Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Onyesheni “Upole Wote Kuelekea Watu Wote”

Onyesheni “Upole Wote Kuelekea Watu Wote”

Onyesheni “Upole Wote Kuelekea Watu Wote”

“Endelea kuwakumbusha . . . wawe wenye kukubali sababu, wakionyesha wazi upole wote kuelekea watu wote.”—TITO 3:1, 2.

1. Kwa nini kwa kawaida si rahisi kuonyesha upole?

MTUME Paulo aliandika hivi: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Wakorintho 11:1) Watumishi wote wa Mungu leo hujitahidi kutii shauri hilo. Ni kweli kwamba si rahisi kufanya hivyo kwa kuwa tumerithi tamaa za kichoyo na nyutu zisizopatana na mfano wa Kristo kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza. (Waroma 3:23; 7:21-25) Hata hivyo, sote tukijitahidi, tunaweza kufanikiwa kuonyesha sifa ya upole. Lakini haitoshi kutegemea nguvu zetu. Ni mambo gani mengine yanayohitajiwa?

2. Tunaweza kuonyeshaje “upole wote kuelekea watu wote”?

2 Upole wa kimungu ni sehemu ya matunda ya roho takatifu. Kadiri tunavyotii mwongozo wa nguvu ya utendaji ya Mungu, ndivyo tunavyodhihirisha matunda ya nguvu hiyo. Ni kwa kufanya hivyo tu tutaweza kuonyesha “upole wote” kuelekea watu wote. (Tito 3:2) Na tuchunguze jinsi tunavyoweza kuiga kielelezo cha Yesu na hivyo kuwawezesha wale wanaoshirikiana nasi ‘wapate burudisho.’—Mathayo 11:29; Wagalatia 5:22, 23.

Katika Familia

3. Ni hali gani katika familia inayodhihirisha roho ya ulimwengu?

3 Upole ni muhimu sana katika familia. Shirika la Afya Ulimwenguni linakadiria kwamba aksidenti na malaria kwa pamoja hazihatarishi sana afya ya wanawake kama vile jeuri katika familia. Kwa mfano, huko London, Uingereza inaripotiwa kwamba asilimia 25 ya visa vyote vya jeuri hutokea nyumbani. Mara nyingi polisi hukutana na watu ambao hudhihirisha hisia zao kwa ‘kupiga kelele na kutumia usemi wenye kuudhi.’ Jambo baya hata zaidi ni kwamba watu fulani waliooana wameruhusu “uchungu wenye nia ya kudhuru” uathiri uhusiano wao. Kwa kusikitisha tabia hiyo inaonyesha “roho ya ulimwengu” na kwa hiyo hairuhusiwi katika familia za Kikristo.—Waefeso 4:31; 1 Wakorintho 2:12.

4. Upole unaweza kusaidiaje familia?

4 Tunahitaji roho ya Mungu ili kuepuka mitazamo ya ulimwengu. “Iliko roho ya Yehova, kuna uhuru.” (2 Wakorintho 3:17) Upendo, fadhili, kujidhibiti, na ustahimilivu huimarisha umoja kati ya waume na wake wasio wakamilifu. (Waefeso 5:33) Tabia-pole hufanya hali ya nyumbani iwe yenye kufurahisha na kupendeza tofauti na kubishana-bishana na ugomvi ambao huvuruga familia nyingi. Jambo analosema mtu ni muhimu, lakini mtazamo wake hudhihirika kwa namna anavyolisema. Unapunguza mikazo unapoeleza mahangaiko na wasiwasi wako kwa upole. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.”—Mithali 15:1.

5. Upole unaweza kuisaidiaje familia iliyogawanyika kidini?

5 Upole ni muhimu hasa katika familia iliyogawanyika kidini. Upole pamoja na matendo ya fadhili, unaweza kuwavuta kwa Yehova wale wasio na mwelekeo ufaao. Petro aliwashauri wake Wakristo hivi: “Iweni katika ujitiisho kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa neno, wapate kuvutwa bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kuwa mashahidi wa kujionea mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na staha yenye kina kirefu. Na msiache urembo wenu uwe ule wa kusuka nywele kwa nje na wa kuvalia madoido ya dhahabu au kuvalia mavazi ya nje, bali acheni uwe yule mtu wa siri wa moyoni katika vao lisilofisidika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.”—1 Petro 3:1-4.

