Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kupata Wapi Maadili Mazuri ya Kiroho?

Unaweza Kupata Wapi Maadili Mazuri ya Kiroho?

Unaweza Kupata Wapi Maadili Mazuri ya Kiroho?

“IKIWA utakuwa mfuasi wa dini fulani kwa sababu tu ni dini ya familia yako, mbona usiwe mfuasi wa dini ya Waselti ambayo ilikuwa dini ya babu zetu walioishi miaka 2,000 iliyopita?,” Rodolphe auliza kwa dhihaka. Msikilizaji wake mchanga anatabasamu.

Rodolphe asema: “Uhusiano wangu pamoja na Mungu ni muhimu sana. Sikubali hata kidogo kulazimishwa kufuata imani fulani ya kidini kwa sababu tu watu wa familia yetu, walioishi makumi au mamia ya miaka iliyopita, walikuwa wafuasi wa dini fulani.” Rodolphe alichanganua mambo kwa makini; hakuchukua jambo hilo muhimu kama urithi tu.

Ingawa leo watu wengine hawakubali zoea la kurithi dini kutoka kizazi kimoja hadi kingine, bado walio wengi hufuata dini ya wazazi wao. Lakini je, inafaa sikuzote mtu ashikilie dini ya wazazi? Biblia inasemaje?

Baada ya miaka 40 jangwani, Yoshua aliyewaongoza Waisraeli baada ya Musa, aliwawekea mambo mawili wachague: “Nanyi kama mkiona ni vibaya kumtumikia BWANA, chagueni hivi leo mtakayemtumikia; kwamba ni miungu ile ambayo baba zenu waliitumikia nga’mbo ya Mto, au kwamba ni miungu ya wale Waamori ambao mnakaa katika nchi yao; lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia BWANA.”—Yoshua 24:15.

Mmojawapo wa baba ambao Yoshua alitaja ni Tera, baba ya Abrahamu, aliyeishi katika jiji la Uru, ambalo wakati huo lilikuwa mashariki ya Mto Frati. Biblia haisemi mengi kuhusu Tera mbali na kutaja kwamba aliabudu miungu mingine. (Yoshua 24:2) Hata ingawa Abrahamu, mwana wa Tera hakufahamu kabisa kusudi la Mungu, alikuwa tayari kuondoka jiji la kwao, Yehova alipomwamuru afanye hivyo. Naam, Abrahamu alichagua dini tofauti na ya baba yake. Kwa kufanya hivyo, Abrahamu alipokea baraka alizoahidiwa na Mungu na wafuasi wa dini nyingi wanamtambua kuwa ‘baba ya wale wote ambao wanamwamini Mungu.’—Waroma 4:11, Biblia Habari Njema.

Biblia pia husimulia kumhusu Ruthu, mzazi wa kale wa Yesu Kristo, aliyechukua hatua inayofaa. Ruthu, mwanamke Mmoabi aliyeolewa na Mwisraeli, alifiwa na mume na akakabili uchaguzi huu: kubaki katika nchi ya kwao au kurudi Israeli na mama-mkwe wake. Kwa kutambua kwamba ibada ya Yehova ilikuwa bora kuliko ibada ya sanamu ya wazazi wake, Ruthu alimwambia hivi mama-mkwe wake: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.”—Ruthu 1:16, 17.

Inapozungumzia umuhimu wa tukio hilo katika Biblia, kamusi iitwayo Dictionnaire de la Bible inasema kwamba simulizi hilo linaonyesha “jinsi kwa mwelekezo wa Mungu mwanamke aliyezaliwa ugenini miongoni mwa wapagani wenye uhasama waliochukiwa na Waisraeli, . . . alivyopata kuwa mzazi wa kale wa Mfalme Daudi mtakatifu, kwa sababu alipenda taifa la Yehova na ibada yake.” Ruthu hakusita kuchagua dini iliyokuwa tofauti na dini ya wazazi wake, na kwa kufanya hivyo alibarikiwa na Mungu.

Sababu zilizofanya wafuasi wa Yesu waache dini ya babu zao zinaelezwa wazi zaidi katika simulizi kuhusu mwanzo wa Ukristo. Mtume Petro alitoa hotuba yenye ushawishi sana na kuwasihi wasikilizaji wake ‘waokolewe kutokana na kizazi hiki kilicho kombo’ kwa kutubu dhambi zao na kubatizwa katika jina la Yesu Kristo. (Matendo 2:37-41) Kisa kimoja kinachojulikana sana ni cha Sauli, Myahudi aliyewanyanyasa Wakristo. Alipokuwa njiani kuelekea Damasko alimwona Kristo katika maono, baada ya hapo Sauli akawa Mkristo na akaitwa mtume Paulo.—Matendo 9:1-9.

