Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Faraja ya Kweli Inaweza Kupatikana Wapi?

Faraja ya Kweli Inaweza Kupatikana Wapi?

Faraja ya Kweli Inaweza Kupatikana Wapi?

“Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo . . . hutufariji katika dhiki yetu yote.”—2 WAKORINTHO 1:3, 4.

1. Ni hali zipi zinazoweza kuwafanya watu wahisi kwamba wanahitaji sana faraja?

UGONJWA wenye kudhoofisha unaweza kumfanya mtu ahisi kwamba maisha yake yameharibika. Matetemeko ya ardhi, dhoruba, na njaa huwaacha watu katika hali ya ufukara. Huenda vita vikasababisha vifo vya washiriki wa familia, vikaharibu nyumba, au kufanya watu waache nyumba na mali zao. Ukosefu wa haki unaweza kuwafanya watu wahisi kwamba hakuna mahali pa kupata kitulizo. Wale wanaopatwa na taabu hizo, wanahitaji sana faraja. Inaweza kupatikana wapi?

2. Kwa nini faraja inayotolewa na Yehova haina kifani?

2 Watu na mashirika fulani hujitahidi kutoa faraja. Maneno yenye fadhili yanathaminiwa. Misaada inayotolewa hutimiza mahitaji kwa muda mfupi. Lakini Yehova pekee, Mungu wa kweli, ndiye anayeweza kuondoa madhara yote na kutoa msaada unaohitajiwa ili misiba kama hiyo isitokee tena. Biblia inasema hivi kumhusu: “Mbarikiwa na awe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tupate kuweza kufariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki kupitia faraja ambayo kwayo sisi wenyewe tunafarijiwa na Mungu.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Yehova hutufariji jinsi gani?

Kuondoa Mambo Yanayosababisha Matatizo

3. Faraja ambayo Mungu hutoa inaonyeshaje mambo yanayosababisha matatizo ya wanadamu?

3 Kwa sababu ya dhambi ya Adamu, wanadamu wote wamerithi hali ya kutokamilika na hiyo husababisha matatizo mengi ambayo hatimaye huleta kifo. (Waroma 5:12) Hali hiyo inakuwa mbaya zaidi kwa sababu Shetani Ibilisi ndiye “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19) Yehova hakusikitishwa tu na hali mbaya inayowakabili wanadamu. Alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee kuwa fidia ili atoe ukombozi, naye alituambia kwamba tunaweza kusamehewa dhambi tuliyorithi kutoka kwa Adamu iwapo tutadhihirisha imani katika Mwana Wake. (Yohana 3:16; 1 Yohana 4:10) Mungu pia alitabiri kwamba Yesu Kristo, ambaye amepewa mamlaka yote mbinguni na duniani, atamharibu Shetani na ulimwengu wake wote mwovu.—Mathayo 28:18; 1 Yohana 3:8; Ufunuo 6:2; 20:10.

4. (a) Yehova ameandaa nini ili kuimarisha tumaini letu katika ahadi zake za kutukomboa? (b) Yehova anatusaidiaje kujua wakati atakapotukomboa?

4 Ili kuimarisha tumaini letu katika ahadi zake, Mungu ameandikisha uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba yote anayotabiri hutimia. (Yoshua 23:14) Katika simulizi la Biblia alitia ndani mambo ambayo amefanya ili kuwakomboa watumishi wake kutoka katika hali ambazo kwa maoni ya wanadamu haingewezekana kuwakomboa. (Kutoka 14:4-31; 2 Wafalme 18:13–19:37) Kupitia kwa Yesu Kristo, Yehova alionyesha kwamba kusudi lake linatia ndani kuwaponya watu “kila namna ya maradhi,” hata kuwafufua wafu. (Mathayo 9:35; 11:3-6) Mambo hayo yote yatatimizwa lini? Biblia inajibu kwa kueleza kuhusu siku za mwisho za ulimwengu huu wa kale zitakazofuatwa na mbingu mpya na dunia mpya ya Mungu. Yale ambayo Yesu alitabiri kuhusu siku hizo yanatimia wakati huu wetu.—Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5.

