Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walishinda Licha ya Mateso

Walishinda Licha ya Mateso

Walishinda Licha ya Mateso

FRIEDA JESS alizaliwa mwaka wa 1911 nchini Denmark, na baadaye yeye na wazazi wake wakahamia Husum kaskazini mwa Ujerumani. Miaka mingi baadaye alipata kazi Magdeburg, na mwaka wa 1930 akabatizwa akawa Mwanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Baada ya Hitler kuanza kutawala mwaka wa 1933, Frieda aliteseka kwa muda wa miaka 23 chini ya tawala mbili za kimabavu.

Mnamo Machi 1933, serikali ya Ujerumani ilipanga kuwe na uchaguzi. Mwanahistoria Dakt. Detlef Garbe, msimamizi wa Jumba la Makumbusho la Kambi ya Mateso ya Neuengamme, karibu na Hamburg, anasema hivi: “Wanazi walitaka kuwalazimisha watu wote wampigie Adolf Hitler kura, aliyekuwa mtawala na kiongozi wao.” Mashahidi wa Yehova walitii himizo la Yesu la kutounga mkono upande wowote wa mambo ya siasa na kutokuwa “sehemu ya ulimwengu,” kwa hiyo, hawakupiga kura. Matokeo yalikuwa nini? Mashahidi walipigwa marufuku.—Yohana 17:16.

Frieda aliendelea na shughuli zake za Kikristo kisirisiri, hata alisaidia kuchapa magazeti ya Mnara wa Mlinzi. Alisema hivi: “Baadhi ya magazeti yaliingizwa kwenye kambi za mateso kisiri kwa ajili ya waamini wenzetu.” Alikamatwa mwaka wa 1940 na kuhojiwa na Gestapo, kisha akafungwa kifungo cha upweke kwa miezi kadhaa. Alivumiliaje? Anasema: “Sala ilinisaidia sana. Nilianza kusali asubuhi na mapema na nilisali mara nyingi kwa siku. Niliimarishwa niliposali na nikasaidiwa nisiwe na wasiwasi kupita kiasi.”—Wafilipi 4:6, 7.

Frieda aliachiliwa, lakini akakamatwa tena na Gestapo mwaka wa 1944. Wakati huu alihukumiwa kifungo cha miaka saba katika gereza la Waldheim. Frieda anaongeza: “Walinzi wa gereza walinipa kazi ya kusafisha bafu na vyoo nikiwa pamoja na wanawake wengine. Mara nyingi nilifanya kazi pamoja na mfungwa mwenzangu kutoka Chekoslovakia. Kwa hiyo, niliongea naye sana kumhusu Yehova na kuhusu imani yangu. Mazungumzo hayo yaliniimarisha.”

Kuachiliwa, Lakini kwa Muda Tu

Wanajeshi wa Sovieti waliwaachilia wafungwa katika gereza la Waldheim mnamo Mei 1945. Frieda akawa huru kurudi Magdeburg kuendelea na utumishi wake, lakini kwa muda mfupi tu. Mashahidi walionewa tena, lakini wakati huu walionewa na watu wenye mamlaka ya eneo lililotekwa na Sovieti. Gerald Hacke wa Taasisi ya Hannah-Arendt ya Utafiti Kuhusu Utawala wa Kimabavu anaandika hivi: “Mashahidi wa Yehova ni mojawapo ya mashirika machache yaliyoendelea kuteswa na tawala zote mbili za kimabavu nchini Ujerumani.”

Kwa nini walionewa tena? Kwa mara nyingine, walionewa kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote wa mambo ya siasa. Serikali ya Ujerumani Mashariki iliagiza watu wapige kura mwaka wa 1948. Hacke anaeleza hivi: “Sababu kuu iliyofanya [Mashahidi wa Yehova wateswe] ilikuwa kwamba hawakupiga kura.” Mashahidi wa Yehova walipigwa marufuku huko Ujerumani Mashariki mnamo Agosti 1950. Wengi walikamatwa, kutia ndani Frieda.