Wakristo wengi wa mapema hawakupata maono kama hayo. Lakini wote walipaswa kuacha Dini ya Kiyahudi au ibada ya miungu mbalimbali ya wapagani. Wale walioukubali Ukristo walifanya hivyo baada ya kupata ujuzi sahihi, na mara nyingi hilo liliwezekana kwa kujadiliana sana kumhusu Yesu akiwa Mesiya. (Matendo 8:26-40; 13:16-43; 17:22-34) Wakristo hao wa mapema walielezwa waziwazi kwamba walipaswa kufanya mabadiliko maishani. Mwito ulitolewa kwa Wayahudi na watu wasio Wayahudi, lakini ujumbe ulikuwa uleule. Ili kumpendeza Mungu walipaswa kufuata njia mpya ya kuabudu, yaani, Ukristo.

Uchaguzi Unaotuhusu

Bila shaka ujasiri ulihitajiwa katika karne ya kwanza ili kuacha mapokeo ya dini ya familia—Dini ya Kiyahudi, ibada ya maliki, ibada ya miungu ya wapagani—na kujiunga na dini iliyodharauliwa na Wayahudi na Waroma. Baada ya muda usio mrefu, wale waliochagua kufanya hivyo waliteswa vikali. Leo, ujasiri unahitajiwa ili kukataa ‘kuwa kama wengine,’ kama anavyosema askofu wa Kanisa Katoliki la Clermont-Ferrand, Hippolyte Simon, katika kitabu chake Vers une France païenne? (Je, Upagani Unaenea Ufaransa?) Ujasiri unahitajiwa ili kushirikiana na dini ndogo ya Mashahidi wa Yehova ambayo nyakati nyingine huchambuliwa.

Paul, kijana mmoja wa Bastia, Corsica, aliyelelewa na wazazi Wakatoliki, alishiriki mara kwa mara katika shughuli mbalimbali za kanisa, kama vile kuuza keki ili kuchangisha pesa kwa ajili ya shirika fulani la kutoa misaada la Kanisa Katoliki. Kwa sababu alitaka kuelewa Biblia vizuri zaidi, alikubali kuizungumzia pamoja na Mashahidi wa Yehova kwa ukawaida. Baada ya muda mfupi alitambua kwamba mambo aliyokuwa akijifunza yangemnufaisha milele. Kwa hiyo, Paul alikubali kanuni za Biblia na akawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Wazazi wake waliheshimu uamuzi wake, na huo haujaharibu uhusiano wa karibu katika familia yao.

Amélie anaishi kusini mwa Ufaransa. Watu wa familia yake wamekuwa Mashahidi wa Yehova kwa vizazi vinne. Kwa nini aliamua kukubali dini ya wazazi wake? Anasema: “Huwi Shahidi wa Yehova kwa sababu wazazi wako ni Mashahidi, au kwa sababu babu na nyanya yako walikuwa Mashahidi wa Yehova. Lakini siku moja utajiambia hivi, ‘Hii ni dini yangu kwa sababu hivyo ndivyo ninavyoamini.’” Kama vile vijana wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, Amélie anajua kwamba ana kusudi maishani na furaha ya kudumu kwa sababu ya imani yake thabiti.

Kwa Nini Ukubali Kanuni za Mungu?

Kitabu cha Mithali sura ya 6, mstari wa 20, kinawatia moyo wale wanaotaka kumpendeza Mungu, kinaposema hivi: “Mwanangu, shika maagizo ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” Badala ya kuwatia moyo watii bila kufikiri, shauri hilo linawahimiza vijana wakubali kanuni za Mungu kwa kuimarisha imani yao na kwa kuchukua msimamo wao upande wa Mungu. Mtume Paulo aliwaomba wenzake ‘wahakikishe mambo yote,’ wachunguze iwapo yale waliyokuwa wakifundishwa yalipatana na Neno la Mungu na mapenzi Yake na kutenda kupatana nayo.—1 Wathesalonike 5:21.

Wawe wamelelewa katika familia za Kikristo au la, Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni sita, vijana kwa wazee, wamefanya uamuzi huo. Baada ya kujifunza Biblia kwa makini, wamepata majibu ya kweli kuhusu kusudi la maisha na wameelewa wazi mapenzi ya Mungu kwa wanadamu. Baada ya kupata ujuzi huo, wamekubali kanuni za Mungu na wanafanya mapenzi ya Mungu kwa kadiri wanavyoweza.

Iwe unasoma gazeti hili kwa ukawaida au la, mbona usikubali Mashahidi wa Yehova wakusaidie kujifunza Biblia na kuchunguza kanuni zake za kiroho? Kwa njia hiyo, utaweza ‘kuonja na kuona ya kuwa BWANA yu mwema’ na kupata ujuzi ambao, ukiutumia maishani, utakuongoza kwenye uhai wa milele.—Zaburi 34:8; Yohana 17:3.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Vizazi vinne vya familia ya Mashahidi wa Yehova nchini Ufaransa

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ruthu aliamua kumtumikia Yehova badala ya miungu ya babu zake