Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakristo wa Mapema na Sheria ya Musa

Wakristo wa Mapema na Sheria ya Musa

Wakristo wa Mapema na Sheria ya Musa

“Sheria imekuwa mfunzi wetu ikiongoza kwa Kristo.”—WAGALATIA 3:24.

1, 2. Waisraeli waliofuata kwa makini Sheria ya Musa walipata faida gani?

KATIKA mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova aliwapa Waisraeli mfumo wa sheria. Aliwaambia kwamba iwapo wangetii sauti yake, angewabariki nao wangeishi maisha ya furaha na ya kuridhisha.—Kutoka 19:5, 6.

2 Mfumo huo wa Sheria, ulioitwa Sheria ya Musa, au “Sheria,” ulikuwa ‘mtakatifu na wa uadilifu na mwema.’ (Waroma 7:12) Uliwasaidia watu kuwa na sifa bora, kama vile fadhili, unyofu, maadili, na ujirani mwema. (Kutoka 23:4, 5; Mambo ya Walawi 19:14; Kumbukumbu la Torati 15:13-15; 22:10, 22) Sheria hiyo pia iliwachochea Wayahudi kupendana. (Mambo ya Walawi 19:18) Isitoshe, iliwakataza kuchangamana au kuoa wake wasio Wayahudi ambao hawakuwa chini ya Sheria hiyo. (Kumbukumbu la Torati 7:3, 4) Sheria ya Musa ilikuwa kama “ukuta” wa kuwatenganisha Wayahudi na wasio Wayahudi, nayo iliwazuia watu wa Mungu wasichafuliwe na fikira na mazoea ya Wapagani.—Waefeso 2:14, 15; Yohana 18:28.

3. Kwa kuwa hakuna mtu ambaye angefuata Sheria kikamilifu, matokeo yalikuwaje?

3 Lakini, hata Wayahudi waliokuwa makini zaidi hawakuweza kufuata Sheria ya Mungu kikamilifu. Je, Yehova alitarajia watimize mengi zaidi ya uwezo wao? La. Mojawapo ya sababu zilizofanya Waisraeli wapewe Sheria ilikuwa “kufanya makosa yawe wazi.” (Wagalatia 3:19) Sheria ilifanya Wayahudi wanyofu watambue kwamba walihitaji sana Mkombozi. Mkombozi huyo alipowasili, Wayahudi waaminifu walishangilia. Wakati wa kukombolewa kutoka kwa laana ya dhambi na kifo ulikuwa umekaribia!—Yohana 1:29.

4. Ni katika njia gani Sheria ilikuwa ‘mfunzi wa kuongoza kwa Kristo’?

4 Sheria ya Musa ilipaswa kuwa ya muda. Alipowaandikia Wakristo wenzake, mtume Paulo aliifafanua kuwa ‘mfunzi wa kuwaongoza kwa Kristo.’ (Wagalatia 3:24) Zamani, mfunzi alikuwa anawapeleka na kuwachukua watoto kutoka shuleni. Yeye hakuwa mwalimu, bali aliwapeleka tu watoto kwa mwalimu. Vivyo hivyo, Sheria ya Musa ilikusudiwa kuwaongoza Wayahudi waliomwogopa Mungu kwa Kristo. Yesu aliahidi kwamba angekuwa pamoja na wafuasi wake “siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:20) Kwa hiyo, kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, “mfunzi” huyo, yaani Sheria, hakuhitajiwa tena. (Waroma 10:4; Wagalatia 3:25) Haya hivyo, Wakristo fulani Wayahudi hawakuelewa mara moja ukweli huo muhimu. Kwa sababu hiyo, waliendelea kufuata matakwa fulani ya Sheria hata baada ya kufufuliwa kwa Yesu. Lakini wengine walirekebisha maoni yao. Kwa kufanya hivyo, walituwekea kielelezo bora. Hebu tuone walifanyaje hivyo.

Uelewevu Mpya Wenye Kusisimua Kuhusu Mafundisho ya Kikristo

5. Petro alipata maagizo gani katika maono, na kwa nini alishtuka?

5 Mnamo mwaka wa 36 W.K., mtume Mkristo Petro alipata maono yenye kustaajabisha. Wakati huo sauti kutoka mbinguni ilimwagiza achinje na kula ndege na wanyama walioonwa kuwa najisi kulingana na Sheria. Petro alishtuka! Hakuwa amewahi kamwe ‘kula kitu chochote kilichotiwa unajisi na kisicho safi.’ Lakini sauti hiyo ikamwambia: “Koma kuviita kuwa najisi vitu ambavyo Mungu ametakasa.” (Matendo 10:9-15) Badala ya kushikilia Sheria kishupavu, Petro alirekebisha maoni yake. Hilo lilimsaidia kuelewa mambo ya ajabu kuhusiana na makusudi ya Mungu.

