Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitahidi Kuwaona Wengine Kama Yehova Anavyowaona

Jitahidi Kuwaona Wengine Kama Yehova Anavyowaona

Jitahidi Kuwaona Wengine Kama Yehova Anavyowaona

“BWANA haangalii kama binadamu aangaliavyo.”—1 SAMWELI 16:7.

1, 2. Maoni ya Yehova kumhusu Eliabu yalitofautianaje na ya Samweli, na hilo linaweza kutufunza nini?

KATIKA karne ya 11 K.W.K., Yehova alimpa nabii Samweli mgawo wa siri. Alimwagiza nabii huyo aende kwa Yese na kumtia mafuta mmoja wa watoto wake wa kiume ili baadaye awe mfalme wa Israeli. Samweli alipomwona Eliabu, mzaliwa wa kwanza wa Yese, alikuwa na uhakika kwamba amempata mtu ambaye Mungu alikuwa amemchagua. Lakini Yehova akasema: “Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. BWANA haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” (1 Samweli 16:6, 7) Samweli hakumwona Eliabu kama Yehova alivyomwona. *

2 Ni rahisi sana kwa wanadamu kuwa na maoni yenye makosa kuwaelekea wengine. Kwa upande mmoja, huenda tukapumbazwa na watu ambao kwa nje wanaonekana kuwa wenye kuvutia lakini wasio na maadili. Kwa upande mwingine, tunaweza kuwa wakali na wagumu kuelekea watu wanyofu ambao huenda nyutu zao hazitupendezi.

3, 4. (a) Ikiwa tatizo litatokea kati ya Wakristo wawili, kila mmoja wao anapaswa kuazimia kufanya nini? (b) Tunapaswa kujiuliza maswali gani tunapogombana vikali na mwamini mwenzetu?

3 Matatizo yanaweza kutokea iwapo sisi ni wepesi kuwahukumu wengine, hata wale ambao tumewajua kwa muda mrefu. Huenda umegombana vikali na Mkristo ambaye alikuwa rafiki yako wa karibu. Je, ungependa kusuluhisha mambo? Ni nini kitakachokusaidia kufanya hivyo?

4 Mbona usitazame kwa makini sifa nzuri za ndugu au dada yako Mkristo? Fanya hivyo kwa kufikiria maneno haya ya Yesu: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” (Yohana 6:44) Kisha jiulize hivi: ‘Kwa nini Yehova alimvuta mtu huyo kwa Mwana Wake? Mtu huyo ana sifa gani nzuri? Je, nimekuwa nikipuuza sifa hizo au kukosa kuzitambua? Ni nini kilichofanya tuwe marafiki? Ni nini kilichonivuta kwake?’ Huenda mwanzoni ikawa vigumu kuona sifa zake nzuri, hasa ikiwa kwa muda fulani umekuwa na kinyongo kumwelekea. Hata hivyo, hiyo ni hatua muhimu ya kusuluhisha mambo kati yenu. Ili kuonyesha jinsi tunavyoweza kufanya hivyo, na tuchunguze sifa nzuri za watu wawili ambao mara kwa mara huonwa kwa njia isiyofaa. Hao ni nabii Yona na mtume Petro.

Kumtazama Yona kwa Unyofu

5. Yona alipewa mgawo gani, naye alifanya nini?

5 Yona alikuwa nabii katika ufalme wa kaskazini wa Israeli katika siku za Mfalme Yeroboamu wa Pili, mwana wa Yoashi. (2 Wafalme 14:23-25) Siku moja, Yehova alimwagiza Yona aondoke Israeli na kusafiri kwenda Ninawi, mji mkuu wa Milki ya Ashuru yenye nguvu. Alipewa mgawo gani? Akawaonye Waninawi kwamba mji wao mkubwa ungeharibiwa. (Yona 1:1, 2) Badala ya kufuata maagizo ya Mungu, Yona alitoroka! Akapanda meli iliyokuwa inasafiri kwenda Tarshishi, mbali sana na Ninawi.—Yona 1:3.

6. Kwa nini Yehova alimchagua Yona kwenda Ninawi?

6 Ni nini huja akilini mwako unapomfikiria Yona? Je, unamwona kuwa nabii asiyetii? Maoni ya kijuujuu yanaweza kufanya ufikiri alikuwa nabii asiyetii. Bila shaka, Mungu hangemchagua nabii asiyetii. Ni lazima Yona awe alikuwa na sifa fulani nzuri. Fikiria sifa zake akiwa nabii.

