Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mchango Wangu Katika Kuendeleza Elimu ya Biblia Ulimwenguni

Mchango Wangu Katika Kuendeleza Elimu ya Biblia Ulimwenguni

Simulizi la Maisha

Mchango Wangu Katika Kuendeleza Elimu ya Biblia Ulimwenguni

LIMESIMULIWA NA ROBERT NISBET

Mimi na ndugu yangu George tulikaribishwa kwenye makao ya kifalme ya Mfalme Sobhuza wa Pili wa Swaziland. Ilikuwa mwaka wa 1936, na bado ninakumbuka waziwazi mazungumzo yetu. Nilipata kuwa na mazungumzo hayo marefu pamoja na mfalme kwa sababu ya kushiriki kazi kubwa ya elimu ya Biblia kwa muda mrefu. Sasa nikiwa na umri wa miaka 95 ninakumbuka kwa shauku kazi niliyotimiza katika mabara matano.

MAMBO yalianza mwaka 1925 wakati muuzaji wa majani-chai aliyeitwa Dobson alipotembelea familia yetu huko Edinburgh, Scotland. Nilikuwa karibu miaka ishirini na nilikuwa nikijifunza kuhusu madawa na wakati uleule nikifanya kazi katika duka la dawa. Ingawa nilikuwa bado mchanga, nilitaka sana kujua mabadiliko makubwa katika familia na dini ambayo yalisababishwa na vita ya ulimwengu ya mwaka wa 1914-1918. Pindi moja Bw. Dobson alitutembelea na kutuachia kitabu The Divine Plan of the Ages. Kitabu hicho kilisimulia kuhusu Muumba mwenye akili na “mpango” hususa kwa njia nzuri yenye kueleweka na inayopatana kabisa na Mungu niliyetaka kuabudu.

Mimi na Mama tulianza kuhudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Mnamo Septemba 1926, mimi na Mama tulionyesha tumejiweka wakfu kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji kwenye kusanyiko huko Glasgow. Wote waliotaka kubatizwa walipewa majoho marefu yaliyokuwa na kanda za kuyafunga kwenye miguu ambayo yangevaliwa juu ya mavazi ya kuogelea. Wakati huo mavazi hayo yalionekana kuwa yenye kufaa kwa tukio muhimu kama hilo.

Katika miaka hiyo ya mapema, mambo mengi yalihitaji kufafanuliwa ili tuyaelewe. Wengi wa washiriki wa kutaniko walisherehekea Krismasi na ni wachache sana walioshiriki mahubiri. Hata baadhi ya wazee walipinga ugawanyaji wa vichapo siku ya Jumapili, kwani waliona kufanya hivyo ni kuvunja Sabato. Hata hivyo, makala za Mnara wa Mlinzi za mwaka wa 1925, zilianza kukazia sana maandiko kama Marko 13:10: “Katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza.”

Kazi ya ulimwenguni pote ingetimizwaje? Mara ya kwanza nilipojaribu kuhubiri nyumba kwa nyumba, nilimwambia mwenye nyumba kwamba nilikuwa ninauza vitabu vizuri vya kidini na nikamwachia kitabu The Harp of God, ambacho kinafafanua mafundisho kumi ya Biblia, kikiyafananisha na kanda za kinubi. Baadaye, tulipewa kadi ya ushuhuda iliyokuwa na ujumbe mfupi ambao ulisomwa na mwenye nyumba. Pia tulitumia hotuba za dakika nne na nusu zilizorekodiwa na ambazo zingeweza kupigwa kwenye santuri tulizobeba. Santuri za wakati huo zilikuwa nzito sana lakini santuri zilizotengenezwa baadaye zilikuwa nyepesi na hata nyingine zingeweza kupigwa zikiwa wima.

Kuanzia mwaka wa 1925 hadi miaka ya 1930, tulifanya kazi ya kuhubiri kwa kadiri tulivyoweza kulingana na hali za wakati huo. Kisha mapema miaka ya 1940 Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ilianzishwa katika makutaniko yote. Tulifundishwa kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa kuongea moja kwa moja na mwenye nyumba ambaye angetusikiliza. Tulijifunza pia umuhimu wa kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani na watu wenye kupendezwa. Kwa njia nyingine, tunaweza kusema kwamba huo ulikuwa mwanzo wa elimu ya Biblia ya ulimwenguni pote.

