Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Wanaofurahisha Moyo wa Yehova

Vijana Wanaofurahisha Moyo wa Yehova

Vijana Wanaofurahisha Moyo wa Yehova

Makala haya ya funzo yaliandikwa hasa kwa ajili ya vijana miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, tunawatia moyo vijana wajifunze makala haya kwa makini na kutoa maelezo wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi kutanikoni.

“Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; Ili nipate kumjibu anilaumuye.”—Mithali 27:11.

1, 2. (a) Ikiwa unavutiwa na mambo ya ulimwengu, je, hiyo inamaanisha kwamba hufai kuwa Mkristo? (Waroma 7:21) (b) Unajifunza nini kutokana na mfano wa Asafu? (Ona sanduku, ukurasa wa 13.)

WAZIA kwamba unanunua nguo. Unapotafuta-tafuta unaona nguo inayokuvutia. Mtindo na rangi zinakufaa kabisa, na bei yake ni nafuu sana. Lakini unapoichunguza kwa makini zaidi unatambua kwamba kitambaa kimechakaa kwenye pindo na nguo hiyo imeshonwa ovyoovyo. Ijapokuwa inavutia, nguo hiyo ni duni. Je, ungenunua nguo duni kama hiyo?

2 Linganisha hilo na hali unayoweza kukabili ukiwa kijana Mkristo. Kama vile nguo hiyo inavyovutia unapoiona kwa mara ya kwanza, ndivyo ilivyo na mambo ya ulimwengu. Kwa mfano, huenda wanafunzi wenzako wanaenda kwenye karamu zinazofurahisha, wanatumia dawa za kulevya na vileo, na wasichana na wavulana wanafanya urafiki bila kusudi la kuoana, na hata wanafanya uasherati. Je, nyakati nyingine unavutiwa na maisha hayo? Je, unatamani kuishi angalau kwa muda mfupi maisha hayo yanayosemekana eti ni yenye uhuru? Ikiwa ndivyo, usikate kauli haraka kwamba wewe ni mwovu na hufai kuwa Mkristo. Ukweli ni kwamba Biblia inaonyesha kuwa hata mtu anayetaka kumpendeza Mungu anaweza kuvutiwa sana na ulimwengu.—2 Timotheo 4:10.

3. (a) Kwa nini ni ubatili kufuatia mambo ya ulimwengu? (b) Mkristo mmoja anaelezaje ubatili wa kufuatia mambo ya ulimwengu?

3 Tafadhali sasa chunguza mambo ya ulimwengu kwa makini kama vile ungechunguza nguo unayotaka kununua. Jiulize hivi: ‘Ulimwengu huu una ubora gani?’ Biblia inasema kwamba “ulimwengu unapitilia mbali.” (1 Yohana 2:17) Raha yoyote inayopatikana humo ni ya muda tu. Isitoshe, mwenendo mpotovu unaleta matokeo mabaya. Hauna faida yoyote. Mkristo mmoja ambaye “ameteseka kwa sababu ya mwenendo mpotovu wa ujanani” anasema hivi: “Huenda ulimwengu ukaonekana kuwa wenye kupendeza na kuvutia. Nao unataka uamini kwamba unaweza kupata raha za ulimwengu bila kuumia. Lakini hilo haliwezekani. Ulimwengu utakudanganya, kisha utakutupa.” * Mbona uharibu ujana wako kwa kuishi maisha mapotovu?

Kulindwa Dhidi ya “Yule Mwovu”

4, 5. (a) Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alimwomba Yehova nini katika sala? (b) Kwa nini ombi hilo lilifaa?

4 Vijana miongoni mwa Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuepuka urafiki na ulimwengu huu kwa sababu wanatambua kwamba ulimwengu huu hauwezi kuwapa vijana kitu chochote chenye thamani halisi. (Yakobo 4:4) Je, wewe ni mmojawapo wa vijana hao waaminifu? Ikiwa ndivyo unastahili pongezi. Ni kweli kwamba si rahisi kuwa tofauti na vijana wengine na kupinga vishawishi vyao, lakini unaweza kupata msaada.

5 Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alisali kwa Yehova ‘awalinde’ wanafunzi wake “kwa sababu ya yule mwovu.” (Yohana 17:15) Yesu alikuwa na sababu nzuri ya kusali hivyo. Alijua kwamba haingekuwa rahisi kwa wafuasi wake kudumisha uaminifu, licha ya umri wao. Kwa nini? Yesu alijua kwamba wanafunzi wake wangemkabili adui mwenye nguvu asiyeonekana, yaani, “yule mwovu,” Shetani Ibilisi. Biblia inasema kwamba roho huyo mwovu “hutembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.”—1 Petro 5:8.