6. Kuonyesha upole kunawezaje kuimarisha uhusiano kati ya wazazi na watoto?

6 Uhusiano kati ya wazazi na watoto unaweza kuwa mbaya hasa ikiwa hawampendi Yehova. Lakini kila familia ya Kikristo inahitaji kuonyesha upole. Paulo aliwashauri akina baba hivi: “Msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Familia inapokuwa na sifa ya upole, uhusiano kati ya wazazi na watoto huimarika zaidi. Dean, mmoja wa watoto watano, akumbuka hivi kuhusu baba yake: “Baba alikuwa mwenye tabia-pole. Sikumbuki nikibishana naye hata nilipokuwa tineja. Alikuwa mpole sana wakati wote, hata alipokasirika. Wakati mwingine aliniadhibu kwa kunifungia chumbani mwangu au kuninyima vitu fulani nilivyopenda, lakini hatukuwahi kubishana. Hakuwa baba tu, bali pia rafiki yetu na hatukutaka kumkatisha tamaa.” Kwa kweli upole husaidia kuimarisha uhusiano kati ya wazazi na watoto.

Katika Huduma

7, 8. Kwa nini ni muhimu kuonyesha upole katika huduma ya shambani?

7 Sehemu nyingine ambapo upole ni muhimu ni katika huduma ya shambani. Tunapohubiri habari njema za Ufalme, tunakutana na watu wenye nyutu mbalimbali. Baadhi yao hufurahia kusikiliza ujumbe wa tumaini tunaowaeleza. Kwa sababu mbalimbali, huenda wengine wasiitikie kwa njia inayofaa. Watu wasipoitikia kwa njia inayofaa, sifa ya upole hutusaidia sana kutimiza kazi yetu ya kuhubiri hadi sehemu ya mbali zaidi ya dunia.—Matendo 1:8; 2 Timotheo 4:5.

8 Mtume Petro aliandika: ‘Takaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu, sikuzote mkiwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hudai kwenu sababu ya tumaini lililo katika nyinyi, lakini mkifanya hivyo kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.’ (1 Petro 3:15) Kwa kuwa tunamwona Kristo kuwa Kielelezo chetu, tunakuwa waangalifu kuonyesha upole na staha tunapohubiria watu wanaosema kwa ukali. Mara nyingi mwenendo huo huwa na matokeo mazuri.

9, 10. Simulia jambo fulani lililoonwa linaloonyesha umuhimu wa kuwa wapole katika huduma ya shambani.

9 Keith alibaki nyuma mke wake alipoenda kumfungulia mtu aliyebisha mlango. Baada ya kutambua kwamba mtu aliyewatembelea alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, mke wa Keith alishutumu Mashahidi kwa hasira kwamba huwatendea watoto wao kikatili. Ndugu huyo alibaki mtulivu na kwa upole akajibu: “Nasikitika kwamba unahisi hivyo. Je, ninaweza kukueleza Mashahidi wa Yehova wanaamini nini?” Keith alikuwa akisikiliza mazungumzo hayo kisha akaja mlangoni kumwambia ndugu huyo aondoke.

10 Baadaye, wenzi hao wakasikitika kwamba walikuwa wamemtendea mgeni wao kwa ukali. Upole wa ndugu huyo ulikuwa umewagusa moyo. Baada ya juma moja, Keith na mkewe walishangaa ndugu huyo aliporudi, nao wakamruhusu awaeleze imani yake inayotegemea Maandiko. Baadaye walisema: “Miaka miwili iliyofuata, tulisikiliza mengi ambayo Mashahidi wengine waliotutembelea walisema.” Walikubali kujifunza Biblia na hatimaye wote wawili wakabatizwa ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova. Ni jambo lenye kuthawabisha kama nini kwa Shahidi yule aliyewatembelea Keith na mke wake mara ya kwanza! Shahidi huyo alikutana nao miaka kadhaa baadaye na akapata kujua kwamba sasa walikuwa ndugu na dada yake wa kiroho. Upole hufanikiwa.

11. Upole unaweza kumsaidiaje mtu akubali ukweli wa Kikristo?

11 Mambo ambayo Harold alijionea akiwa jeshini yalimtia uchungu na kumfanya atilie shaka kama kuna Mungu. Matatizo ya Harold yaliongezeka alipopata aksidenti iliyosababishwa na dereva mlevi na kumlemaza kabisa. Mashahidi wa Yehova walipomtembelea Harold nyumbani mwake aliwaambia wasimtembelee tena. Lakini siku moja, Shahidi aitwaye Bill alikusudia kumtembelea mtu fulani mwenye kupendezwa aliyeishi karibu sana na Harold. Bill alikosea na kubisha mlango wa Harold. Wakati Harold aliyekuwa akitembea kwa kutumia mikongojo, alipofungua mlango, Bill aliomba radhi mara moja na kumweleza kwamba alikusudia kumtembelea mtu aliyeishi karibu naye. Harold alifanyaje? Bill hakujua kwamba Harold alikuwa ameona kwenye televisheni Mashahidi wakifanya kazi pamoja kujenga Jumba la Ufalme jipya kwa muda mfupi sana. Alivutiwa kuona watu wengi sana wakifanya kazi kwa umoja, na jambo hilo lilibadili mtazamo wake kuelekea Mashahidi. Kwa kuwa Bill alimwomba Harold msamaha kwa fadhili, na pia alikuwa mpole na mwenye utu wa kupendeza, Harold alikubali kutembelewa na Mashahidi. Alijifunza Biblia, akafanya maendeleo, na kubatizwa kuwa mtumishi wa Yehova.