Kitia Moyo Kutoka kwa Ndugu Rutherford

Kwa kuwa nilitaka sana kufanya mengi zaidi katika kazi ya ufundishaji nilianza huduma ya wakati wote ya upania mwaka 1931. Nilipaswa kuanza mara moja baada ya kusanyiko lililofanywa jijini London. Hata hivyo, siku moja wakati wa chakula cha mchana, Ndugu Joseph Rutherford, aliyekuwa akisimamia kazi wakati huo alitaka kuzungumza nami. Alikuwa na mpango wa kutuma painia fulani Afrika. “Je, ungependa kwenda?” akaniuliza. Ingawa nilishangaa kidogo, nilisema hivi kwa uhakika: “Ndiyo, nitakwenda.”

Wakati huo mradi mkuu ulikuwa kugawa vichapo vingi vya Biblia iwezekanavyo na hiyo ilimaanisha kusafiri kila wakati. Nilitiwa moyo kubaki mseja, kama walivyokuwa ndugu wengi wenye madaraka mbalimbali ya usimamizi wakati huo. Eneo nililopaswa kuhubiri lilianzia Cape Town, kusini mwa Afrika, kuelekea upande wa mashariki wa bara hilo, kutia ndani visiwa vya pwani ya Bahari ya Hindi. Ili kufikia mpaka wa magharibi wa eneo hilo, ilinibidi kuvuka mchanga wenye joto wa Jangwa la Kalahari na kusafiri hadi chanzo cha Mto Nile kwenye Ziwa Viktoria. Nikiwa na painia mwenzangu tulipaswa kukaa kwa muda wa miezi sita kila mwaka kwenye nchi moja au zaidi katika eneo hilo kubwa la Afrika.

Makatoni Mia Mbili Yenye Vichapo vya Biblia

Nilipofika Cape Town nilionyeshwa makatoni 200 ya vichapo vilivyopaswa kupelekwa Afrika Mashariki. Vichapo hivyo vilikuwa vimechapishwa katika lugha nne za Ulaya na nne za Asia, lakini hakukuwa na vichapo vyovyote katika lugha za Afrika. Nilipouliza kwa nini vichapo hivyo vilikuwa vimeletwa hata kabla sijafika, niliambiwa kwamba vilikusudiwa kupewa Frank na Gray Smith, mapainia wawili waliokuwa wameenda kuhubiri Kenya. Mara tu walipofika Kenya, wote wawili walishikwa na malaria na kwa kuhuzunisha Frank akafa.

Ingawa habari hizo zilinifanya nifikirie kwa uzito hali yangu, sikuvunjika moyo. Mimi na painia mwenzangu, David Norman, tuliondoka Cape Town kwa meli kwenda katika mgawo wetu wa kwanza huko Tanzania, umbali wa kilometa 5,000 hivi. Wakala mmoja wa safari mjini Mombasa, Kenya, alitutunzia vichapo na alivisafirisha mahali popote tulipomwomba. Mwanzoni, tulihubiri katika maeneo ya biashara, yaani, kwenye maduka na maofisi katika kila mji. Baadhi ya vichapo tulivyotumia ni seti iliyokuwa na vitabu 9 na vijitabu 11, ambavyo viliitwa upinde kwa sababu vilikuwa vya rangi mbalimbali.

Baadaye tuliamua kutembelea kisiwa cha Zanzibar, kilicho kilometa 30 hivi kutoka pwani ya mashariki. Kwa karne kadhaa Zanzibari ilikuwa kituo cha biashara ya watumwa lakini kilichojulikana sana kwa sababu ya karafuu, zilizokuwa zinanukia kila mahali mjini. Ilikuwa vigumu sana kukumbuka vijia vya mji huo kwa kuwa ulikuwa umejengwa bila utaratibu. Barabara zilikuwa zimejipinda na zenye kutatanisha hivyo ilikuwa rahisi sana kwetu kupotea. Hoteli tulimoishi ilikuwa nzuri na yenye kustarehesha, lakini milango yake iliyofungwa kwa komeo na kuta zake pana zilifanya ionekane kama gereza. Hata hivyo tulipata matokeo mazuri huko na tulifurahi kuona kwamba Waarabu, Wahindi, na wengineo walikubali vichapo vyetu.

Magari-Moshi, Mashua, na Magari

Siku hizo haikuwa rahisi kusafiri katika Afrika Mashariki. Kwa mfano, tulipokuwa njiani kutoka Mombasa kuelekea nyanda za juu za Kenya, gari-moshi tulimokuwa tukisafiria lilizuiwa na nzige. Mamilioni ya nzige yalifunika ardhi na reli, na kufanya magurudumu ya gari-moshi yateleze kwenye reli. Ilibidi reli ioshwe kwanza kwa mvuke kutoka kwa gari-moshi kabla ya gari hilo kupita. Kwa kufanya hivyo, tulisafiri polepole hadi tulipopita kundi hilo la nzige. Tulifurahi kama nini gari-moshi lilipoanza kupanda kuelekea nyanda za juu ambapo hali ya hewa ni baridi kidogo!