Faraja kwa Watu Wanaoteseka

5. Alipowafariji Waisraeli wa kale, Yehova alitaka wafikirie mambo gani?

5 Tunajifunza jinsi Yehova alivyowafariji Waisraeli wa kale kutokana na namna alivyoshughulika nao. Aliwakumbusha sifa zake. Hilo liliimarisha tumaini lao katika ahadi zake. Yehova aliwafanya manabii wake waonyeshe waziwazi tofauti iliyopo kati yake akiwa Mungu wa kweli aliye hai, na sanamu, zisizoweza kujisaidia wala kuwasaidia waabudu wake. (Isaya 41:10; 46:1; Yeremia 10:2-15) Yehova alipomwambia Isaya, ‘Wafariji, wafariji watu wangu,’ alimhimiza nabii wake atumie mifano na ufafanuzi mbalimbali kuhusu uumbaji Wake ili kukazia ukuu wa Yehova aliye Mungu wa pekee wa kweli.—Isaya 40:1-31, ZSB.

6. Yehova alitaja nini nyakati nyingine ili kuonyesha wakati ambapo ukombozi ungetazamiwa?

6 Pindi fulani, Yehova aliwafariji watu wake kwa kutaja wakati hususa ambapo wangekombolewa, iwe ni baada ya muda mfupi au mrefu. Wakati wa kuwakomboa Waisraeli walioteseka Misri ulipokaribia, aliwaambia hivi: “Liko pigo moja bado, nitakaloleta juu ya Farao na juu ya Misri; baadaye atawapa ninyi ruhusa mtoke huku.” (Kutoka 11:1) Wakati mataifa matatu yalipoungana na kuvamia Yuda katika siku za Mfalme Yehoshafati, Yehova aliwaambia kwamba angewakomboa “kesho.” (2 Mambo ya Nyakati 20:1-4, 14-17) Kwa upande mwingine, kukombolewa kwao kutoka Babiloni kulikuwa kumetabiriwa na Isaya miaka 200 mapema, na habari zaidi zilitolewa na nabii Yeremia miaka 100 hivi kabla ya ukombozi huo. Unabii huo uliwatia moyo sana watumishi wa Mungu wakati kukombolewa kwao kulipokaribia!—Isaya 44:26–45:3; Yeremia 25:11-14.

7. Mara nyingi ahadi za ukombozi zilitia ndani nini, na Waisraeli waaminifu walitendaje kuhusiana nazo?

7 Jambo la kupendeza ni kwamba ahadi zilizowafariji watu wa Mungu mara nyingi zilitia ndani habari kumhusu Mesiya. (Isaya 53:1-12) Habari hiyo iliwapa watu waaminifu tumaini walipokabili majaribu mbalimbali, kizazi baada ya kizazi. Tunasoma hivi katika Luka 2:25: “Tazama! palikuwa na mtu mmoja katika Yerusalemu aliyeitwa jina Simeoni, na mwanamume huyu alikuwa mwadilifu na mwenye kumstahi Mungu, akingojea liwazo la Israeli [au, faraja; yaani, kuja kwa Mesiya], na roho takatifu ilikuwa juu yake.” Simeoni alijua tumaini la Maandiko kumhusu Mesiya, na alionyesha katika maisha yake kwamba alitarajia kuona utimizo wa ahadi hizo. Hakuelewa jinsi ahadi hizo zingetimizwa, naye alikufa kabla ya kuona wokovu uliokuwa umetabiriwa, lakini alifurahi alipomtambua Yule ambaye angekuwa ‘njia ya Mungu ya kuokoa.’—Luka 2:30.

Faraja Iliyotolewa Kupitia Kristo

8. Msaada ambao Yesu alitoa ulitofautianaje na msaada ambao watu wengi walifikiri walihitaji?

8 Yesu Kristo alipokuwa akiendelea na huduma yake duniani, mara nyingi hakutoa msaada ambao watu walifikiri walihitaji. Baadhi yao walitazamia kwamba Mesiya angewakomboa kutoka katika utawala wa Roma waliouchukia. Lakini Yesu hakuunga mkono mapinduzi; aliwaambia, “mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari.” (Mathayo 22:21) Kusudi la Mungu lilihusisha mengi zaidi ya kuwakomboa watu kutoka katika utawala fulani wa kisiasa. Watu walitaka kumfanya Yesu awe mfalme, lakini alisema kwamba ‘angetoa nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.’ (Mathayo 20:28; Yohana 6:15) Wakati wake wa kuwa mfalme haukuwa umefika, na Yehova ndiye angempa mamlaka ya kutawala wala si wanadamu wasioridhika.

