Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Jipeni Moyo! Mimi Nimeushinda Ulimwengu”

“Jipeni Moyo! Mimi Nimeushinda Ulimwengu”

“Jipeni Moyo! Mimi Nimeushinda Ulimwengu”

SIKU ambayo Yesu alikufa—Nisani 14 kulingana na kalenda ya Wayahudi—ilianza Alhamisi, Machi 31, mwaka wa 33 W.K. baada ya jua kutua. Jioni hiyo, Yesu na mitume wake walikusanyika kwenye chumba cha juu katika nyumba fulani huko Yerusalemu ili kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa. Alipokuwa akijitayarisha “kuhama kutoka katika ulimwengu huu kwenda kwa Baba,” Yesu alionyesha kwamba aliwapenda mitume wake hadi mwisho. (Yohana 13:1) Jinsi gani? Kwa kuwafundisha mambo mazuri sana na hivyo kuwatayarisha kwa ajili ya yale ambayo yangewapata baadaye.

Baadaye usiku huo, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Alimaanisha nini kwa maneno hayo ya ujasiri? Alimaanisha hivi kwa sehemu: ‘Maovu ya ulimwengu hayakunitia uchungu wala kufanya nitake kulipiza kisasi. Sikuruhusu ulimwengu unibadili nifuate njia zake. Nyinyi pia mnaweza kufanya hivyo.’ Mambo ambayo Yesu aliwafundisha mitume wake waaminifu saa chache kabla ya kufa yangewasaidia pia waushinde ulimwengu.

Uovu umeenea sana duniani leo. Tunafanyaje kunapokuwa na ukosefu wa haki na jeuri isiyo na sababu? Je, mambo hayo hututia uchungu au hufanya tutake kulipiza kisasi? Tunaathiriwaje na kuzorota kwa maadili leo? Zaidi ya hayo, tunahitaji kupigana na ulimwengu mwovu, hali yetu ya kutokamilika, na maelekeo yenye dhambi. Je, kweli tunaweza kutarajia kushinda bila msaada wa Mungu? Tunawezaje kupata msaada wake? Tunahitaji kusitawisha sifa gani ili kushinda maelekeo yetu ya kimwili? Ili kupata majibu, na tuone yale ambayo Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wapendwa siku yake ya mwisho duniani.

Shinda Kiburi kwa Unyenyekevu

Kwa mfano, fikiria tatizo la kiburi au majivuno. Biblia inasema hivi kuhusu sifa hiyo: “Kiburi hutangulia uangamivu; na roho yenye kutakabari [“majivuno,” NW] hutangulia maanguko.” (Mithali 16:18) Maandiko pia yanatushauri hivi: “Ikiwa yeyote afikiri yeye ni kitu wakati yeye si kitu, anadanganya akili yake mwenyewe.” (Wagalatia 6:3) Naam, kiburi huleta madhara na hupotosha. Ni jambo la hekima kuchukia “kiburi na majivuno.”—Mithali 8:13.

Je, mitume wa Yesu walikuwa na tatizo la kiburi na majivuno? Wakati mmoja, walibishana ni nani kati yao aliyekuwa mkuu zaidi. (Marko 9:33-37) Pindi nyingine, Yakobo na Yohana waliomba wapewe vyeo maarufu katika Ufalme. (Marko 10:35-45) Yesu alitaka sana kuwasaidia wanafunzi wake waepuke mwelekeo huo. Hivyo walipokuwa wakila mlo wa Sikukuu ya Kupitwa, Yesu alisimama, akajifunga taulo kiunoni, akaanza kuwaosha miguu. Alihakikisha kwamba wameelewa kabisa jambo alilotaka kuwafundisha. Yesu aliwaambia hivi: “Ikiwa mimi, nijapokuwa Bwana na Mwalimu, niliosha miguu yenu, nyinyi pia mwapaswa kuoshana miguu.” (Yohana 13:14) Tunapaswa kusitawisha unyenyekevu badala ya kiburi.

Hata hivyo, si rahisi kushinda kiburi. Baadaye jioni hiyo, baada ya Yesu kumfukuza Yudasi Iskariote, aliyekuwa anataka kumsaliti, kulitokea mabishano makali kati ya mitume wake 11. Walibishania nini? Walitaka kujua ni nani kati yao aliye mkuu zaidi! Badala ya kuwagombeza, kwa subira Yesu alikazia tena umuhimu wa kuwatumikia wengine. Alisema: “Wafalme wa mataifa hupiga ubwana juu yao, na wale walio na mamlaka juu yao huitwa Wafadhili. Ingawa hivyo, nyinyi hampaswi kuwa hivyo. Lakini acheni yeye aliye mkubwa zaidi ya wote miongoni mwenu awe kama aliye mchanga zaidi ya wote, na yule anayetenda kama mkuu kama yule anayehudumu.” Akiwakumbusha mfano wake mwenyewe, anaendelea kusema hivi: “Mimi nimo katikati yenu kama yule anayehudumu.”—Luka 22:24-27.

