Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upole Ni Sifa Muhimu Sana ya Kikristo

Upole Ni Sifa Muhimu Sana ya Kikristo

Upole Ni Sifa Muhimu Sana ya Kikristo

“Jivikeni wenyewe . . . upole.”—WAKOLOSAI 3:12.

1. Ni nini hufanya upole kuwa sifa ya kipekee?

INAPENDEZA kuwa pamoja na mtu mpole. Hata hivyo, Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema, “ulimi laini [“wa upole,” NW] huvunja mfupa.” (Mithali 25:15) Upole ni sifa ya kipekee, yenye kupendeza na yenye nguvu.

2, 3. Kuna uhusiano gani kati ya upole na roho takatifu, na tutachunguza nini katika makala hii?

2 Mtume Paulo alitaja sifa ya upole kati ya “matunda ya roho,” yanayotajwa kwenye Wagalatia 5:22, 23. Mara nyingi neno la Kigiriki linalotafsiriwa “upole” katika mstari wa 23 wa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pia humaanisha uanana. Kwa kweli, katika lugha nyingi ni vigumu kupata neno lililo na maana sawa kabisa na neno hili la Kigiriki kwa sababu neno la awali halielezei uanana wa kijuujuu tu, bali upole wa ndani na neema; si mwenendo wa mtu bali hali ya mtu ya akilini na moyoni.

3 Na tuchunguze mifano minne ya Biblia inayotusaidia kuelewa kikamili maana na umuhimu wa sifa ya upole. (Waroma 15:4) Kwa kufanya hivyo, tutajifunza maana ya sifa hiyo na jinsi tunavyoweza kuisitawisha na kuionyesha katika yote tunayofanya.

“Ya Thamani Kubwa Machoni pa Mungu”

4. Tunajuaje kwamba Yehova huthamini sifa ya upole?

4 Kwa kuwa upole ni mojawapo ya matunda ya roho ya Mungu, ni wazi kwamba sifa hiyo ni sehemu ya utu wa ajabu wa Mungu. Mtume Petro aliandika kwamba “roho ya utulivu na ya upole” ni “ya thamani kubwa machoni pa Mungu.” (1 Petro 3:4) Naam, Yehova huonyesha sifa ya upole, naye huithamini sana. Bila shaka, hiyo ni sababu ya kutosha kwa watumishi wote wa Mungu kusitawisha sifa ya upole. Hivyo basi, Mungu mweza yote, Mwenye Mamlaka kuu ulimwenguni, huonyeshaje upole?

5. Upole wa Yehova unatupatia tumaini gani la wakati ujao?

5 Wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, walikataa kimakusudi kutii amri ya Mungu iliyokuwa wazi ya kutokula kutokana na mti wa ujuzi wa mema na mabaya. (Mwanzo 2:16, 17) Kitendo hicho cha kukataa kimakusudi kutii kilisababisha dhambi, kifo, na hivyo wao pamoja na uzao wao wakatenganishwa na Mungu. (Waroma 5:12) Ingawa Yehova alikuwa na haki kamili ya kuwahukumu, hakuifutulia mbali kwa ukali familia ya wanadamu kuwa isiyoweza kurekebishwa na kukombolewa. (Zaburi 130:3) Badala yake, kupitia neema yake na utayari wake wa kutodai mengi, ambao ni wonyesho wa sifa ya upole, Yehova aliandaa njia ambayo wanadamu wenye dhambi wanaweza kumkaribia na kupata kibali chake. Naam, kupitia zawadi ya dhabihu ya fidia ya Mwana wake, Yesu Kristo, Yehova hutuwezesha kukaribia kiti chake cha enzi kilichotukuka bila hofu au woga.—Waroma 6:23; Waebrania 4:14-16; 1 Yohana 4:9, 10, 18.