Frieda alijikuta tena mahakamani na akahukumiwa kifungo cha miaka sita. “Wakati huu nilikuwa pamoja na waamini wenzangu, na kushirikiana nao kulinisaidia sana.” Baada ya kuachiliwa huru mwaka wa 1956, alihamia Ujerumani Magharibi. Sasa, Frieda aliye na miaka 90 anaishi Husum, na bado anamtumikia Yehova, Mungu wa kweli.

Frieda aliteswa kwa miaka 23 chini ya tawala mbili za kimabavu. “Wanazi walijaribu kuniangamiza; Wakomunisti nao wakajaribu kuniponda roho. Nilipataje nguvu ya kuvumilia? Nilijifunza Biblia kwa bidii nilipokuwa huru, nilisali nilipokuwa peke yangu, nilishirikiana na waamini wenzangu ilipowezekana, na niliongea na wengine kuhusu imani yangu nafasi ilipopatikana.”

Ufashisti Nchini Hungaria

Mashahidi wa Yehova walionewa kwa miaka mingi nchini Hungaria pia. Baadhi yao waliteswa na tawala tatu za kimabavu. Ádám Szinger alikuwa mmoja wao. Ádám alizaliwa huko Paks, Hungaria, mwaka wa 1922 na alilelewa na wazazi Waprotestanti. Wanafunzi wa Biblia walimtembelea Ádám nyumbani kwake mwaka wa 1937, na mara moja akapendezwa na ujumbe wao. Kile ambacho alijifunza katika Biblia kilimsadikisha kwamba mafundisho ya kanisa lake hayakupatana na Biblia. Kwa hiyo aliacha Kanisa la Protestanti, kisha akajiunga na Wanafunzi wa Biblia katika huduma yao.

Ufashisti ulikuwa ukipata nguvu nchini Hungaria. Mara kadhaa polisi walimwona Ádám akihubiri nyumba kwa nyumba, na kumkamata ili wamhoji. Mashahidi walizidi kukandamizwa, na kazi yao ikapigwa marufuku mwaka wa 1939. Ádám alikamatwa mwaka wa 1942, akapelekwa gerezani, na kupigwa vibaya sana. Ni nini kilichomsaidia kijana mwenye umri wa miaka 19 kuvumilia mateso na kufungwa kwa miezi mingi gerezani? “Nilipokuwa ningali nyumbani, nilijifunza Biblia kindani na kuelewa vizuri makusudi ya Yehova.” Baada ya kuachiliwa kutoka gerezani ndipo Ádám alipobatizwa akawa Shahidi wa Yehova. Alibatizwa usiku mmoja mnamo Agosti 1942, katika mto ulio karibu na nyumba yao.

Katika Gereza Nchini Hungaria na Katika Kambi za Kazi Ngumu Nchini Serbia

Wakati vita ya pili ya ulimwengu ilipokuwa ikiendelea, Hungaria ilijiunga na Ujerumani kupinga Muungano wa Sovieti, na mwishoni mwa mwaka wa 1942 Ádám aliitwa kujiandikisha jeshini. Anasema hivi: “Niliwaambia kwamba singekubali kuwa mwanajeshi kwa sababu ya yale ambayo nilikuwa nimejifunza katika Biblia. Nikaeleza msimamo wangu wa kutounga mkono upande wowote.” Alihukumiwa kifungo cha miaka 11. Lakini Ádám hakukaa huko Hungaria kwa muda mrefu.

Mwaka wa 1943, Mashahidi wa Yehova 160 hivi walikusanywa na wakaingizwa katika meli ya mizigo iliyosafiri kwenye Mto Danube na wakapelekwa hadi Serbia. Ádám alikuwa mmoja wao. Wakiwa huko Serbia, wafungwa hao walikuwa chini ya utawala wa Nazi. Walifungwa katika kambi ya kazi ngumu huko Bor na kulazimishwa kufanya kazi katika migodi ya shaba. Mwaka mmoja hivi baadaye, wakarudishwa Hungaria, ambapo Ádám aliachiliwa na wanajeshi wa Sovieti mapema mwaka wa 1945.