9. (a) Yesu alihubiri ujumbe gani wa faraja? (b) Yesu alionyeshaje kwamba ujumbe aliohubiri ulihusu hali mbalimbali ambazo watu walikabili? (c) Huduma ya Yesu ingekuwa na matokeo gani ya baadaye?

9 Yesu alileta faraja kupitia “habari njema ya ufalme wa Mungu.” Huo ndio ujumbe ambao Yesu alihubiri popote alipoenda. (Luka 4:43) Alikazia jinsi ujumbe huo ulivyohusu matatizo ya kawaida ya watu kwa kuonyesha yale atakayowafanyia wanadamu akiwa Mesiya, chini ya Utawala wake wa Ufalme. Aliwapa watu walioteseka kusudi maishani kwa kuwarudishia uwezo wao wa kuona na kusema (Mathayo 12:22; Marko 10:51, 52), kuwaponya vilema (Marko 2:3-12), kuwaponya Waisraeli wenzake magonjwa yenye kuchukiza (Luka 5:12, 13), na magonjwa mengine mabaya sana. (Marko 5:25-29) Kwa kuwafufua watoto waliokuwa wamekufa, aliwafariji sana watu wa familia zao waliokuwa wakiomboleza. (Luka 7:11-15; 8:49-56) Alidhihirisha uwezo wake wa kudhibiti dhoruba hatari na kutosheleza mahitaji ya umati wa watu waliohitaji chakula. (Marko 4:37-41; 8:2-9) Isitoshe, Yesu aliwafundisha kanuni za maisha ambazo zingeweza kuwasaidia kushughulikia matatizo kwa njia inayofaa na ambazo zingewapa tumaini la kupata utawala wa haki chini ya Mesiya. Kwa hiyo, Yesu alipoendelea na huduma yake, mbali na kuwafariji waliomsikiliza kwa imani, huduma yake ingewapa watu kitia-moyo maelfu ya miaka baadaye.

10. Ni mambo gani yanayowezekana kupitia dhabihu ya Yesu?

10 Zaidi ya miaka 60 baada ya Yesu kutoa uhai wake wa kibinadamu kuwa dhabihu na kufufuliwa kwenda mbinguni, mtume Yohana aliongozwa na roho kuandika hivi: “Watoto wangu wadogo, nawaandikia nyinyi mambo haya ili msifanye dhambi. Na bado, ikiwa yeyote afanya hasa dhambi, tuna msaidiaji kwa Baba, Yesu Kristo, aliye mwadilifu. Na yeye ni dhabihu yenye kufunika kwa ajili ya dhambi zetu, lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya zile za ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:1, 2) Tunapata faraja kubwa kutokana na dhabihu kamilifu ya kibinadamu ya Yesu. Tunajua kwamba tunaweza kupata msamaha wa dhambi, dhamiri safi, uhusiano mzuri pamoja na Mungu, na tumaini la kuishi milele.—Yohana 14:6; Waroma 6:23; Waebrania 9:24-28; 1 Petro 3:21.

Roho Takatifu Hutoa Faraja

11. Kabla ya kifo chake, Yesu aliahidi kwamba angefanya mpango gani mwingine wa kutoa faraja?

11 Alipokuwa pamoja na mitume wake jioni ya mwisho kabla ya kutoa uhai wake kuwa dhabihu, Yesu alisema kuhusu mpango mwingine ambao Baba yake wa kimbingu alikuwa amefanya ili kuwapa faraja. Yesu alisema hivi: “Nami hakika nitamwomba Baba naye atawapa nyinyi msaidiaji mwingine [mfariji; pa·raʹkle·tos, katika Kigiriki] awe pamoja nanyi milele, roho ya ile kweli.” Yesu aliwahakikishia hivi: “Msaidiaji, roho takatifu, . . . itawafundisha nyinyi mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.” (Yohana 14:16, 17, 26) Roho takatifu iliwapa faraja jinsi gani?