6. Mungu alionyeshaje upole aliposhughulika na Kaini?

6 Muda mrefu kabla Yesu hajaja duniani, upole wa Yehova ulionyeshwa wakati Kaini na Abeli, wana wa Adamu, walipomtolea Mungu dhabihu. Kwa kuwa Yehova alijua hali ya mioyo yao, alikataa dhabihu ya Kaini lakini “akapendezwa” na Abeli na dhabihu yake. Maoni ya Mungu yenye fadhili kumwelekea Abeli mwaminifu na dhabihu yake yalifanya Kaini atende kwa njia isiyofaa. Biblia inasema, ‘Kaini alikasirika sana na uso wake ukakunjamana.’ Yehova alifanyaje? Je, aliudhiwa na mtazamo mbaya wa Kaini? La. Kwa upole, alimwuliza Kaini kwa nini alikasirika sana hivyo. Yehova hata alimwambia Kaini jambo ambalo angefanya ili kupata “kibali.” (Mwanzo 4:3-7; linganisha Biblia Habari Njema.) Kwa kweli, Yehova ndiye mfano mkamilifu wa upole.—Kutoka 34:6.

Upole Huvutia na Kuburudisha

7, 8. (a) Tunawezaje kupata kuelewa sifa ya upole ya Yehova? (b) Maneno ya Mathayo 11:27-29 hufunua nini juu ya Yehova na Yesu?

7 Njia iliyo bora zaidi ya kupata kuelewa sifa za Yehova zisizo na kifani ni kujifunza kuhusu maisha na huduma ya Yesu Kristo. (Yohana 1:18; 14:6-9) Alipokuwa akihubiri wilayani Galilaya, katika mwaka wa pili wa mahubiri yake, Yesu alifanya miujiza mingi huko Korazini, Bethsaida, Kapernaumu, na maeneo mengine ya karibu. Hata hivyo, watu wengi hawakumwamini kwa sababu walikuwa wenye kiburi na ubaridi. Yesu alifanyaje? Ingawa aliwakumbusha kinaganaga matokeo ya ukosefu wao wa imani, alisikitishwa na hali mbaya ya kiroho ya ʽam ha·ʼaʹrets, yaani, watu wa kawaida na wa hali ya chini.—Mathayo 9:35, 36; 11:20-24.

8 Mambo ambayo Yesu alifanya baadaye yalionyesha kwamba ‘alimjua Baba kabisa’ na alimwiga. Yesu aliwatolea watu wa kawaida mwaliko huu wenye kuchangamsha: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi. Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.” Maneno hayo yaliwafariji na kuwaburudisha kama nini watu hao walioonewa! Maneno hayo hutufariji pia na kutuburudisha leo. Tukijivika upole kwa unyofu, basi tutakuwa miongoni mwa wale ambao ‘Mwana anapenda kufunua’ Baba yake kwao.—Mathayo 11:27-29.

9. Ni sifa gani inayohusiana sana na upole, na ni kwa njia gani Yesu ni kielelezo bora kuhusiana na sifa hiyo?

9 Sifa nyingine inayohusiana sana na upole ni unyenyekevu, yaani kuwa na “hali ya chini moyoni.” Kinyume chake, kiburi humfanya mtu ajitukuze na mara nyingi anaweza kuwatendea wengine kwa ukali, bila huruma. (Mithali 16:18, 19) Yesu alionyesha unyenyekevu wakati wa huduma yake yote duniani. Hata alipoingia Yerusalemu siku sita kabla ya kifo chake akiwa amebebwa na mwana-punda, Yesu alishangiliwa kama Mfalme wa Wayahudi, naye alikuwa tofauti sana na watawala wa ulimwengu. Alitimiza unabii wa Kimesiya wa Zekaria: “Tazama! Mfalme wako anakuja kwako, mwenye tabia-pole, na amepanda juu ya punda, ndiyo, juu ya mwana-punda, uzao wa mnyama wa kubeba mizigo.” (Mathayo 21:5; Zekaria 9:9) Nabii mwaminifu Danieli aliona maono ambapo Yehova alimpa Mwana wake mamlaka ya kutawala. Hata hivyo, katika unabii mwingine wa mapema anamtaja Yesu kuwa “aliye mnyonge.” Kwa kweli, upole na unyenyekevu ni sifa zinazohusiana sana.—Danieli 4:17; 7:13, 14.