7. Yona alimtumikia Yehova chini ya hali gani huko Israeli, na kufahamu hilo kunaathirije maoni yako kumhusu?

7 Yona alikuwa amefanya kazi ngumu kwa uaminifu huko Israeli, eneo lisilokuwa na matokeo. Nabii Amosi aliyeishi karibu wakati mmoja na Yona, alisema kwamba siku hizo Waisraeli walipenda vitu vya kimwili na anasa. * Uovu ulikuwa umeenea sana nchini, lakini Waisraeli hawakujali hata kidogo. (Amosi 3:13-15; 4:4; 6:4-6) Hata hivyo, Yona aliendelea kwa uaminifu na mgawo wake wa kuwahubiria. Ikiwa wewe ni mhubiri wa habari njema, unajua jinsi ilivyo vigumu kuzungumza na watu ambao wameridhika na maisha na wasiojali. Hivyo basi, ingawa Yona alikuwa na udhaifu, tusisahau uaminifu wake na uvumilivu wake alipowahubiria Waisraeli wasio na imani.

8. Ni magumu gani ambayo yangemkabili nabii Mwisraeli huko Ninawi?

8 Mgawo wake wa kwenda Ninawi ulikuwa mgumu hata zaidi. Ili kufika kwenye jiji hilo, Yona alilazimika kutembea umbali wa kilometa 800 hivi, safari yenye kuchosha ambayo ingechukua angalau muda wa mwezi mmoja. Akiwa huko, nabii huyo angelazimika kuwahubiria Waashuru waliokuwa wakatili. Mara nyingi vita vyao vilitia ndani mateso ya kinyama. Hata walijivunia ukatili wao. Si ajabu kwamba Ninawi uliitwa “mji wa damu”!—Nahumu 3:1, 7.

9. Yona alionyesha sifa gani tufani kubwa ilipotisha mabaharia?

9 Yona hakutaka kutii agizo la Yehova, hivyo akapanda meli iliyompeleka mbali sana na mahali alipotumwa. Hata hivyo, Yehova hakumwacha wala kutuma nabii mwingine badala ya Yona, bali alijaribu kumsaidia aone umuhimu wa mgawo wake. Mungu alisababisha tufani kubwa baharini. Meli iliyombeba Yona ilipeperushwa huku na huko na mawimbi. Watu wasio na hatia walikuwa karibu kuangamia kwa sababu ya Yona! (Yona 1:4) Yona angefanyaje? Kwa kuwa hakutaka mabaharia waliokuwa katika meli hiyo waangamie kwa sababu yake, Yona aliwaambia hivi: “Nikamateni, mnitupe baharini; basi bahari itatulia.” (Yona 1:12) Hatimaye, mabaharia walipomtupa baharini, Yona hangetarajia Yehova amwokoe. (Yona 1:15) Hata hivyo, Yona alikuwa tayari kufa ili mabaharia hao wasiangamie. Kwa kufanya hivyo, yeye alionyesha kwamba alikuwa na ujasiri, unyenyekevu, na upendo.

10. Ni nini kilichotukia Yehova alipomtuma tena nabii Yona?

10 Hatimaye, Yehova alimwokoa Yona. Je, mambo ambayo Yona alikuwa ametenda karibuni yangefanya asistahili tena kuwa mwakilishi wa Mungu? La, kwa huruma na upendo, Yehova alimtuma tena nabii huyo kuwahubiria Waninawi. Yona alipofika Ninawi, aliwatangazia wakazi wake kwa ujasiri kwamba Mungu alikuwa ameuona uovu wao mwingi na kwamba mji wao ungeharibiwa baada ya siku 40. (Yona 1:2; 3:4) Waninawi waliposikia ujumbe wa Yona uliokuwa wazi, walitubu na mji wao haukuangamizwa.

11. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yona alijifunza somo muhimu?