6. Tunajuaje kwamba Shetani hawahurumii vijana?

6 Tangu zamani, Shetani amefurahia kuwatesa wanadamu kikatili. Fikiria misiba mibaya ambayo Shetani alimletea Ayubu na familia yake. (Ayubu 1:13-19; 2:7) Huenda ukakumbuka mambo ambayo umesikia maishani mwako yanayoonyesha roho yenye jeuri ya Shetani. Ibilisi anatembea-tembea akitafuta mtu wa kunyafua, naye hawahurumii vijana. Kwa mfano, mwanzoni mwa karne ya kwanza W.K., Herode alitunga hila ya kuwaua wavulana wote Bethlehemu waliokuwa na umri wa miaka miwili au kwenda chini. (Mathayo 2:16) Inaelekea Shetani ndiye aliyemchochea Herode kufanya hivyo, kwa sababu alitaka kumwua yule mtoto ambaye siku moja angekuwa Mesiya aliyeahidiwa na kuleta hukumu ya Mungu juu ya Shetani! (Mwanzo 3:15) Ni wazi kwamba Shetani hawahurumii vijana hata kidogo. Lengo lake hasa ni kunyafua wanadamu wengi iwezekanavyo. Anafanya hivyo hasa wakati huu kwa sababu amevurumishwa kutoka mbinguni hadi duniani, “akiwa na hasira kubwa, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:9, 12.

7. (a) Yehova anatofautianaje sana na Shetani? (b) Yehova anahisije unapofurahia maisha?

7 Tofauti na Shetani, aliye na “hasira kubwa,” Yehova ni mwenye “huruma nyororo.” (Luka 1:78) Upendo wake hauna kifani. Muumba ana upendo mwingi sana hivi kwamba Biblia inasema: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Kuna tofauti kubwa kama nini kati ya mungu wa ulimwengu huu na Mungu ambaye una pendeleo la kumwabudu! Shetani anataka kunyafua, lakini Yehova “hataki yeyote aangamizwe.” (2 Petro 3:9) Anaona uhai wa kila mwanadamu kuwa wenye thamani kutia ndani uhai wako. Yehova anapokushauri katika Neno lake usiwe sehemu ya ulimwengu, hataki kukuzuia usifurahie maisha au kukunyima uhuru. (Yohana 15:19) Badala yake anakulinda kwa sababu ya yule mwovu. Baba yako wa mbinguni anataka uwe na maisha bora badala ya maisha ya raha ya muda ya ulimwengu huu. Anataka upate “uhai ulio halisi,” yaani, uhai wa milele katika dunia paradiso. (1 Timotheo 6:17-19) Yehova anataka ufanikiwe, naye anakusihi ufikie mradi huo. (1 Timotheo 2:4) Isitoshe, Yehova anakupa mwaliko wa pekee. Ni mwaliko gani huo?

‘Furahisha Moyo Wangu’

8, 9. (a) Unaweza kumpa Yehova zawadi gani? (b) Shetani anamlaumuje Yehova, kama inavyoonyeshwa na kisa cha Ayubu?

8 Je, umewahi kumnunulia rafiki yako wa karibu zawadi, na kumwona akitabasamu kwa mshangao na uthamini anapoipokea? Yaelekea ulifikiri sana ni zawadi ya aina gani ambayo ingemfaa mtu huyo. Sasa fikiria swali hili: Unaweza kumpa Muumba wako, Yehova Mungu, zawadi gani? Huenda mwanzoni ukaona kwamba jambo hilo haliwezekani. Mungu Mweza Yote anahitaji nini kutoka kwa mwanadamu duni? Unaweza kumpa nini ambacho hana? Biblia inajibu hivi kwenye Mithali 27:11: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.”

9 Huenda kupitia funzo lako la Biblia unajua kwamba Shetani Ibilisi ndiye anayemlaumu Yehova. Anadai kwamba wale wanaomtumikia Mungu wanamtumikia kwa sababu za ubinafsi wala si kwa sababu ya upendo. Shetani anadai kwamba wataacha ibada ya kweli wakipata magumu. Kwa mfano, fikiria kile ambacho Shetani alimwambia Yehova kumhusu mtu mwadilifu Ayubu: “Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi. Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako.”—Ayubu 1:10, 11.

10. (a) Tunajuaje kwamba Shetani hakutilia shaka uaminifu wa Ayubu peke yake? (b) Unahusikaje katika suala la enzi kuu?