12. Watu wengi wamepataje faraja kwa sababu roho takatifu iliwasaidia wanafunzi wa Yesu kukumbuka mambo?

12 Mitume walikuwa wamefundishwa mambo mengi na Yesu. Bila shaka hawakusahau kamwe kwamba aliwafundisha, lakini je, walikumbuka yale aliyosema? Je walisahau mafundisho muhimu kwa sababu ya kutokamilika? Yesu aliwahakikishia kwamba roho takatifu ‘ingewakumbusha mambo yote aliyowaambia.’ Kwa hiyo, miaka minane hivi baada ya Yesu kufa, Mathayo aliandika Injili ya kwanza, inayotia ndani Mahubiri ya Mlimani ya Yesu yenye kuchangamsha, mifano mingi aliyotoa kuhusu Ufalme, na habari kamili kuhusu ishara ya kuwapo kwake. Zaidi ya miaka 50 baadaye, mtume Yohana aliandika masimulizi yanayoaminika yenye habari nyingi kuhusu siku chache za mwisho za maisha ya Yesu duniani. Masimulizi hayo yaliyoandikwa chini ya uongozi wa roho yamewafariji watu sana mpaka siku zetu.

13. Roho takatifu iliwafundishaje Wakristo wa mapema?

13 Mbali na kuwakumbusha tu maneno ya Yesu, roho takatifu iliwafundisha na kuwaongoza wanafunzi hao waelewe kusudi la Mungu vizuri zaidi. Yesu alipokuwa na wanafunzi wake, aliwaambia mambo ambayo hawakuyaelewa waziwazi wakati huo. Hata hivyo, baadaye Yohana, Petro, Yakobo, Yuda, na Paulo, waliongozwa na roho takatifu kueleza katika maandishi yao mambo mengi zaidi kuhusu kusudi la Mungu. Kwa hiyo, roho takatifu iliwafundisha na hivyo kuwapa wanafunzi uhakikisho mzuri kwamba waliongozwa na Mungu.

14. Roho takatifu iliwasaidiaje watu wa Yehova?

14 Uwezo wa kufanya miujiza kupitia kwa roho ulionyesha wazi kwamba sasa kibali cha Mungu kilikuwa juu ya kutaniko la Kikristo wala si juu ya taifa la Israeli la asili. (Waebrania 2:4) Jambo jingine muhimu lililowatambulisha wanafunzi wa kweli wa Yesu ni kwamba walidhihirisha matunda ya roho maishani mwao. (Yohana 13:35; Wagalatia 5:22-24) Pia, roho hiyo iliwaimarisha washiriki wa kutaniko hilo watoe ushahidi kwa ujasiri, bila woga.—Matendo 4:31.

Msaada Wakati wa Mateso Makali

15. (a) Wakristo wamekabili magumu gani zamani na wakati huu? (b) Kwa nini wale wanaotoa kitia-moyo huenda nyakati nyingine wakahitaji kutiwa moyo?

15 Wote waliojitoa kwa Yehova na walio waaminifu kwake watanyanyaswa kwa njia fulani. (2 Timotheo 3:12) Hata hivyo, Wakristo wengi wamepatwa na mateso makali sana. Wakati wetu, baadhi yao wameshambuliwa na watu wenye ghasia na kupelekwa kwenye kambi za mateso, magereza, kambi za kazi ngumu, ambako wametendwa kinyama. Serikali nyingine zimewatesa au kuruhusu watu fulani wasiotii sheria wawatende Wakristo kwa jeuri pasipo kuwaadhibu. Isitoshe, Wakristo wamekabili matatizo mabaya ya afya au ya familia. Mkristo mkomavu anaweza pia kukabili magumu anapowasaidia waamini wenzake kushughulikia matatizo mazito. Katika hali kama hizo, yule anayetoa kitia-moyo huenda akahitaji kutiwa moyo pia.