Kutanikoni

12. Washiriki wa kutaniko la Kikristo wanapaswa kukataa tabia gani za kilimwengu?

12 Sehemu ya tatu ambapo upole ni muhimu ni katika kutaniko la Kikristo. Ni jambo la kawaida kwa jamii ya sasa kugombana. Mijadala, mabishano, na mizozo ni mambo ya kawaida miongoni kwa watu walio na maoni ya kilimwengu kuhusu maisha. Mara kwa mara, tabia hizo huathiri kutaniko la Kikristo polepole nazo hudhihirika pale Wakristo wanapogombana na kubishana. Ndugu wenye madaraka huhuzunika wanapolazimika kurekebisha hali hizo. Hata hivyo, kwa kuwa ndugu hao wanampenda Yehova na ndugu zao, wao hujaribu kuwasaidia wakosaji watubu na kugeuka.—Wagalatia 5:25, 26.

13, 14. Matokeo ya ‘kuagiza kwa upole wale wasio na mwelekeo ufaao’ yanaweza kuwaje?

13 Katika karne ya kwanza, Paulo na mwandamani wake Timotheo walikabili matatizo kutoka kwa washiriki fulani kutanikoni. Paulo alimwonya Timotheo ajihadhari na akina ndugu waliofanana na vyombo ‘vya kusudi lenye kukosa heshima.’ Paulo alitoa hoja hii: “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali ahitaji kuwa mwanana kuelekea wote, mwenye sifa za ustahili kufundisha, akifuliza kujizuia mwenyewe chini ya uovu, akiagiza kwa upole wale wasio na mwelekeo ufaao.” Tunapodumisha upole hata tunapochokozwa, mara nyingi wale wanaotupinga hubadili maoni yao yenye uchambuzi kutuelekea. Kama Paulo anavyoandika, huenda Yehova naye “akawapa toba inayoongoza kwenye ujuzi sahihi juu ya kweli.” (2 Timotheo 2:20, 21, 24, 25) Ona kwamba Paulo anahusianisha uanana na kujidhibiti na upole.

14 Paulo alitenda kupatana na yale aliyohubiri. Aliposhughulika na “mitume walio bora sana” katika kutaniko la Korintho, aliwahimiza akina ndugu hivi: “Basi mimi mwenyewe, Paulo, nawasihi sana nyinyi kwa upole na fadhili ya Kristo, ingawa mimi ni wa hali ya chini katika kuonekana miongoni mwenu, lakini nisipokuwapo mimi ni jasiri kuwaelekea nyinyi.” (2 Wakorintho 10:1; 11:5) Paulo alimwiga Kristo kikweli. Ona kwamba aliwasihi ndugu hao “kwa upole” wa Kristo. Hivyo aliepuka mtazamo wenye kukandamiza na wa kiimla. Bila shaka himizo lake liliwavutia wote kutanikoni waliokuwa na mioyo yenye usikivu. Alirekebisha mahusiano yaliyokuwa yameharibika na kusaidia kuleta amani na umoja kutanikoni. Sisi sote tunaweza kujitahidi kumwiga. Hasa wazee wanahitaji kuiga kielelezo cha Kristo na Paulo.

15. Kwa nini upole ni muhimu tunapotoa shauri?

15 Bila shaka, hutupaswi kungoja hadi amani na umoja wa kutaniko uwe hatarini ndipo tutekeleze daraka letu la kuwasaidia wengine. Ndugu wanahitaji mwongozo wenye upendo hata kabla ya mahusiano kuharibika. Paulo alihimiza hivi: “Akina ndugu, hata ingawa mtu achukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya yeye kuijua, nyinyi mlio na sifa za ustahili wa kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu wa namna hiyo.” Lakini jinsi gani? “Katika roho ya upole, huku kila mmoja wenu akifuliza kujiangalia mwenyewe, kwa kuhofu wewe pia usipate kushawishwa.” (Wagalatia 6:1) Si rahisi sikuzote kudumisha “roho ya upole,” hasa kwa sababu Wakristo wote, kutia ndani wale waliowekwa rasmi, wanaathiriwa na maelekeo yenye dhambi. Hata hivyo, upole ndio utakaowasaidia wakosaji wafanye marekebisho yanayohitajiwa.

16, 17. Ni nini kinachoweza kufanya shauri likubaliwe?