10 Kama Biblia inavyoonyesha, Shetani alitilia shaka uaminifu wa Ayubu na pia wengine wote wanaomtumikia Mungu, kutia ndani wewe. Naam, Shetani alimwambia Yehova hivi alipokuwa akizungumza kuwahusu wanadamu kwa ujumla: “Yote aliyo nayo mtu [si Ayubu tu bali mtu yeyote] atayatoa kwa ajili ya uhai wake.” (Ayubu 2:4) Je, unaona jinsi unavyohusika katika suala hilo muhimu? Kama inavyoonyeshwa na Mithali 27:11, Yehova anasema kwamba unaweza kumpa msingi wa kumjibu Shetani anayemlaumu. Wazia Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu anakusihi wewe utoe jibu kuhusiana na suala kuu lililopo. Hilo ni daraka na pendeleo kubwa sana. Je, unaweza kutimiza yale ambayo Yehova anakusihi ufanye? Ayubu aliyatimiza. (Ayubu 2:9, 10) Ndivyo alivyofanya Yesu na vilevile wengine wengi tangu zamani, kutia ndani vijana. (Wafilipi 2:8; Ufunuo 6:9) Unaweza kufanya vivyo hivyo. Hata hivyo, unapaswa kujua kwamba ni lazima uunge mkono upande mmoja katika suala hilo. Kupitia mwenendo wako utaonyesha kwamba unatetea lawama ya Shetani au jibu la Yehova. Utatetea nini?

Yehova Anakujali!

11, 12. Je, uchaguzi wako wa kumtumikia au kutomtumikia Yehova ni muhimu kwake? Eleza.

11 Je, uchaguzi wako ni muhimu machoni pa Yehova? Je, uaminifu ambao watu wengi wameonyesha hautoshi kumpa sababu ya kumjibu Shetani? Ibilisi alidai kwamba hakuna mtu anayemtumikia Yehova kwa sababu ya kumpenda, dai ambalo limekwisha thibitishwa kuwa la uwongo. Lakini bado Yehova anataka uunge mkono upande wake katika suala la enzi kuu kwa sababu anakujali. Yesu alisema hivi: “Si jambo la kutamanika kwa Baba yangu aliye mbinguni kwa mmoja wa wadogo hawa kuangamia.”—Mathayo 18:14.

12 Ni wazi kwamba, Yehova anapendezwa na uchaguzi wako. Jambo muhimu zaidi ni kwamba anaathiriwa nao. Biblia inaonyesha wazi kwamba Yehova ana hisia ambazo huchochewa na mwenendo mzuri au mbaya wa binadamu. Kwa mfano, Yehova ‘alihuzunika,’ Waisraeli walipomwasi tena na tena. (Zaburi 78:40, 41) Kabla ya Gharika ya siku za Noa, wakati ‘maovu ya mwanadamu yalipokuwa makubwa,’ Yehova ‘alihuzunika moyo.’ (Mwanzo 6:5, 6) Fikiria maana ya jambo hilo. Ukiamua kuwa na mwenendo mbaya, utamhuzunisha Muumba wako. Hiyo haimaanishi kwamba Mungu ni dhaifu au anaongozwa na hisia tu. Badala yake anakupenda na kukujali. Kwa upande mwingine, unapofanya yanayofaa unafurahisha moyo wa Yehova. Yeye hufurahi kwa sababu anapata sababu nyingine ya kumjibu Shetani, na pia kwa sababu anaweza kukupa thawabu. Ndivyo anavyotaka kufanya. (Waebrania 11:6) Yehova Mungu ni Baba mwenye upendo kama nini!

Baraka Tele Sasa

13. Tunabarikiwaje sasa kwa kumtumikia Yehova?

13 Baraka za kumtumikia Yehova hazitapatikana tu wakati ujao. Vijana wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wana sababu nzuri za kuwa na shangwe na uradhi sasa. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Maagizo ya BWANA ni ya adili, huufurahisha moyo.” (Zaburi 19:8) Yehova anajua vizuri zaidi kile kinachotufaa kuliko mwanadamu yeyote. Yehova alisema hivi kupitia nabii Isaya: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata. Laiti ungalisikiliza amri zangu! ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari.”—Isaya 48:17, 18.

14. Kanuni za Biblia zinawezaje kukusaidia kuepuka deni lenye kulemea?

14 Kufuata kanuni za Biblia kutakusaidia kuepuka huzuni na uchungu mwingi. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba wale wanaopenda pesa “wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Je, baadhi ya rafiki zako wamepatwa na matokeo mabaya yanayotajwa katika andiko hilo? Baadhi ya wanaume na wanawake vijana wana madeni makubwa kwa sababu wanataka kuwa na nguo za mitindo maarufu na vitu vya karibuni. Kununua vitu usivyoweza kugharimia na hivyo kujikuta umelemewa kwa muda mrefu na mkopo wenye riba kubwa, ni utumwa unaoumiza!—Mithali 22:7.

