Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kabla na Baada ya Maisha Yake Kubadilika Kabisa

Kabla na Baada ya Maisha Yake Kubadilika Kabisa

“Mkaribieni Mungu, Naye Atawakaribia”

Kabla na Baada ya Maisha Yake Kubadilika Kabisa

MAISHA ya Matsepang hayakuwa yenye furaha wala kusudi. Alikuwa msichana mdogo aliyeishi Lesotho, nchi iliyo katikati ya Afrika Kusini. Matsepang alikuwa Mkatoliki tangu utoto. Hata hivyo, badala ya kusaidiwa kumkaribia Mungu, kwa miaka mingi Matsepang alitendwa vibaya na watawa waliotumia pesa kumshawishi afanye mambo yasiyofaa kiadili.

Kwa sababu hiyo Matsepang alipoteza imani katika dini na hakuamini kwamba kuna Muumba mwenye upendo anayewajali wanadamu kikweli. Aliumia sana kihisia na kuhisi kwamba hafai kitu kwa sababu alitendwa vibaya kiadili na hakuna aliyemjali. Hivyo alipokua na kuwa mtu mzima, Matsepang alikuwa mwenye jeuri na mchokozi sana, na baadaye akawa mhalifu.

Hatimaye Matsepang alijiunga na genge lililoibia watu kwenye magari-moshi. Alikamatwa na kuhukumiwa kifungo gerezani huko Afrika Kusini. Baadaye, alirudishwa nyumbani kwao Lesotho, ambako aliendelea na uhalifu, ulevi, jeuri, na ukosefu wa maadili.

Matsepang alishuka moyo sana hivi kwamba alisali kwa bidii ili Mungu amsaidie. Alimwahidi hivi: “Mungu, nikiendelea kuwa hai, nitafanya yote niwezayo kukutumikia.”

Muda mfupi baadaye, Matsepang alitembelewa na mishonari ambao ni Mashahidi wa Yehova. Walijitolea kujifunza Biblia pamoja naye na kupitia funzo hilo, akatambua kwamba Mungu anajali. Pia alitambua kwamba Shetani, “baba ya uwongo,” hutumia mbinu za ujanja na za udanganyifu kufanya watu wajihisi kwamba hawafai na wafikiri ya kuwa Yehova hawezi kuwapenda kamwe.—Yohana 8:44; Waefeso 6:11.

Kwa upande mwingine, Matsepang alifarijika kama nini alipojifunza kwamba tunaweza kuwa watu wenye kuheshimika kiadili tukitubu dhambi zetu za awali, kumwomba Mungu atusamehe, na kujitahidi kumpendeza! Alisaidiwa kuelewa kwamba “Mungu ni mkubwa zaidi kuliko mioyo yetu” na hutuona kwa njia ambayo huenda ikawa tofauti sana na jinsi tunavyojiona.—1 Yohana 3:19, 20.

Matsepang alifurahi kusoma maneno haya ya mtunga-zaburi Daudi: “BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” (Zaburi 34:18) Akiwa ‘amepondeka roho,’ Matsepang alitambua kwamba Yehova hawaachi watumishi wake, hata wanaposhuka moyo au kuhisi kuwa hawafai. Alifurahi kujifunza kwamba Mungu huwajali kondoo zake wote na kuwategemeza wakati wa magumu. (Zaburi 55:22; 1 Petro 5:6, 7) Maneno haya, “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia,” yalimgusa moyo sana.—Yakobo 4:8.

Baada ya muda mfupi, ingeweza kuonekana kwamba nguvu za Neno la Mungu zilikuwa zimebadili maisha yake. Alianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na kuacha mazoea yasiyopatana na Maandiko. Ikawaje? Sasa anahisi kwamba Mungu anampenda na anamkubali. Tangu abatizwe kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, ametumia muda wa saa nyingi sana katika huduma ya Kikristo akiwa mtangazaji wa habari njema za Ufalme wa Mungu. Licha ya maumivu makali ya kihisia yaliyompata wakati uliopita, sasa Matsepang anaishi maisha yenye furaha na kusudi. Huo ni mfano mzuri kama nini unaoonyesha kwamba Biblia ina nguvu za kuboresha maisha!—Waebrania 4:12.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Mungu, nikiendelea kuwa hai, nitafanya yote niwezayo kukutumikia”

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Kanuni za Biblia Zinazofanya Kazi

Zifuatazo ni baadhi ya kanuni za Biblia ambazo zimewafariji watu waliotendwa vibaya:

“Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu, faraja zako [Mungu] zaifurahisha roho yangu.” (Zaburi 94:19) “Faraja” za Yehova zinazopatikana katika Neno lake hufariji sana. Tunapozitafakari na kusali tunasaidiwa kuondoa mawazo yenye kutusumbua na tunasitawisha tumaini katika Mungu ambaye ni Rafiki anayetujali.

“[Yehova] huwaponya waliopondeka moyo, na kuziganga jeraha zao.” (Zaburi 147:3) Tunaweza kumkaribia Yehova kwa uhakika bila kuhisi hatia moyoni iwapo tunashukuru kwa rehema na maandalizi yake ya kufunika dhambi zetu kwa dhabihu ya fidia ya Yesu. Jambo hilo linaweza kutuletea faraja na amani ya akili isiyo na kifani.

“Hakuna mtu awezaye kuja kwangu [Yesu Kristo] isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye; nami hakika nitamfufua siku ya mwisho.” (Yohana 6:44) Kupitia roho takatifu na kazi ya kuhubiri Ufalme, Yehova hutuvuta kwa Mwana wake na kutupatia tumaini la uhai udumuo milele.