Ingawa ilikuwa rahisi kusafiri kwenda miji iliyoko pwani kwa gari-moshi na mashua, maeneo ya mashambani yangeweza kufikika kwa urahisi zaidi kwa kutumia gari. Nilifurahi ndugu yangu George alipojiunga nami, kwa kuwa tuliweza kununua gari kubwa ambalo lilikuwa na nafasi ya kuweka vitanda, mahali pa kupikia, stoo, na madirisha ya kuzuia mbu. Tulikuwa na vipaza-sauti vilivyowekwa kwenye paa. Hivyo tungeweza kuhubiri nyumba kwa nyumba mchana na kualika watu waje kusikiliza hotuba jioni kwenye masoko. Watu walipenda sana hotuba yenye kichwa “Is Hell Hot” iliyokuwa imerekodiwa katika santuri. Pindi moja tulisafiri kutoka Afrika Kusini hadi Kenya umbali wa kilometa 3,000 katika gari letu kubwa, na tulifurahi kwamba tulikuwa na vijitabu mbalimbali katika lugha nyingi za Kiafrika, ambavyo wenyeji walifurahi kuvipokea.

Jambo la kufurahisha ni kwamba katika safari hizo, tuliweza kuona wanyama wa mwituni wanaopatikana Afrika. Bila shaka, kwa sababu ya usalama tulikaa ndani ya gari giza lilipoingia, lakini imani yetu iliimarishwa kuona wanyama mbalimbali walioumbwa na Yehova wakiwa katika mazingira yao ya asili.

Upinzani Waanza

Ingawa tulijihadhari na wanyama wa mwituni, tulihitaji kujihadhari hata zaidi tulipokuwa tukishughulika na maofisa wa serikali na viongozi wa kidini wenye hasira kali walioanza kupinga waziwazi kazi yetu ya kuhubiri Ufalme. Tatizo kubwa zaidi tulilokabili lilihusu muumini mmoja shupavu aliyejiita Mwana Lesa, yaani “Mwana wa Mungu,” ambaye alikuwa kiongozi wa kikundi kilichoitwa Kitawala, jina ambalo kwa kusikitisha linamaanisha “Mnara wa Mlinzi.” Muda mfupi kabla hatujawasili, mtu huyo aliwaua Waafrika wengi kwa kuwazamisha akidai kwamba anawabatiza. Hatimaye alikamatwa na kunyongwa. Baadaye, nilipata fursa ya kuzungumza na mtu aliyemnyonga na kumweleza kwamba mtu huyo hakuwa na uhusiano wowote na shirika letu la Watch Tower Society.

Pia tulikuwa na matatizo na Wazungu wengi kutoka Ulaya ambao kwa sababu za kifedha hawakufurahia kazi yetu ya kuwaelimisha watu. Msimamizi mmoja wa mahali pa kuwekea bidhaa alilalamika: “Ikiwa mzungu ataendelea kukaa katika nchi hii, lazima Mwafrika asitambue kwamba anatumikishwa.” Kwa sababu hiyo mkuu wa kampuni moja ya kuchimba dhahabu alinifukuza ofisini mwake. Kisha kwa hasira akanisindikiza mpaka barabarani.

Hatimaye serikali ya Rhodesia (ambayo sasa ni Zimbabwe) ilituamuru tuondoke nchini hasa kwa sababu ya ushawishi kutoka kwa wapinzani wa kidini na wafanya-biashara. Tulikata rufani kuhusiana na uamuzi huo na tuliruhusiwa kubaki nchini humo, kwa masharti kwamba tusiwahubirie Waafrika. Ofisa mmoja alisema kwamba vichapo vyetu “havikuwafaa Waafrika.” Hata hivyo, katika nchi nyingine kazi yetu ya kuwaelimisha Waafrika iliendelea bila tatizo, na hata waliifurahia. Mojawapo ya nchi hizo ni Swaziland.

Mfalme wa Swaziland Atukaribisha

Swaziland ni nchi ndogo inayojitawala ambayo ina ukubwa wa kilometa 17,364 za mraba. Nchi hiyo iko katikati mwa Afrika Kusini. Nchini humo tulikutana na Mfalme Sobhuza wa Pili mwenye ufasaha, anayetajwa mwanzoni mwa makala hii. Kwa kuwa mfalme huyo alisomea chuo kikuu cha Uingereza, alizungumza Kiingereza vizuri. Mfalme huyo ambaye hakuwa amevalia kirasmi, alitukaribisha vizuri sana.