15. Kanuni za Biblia zinakulindaje na matokeo yenye kuhuzunisha ya uasherati?

15 Fikiria pia uasherati. Ulimwenguni pote vijana wengi wasiofunga ndoa hupata mimba kila mwaka. Baadhi yao huzaa watoto wasiowataka wala wasio na uwezo wa kuwalea. Wengine hutoa mimba na hivyo husumbuliwa sana na dhamiri. Kisha kuna wanaume na wanawake vijana ambao hupata magonjwa yanayoambukizwa kupitia ngono, kama vile UKIMWI. Bila shaka kupoteza uhusiano mzuri pamoja na Yehova ndilo tokeo baya zaidi linaloweza kumpata mtu anayemjua Yehova. * (Wagalatia 5:19-21) Biblia ina sababu nzuri ya kusema hivi: “Ukimbieni uasherati.”—1 Wakorintho 6:18.

Kumtumikia “Mungu Mwenye Furaha”

16. (a) Tunajuaje kwamba Yehova anataka uufurahie ujana wako? (b) Kwa nini Yehova anakuwekea miongozo ya kufuata?

16 Biblia inamtaja Yehova kuwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Anataka wewe uwe mwenye furaha pia. Neno lake mwenyewe linasema hivi: “Uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako.” (Mhubiri 11:9) Lakini Yehova anaona matokeo ya muda mrefu ya mwenendo mzuri au mbaya. Ndiyo sababu anakusihi: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku zilizo mbaya, wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo.”—Mhubiri 12:1.

17, 18. Kijana mmoja Mkristo alisema nini kuhusu furaha anayopata kwa kumtumikia Yehova, nawe unawezaje kupata furaha hiyo?

17 Leo vijana wengi wamepata furaha kwa kumtumikia Yehova. Kwa mfano, Lina mwenye umri wa miaka 15 anasema hivi: “Ninaweza kujiheshimu na kujitumaini. Nina afya nzuri kwa sababu sivuti sigara wala situmii dawa za kulevya. Ninapata mwongozo mzuri katika kutaniko ambao hunisaidia kushinda vishawishi vya Shetani. Ninafurahi sana kwa sababu ya ushirika wenye kujenga kwenye Jumba la Ufalme. Zaidi ya yote, nina tumaini lisilo na kifani la kuishi milele duniani.”

18 Kama Lina, vijana wengi Wakristo wanapigania imani kwa bidii na hiyo inawaletea shangwe. Wanajua kwamba ijapokuwa maisha yao ni magumu nyakati nyingine, wana kusudi maishani na tumaini halisi la wakati ujao. Kwa hiyo endelea kumtumikia Mungu anayekujali sana. Furahisha moyo wake, naye atakufurahisha sasa na milele!—Zaburi 5:11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ona makala “Kweli Ilinirudishia Uhai Wangu,” katika toleo la Amkeni! la Oktoba 22, 1996.

^ fu. 15 Inafariji kujua kwamba mtu anapotubu, anapoacha kufanya mabaya, na kukiri dhambi zake, Yehova “atamsamehe kabisa.”—Isaya 55:7.

Je, Unakumbuka?

• Unakabili hatari gani kutoka kwa “yule mwovu,” Shetani?

• Unawezaje kuufurahisha moyo wa Yehova?

• Biblia inaonyeshaje kwamba Yehova anakujali?

• Baadhi ya baraka tunazopata kwa kumtumikia Yehova ni zipi?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 13]

Mtu Mwadilifu Karibu Ajikwae

Asafu alikuwa mwanamuziki Mlawi mashuhuri kwenye hekalu la Yehova katika taifa la Israeli la kale. Hata alitunga nyimbo zilizotumiwa katika ibada ya watu wote. Ijapokuwa alikuwa na mapendeleo ya pekee, kwa muda fulani, Asafu alijikuta akivutiwa na mwenendo wa watu wasiomwogopa Mungu walioonekana kuwa wanavunja sheria za Mungu bila kuadhibiwa. Baadaye Asafu alisema hivi: “Miguu yangu ilikuwa karibu na kupotoka, hatua zangu zilikuwa karibu na kuteleza. Maana naliwaonea wivu wenye kujivuna, nilipoiona hali ya amani ya wasio haki.”—Zaburi 73:2, 3.

Baadaye Asafu alienda kwenye patakatifu pa Mungu na kusali kuhusu jambo hilo. Alipoweza kuchanganua tena mambo kwa njia ya kiroho, alielewa kwamba Yehova anachukia ubaya na kwamba mwishowe, waovu na waadilifu watavuna wanayopanda. (Zaburi 73:17-20; Wagalatia 6:7, 8) Kwa kweli, waovu wako kwenye utelezi. Hatimaye wataanguka Yehova atakapoharibu ulimwengu huu usiomwogopa.—Ufunuo 21:8.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yehova anakujali sana lakini Shetani ana lengo la kukunyafua

[Picha katika ukurasa wa 16]

Vijana wengi wanapata furaha kubwa kwa kumtumikia Yehova pamoja na Wakristo wenzao