6, 7. Ni nini kilichomfanya Petro akate kauli kwamba angeweza kuwahubiria watu wasio Wayahudi, na yaelekea alikata kauli gani nyingine?

6 Hivi ndivyo ilivyokuwa. Watu watatu walienda kwenye nyumba alikoishi Petro na kumwomba aende nao kwenye nyumba ya mtu asiye Myahudi aitwaye Kornelio ambaye hakuwa ametahiriwa. Petro aliwakaribisha watu hao nyumbani. Alipoelewa maana ya maono hayo, Petro aliondoka pamoja nao siku iliyofuata kwenda kwa nyumba ya Kornelio. Huko Petro alitoa ushahidi kamili kumhusu Yesu Kristo. Kisha akasema: “Kwa hakika nahisi kwamba Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” Kornelio pamoja na jamaa zake na marafiki wake wa karibu walidhihirisha imani katika Yesu, na “roho takatifu ikaangukia wote wale wenye kusikia lile neno.” Alipotambua kwamba jambo hilo lilitendeka kwa nguvu za Yehova, Petro ‘aliwaamuru wabatizwe katika jina la Yesu Kristo.’—Matendo 10:17-48.

7 Ni nini kilichomwezesha Petro akate kauli kwamba watu wasio Wayahudi ambao hawakuwa chini ya Sheria ya Musa wangeweza kuwa wafuasi wa Yesu Kristo? Ni utambuzi wa kiroho. Petro alitambua kwamba watu wasio Wayahudi ambao hawakuwa wametahiriwa wangeweza kubatizwa kwa kuwa Mungu alionyesha kwamba amewakubali kwa kuwamwagia roho yake. Wakati huohuo, yaelekea Petro alitambua kwamba Mungu hakuwatazamia Wakristo wasio Wayahudi wafuate Sheria ya Musa ili wastahili kubatizwa. Kama ungaliishi wakati huo, je, ungalikubali kurekebisha maoni yako kama Petro?

Wengine Waliendelea Kufuata “Mfunzi”

8. Baadhi ya Wakristo walioishi Yerusalemu walikuwa na maoni gani tofauti na ya Petro kuhusu tohara, na kwa nini?

8 Petro alienda Yerusalemu baada ya kuondoka nyumbani kwa Kornelio. Wanafunzi kadhaa Wayahudi katika kutaniko la Yerusalemu hawakufurahi waliposikia kwamba watu wasio Wayahudi ambao hawakuwa wametahiriwa walikuwa “wamepokea neno la Mungu.” (Matendo 11:1-3) Ingawa wale “waliokuwa wakiunga mkono kutahiriwa” walikubali kwamba watu wasio Wayahudi wangeweza kuwa wafuasi wa Yesu, bado walisisitiza kwamba watu hao walipaswa kufuata Sheria ili kuokolewa. Kwa upande mwingine, katika maeneo ya watu wasio Wayahudi, ambayo yalikuwa na Wakristo wachache Wayahudi, tohara haikuwa suala muhimu. Maoni hayo mawili tofauti yaliendelea kwa muda wa miaka 13 hivi. (1 Wakorintho 1:10) Hilo lilikuwa jaribu la imani lililoje kwa Wakristo hao wa mapema na hasa watu wasio Wayahudi walioishi katika maeneo yaliyokuwa na Wayahudi wengi!

9. Kwa nini ilikuwa muhimu kutatua suala la tohara?

9 Hatimaye suala hilo lilipamba moto mwaka wa 49 W.K. wakati Wakristo kutoka Yerusalemu walipokuja Antiokia ya Siria ambako Paulo alikuwa akihubiri. Walianza kufundisha kwamba watu wasio Wayahudi waliogeuzwa imani walipaswa kutahiriwa kulingana na Sheria. Ndipo kukatokea ugomvi mkali na mabishano kati yao na Paulo na Barnaba! Kama suala hilo halingetatuliwa, baadhi ya Wakristo hao, wawe Wayahudi au wasio Wayahudi, wangekwazwa. Hivyo, mipango ilifanywa ili Paulo na wengine wachache waende Yerusalemu na kuomba baraza linaloongoza la Kikristo litatue suala hilo kabisa.—Matendo 15:1, 2, 24.

