Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Vijana Mnafanya Maendeleo ya Kiroho?

Je, Vijana Mnafanya Maendeleo ya Kiroho?

Je, Vijana Mnafanya Maendeleo ya Kiroho?

“IJAPOKUWA nilikuwa nikihudhuria mikutano ya Kikristo, sikutaka kumtumikia Yehova,” asema Hideo anapokumbuka wakati alipokuwa akimalizia shule ya msingi. “Mara nyingi niliwaza kwamba nilikuwa mtu anayependwa na wanadarasa wenzake, aliyetembea kwa madaha huku akiwa na rafiki yake wa kike. Sikuwa na miradi hususa, na sikutaka kufanya maendeleo yoyote ya kiroho.” Kama Hideo, yaelekea vijana wengi hujikalia tu, bila kutaka kutimiza miradi yoyote inayofaa au kufanya maendeleo yoyote.

Ikiwa wewe ni kijana, labda unasisimuka wakati unaposhiriki katika michezo au shughuli fulani ya kujifurahisha. Hata hivyo, huenda mambo ya kiroho hayakusisimui. Je, inawezekana kusisimuliwa na miradi ya kiroho? Fikiria maneno haya ya mtunga-zaburi: “Ushuhuda wa BWANA ni amini, humtia mjinga hekima.... Amri ya BWANA ni safi, huyatia macho nuru.” (Zaburi 19:7, 8) Neno la Mungu linaweza kumwongoza “mjinga” atende kwa hekima, na ‘kuyatia macho yake nuru.’ Naam, mambo ya kiroho yanaweza kukusisimua. Lakini unahitaji kufanya nini ili mambo ya kiroho yakusisimue? Utaanzia wapi?

Chochewa Kumtumikia Mungu

Kwanza, ni lazima uchochewe. Fikiria kisa cha Yosia, mfalme kijana wa Yuda. Kitabu cha Sheria ya Yehova kilipopatikana hekaluni, Yosia aliagiza kisomwe naye aliguswa moyo sana na mambo aliyosikia. Kwa sababu hiyo, ‘Yosia aliyaondolea mbali machukizo yote katika nchi zote zilizokuwa milki ya wana wa Israeli.’ (2 Mambo ya Nyakati 34:14-21, 33) Kusoma Neno la Mungu kulimchochea Yosia kutegemeza ibada safi.

Wewe pia unaweza kusitawisha tamaa ya kumtumikia Yehova iwapo utasoma Biblia na kutafakari yale unayosoma. Mambo hayo ndiyo yaliyomchochea Hideo. Alianza kushirikiana kwa ukaribu na painia mwenye umri mkubwa, mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Painia huyo alikuwa mwanafunzi wa Biblia mwenye bidii aliyejitahidi kufuata mambo aliyojifunza. Hideo alitiwa moyo sana na kielelezo cha painia huyo, akaanza kufuata yale aliyojifunza na kusitawisha tamaa ya kumtumikia Mungu na watu wengine. Maendeleo yake ya kiroho yalimsaidia kuwa na kusudi maishani.

Vijana wanaweza kuchochewa kwa kusoma Biblia kila siku. Takahiro anaeleza: “Kila mara nilipoenda kulala kisha nikakumbuka kwamba sikuwa nimesoma Biblia siku hiyo, Ningeamka na kuisoma. Kwa kufanya hivyo, nilihisi kwamba Yehova alikuwa akiniongoza. Kusoma Biblia kila siku kulichangia sana maendeleo yangu ya kiroho. Niliazimia kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova hivyo nikaanza upainia wa kawaida muda mfupi tu baada ya kumaliza shule ya sekondari. Nami nafurahia sana kufanya upainia.”

Mbali na kusoma Biblia, ni nini kingine kinachoweza kukuchochea kumsifu Yehova? Tomohiro alifundishwa kweli ya Biblia na mama yake. Anasema hivi: “Niliguswa moyo sana na upendo wa Yehova na dhabihu ya fidia ya Yesu baada ya kusoma kwa makini kitabu Life Does Have a Purpose nikiwa na umri wa miaka 19. Kuthamini upendo wa Mungu kulinichochea kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova.” (2 Wakorintho 5:14, 15) Kama Tomohiro vijana wengi wanatiwa moyo kufanya maendeleo ya kiroho kwa kuendelea kujifunza Biblia kwa bidii.

Hata hivyo, namna gani ikiwa bado huna tamaa ya kumtumikia Yehova? Ni nani anayeweza kukusaidia? Mtume Paulo aliandika: ‘Kwa maana Mungu ndiye anayetenda ndani yenu ili nyinyi mwe na nia na kutenda pia.’ (Wafilipi 2:13) Ukimwomba Yehova akusaidie, atakupatia kwa wingi roho yake takatifu, itakayokutia nguvu uwe na ‘nia’ na pia ‘utende.’ Hiyo inamaanisha kwamba roho takatifu ya Mungu itazidisha tamaa yako ya kufanya yote uwezayo katika utumishi wa Yehova na itakusaidia kukua kiroho. Kwa vyovyote, uwe na hakika kwamba Yehova atautia nguvu na kuuimarisha moyo wako!

Jiwekee Miradi

Ikiwa umeamua kumtumikia Yehova kikamili zaidi, unahitaji kujiwekea miradi ili ufanye maendeleo ya kiroho. Mana, msichana Mkristo alisema: “Kuweka miradi kulinisaidia sana. Badala ya kurudi nyuma, ningeweza kusonga mbele kwa ujasiri. Nilisali kwa Yehova kwa bidii ili aniongoze kutimiza miradi yangu, nami niliweza kufanya maendeleo bila kukengeushwa.”