11 Bado Yona hakuwa na maoni yanayofaa. Ingawa hivyo, Yehova alitumia mfano unaofaa, na kwa subira akamsaidia Yona afahamu kwamba Yeye haangalii sura ya nje bali huchunguza moyo. (Yona 4:5-11) Masimulizi ya unyofu ya Yona yanaonyesha kwamba alijifunza somo muhimu. Sababu nyingine inayothibitisha kwamba Yona alikuwa mnyenyekevu ni kule kukubali kuandika hata mambo madogo-madogo yenye kuaibisha kuhusu kasoro zake. Ujasiri unahitajiwa ili kukubali makosa!

12. (a) Tunajuaje kwamba Yesu ana maoni kama ya Yehova kuwahusu wanadamu? (b) Tunatiwa moyo tuwe na maoni gani kuhusu watu tunaohubiria habari njema? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 18.)

12 Karne nyingi baadaye, Yesu Kristo alitaja tukio moja lenye kutia moyo katika maisha ya Yona. Alisema: “Kama vile Yona alivyokuwa katika tumbo la samaki mkubwa mno siku tatu mchana na usiku, ndivyo Mwana wa binadamu atakavyokuwa katika moyo wa dunia siku tatu mchana na usiku.” (Mathayo 12:40) Yona atakapofufuliwa, atapata kujua kwamba Yesu alilinganisha wakati ambao Yeye alikuwa kaburini na wakati ambao Yona alikuwa katika tumbo la samaki. Je, hatufurahi kumtumikia Mungu ambaye hawaachi watumishi wake wanapokosea? Mtunga-zaburi aliandika: “Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo BWANA anavyowahurumia wamchao. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:13, 14) Kwa kweli, “mavumbi” hayo, yanayotia ndani wanadamu wasio wakamilifu leo, yanaweza kutimiza mengi kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu!

Maoni Yanayofaa Kumhusu Petro

13. Ni kasoro gani za Petro ambazo huenda ukakumbuka, lakini kwa nini Yesu alimchagua kuwa mtume?

13 Hebu tuzungumzie kwa ufupi mfano wa pili unaohusu mtume Petro. Kama ungeulizwa ueleze Petro alikuwa mtu wa aina gani, je, ungesema mara moja kwamba alikuwa mtu mwenye kutenda bila kufikiri au hata mwenye kimbelembele? Mara kwa mara Petro alitenda hivyo. Lakini je, Yesu angemchagua Petro kuwa mmoja wa mitume wake 12 iwapo kwa kweli Petro alitenda bila kufikiri au alikuwa mwenye kimbelembele? (Luka 6:12-14) La, hasha! Yesu hakuzingatia kasoro za Petro bali sifa zake nzuri.

14. (a) Ni mambo gani ambayo huenda yalifanya Petro awe mwepesi wa kusema? (b) Kwa nini tunapaswa kushukuru kwamba Petro aliuliza maswali mara kwa mara?

14 Mara kwa mara Petro alizungumza kwa niaba ya mitume wengine. Huenda watu fulani wakaona hilo kuwa ukosefu wa kiasi. Lakini hivyo ndivyo ilivyokuwa kweli? Wengine husema kwamba huenda Petro alikuwa na umri mkubwa kuliko mitume wenzake, labda hata kuliko Yesu mwenyewe. Ikiwa ndivyo ilivyo, huenda hiyo ndiyo sababu mara nyingi Petro alikuwa mwepesi wa kusema. (Mathayo 16:22) Hata hivyo, kuna jambo jingine tunalopaswa kufikiria. Petro alikuwa mtu wa kiroho. Tamaa yake ya kutaka kujua mengi ilimchochea kuuliza maswali. Maswali yake yametunufaisha. Yesu alisema mambo kadhaa muhimu alipojibu maswali ya Petro, nayo yameandikwa katika Biblia. Kwa mfano, alizungumza kuhusu “msimamizi-nyumba mwaminifu” alipokuwa akijibu swali la Petro. (Luka 12:41-44) Pia fikiria swali hili la Petro: “Sisi tumeacha vitu vyote na kukufuata wewe; kwa kweli kutakuwa nini kwa ajili yetu?” Swali hilo lilifanya Yesu atoe ahadi hii yenye kuimarisha: “Kila mtu ambaye ameziacha nyumba au kuacha akina ndugu au akina dada au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili ya jina langu atapokea mara nyingi zaidi naye atarithi uhai udumuo milele.”—Mathayo 15:15; 18:21, 22; 19:27-29.

15. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Petro alikuwa mshikamanifu kikweli?

15 Petro alikuwa na sifa nyingine nzuri ya ushikamanifu. Wanafunzi wengi walipoacha kumfuata Yesu kwa kukosa kuelewa mojawapo ya mafundisho yake, Petro ndiye aliyezungumza kwa niaba ya wale mitume 12 na kusema: “Bwana, tutaenda zetu kwa nani? Wewe una semi za uhai udumuo milele.” (Yohana 6:66-68) Bila shaka, maneno hayo yalimfurahisha Yesu sana. Baadaye, wakati umati wenye ghasia ulipokuja kumkamata Bwana-Mkubwa, wengi wa mitume wake walitoroka. Hata hivyo, Petro alifuata umati huo kwa mbali na kuingia katika ua wa kuhani wa cheo cha juu. Aliingia humo kwa sababu alikuwa na ujasiri wala si woga. Yesu alipokuwa akihojiwa, Petro alijiunga na kikundi cha Wayahudi ambao walikuwa wakiota moto uliokuwa ukiwaka. Mmoja wa watumishi wa kuhani wa cheo cha juu alimtambua na kumshtaki kwamba alikuwa na Yesu. Naam, Petro alimkana Bwana-Mkubwa wake, lakini tusisahau kwamba alijikuta katika hali hiyo hatari kwa sababu alikuwa mshikamanifu kwa Yesu na alimjali. Mitume wengine hawakuwa na ujasiri wa kukabili hali hiyo.—Yohana 18:15-27.

16. Ni kwa sababu gani ifaayo tumezungumzia sifa nzuri za Yona na Petro?

16 Sifa nzuri za Petro zilikuwa nyingi kuliko kasoro zake. Na ndivyo na Yona. Tofauti na vile ambavyo kwa kawaida tungewaona Yona na Petro, tumejitahidi kuona sifa zao nzuri. Vivyo hivyo, tunapaswa kujizoeza kuwaona ndugu na dada zetu wa kiroho inavyofaa. Tukifanya hivyo tutakuwa na mahusiano mazuri nao. Kwa nini tuwe na maoni yanayofaa kuhusu ndugu na dada zetu?

Kutumia Habari Hiyo Leo

17, 18. (a) Kwa nini huenda Wakristo wakakosa kuelewana? (b) Ni shauri gani la Biblia linaloweza kutusaidia kutatua matatizo kati yetu na waamini wenzetu?

17 Leo wanaume, wanawake, na watoto wa hali zote za uchumi, elimu na jamii wanamtumikia Yehova kwa umoja. (Ufunuo 7:9, 10) Katika kutaniko la Kikristo kuna watu wenye nyutu mbalimbali. Kwa kuwa tunashirikiana kwa ukaribu tunapomtumikia Mungu, bila shaka nyakati nyingine kutatokea mkwaruzano.—Waroma 12:10; Wafilipi 2:3.

18 Ingawa tutaona kasoro za ndugu zetu, hatutazikazia fikira. Tunajitahidi kumwiga Yehova, ambaye mtunga-zaburi aliimba hivi kumhusu: “BWANA, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Badala ya kukazia fikira kasoro zinazoweza kutugawanya, ‘tunafuatia mambo yafanyayo kuwe na amani na mambo yaliyo ya kujengana.’ (Waroma 14:19) Tunajitahidi kuwaona watu kama Yehova anavyowaona na badala ya kuzingatia kasoro zao, sisi hukazia fikira sifa zao nzuri. Kufanya hivyo hutusaidia ‘twendelee kuchukuliana mtu na mwenzake.’—Wakolosai 3:13.