Baada ya Mabishano Walipatana!

10. Baraza linaloongoza lilifikiria mambo gani kabla ya kufanya uamuzi kuhusu hali ya watu wasio Wayahudi?

10 Kwenye mkutano uliofanywa, yaelekea wengine waliunga mkono tohara huku wengine wakiipinga. Lakini hawakuacha hisia zao ziwaongoze. Baada ya kubishana sana, mtume Petro na Paulo walieleza ishara ambazo Yehova alikuwa amewafanyia watu wasiotahiriwa. Waliwaeleza kwamba Mungu alikuwa amewamwagia roho takatifu watu wasio Wayahudi ambao hawakuwa wametahiriwa. Ni kana kwamba waliwauliza, ‘Je, kwa kweli kutaniko la Kikristo linaweza kuwakataa watu ambao Mungu amewakubali?’ Ndipo mwanafunzi Yakobo akasoma Maandiko yaliyowasaidia wote waliohudhuria kuelewa mapenzi ya Yehova kuhusiana na suala hilo.—Matendo 15:4-17.

11. Ni jambo gani ambalo halikuhusishwa wakati uamuzi ulipofanywa kuhusu tohara, na ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova alibariki uamuzi huo?

11 Wote walingojea uamuzi wa baraza linaloongoza. Je, wangependelea tohara kwa sababu walikuwa Wayahudi? La. Wanaume hao waaminifu waliazimia kufuata Maandiko na mwongozo wa roho takatifu ya Mungu. Baada ya kusikiliza ushuhuda wote uliotolewa kuhusu suala hilo, washiriki wote katika baraza linaloongoza walikubali kwamba haikuwa lazima Wakristo wasio Wayahudi watahiriwe na kufuata Sheria ya Musa. Ndugu walipopata habari hizo walishangilia na makutaniko yakaanza “kuongezeka idadi siku baada ya siku.” Wakristo waliotii mwongozo wa kiroho uliokuwa wazi walipata jibu linalotegemea Maandiko! (Matendo 15:19-23, 28, 29; 16:1-5) Hata hivyo, kuna swali jingine muhimu ambalo halikuwa limejibiwa.

Namna Gani Wakristo Wayahudi?

12. Ni swali gani ambalo halikuwa limeshughulikiwa?

12 Baraza linaloongoza lilikuwa limeonyesha wazi kwamba haikuwa lazima Wakristo wasio Wayahudi watahiriwe. Lakini namna gani Wakristo Wayahudi? Washiriki wa baraza linaloongoza hawakuwa wameshughulikia swali hilo katika uamuzi wao.

13. Kwa nini lilikuwa kosa kusisitiza kwamba ilikuwa lazima kufuata Sheria ya Musa ili kuokolewa?

13 Baadhi ya Wayahudi Wakristo waliokuwa “wenye bidii kuhusu Sheria” waliendelea kuwatahiri watoto wao na kufuata matakwa fulani ya Sheria. (Matendo 21:20) Mbali na kutahiri watoto, wengine hata walisisitiza kwamba ni lazima Wakristo Wayahudi wafuate Sheria ili waokolewe. Walikuwa wamekosea sana kwa kufanya hivyo. Kwa mfano, Mkristo hangeweza kutoa dhabihu ya mnyama ili asamehewe dhambi. Dhabihu ya Kristo ilibatilisha dhabihu hizo. Namna gani takwa la Sheria kwamba Wayahudi wasishirikiane kwa ukaribu na watu wasio Wayahudi? Ingekuwa vigumu sana kwa waeneza-evanjeli wenye bidii kufuata matakwa hayo na bado waendelee na kazi yao ya kufundisha watu wasio Wayahudi mambo yote ambayo Yesu alikuwa amefundisha. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8; 10:28) * Hakuna uthibitisho kwamba jambo hilo lilifafanuliwa katika mkutano wa baraza linaloongoza. Hata hivyo, kutaniko halikuachwa bila msaada.