16 Katika Kigiriki cha awali, neno linalotafsiriwa ‘kurekebisha’ linaweza pia kumaanisha kunyoosha mifupa iliyovunjika, jambo ambalo husababisha maumivu makali. Daktari mwenye kufariji ambaye hunyoosha mfupa uliovunjika hueleza manufaa ya kufanya hivyo. Utulivu wake unafariji. Maneno machache yenye kufariji husaidia kumtuliza mgonjwa. Vivyo hivyo, huenda marekebisho ya kiroho yakawa yenye maumivu. Lakini upole utafanya iwe rahisi zaidi kukubali marekebisho hayo, hivyo kurudisha mahusiano mazuri na kumwezesha mkosaji abadili mwenendo wake. Wakati mwenye kutoa shauri anapokuwa mpole, anaweza kufanya shauri linalofaa la Kimaandiko likubaliwe hata kama lilikuwa limekataliwa mwanzoni.—Mithali 25:15.

17 Tunapowasaidia wengine wafanye marekebisho, huenda kukawa na hatari ya shauri letu kueleweka kuwa uchambuzi. Mwandishi mmoja anasema: “Tunahitaji kuwa wapole zaidi tunapowakaripia wengine, kwa kuwa tunapofanya hivyo tunakuwa na mwelekeo wa kukazia mambo sana.” Kusitawisha upole unaotokana na unyenyekevu kutamsaidia Mkristo anayetoa shauri aepuke hatari hiyo.

“Kuelekea Watu Wote”

18, 19. (a) Kwa nini huenda ikawa vigumu kwa Wakristo kuonyesha upole wanaposhughulika na wenye mamlaka? (b) Ni nini kitakachowasaidia Wakristo waonyeshe upole kwa wenye mamlaka, na huenda matokeo yakawaje?

18 Wengi huona ni vigumu kuonyesha upole wanaposhughulika na wenye mamlaka. Kwa kweli, baadhi ya watu wenye mamlaka huwatendea watu kwa ukali bila kuonyesha hisia-mwenzi. (Mhubiri 4:1; 8:9) Hata hivyo, upendo wetu kwa Yehova utatusaidia kutambua mamlaka yake kuu na hivyo kuzipa serikali utii wa kadiri ambao tunastahili kuzipa. (Waroma 13:1, 4; 1 Timotheo 2:1, 2) Hata wakati wale wenye mamlaka ya juu wanapojaribu kutuzuia kuhubiri, sisi hutafuta kwa shangwe njia tunazoweza kutumia kutoa dhabihu zetu za sifa.—Waebrania 13:15.

19 Sisi si wataka-vita kamwe. Tunajitahidi kujadiliana na watu bila kulegeza msimamo wetu kuhusiana na kanuni za uadilifu. Kwa njia hiyo, ndugu zetu wanafanikiwa kuendelea na huduma yao katika nchi 234 ulimwenguni. Tunafuata shauri la Paulo la ‘kuwa katika ujitiisho na kuwa watiifu kwa serikali na mamlaka zikiwa watawala, kuwa tayari kwa ajili ya kila kazi njema, tusiseme kwa ubaya juu ya yeyote, tusiwe wataka-vita, tuwe wenye kukubali sababu, tukionyesha wazi upole wote kuelekea watu wote.’—Tito 3:1, 2.

20. Wale wanaoonyesha upole watapata baraka gani?

20 Wote wanaoonyesha upole watabarikiwa sana. Yesu alisema, “Wenye furaha ni wenye tabia-pole, kwa kuwa wao watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Kwa kudumisha upole, ndugu watiwa-mafuta wa Kristo watapata furaha na pendeleo la pekee la kuwa watawala wa Ufalme juu ya dunia. Nao “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” unaendelea kuonyesha upole wakitazamia kwa hamu kuishi katika Paradiso duniani. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16; Zaburi 37:11) Hayo ni matazamio mazuri kama nini! Basi, na tusipuuze kamwe kikumbusho hiki ambacho Paulo aliwapa Wakristo wa Efeso: “Kwa hiyo, mimi, niliye mfungwa katika Bwana, nawasihi nyinyi sana mtembee kwa kustahili wito ambao kwa huo mliitwa, mkiwa na hali kamili ya akili ya kujishusha chini na upole.”Waefeso 4:1, 2.

Kwa Kupitia

• Tunapata baraka gani tunapoonyesha upole

• katika familia?

• katika huduma ya shambani?

• kutanikoni?

• Wenye tabia-pole wanaahidiwa baraka gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Upole ni muhimu hasa katika familia zilizogawanyika kidini

[Picha katika ukurasa wa 21]

Upole huimarisha uhusiano katika familia

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mtumwa wa Bwana huagiza kwa upole wale wasio na mwelekeo ufaao

[Picha katika ukurasa wa 24]

Mwenye kutoa shauri anaweza kumsaidia mkosaji kwa kuwa mpole