Je, mitume walielewa mfano huo? Ndiyo, kwa kuwa miaka kadhaa baadaye mtume Petro aliandika hivi: “Nyinyi nyote mwe wenye akili zenye kufanana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na shauku ya kidugu, wenye huruma kwa njia ya wororo, wanyenyekevu katika akili.” (1 Petro 3:8) Ni muhimu kama nini sisi pia tushinde kiburi kwa unyenyekevu! Ni jambo la hekima kuepuka kufuatia umashuhuri, mamlaka, au cheo. Biblia inasema: “Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili isiyostahiliwa.” (Yakobo 4:6) Vivyo hivyo, mithali ya kale yenye hekima inasema: “Thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha BWANA ni utajiri, na heshima, nayo ni uzima.”—Mithali 22:4.

Unawezaje Kushinda Chuki?

Fikiria chuki ambayo imeenea sana ulimwenguni, iwe imesababishwa na woga, ujinga, upendeleo, uonevu, ukosefu wa haki, uzalendo, ukabila, au ubaguzi wa rangi. (2 Timotheo 3:1-4) Chuki pia ilikuwa imeenea sana siku za Yesu. Mbali na kuwachukia na kuwatenga wakusanya-kodi, Wayahudi pia hawakushirikiana na Wasamaria. (Yohana 4:9) Waliwadharau watu wa mataifa mengine. Hata hivyo, hatimaye ibada ambayo Yesu alianzisha ingehusisha watu kutoka kwa mataifa yote. (Matendo 10:34, 35; Wagalatia 3:28) Hivyo, kwa upendo Yesu aliwafundisha wanafunzi wake jambo jipya.

Yesu alisema: “Mimi ninawapa nyinyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile nimewapenda nyinyi, kwamba nyinyi pia mpendane.” Walipaswa kujizoeza kuonyesha upendo huo kwa kuwa aliendelea kusema: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35) Amri hiyo ilikuwa mpya kwa kuwa walitakiwa kufanya mengi zaidi ya ‘kuwapenda majirani wao kama nafsi yao.’ (Mambo ya Walawi 19:18) Katika njia gani? Yesu alifafanua jambo hilo kwa kusema: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile mimi nimewapenda nyinyi. Hakuna aliye na upendo mkubwa zaidi kuliko huu, kwamba mtu fulani aisalimishe nafsi yake kwa niaba ya marafiki wake.” (Yohana 15:12, 13) Kila mmoja wao angekuwa tayari kufa kwa ajili ya wengine.

Wanadamu wasio wakamilifu wanawezaje kuondoa chuki maishani mwao? Kwa kusitawisha upendo wa kujidhabihu badala ya chuki. Mamilioni ya watu wanyofu kutoka makabila, tamaduni, dini, na wenye maoni mbalimbali ya kisiasa, wanafanya hivyo. Wanafanywa kuwa jamii moja isiyo na chuki, yaani, udugu wa ulimwenguni pote wa Mashahidi wa Yehova. Wanatii maneno haya ambayo mtume Yohana aliongozwa na roho ya Mungu kuandika: “Kila mtu ambaye huchukia ndugu yake ni muua-binadamu-kikatili, nanyi mwajua kwamba hakuna muua-binadamu-kikatili aliye na uhai udumuo milele ukikaa katika yeye.” (1 Yohana 3:15) Wakristo wa kweli hawapigani katika vita yoyote bali hujitahidi sana kupendana.

Hata hivyo, tunapaswa kuwaonaje watu ambao si waamini wenzetu ambao huenda wakatuchukia? Alipokuwa kwenye mti wa mateso, Yesu alisali hivi kuhusu wale waliomwua: “Baba, wasamehe, kwa maana hawajui wanalofanya.” (Luka 23:34) Wakati watu waliojawa na chuki walipompiga Stefano kwa mawe, alisema hivi kabla ya kufa: “Yehova, usihesabu dhambi hii dhidi yao.” (Matendo 7:60) Yesu na Stefano waliwatakia mema hata wale waliowachukia. Hawakuwa na uchungu wowote mioyoni mwao. Biblia inatuhimiza hivi: “Acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote.”—Wagalatia 6:10.

‘Msaidiaji wa Milele’

Kwenye mkutano pamoja na mitume wake waaminifu 11, Yesu aliwajulisha kwamba baada ya muda mfupi hangekuwa pamoja nao tena kimwili. (Yohana 14:28; 16:28) Lakini aliwahakikishia hivi: “Nitamwomba Baba naye atawapa nyinyi msaidiaji mwingine awe pamoja nanyi milele.” (Yohana 14:16) Msaidiaji aliyeahidiwa ni roho takatifu ya Mungu. Ingewafundisha mambo mazito ya Maandiko na kuwakumbusha mambo ambayo Yesu alikuwa amewafundisha wakati wa huduma yake duniani.—Yohana 14:26.