14. Barua ambazo Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika zilitoa mwongozo gani kuhusu Sheria?

14 Hawakupata mwongozo kupitia barua iliyotoka kwa baraza linaloongoza, bali kupitia barua nyingine ambazo mitume waliongozwa na roho kuandika. Kwa mfano, mtume Paulo aliwaandikia Wayahudi na watu wasio Wayahudi waliokuwa wakiishi Roma ujumbe wenye nguvu. Katika barua hiyo, alieleza kwamba Myahudi halisi ‘ni aliye hivyo kwa ndani, na tohara yake ni ile ya moyo kwa roho.’ (Waroma 2:28, 29) Katika barua hiyohiyo, Paulo alitumia mfano ili kuthibitisha kwamba Wakristo hawako chini ya Sheria. Alisema kwamba mwanamke hawezi kuolewa na wanaume wawili. Lakini ikiwa mume wake amekufa, yuko huru kuolewa tena. Kisha Paulo akatumia mfano kuonyesha kwamba Wakristo watiwa-mafuta hawawezi kuwa chini ya Sheria ya Musa na wakati huohuo wawe wafuasi wa Kristo. Walipaswa wawe “wafu kwa Sheria” ili waunganishwe na Kristo.—Waroma 7:1-5.

Hawakuelewa Haraka

15, 16. Kwa nini baadhi ya Wakristo Wayahudi walikosa kuelewa kwamba hawakuwa chini ya Sheria, na hilo laonyeshaje uhitaji wa kuwa macho kiroho?

15 Paulo alitoa hoja kuhusu Sheria kwa njia yenye kusadikisha. Kwa nini basi baadhi ya Wayahudi Wakristo walikosa kuelewa kwamba hawakuwa chini ya Sheria? Sababu moja ni kwamba walikosa ufahamu wa kiroho. Kwa mfano, walipuuza chakula kigumu cha kiroho. (Waebrania 5:11-14) Pia hawakuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. (Waebrania 10:23-25) Huenda sababu nyingine iliyofanya wengine wasielewe kwamba hawakuwa chini ya Sheria ni jinsi Sheria yenyewe ilivyokuwa. Sheria ilikazia vitu ambavyo wangeweza kuona na kugusa, kama vile hekalu na ukuhani. Ilikuwa rahisi mtu asiye wa kiroho kukubali Sheria kuliko kukubali kanuni zenye kina za Kikristo zilizotegemea mambo halisi yasiyoonekana.—2 Wakorintho 4:18.

16 Katika barua yake kwa Wagalatia Paulo alionyesha sababu nyingine iliyofanya wengine waliodai kuwa Wakristo watake kufuata Sheria. Alieleza kwamba watu hao walitaka waheshimiwe, na kuonwa kuwa wafuasi wa dini mashuhuri. Badala ya kuwa tofauti katika jamii, walikuwa tayari kufanya jambo lolote ili wakubaliwe na wengine. Walitaka hasa kibali cha wanadamu badala ya kibali cha Mungu.—Wagalatia 6:12.

17. Ni wakati gani maoni yanayofaa kuhusu kufuata sheria yalipoeleweka kikamili?

17 Wakristo wenye utambuzi ambao walijifunza mambo ambayo Paulo na wengine waliongozwa kwa roho ya Mungu kuandika, walifanya maamuzi yanayofaa kuhusu Sheria. Hata hivyo, kabla ya mwaka wa 70 W.K., si Wakristo wote Wayahudi walioelewa Sheria ya Musa kikamili. Walipata kuielewa kikamili wakati Mungu aliporuhusu Yerusalemu, hekalu lake, na rekodi za ukuhani ziharibiwe. Hilo lilifanya isiwezekane kwa yeyote kufuata matakwa yote ya Sheria.

Kutumia Habari Hiyo Leo

18, 19. (a) Ni mitazamo gani tunayopaswa kuwa nayo, na ni ipi tunayopaswa kuepuka ili kudumisha hali nzuri ya kiroho? (b) Mfano wa Paulo unatufunza nini kuhusu kufuata mwongozo tunaopata kutoka kwa ndugu wenye madaraka? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 24.)

18 Baada ya kuchunguza matukio hayo ya zamani, huenda ukajiuliza: ‘Kama ningaliishi wakati huo, ningaliitikiaje kufunuliwa hatua kwa hatua kwa mapenzi ya Mungu? Je, ningalisisitiza kufuata Sheria? Au ningalikuwa mwenye subira hadi wakati ambapo mambo yangeeleweka vizuri? Na yakieleweka, je, ningalikubali kwa moyo wote maoni mapya?’