Hungaria Yatawaliwa na Wakomunisti

Lakini uhuru haukudumu kwa muda mrefu. Mwishoni mwa mwaka wa 1940, Wakomunisti wenye mamlaka walizuia kazi ya Mashahidi wa Yehova, kama vile tu Wafashisti walivyofanya kabla ya vita. Kufikia mwaka wa 1952, Ádám alikuwa na umri wa miaka 29, na alikuwa ameoa na akapata watoto wawili. Mwaka huo alikamatwa na kushtakiwa alipokataa tena kujiandikisha jeshini. Ádám alijitetea hivi mahakamani: “Hii si mara yangu ya kwanza kukataa kujiandikisha jeshini. Wakati wa vita nilifungwa gerezani kwa sababu hiyohiyo, kisha nikahamishwa Serbia. Sikubali kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri yangu. Mimi ni Shahidi wa Yehova, na siwezi kuunga mkono upande wowote wa siasa.” Ádám alihukumiwa kifungo cha miaka minane gerezani, baadaye kikapunguzwa kuwa miaka minne.

Ádám alizidi kuonewa hadi katikati ya miaka ya 1970, hiyo ikiwa zaidi ya miaka 35 baada ya Wanafunzi wa Biblia kuwatembelea wazazi wake kwa mara ya kwanza. Katika kipindi hicho chote, mahakama sita zilimhukumu vifungo mbalimbali vya jumla ya miaka 23 katika angalau magereza na kambi kumi. Alivumilia mateso ambayo yaliendelezwa na tawala tatu, yaani, Wafashisti wa kabla ya vita ya pili ya ulimwengu nchini Hungaria, Wanazi nchini Serbia, na Wakomunisti wakati wa vita baridi nchini Hungaria.

Ádám angali anaishi mjini kwao, Paks, akimtumikia Mungu kwa uaminifu. Je, ana vipawa visivyo vya kawaida ambavyo vilimwezesha kuvumilia magumu kwa ushindi? La. Anaeleza:

“Funzo la Biblia, sala, na kushirikiana na waamini wenzangu, yalikuwa mambo muhimu. Lakini ningependa kukazia mambo mengine mawili. Kwanza, Yehova ndiye Chanzo cha nguvu. Uhusiano wa karibu naye ulikuwa msaada mkubwa kwangu. Na pili, nilikumbuka sura ya 12 ya Waroma, inayosema hivi: ‘Msijilipizie kisasi.’ Kwa hiyo, sikuweka kinyongo kamwe. Mara nyingi nilikuwa na nafasi ya kulipiza kisasi, lakini sikufanya hivyo kamwe. Hatupaswi kutumia nguvu ambayo Yehova anatupatia kulipa ovu kwa ovu.”

Mateso Yote Yatakoma

Sasa Frieda na Ádám wanaweza kumwabudu Yehova kwa uhuru. Hata hivyo, mambo waliyopitia yanafunua nini kuhusu mateso ya kidini? Kwamba kuwatesa Wakristo wa kweli kwa sababu ya imani yao hakutafua dafu. Ijapokuwa mali nyingi zilitumiwa kuwatesa vikali Mashahidi wa Yehova, watesaji hawakufaulu kutimiza lengo lao. Leo, Mashahidi wa Yehova wanaendelea kuongezeka huko Ulaya ambapo tawala zile mbili kuu za kimabavu zilitawala.

Mashahidi walitendaje walipoteswa? Kama vile masimulizi yao yanavyoonyesha, Frieda na Ádám walifuata ushauri huu wa Biblia: “Usijiache mwenyewe ushindwe na lililo ovu, bali fuliza kushinda lililo ovu kwa lililo jema.” (Waroma 12:21) Je, kwa kweli wema unaweza kushinda uovu? Ndiyo, wema pamoja na imani yenye nguvu katika Mungu vyaweza kushinda uovu. Mashahidi wa Yehova walishinda mateso huko Ulaya kwa nguvu ya roho ya Mungu. Jambo hilo linaonyesha matokeo mema ya imani ya Wakristo wanyenyekevu inayotokana na roho takatifu. (Wagalatia 5:22, 23) Hilo ni jambo ambalo watu wote katika ulimwengu huu wenye jeuri wanaweza kulifikiria kwa uzito.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Frieda Jess (sasa Thiele) alipokamatwa na wakati huu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ádám Szinger alipofungwa na wakati huu