10. Kwa nini upole wa Kikristo si udhaifu?

10 Yehova na Yesu walionyesha sifa ya upole kwa njia yenye kupendeza na hilo hutusaidia kuwakaribia. (Yakobo 4:8) Bila shaka, upole si udhaifu. Yehova, Mungu mweza yote, ana nguvu nyingi sana zenye msukumo. Yeye huchukia sana ukosefu wa uadilifu. (Isaya 30:27; 40:26) Vivyo hivyo, Yesu aliazimia kabisa kutolegeza msimamo wake, hata aliposhambuliwa na Shetani Ibilisi. Hakuvumilia biashara haramu iliyofanywa na viongozi wa kidini wa siku zake. (Mathayo 4:1-11; 21:12, 13; Yohana 2:13-17) Hata hivyo, alidumisha upole aliposhughulika na kasoro za wanafunzi wake, na alivumilia kwa subira udhaifu wao. (Mathayo 20:20-28) Msomi mmoja wa Biblia alifafanua vizuri sifa ya upole aliposema: “Upole huo unaambatana na nguvu kama za chuma.” Na tuonyeshe sifa hiyo kama ya Kristo, yaani, upole.

Mwenye Tabia-Pole Zaidi ya Wote Katika Siku Zake

11, 12. Kwa kuzingatia malezi ya Musa, ni nini kilichofanya sifa yake ya upole iwe ya kipekee?

11 Mfano wa tatu tutakaochunguza ni ule wa Musa. Biblia humfafanua kuwa “mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hesabu 12:3) Ufafanuzi huo uliandikwa chini ya uongozi wa roho ya Mungu. Musa alikubali mwongozo wa Yehova kwa sababu ya sifa yake ya upole iliyokuwa ya kipekee.

12 Musa alilelewa katika mazingira yasiyo ya kawaida. Yehova alihakikisha kwamba mtoto huyo wa wazazi waaminifu Waebrania alinusurika wakati wa usaliti na mauaji. Musa alitunzwa na mama yake alipokuwa mtoto, naye alimfunza juu ya Mungu wa kweli, Yehova. Baadaye Musa alihamishwa kutoka nyumbani na kupelekwa katika mazingira yaliyokuwa tofauti kabisa. Stefano, Mkristo mfia-imani wa mapema alisema kwamba ‘Musa alifunzwa katika hekima yote ya Wamisri.’ “Kwa kweli, [Musa] alikuwa mwenye nguvu katika maneno na vitendo.” (Matendo 7:22) Imani yake ilidhihirika wazi wakati alipoona jinsi ndugu zake walivyotendewa isivyo haki na wasimamizi-kazi wa Farao. Ilimbidi Musa atoroke Misri hadi nchi ya Midiani baada ya kumwua Mmisri aliyekuwa akimpiga Mwebrania.—Kutoka 1:15, 16; 2:1-15; Waebrania 11:24, 25.

13. Musa aliathiriwaje na ile miaka 40 aliyoishi Midiani?

13 Akiwa na umri wa miaka 40, ilimbidi Musa ajiruzuku akiwa jangwani. Alipokuwa Midiani alikutana na mabinti saba wa Reueli na akawasaidia kuteka maji ili kunywesha mifugo mingi ya baba yao. Waliporudi nyumbani wasichana hao walimweleza Reueli kwa furaha kwamba “Mmisri mmoja” aliwaokoa kutoka kwa wachungaji wenye kuwasumbua. Reueli alimkaribisha Musa aishi pamoja na familia yake. Magumu aliyopata hayakumtia uchungu wala kumzuia kufanya marekebisho ili kuishi katika mazingira mapya. Hakuyumba-yumba katika tamaa yake ya kufanya mapenzi ya Yehova. Katika kipindi kirefu cha miaka 40, alipokuwa akitunza kondoo za Reueli, Musa alioa Sipora, akalea wana wake, akasitawisha na kuboresha sifa iliyokuja kumtambulisha. Naam, Musa alijifunza upole kupitia magumu.—Kutoka 2:16-22; Matendo 7:29, 30.