Roho takatifu inaweza kutusaidiaje leo? Biblia, Neno la Mungu, iliandikwa kwa roho yake. Watu waliotumiwa kutoa unabii na kuiandika Biblia ‘walichukuliwa na roho takatifu.’ (2 Petro 1:20, 21; 2 Timotheo 3:16) Tunapojifunza Biblia na kufuata yale tunayojifunza tunakuwa na ujuzi, hekima, uelewevu, ufahamu, utambuzi, na uwezo wa kufikiri. Hivyo tunakuwa tayari kukabiliana na mikazo ya ulimwengu huu mwovu.

Roho takatifu pia hutusaidia kwa njia nyingine. Roho takatifu ya Mungu ni nguvu yenye kunufaisha nayo huwawezesha wale wanaokubali iwaongoze waonyeshe sifa za kimungu. Biblia inasema: “Matunda ya roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.” Tunahitaji sifa hizo ili kushinda maelekeo ya kimwili kuhusiana na ukosefu wa adili, zogo, wivu, hasira za ghafula, na mengineyo.—Wagalatia 5:19-23.

Kwa kutegemea roho ya Mungu tunaweza kupata pia “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili kukabiliana na magumu au huzuni yoyote ile. (2 Wakorintho 4:7) Ingawa huenda roho takatifu isituondolee majaribu au vishawishi, kwa hakika inaweza kutusaidia kuvumilia. (1 Wakorintho 10:13) Mtume Paulo aliandika: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.” (Wafilipi 4:13) Mungu hutupatia nguvu hiyo kupitia roho yake takatifu. Tunashukuru kama nini kwa roho hiyo! Wale ‘wanaompenda Yesu na kushika amri zake’ wameahidiwa roho hiyo.—Yohana 14:15.

“Kaeni Katika Upendo Wangu”

Usiku wake wa mwisho akiwa binadamu, Yesu pia aliwaambia mitume wake hivi: “Yeye aliye na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye ambaye hunipenda. Naye anipendaye mimi atapendwa na Baba yangu.” (Yohana 14:21) Aliwasihi hivi: “Kaeni katika upendo wangu.” (Yohana 15:9) Kukaa katika upendo wa Baba na wa Mwana kutatusaidiaje kupigana na maelekeo yenye dhambi na ulimwengu mwovu?

Je, kweli tunaweza kudhibiti maelekeo yetu yenye dhambi tusipokuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo? Sababu kubwa zaidi inayoweza kutuchochea kufanya hivyo ni tamaa ya kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu na Mwana wake. Ernesto, * mwanamume kijana aliyepambana vikali na maisha yake yasiyo ya adili tangu alipokuwa tineja, anasema hivi: “Nilitaka kumpendeza Mungu, na nilijifunza katika Biblia kwamba maisha yangu hayakumpendeza. Kwa hiyo nikaamua kubadilika na kuishi kulingana na viwango vyake. Kila siku, nilipambana na mawazo machafu na yasiyofaa yaliyojaa akilini mwangu. Lakini niliazimia kuyaondoa kabisa, hivyo nikasali kwa Mungu bila kukoma ili anisaidie. Baada ya miaka miwili mambo yaliboreka, ijapokuwa bado ninaendelea kujitia nidhamu.”

Ili kupigana na ulimwengu mwovu, fikiria sala ya mwisho ambayo Yesu alitoa kabla ya kuondoka kwenye chumba cha juu huko Yerusalemu. Kwa niaba ya wanafunzi wake, alisali hivi kwa Baba yake: “Nakuomba wewe, si uwachukue kutoka ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu. Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:15, 16) Sala hiyo inatia moyo kama nini! Yehova huwalinda wale anaowapenda na huwatia nguvu waendeleapo kujitenga na ulimwengu.

‘Dhihirisha Imani’

Kutii amri za Yesu kunaweza kutusaidia kushinda katika pambano letu dhidi ya ulimwengu mwovu na maelekeo yetu yenye dhambi. Ingawa ushindi huo ni muhimu, hauwezi kutuondolea ulimwengu mwovu au dhambi tuliyorithi. Lakini hatupaswi kukata tamaa.

Biblia inasema: “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.” (1 Yohana 2:17) Yesu alitoa uhai wake ili kukomboa “kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye” kutoka kwa dhambi na kifo. (Yohana 3:16) Tunapoendelea kupata ujuzi kuhusu mapenzi na makusudi ya Mungu, basi na tutii shauri hili la Yesu: “Dhihirisheni imani katika Mungu, dhihirisheni imani pia katika mimi.”—Yohana 14:1.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 22 Jina limebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 6, 7]

Yesu aliwahimiza mitume wake ‘wakae katika upendo wake’

[Picha katika ukurasa wa 7]

Hivi karibuni wanadamu watawekwa huru kutokana na dhambi na madhara yake