19. Taja hatua zinazofaa ambazo huenda Mkristo akachukua kutatua hali mbaya ya kutoelewana.

19 Namna gani ikiwa hali za kutoelewana zenye kutusumbua zitatokea ambazo hatuwezi kutatua? (Zaburi 4:4) Je, hali kama hiyo imetokea kati yako na mwamini mwenzako? Mbona usijitahidi kulitatua? (Mwanzo 32:13-15) Kwanza, mfikie Yehova kwa sala, ukimwomba akuongoze. Kisha, kwa kuzingatia sifa nzuri za mwamini huyo, mfikie “kwa upole ulio wa hekima.” (Yakobo 3:13) Mwambie kwamba unataka msuluhishe jambo hilo. Kumbuka shauri hili lililoongozwa kwa roho ya Mungu: ‘Uwe mwepesi sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema, wa polepole juu ya hasira ya kisasi.’ (Yakobo 1:19) Shauri hilo la kuwa “wa polepole juu ya hasira ya kisasi” lamaanisha kwamba huenda mwenzako akatenda au kusema jambo linaloweza kukukasirisha. Jambo hilo likitokea mwombe Yehova akusaidie uwe mwenye kujidhibiti. (Wagalatia 5:22, 23) Mpatie ndugu yako nafasi ajieleze na umsikilize kwa makini. Usimkatize hata kama hukubaliani na yote anayosema. Huenda akawa na maoni yenye makosa, lakini bado hayo ni maoni yake. Jaribu kuliona tatizo hilo jinsi anavyoliona. Huenda hiyo ikatia ndani kujiona kama vile anavyokuona.—Mithali 18:17.

20. Tunapotatua tofauti kati yetu, ni hatua zipi zinazoweza kutusaidia tupatane?

20 Nafasi yako ya kuzungumza inapofika, sema kwa neema. (Wakolosai 4:6) Mtajie ndugu yako sifa zake zinazokupendeza. Omba msamaha kwa lolote ambalo huenda ulifanya na kusababisha kutoelewana huko. Iwapo jitihada zako za unyenyekevu zitafanya mpatane, mshukuru Yehova. Zisipofaulu, endelea kuomba mwongozo wa Yehova huku ukitafuta fursa zaidi za kufanya amani.—Waroma 12:18.

21. Mazungumzo haya yamekusaidiaje kuwaona wengine kama Yehova anavyowaona?

21 Yehova anawapenda watumishi wake wote. Anafurahia kututumia sisi sote katika utumishi wake licha ya kasoro zetu. Upendo wetu kwa ndugu na dada zetu utaongezeka tunapojifunza mengi zaidi juu ya jinsi anavyowaona wengine. Iwapo upendo wetu kwa Mkristo mwenzetu umepoa, unaweza kuchochewa tena. Tutabarikiwa sana tukijitahidi kuwa na maoni yanayofaa kuelekea wengine. Naam, kuwaona kama Yehova anavyowaona.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Baadaye ilidhihirika kwamba Eliabu hakuwa na sifa zinazofaa kuwa mfalme wa Israeli hata ingawa alikuwa na sura nzuri. Eliabu pamoja na Waisraeli wengine walijikunyata kwa woga wakati jitu la Wafilisti, Goliathi, lilipowaita Waisraeli wakapigane.—1 Samweli 17:11, 28-30.

^ fu. 7 Yeroboamu wa Pili alizidisha utajiri wa ufalme wa kaskazini kutokana na ushindi mkubwa aliopata, kurudishwa kwa maeneo yaliyokuwa yametekwa, na ushuru ambao yaelekea alikusanya.—2 Samweli 8:6; 2 Wafalme 14:23-28; 2 Mambo ya Nyakati 8:3, 4; Amosi 6:2.

Ungejibuje?

• Yehova anazionaje kasoro za watumishi wake waaminifu?

• Yona na Petro walikuwa na sifa gani nzuri?

• Umeazimia kuwa na maoni gani kuwahusu ndugu zako Wakristo?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 18]

Fikiria Jinsi Mungu Anavyowaona Wengine

Unapotafakari masimulizi ya Biblia kuhusu Yona, je, unaona uhitaji wa kubadili maoni yako kuhusu watu unaowahubiria habari njema kwa ukawaida? Kama Waisraeli, huenda watu hao wakaonekana kuwa wameridhika na maisha na wasiojali, au huenda wakawa wenye kupinga ujumbe wa Mungu. Lakini Yehova Mungu anawaonaje? Huenda siku moja, hata watu fulani mashuhuri katika mfumo huu wa mambo wakamgeukia Yehova kama vile mfalme wa Ninawi alivyotubu baada ya kuhubiriwa na Yona.—Yona 3:6, 7.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Je, unawaona wengine kama Yehova anavyowaona?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yesu alizungumzia tukio fulani lenye kutia moyo katika maisha ya Yona