14. Eleza jambo fulani lililotukia Musa alipokuwa kiongozi wa Israeli ambalo linaonyesha kwamba alikuwa mpole.

14 Bado Musa alikuwa na sifa ya upole hata baada ya Yehova kumchagua kuwa kiongozi wa taifa la Israeli. Mwanamume mmoja kijana alimwambia Musa kwamba Eldadi na Medadi walikuwa wakitoa unabii kambini ijapokuwa hawakuwapo Yehova alipomwaga roho yake juu ya wanaume wazee 70 ambao wangemsaidia Musa. Yoshua akasema: “Ee bwana wangu Musa, uwakataze.” Musa akamjibu hivi kwa upole: “Je! Umekuwa na wivu kwa ajili yangu; ingekuwa heri kama watu wote wa BWANA wangekuwa manabii na kama BWANA angewatia roho yake.” (Hesabu 11:26-29) Upole ulituliza hali hiyo ya wasiwasi.

15. Ingawa Musa hakuwa mkamilifu, kwa nini tunapaswa kuiga kielelezo chake bora?

15 Pindi moja Musa alishindwa kuonyesha upole. Alipokuwa Meriba, karibu na Kadeshi, Musa alikosa kumtukuza Yehova, Mfanya-Miujiza. (Hesabu 20:1, 9-13) Hata hivyo, ingawa Musa hakuwa mkamilifu, tunavutiwa na imani yake thabiti na upole wake wa kipekee.—Waebrania 11:23-28.

Tofauti Kati ya Upole na Ukali

16, 17. Tunapata onyo gani kutokana na masimulizi juu ya Nabali na Abigaili?

16 Tunapata kielelezo chenye kuonya katika siku za Daudi, muda mfupi baada ya kifo cha Samweli aliyekuwa nabii wa Mungu. Kielelezo hicho kinahusu Nabali na mke wake Abigaili. Watu hao walitenda kwa njia iliyokuwa tofauti kama nini! Abigaili alikuwa “mwenye akili njema,” naye mumewe alikuwa “hana adabu [“mkali,” NW], tena mwovu katika matendo yake.” Nabali alikataa kikatili kuwapa chakula wanaume wa Daudi waliokuwa wamesaidia kuilinda mifugo yake mingi isiibwe. Daudi na wanaume wake walikasirika kwa njia ya uadilifu, wakachukua panga zao na kwenda kumkabili Nabali.—1 Samweli 25:2-13.

17 Abigaili aliposikia yaliyokuwa yametokea, alifanya haraka kutayarisha mikate, divai, nyama, na keki za zabibu na tini na kwenda kumlaki Daudi. Alimsihi hivi: “Juu yangu, bwana wangu, juu yangu mimi na uwe uovu; tafadhali mjakazi wako na anene masikioni mwako, nawe uyasikilize maneno ya mjakazi wako.” Ombi la upole la Abigaili lilimtuliza Daudi. Baada ya kumsikiliza Abigaili, Daudi alisema: “Na ahimidiwe BWANA, Mungu wa Israeli, ambaye amekuleta hivi leo kunilaki; na ibarikiwe busara yako, na ubarikiwe wewe, uliyenizuia hivi leo nisimwage damu.” (1 Samweli 25:18, 24, 32, 33) Hatimaye, Nabali alikufa kwa sababu ya ukali wake. Mwishowe, Abigaili alipata shangwe ya kuwa mke wa Daudi kwa sababu ya sifa zake nzuri. Upole wake ni kielelezo kizuri kwa wote wanaomtumikia Yehova leo.—1 Samweli 25:36-42.