16. Daudi alipata msaada gani alipokabili magumu?

16 Mfalme Sauli alipotaka kumwua Daudi, Daudi alimwendea Mungu ili kupata msaada: “Ee Mungu, uyasikie maombi yangu,” aliomba. “Nitaukimbilia uvuli wa mbawa zako.” (Zaburi 54:2, 4; 57:1) Je, Daudi alipata msaada? Ndiyo. Pindi hiyo, Yehova alimtuma nabii Gadi na kuhani Abiathari kumpa Daudi mwongozo, na Yonathani, mwana wa Sauli, amwimarishe mwanamume huyo kijana. (1 Samweli 22:1, 5; 23:9-13, 16-18) Yehova aliwaruhusu pia Wafilisti kushambulia nchi hiyo, hivyo alimkengeusha Sauli asimfuate Daudi.—1 Samweli 23:27, 28.

17. Yesu alipata wapi msaada alipokabili mateso makali?

17 Yesu Kristo mwenyewe aliteswa vikali alipokaribia kufa. Alijua kabisa matokeo ambayo mwenendo wake ungeleta kwa jina la Baba yake wa mbinguni na wakati ujao wa wanadamu wote. Alisali kwa bidii, hata ‘aliingia katika maumivu makali.’ Mungu alihakikisha kwamba Yesu alipata msaada aliohitaji wakati huo mgumu.—Luka 22:41-44.

18. Mungu aliwapa Wakristo wa mapema walioteswa vikali faraja gani?

18 Baada ya kutaniko la karne ya kwanza kuanzishwa, Wakristo waliteswa vikali sana hivi kwamba wote walitawanyika, na mitume peke yao ndio waliobaki Yerusalemu. Wanaume na wanawake waliburutwa kutoka katika nyumba zao. Mungu aliwafariji jinsi gani? Aliwahakikishia kupitia Neno lake kwamba walikuwa na “miliki bora na yenye kudumu,” yaani, urithi wa milele wa mbinguni pamoja na Kristo. (Waebrania 10:34; Waefeso 1:18-20) Walipoendelea kuhubiri, waliona uthibitisho kwamba roho ya Mungu ilikuwa pamoja nao, na yale waliyojionea yaliwapa sababu nyingine ya kufurahi.—Mathayo 5:11, 12; Matendo 8:1-40.

19. Ingawa Paulo aliteswa vikali, alihisije kuhusu faraja ambayo Mungu hutoa?

19 Hatimaye, Sauli (Paulo), aliyekuwa mtesi mkali, aliteswa pia kwa sababu alikuwa amegeuka na kuwa Mkristo. Kwenye kisiwa cha Saiprasi, kulikuwa na mlozi aliyejaribu kumzuia Paulo asiendelee na huduma yake kwa kutumia ulaghai na udanganyifu. Huko Galatia, watu walimpiga Paulo kwa mawe na kumwacha wakiwazia alikuwa amekufa. (Matendo 13:8-10; 14:19) Huko Makedonia alipigwa kwa fito. (Matendo 16:22, 23) Baada ya kushambuliwa na watu wenye ghasia huko Efeso aliandika hivi: “Tulikuwa chini ya mkazo mkali mno upitao nguvu yetu, hivi kwamba tulikuwa bila hakika kabisa hata juu ya uhai wetu. Kwa kweli, tulihisi ndani yetu wenyewe kwamba tulikuwa tumeipokea hukumu ya kifo.” (2 Wakorintho 1:8, 9) Lakini katika barua hiyohiyo, Paulo aliandika maneno yenye kufariji yaliyonukuliwa katika fungu la 2 la makala hii.—2 Wakorintho 1:3, 4.

20. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

20 Unawezaje kutoa faraja kama hiyo? Kuna watu wengi leo wenye huzuni wanaohitaji faraja kwa sababu ya misiba inayowaathiri maelfu ya watu kwa ghafula, au kwa sababu ya taabu wanazokabili. Katika makala inayofuata, tutazungumzia jinsi ya kutoa faraja katika hali hizo mbili.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini faraja kutoka kwa Mungu haina kifani?

• Ni faraja gani inayotolewa kupitia Kristo?

• Roho takatifu imetoa faraja jinsi gani?

• Toa mifano inayoonyesha jinsi Mungu alivyowafariji watumishi wake walipokabili mateso makali.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Biblia inatuonyesha kwamba Yehova aliwafariji watu wake kwa kuwakomboa

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yesu alitoa faraja kwa kufundisha, kuponya, na kufufua wafu

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yesu alipata msaada kutoka juu