwengu huu wenye msukosuko. Mgogoro wa kijamii unaweza kutokea ghafula. Nchi zilizokuwa na uhuru wa ibada zinaweza kuchukizwa na dini. Tutakuwa tayari kukabiliana na jambo lolote linaloweza kutokea iwapo tutamtumaini Yehova kabisa kama Hezekia bila kuyumba-yumba.

Kumtumaini Yehova Humaanisha Nini?

16, 17. Tunaonyeshaje kwamba tunamtumaini Yehova?

16 Hatuwezi kumtumaini Yehova kwa maneno tu. Ni lazima tumtumaini kutoka moyoni na kuonyesha hivyo kwa matendo. Tukimtumaini Yehova, tutalitumaini kabisa Neno lake, Biblia. Tutalisoma na kulitafakari kila siku na kuliruhusu liongoze maisha yetu. (Zaburi 119:105) Kumtumaini Yehova kunahusisha pia kutumaini nguvu za roho takatifu. Kwa msaada wa roho takatifu, tunaweza kukuza sifa zinazompendeza Yehova na kuacha mazoea mabaya yaliyotia mizizi. (1 Wakorintho 6:11; Wagalatia 5:22-24) Kwa msaada wa roho takatifu, wengi wameacha kuvuta sigara au kutumia dawa za kulevya. Wengine wameacha maisha yasiyo ya adili. Naam, tunapomtumaini Yehova, tunategemea uwezo wake wala si wetu.—Waefeso 3:14-18.

17 Kumtumaini Yehova humaanisha pia kuwatumaini wale anaowatumaini. Kwa mfano, Yehova amemweka “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ashughulikie mambo ya Ufalme duniani. (Mathayo 24:45-47) Tunatumaini mipango ya Yehova na hivyo hatujitegemei wala kumpuuza mtumwa huyo aliyewekwa rasmi. Pia, kuna wazee wanaotumika katika makutaniko ya Kikristo, na mtume Paulo alisema wamewekwa rasmi na roho takatifu. (Matendo 20:28) Sisi huonyesha kwamba tunamtumaini Yehova kwa kuunga mkono mpango wa kuwa na wazee katika makutaniko.—Waebrania 13:17.

Fuata Kielelezo cha Paulo

18. Wakristo hufuataje kielelezo cha Paulo leo, lakini hawatumaini nini?

18 Mtume Paulo alikabili mikazo mingi katika huduma yake kama tunayokabili. Katika siku zake, wenye mamlaka walielezwa habari zisizo za kweli kuhusu Ukristo. Nyakati nyingine Paulo alijaribu kusahihisha maoni hayo yasiyo ya kweli au kuthibitisha kisheria kazi ya kuhubiri. (Matendo 28:19-22; Wafilipi 1:7) Wakristo hufuata kielelezo chake leo. Iwezekanapo, tunatumia njia yoyote ile kuwajulisha wengine kuhusu kazi yetu. Nasi hujitahidi kutetea na kuthibitisha kisheria habari njema. Hata hivyo, hatutumaini kabisa jitihada hizo kwa kuwa twajua kwamba kufanikiwa au kutofanikiwa kwetu hakutegemei kushinda kesi mahakamani au kusifiwa na vyombo vya habari. Badala yake, tunamtumaini Yehova. Tunakumbuka kitia-moyo ambacho Yehova aliwapa Waisraeli wa kale: “Nguvu zenu zitakuwa katika kutulia na kutumaini.”—Isaya 30:15.

19. Mateso yameimarishaje tumaini la ndugu zetu katika Yehova?

19 Nyakati za kisasa, kazi yetu imepigwa marufuku au imewekewa vizuizi Ulaya Mashariki na Magharibi, nchi fulani za Asia na Afrika, na nchi nyingine za Amerika Kusini na Kaskazini. Je, hii yamaanisha kwamba tumaini letu katika Yehova limekuwa bure? La. Ingawa nyakati nyingine ameruhusu tuteswe vikali akiwa na sababu nzuri, kwa upendo Yehova amewaimarisha wale ambao wamevumilia mateso hayo. Wakristo wengi wamekuza imani na tumaini thabiti katika Mungu kwa kuvumilia mateso.

20. Ingawa tunaweza kunufaika kwa kutambuliwa kisheria, hatuwezi kamwe kufanya nini?

20 Hata hivyo, katika nchi nyingi tunatambuliwa kisheria na wakati mwingine tunasifiwa na vyombo vya habari. Tunashukuru kwamba jambo hilo hutusaidia kutimiza kusudi la Yehova. Tukiwa na kibali cha Yehova, tunatumia uhuru huo kumtumikia waziwazi na kikamili badala ya kujitafutia mambo makuu maishani. Hatuwezi kamwe kuvunja msimamo wetu wa kutokuwamo, kupunguza bidii yetu ya kuhubiri, au kumtumikia Yehova kwa moyo nusu-nusu ili tusifiwe tu na wenye mamlaka. Sisi ni raia wa Ufalme wa Kimesiya na tunatetea kabisa enzi kuu ya Yehova. Hatuutumaini mfumo huu wa mambo, bali ulimwengu mpya. Katika ulimwengu mpya, Ufalme wa Kimesiya wa mbinguni ndio utakaokuwa serikali pekee itakayotawala dunia. Serikali hiyo haiwezi kutikiswa au kuangushwa kutoka mbinguni kwa mabomu, makombora au kushambuliwa kwa silaha za nyukilia. Haiwezi kushindwa na itatimiza kusudi la Yehova.—Danieli 2:44; Waebrania 12:28; Ufunuo 6:2.

21. Tumeazimia kufanya nini?

21 Paulo asema: “Sisi si namna irudiyo nyuma kwenye uangamivu, bali namna iliyo na imani kuelekea kuhifadhi hai nafsi.” (Waebrania 10:39) Sote na tumtumikie Yehova kwa uaminifu hadi mwisho. Tuna kila sababu ya kumtumaini Yehova kabisa sasa na kwa umilele.—Zaburi 37:3; 125:1.

Umejifunza Nini?

• Kwa nini Yoshua na Kalebu walileta habari nzuri?

• Tuna sababu zipi za kumtumaini Yehova kabisa?

• Kumtumaini Yehova humaanisha nini?

• Tumeazimia kufanya nini huku tukimtumaini Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kwa nini Yoshua na Kalebu walileta habari nzuri?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Uumbaji huimarisha tumaini letu katika Yehova

[Hisani]

All three images: Courtesy of Anglo-Australian Observatory, photograph by David Malin

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kumtumaini Yehova humaanisha kuwatumaini wale anaowatumaini