Tulizungumza kuhusu Paradiso ya kidunia ambayo Mungu alikusudia kuwapa watu walio na mwelekeo unaofaa. Ijapokuwa hakupendezwa sana na habari hizo, alisema kwamba alikuwa akifikiria jambo kama hilo. Mfalme alikuwa ameazimia kuboresha kiwango cha maisha cha watu maskini na wasio na elimu. Hakupendezwa na shughuli za mishonari wengi wa dini zinazojiita za Kikristo, ambao walionekana kupendezwa zaidi na idadi ya washiriki wa makanisa yao kuliko kuwaelimisha watu. Hata hivyo, mfalme alifahamu utendaji wa mapainia wetu kadhaa, naye alitupongeza kwa kazi yetu ya kuwaelimisha watu Biblia, hasa kwa kuwa tulikuwa tayari kufanya kazi hiyo bila malipo au bila masharti mengine.

Elimu ya Biblia Yapamba Moto

Katika mwaka wa 1943, Shule ya Biblia ya Gileadi ilianzishwa ili kuzoeza mishonari. Ilikazia kuwasaidia watu wenye kupendezwa waliopatikana badala ya kuwaachia tu vichapo vya Biblia. Katika mwaka wa 1950, mimi na George tulialikwa kuhudhuria darasa la 16 la shule ya Gileadi. Nikiwa huko nilikutana na Jean Hyde, dada mwenye sifa nzuri kutoka Australia aliyepewa mgawo wa umishonari huko Japani baada ya sote wawili kuhitimu. Urafiki wetu haukusitawi sana kwa kuwa wakati huo useja ulikaziwa sana.

Baada ya mazoezi tuliyopata Gileadi, mimi na George tulipewa mgawo wa kwenda Mauritius, kisiwa kilicho katika Bahari ya Hindi. Tulifanya urafiki na wenyeji, tukajifunza lugha yao, na kuwafunza Biblia. Baadaye ndugu yangu mdogo William na Muriel mke wake walihitimu kutoka Gileadi pia. Walitumwa Kenya, eneo nililokuwa nimetumwa zamani.

Miaka minane ilipita haraka, kisha kwenye kusanyiko la kimataifa lililofanywa New York mwaka wa 1958, nilikutana tena na Jean Hyde. Tulianzisha urafiki tena kisha tukawa wachumba. Mgawo wangu ulibadilishwa, nikatoka Mauritius kwenda Japan, ambako mimi na Jean tulioana mwaka 1959. Kwa furaha tulianza kazi ya umishonari huko Hiroshima, ambako wakati huo kulikuwa na kutaniko moja ndogo. Leo jiji hilo lina makutaniko 36.

Twaondoka Japan

Baada ya miaka kadhaa, tulipatwa na matatizo ya kiafya ambayo yalifanya utumishi wetu wa mishonari kuzidi kuwa mgumu, na hatimaye tukalazimika kuondoka Japan kwenda kuishi Australia, nchi anakotoka Jean. Tulihuzunika sana siku tuliyoondoka Hiroshima. Tuliwaaga marafiki wetu wote wapendwa kwenye kituo cha gari-moshi.

Sasa tunaishi Australia, na tunaendelea kumtumikia Yehova kwa kadiri tuwezavyo katika kutaniko la Armidale katika jimbo la New South Wales. Tumefurahi sana kuwafundisha watu wengi kweli za Biblia kwa miaka 80 hivi! Nimeona ukuzi wa ajabu katika mpango wa kufundisha watu Biblia na nimejionea matukio muhimu ya kiroho. Hakuna mtu au kikundi cha watu kinachoweza kujivunia mambo hayo. Kwa kweli, kama mtunga-zaburi alivyosema, “neno hili limetoka kwa BWANA, nalo ni ajabu machoni petu.”—Zaburi 118:23.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ndugu yangu George na gari letu tulilotumia kama nyumba

[Picha katika ukurasa wa 28]

Mimi nikiwa kwenye Ziwa Viktoria

[Picha katika ukurasa wa 29]

Wanafunzi wa shule ya sekondari waliohudhuria hotuba ya watu wote huko Swaziland mwaka wa 1938

[Picha katika ukurasa wa 30]

Mimi na Jean siku ya arusi yetu mwaka wa 1959 na leo