Unapaswa kuweka miradi inayofaa na unayoweza kutimiza. Kati ya miradi unayoweza kutimiza ni kusoma sura moja ya Biblia kila siku. Unaweza pia kuanza mradi wa kufanya utafiti. Kwa mfano, kwa kutumia kichapo Watch Tower Publications Index ambacho kinapatikana katika Kiingereza, unaweza kujifunza sifa za Yehova ambazo zimeorodheshwa chini ya kichwa kidogo “Qualities by Name” (“Sifa Mojamoja”) chini ya kichwa kikuu “Jehovah” (“Yehova”) Kuna vichwa mbalimbali 40 ambavyo unaweza kuchunguza, na bila shaka utafiti huo utafanya uwe na uhusiano wa karibu na Yehova na utakuchochea kufanya mengi zaidi katika utumishi wake. Miradi mingine unayoweza kutimiza inatia ndani kutoa maelezo angalau mara moja kwenye mikutano ya Kikristo ambayo wahudhuriaji wanahitajika kushiriki, kujitahidi kujua vizuri angalau mshiriki mmoja wa kutaniko katika kila mkutano, kusali kwa Yehova kila siku, na kuwaeleza wengine kumhusu.

Unaweza kuweka mradi wa kujiunga na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ikiwa bado hujafanya hivyo. Je, umekuwa ukishiriki mahubiri? Ikiwa bado, basi huenda ukahitaji kujitahidi kuwa mhubiri asiyebatizwa. Baada ya kufanya hayo, hatua nyingine unayoweza kuchukua ni kufikiria kwa uzito uhusiano wako pamoja na Yehova na juu ya kujiweka wakfu kwake. Vijana wengi hujitahidi kuishi kupatana na wakfu wao kwa kujiunga na huduma ya wakati wote.

Ingawa ni vizuri kuwa na miradi maishani, jihadhari usisitawishe roho ya kushindana. Utafurahia zaidi mambo unayofanya usipojilinganisha na wengine.—Wagalatia 5:26; 6:4.

Huenda ukahisi kwamba huna uzoefu na ni vigumu kwako kuweka miradi ifaayo. Ikiwa ndivyo, basi fuata shauri hili la Biblia: “Tega sikio lako uyasikie maneno ya wenye hekima.” (Mithali 22:17) Omba msaada kutoka kwa wazazi wako au Wakristo wengine wakomavu. Bila shaka wazazi na watu wengineo wanahitaji kuwa wenye busara na wenye kutia moyo kuhusiana na hilo. Vijana wakihisi kwamba wanakazwa kutimiza miradi ambayo wamewekewa na wengine wanaweza kukosa furaha na hata huenda kuweka miradi kukakosa maana. Ilikuwa hivyo kwa msichana mmoja aliyesema: “Wazazi wangu waliniwekea mradi mmoja baada ya mwingine, kama vile kujiunga na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, kuhubiri, kubatizwa, na kuwa painia. Nilijitahidi sana kutimiza miradi hiyo yote. Badala ya kunipongeza baada ya kutimiza mradi fulani, wazazi wangu waliniwekea mradi mwingine. Kwa sababu hiyo sikuzote nilihisi ninalazimishwa kutimiza miradi. Nilichoka na kuhisi kwamba sikuwa ninatimiza chochote.” Tatizo lilikuwa nini? Miradi yote ilifaa lakini ilikuwa imewekwa na wengine. Ili ufaulu ni lazima wewe mwenyewe uchochewe kujiwekea miradi!

Mfikirie Yesu Kristo. Alipokuja duniani, alijua kile ambacho Yehova Baba yake alitazamia afanye. Yesu hakuona kufanya mapenzi ya Yehova kuwa mradi tu, bali mgawo aliopaswa kutimiza. Yesu aliuonaje mgawo wake? Alisema: “Chakula changu ni kwamba mimi nifanye mapenzi yake aliyenituma na kumaliza kazi yake.” (Yohana 4:34) Yesu alifurahia kufanya mapenzi ya Yehova na alifanya yale aliyotazamiwa na Baba yake afanye. Yesu aliona kufanya mapenzi ya Baba yake kama chakula naye alipata furaha na uradhi katika kutimiza mgawo aliopewa naye. (Waebrania 10:5-10) Wewe pia unaweza kupata furaha unapochochewa ifaavyo kufanya mambo ambayo wazazi wako wanakutia moyo ufanye.

Usife Moyo Katika Kufanya Lililo Bora

Ukisha weka mradi fulani jitahidi kuutimiza. Andiko la Wagalatia 6:9 linasema: “Acheni tusife moyo katika kufanya lililo bora, kwa maana katika majira yapasayo tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.” Usitegemee nguvu zako wala uwezo wako mwenyewe. Utakabili vizuizi na hata wakati mwingine huenda ukaona kana kwamba umeshindwa. Lakini Biblia inatuhakikishia hivi: “Katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:6) Yehova atakutegemeza unapojitahidi kutimiza miradi yako ya kiroho.

Naam, kwa kusitawisha tamaa ya kumtumikia Yehova na kujitahidi kutimiza miradi ya kiroho utaweza kufanya “kusonga mbele kwako kupate kuwa dhahiri kwa watu wote.” (1 Timotheo 4:15) Kisha utafurahia maisha yenye kusudi katika utumishi wa Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kusoma Biblia na kutafakari yale unayosoma kutakuchochea umtumikie Yehova

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yesu alifanya yale aliyotazamiwa na Baba yake afanye