Fuatia Upole

18, 19. (a) Ni mabadiliko gani yanayokuwa wazi tunapojivika upole? (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia tujichunguze ifaavyo?

18 Kwa hiyo ni lazima tuwe na sifa ya upole. Upole si uanana tu, bali ni sifa inayovutia na kuwaburudisha wengine. Huenda zamani tulizoea kuzungumza kwa ukali na kutenda bila huruma. Hata hivyo baada ya kujifunza kweli ya Biblia, tulibadilika tukawa na utu wenye kupendeza. Paulo alizungumzia badiliko hilo alipowahimiza Wakristo wenzake hivi: “Jivikeni wenyewe shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu.” (Wakolosai 3:12) Biblia inafananisha badiliko hilo na jinsi wanyama wakali wa mwituni kama mbwa-mwitu, chui, simba, dubu, na nyoka wanavyobadilika na kuwa kama wanyama wapole wa kufugwa kama vile mwana-kondoo, mwana-mbuzi, ndama, na ng’ombe. (Isaya 11:6-9; 65:25) Mabadiliko hayo huwa ya kipekee sana hivi kwamba wengine hushangaa wanapoyaona. Lakini sisi tunajua kwamba mabadiliko hayo yanawezekana tu kupitia roho ya Mungu, kwa kuwa upole ni mojawapo ya matunda yenye kutokeza sana ya roho hiyo.

19 Je, hiyo inamaanisha kwamba baada ya kufanya mabadiliko yanayohitajiwa na kujiweka wakfu kwa Yehova, hatuhitaji tena kujitahidi kuendelea kuwa na sifa ya upole? La, hasha. Kwa mfano, ili mavazi mapya yabaki safi na nadhifu lazima yaendelee kutunzwa. Kuchunguza Neno la Mungu na kutafakari mifano iliyomo hutusaidia kujichunguza upya. Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho ambalo ni kama kioo hufunua nini kukuhusu?—Yakobo 1:23-25.

20. Tunaweza kufanikiwaje kuonyesha sifa ya upole?

20 Kwa kawaida nyutu za watu hutofautiana. Ni rahisi kwa baadhi ya watumishi wa Mungu kuonyesha sifa ya upole kuliko wengine. Hata hivyo Wakristo wote wanahitaji kusitawisha matunda ya roho ya Mungu kutia ndani upole. Paulo alimshauri Timotheo hivi kwa upendo: “Fuatia uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, tabia-pole.” (1 Timotheo 6:11) Neno “fuatia” hudokeza kwamba jitihada inahitajiwa. Biblia moja hutafsiri shauri hilo kuwa ‘zingatia.’ (BHN) Ukijitahidi kutafakari mifano bora iliyo katika Neno la Mungu, itabaki akilini mwako daima kana kwamba imepandwa. Itakujenga na kukuongoza maishani.—Yakobo 1:21.

21. (a) Kwa nini tufuatie upole? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala yetu inayofuata?

21 Jinsi tunavyojiendesha tunapokuwa na wengine huonyesha ni kwa kadiri gani sisi hudhihirisha upole. “Ni nani aliye mwenye hekima na mwenye kuelewa miongoni mwenu?” mwanafunzi Yakobo anauliza. “Acheni aonyeshe kutokana na mwenendo wake bora kazi zake kwa upole ulio wa hekima.” (Yakobo 3:13) Tunaweza kuonyeshaje sifa hiyo ya Kikristo nyumbani, katika huduma ya Kikristo, na kutanikoni? Makala inayofuata inatoa mwongozo unaofaa.

Kwa Kupitia

• Ulijifunza nini kuhusu upole kutokana na kielelezo cha

• Yehova?

• Yesu?

• Musa?

• Abigaili?

• Kwa nini tunahitaji kufuatia upole?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kwa nini Yehova alipendezwa na Abeli na dhabihu yake?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Yesu alionyesha kwamba upole na unyenyekevu ni sifa zinazohusiana

[Picha katika ukurasa wa 18]

Musa aliweka kielelezo bora cha upole