19 Bila shaka, hatuwezi kuwa na hakika kuhusu jinsi ambavyo tungaliitikia kama tungaliishi wakati huo. Lakini tunaweza kujiuliza: ‘Ninaitikiaje leo kunapokuwa na uelewevu mpya wa Biblia? (Mathayo 24:45) Mwongozo wa Kimaandiko unapotolewa, je, ninajaribu kuufuata na kuelewa kusudi lake badala ya kushika tu sheria kama ilivyoandikwa? (1 Wakorintho 14:20) Je, ninamngoja Yehova kwa subira hata nisipojibiwa maswali yangu?’ Ni muhimu kutumia ifaavyo chakula cha kiroho kinachotolewa leo ili “tusipate kamwe kupeperushwa mbali.” (Waebrania 2:1) Na tusikilize kwa makini Yehova anapotoa mwongozo kupitia Neno lake, roho yake, na tengenezo lake la kidunia. Tukifanya hivyo, Yehova atatupatia uzima wa milele wenye kufurahisha na kuridhisha.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Petro alipotembelea Antiokia ya Siria, alifurahia ushirika mchangamfu pamoja na waamini wasio Wayahudi. Hata hivyo, Wakristo Wayahudi walipowasili kutoka Yerusalemu, Petro ‘alianza kujiondoa na kujitenga mwenyewe, kwa kuwahofu hao wa tabaka ya waliotahiriwa.’ Tunaweza kuwazia jinsi wageuzwa-imani hao wasio Wayahudi walivyoumia wakati mtume huyo aliyeheshimika alipokataa kula pamoja nao.—Wagalatia 2:11-13.

Ungejibuje?

• Ni katika njia gani Sheria ya Musa ilikuwa kama ‘mfunzi wa kuongoza kwa Kristo’?

• Eleza jinsi Petro na watu “waliokuwa wakiunga mkono kutahiriwa” walivyoitikia kwa njia tofauti uelewevu mpya wa ile kweli.

• Umejifunza nini kuhusu njia ambayo Yehova hufunua kweli leo?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]

Paulo Akabili Jaribu kwa Unyenyekevu

Baada ya safari ya umishonari iliyofanikiwa, Paulo aliwasili Yerusalemu mwaka wa 56 W.K. Huko alipatwa na jaribu fulani. Habari zilikuwa zimefika kutanikoni kwamba alikuwa akifundisha ya kuwa Sheria ilikuwa imebatilishwa. Wanaume wazee walihofu kwamba Wakristo Wayahudi waliokuwa wamegeuzwa imani karibuni wangekwazwa na jinsi Paulo alivyozungumza waziwazi kuhusu Sheria na huenda wangekata kauli kwamba Wakristo hawakuheshimu mipango ya Yehova. Katika kutaniko, kulikuwa na Wakristo Wayahudi wanne waliokuwa wameweka nadhiri, labda ya kuwa Wanadhiri. Walipaswa kwenda hekaluni ili kukamilisha matakwa ya nadhiri hiyo.

Wanaume wazee walimwomba Paulo aende hekaluni pamoja nao na kugharimia mahitaji yao. Paulo alikuwa ameongozwa na roho ya Mungu kuandika angalau barua mbili ambapo alisema kwamba haikuwa lazima kushika Sheria ili kuokolewa. Hata hivyo, alijali dhamiri za wengine. Alikuwa ameandika hivi awali: “Kwa wale walio chini ya sheria nilipata kuwa kama aliye chini ya sheria . . . ili niweze kuwapata wale walio chini ya sheria.” (1 Wakorintho 9:20-23) Ingawa hakuachilia mambo wakati kanuni za Kimaandiko zilipohusika, Paulo aliona kwamba angeweza kukubaliana na maoni ya wanaume wazee. (Matendo 21:15-26) Hakukosea kufanya hivyo. Mpango wa nadhiri haukupingana na Maandiko, nalo hekalu lilitumiwa kwa ajili ya ibada safi wala si ibada ya sanamu. Ili asiwakwaze wengine, Paulo alikubaliana na ombi la wanaume hao wazee. (1 Wakorintho 8:13) Yaelekea Paulo alihitaji sifa ya unyenyekevu ili kufanya hivyo, jambo linalofanya tumheshimu hata zaidi.

[Picha katika ukurasa wa 22, 23]

Kwa miaka kadhaa, Wakristo waliendelea kuwa na maoni yaliyotofautiana kuhusu Sheria ya Musa