Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tatian Alitetea Imani au Alikuwa Mwasi?

Je, Tatian Alitetea Imani au Alikuwa Mwasi?

Je, Tatian Alitetea Imani au Alikuwa Mwasi?

MTUME Paulo alipokaribia mwisho wa safari yake ya tatu ya umishonari, alifanya mkutano na wanaume wazee wa kutaniko la Efeso. Aliwaambia hivi: “Mimi najua kwamba baada ya kwenda zangu mbwa-mwitu wenye kuonea wataingia miongoni mwenu na hawatalitendea kundi kwa wororo, na kutoka miongoni mwenu nyinyi wenyewe wanaume watainuka na kusema mambo yaliyopotoka ili kuvuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.”—Matendo 20:29, 30.

Kama Paulo alivyosema, mabadiliko na uasi-imani uliokuwa umetabiriwa ulitukia katika karne ya pili. Harakati ya kidini na ya kifalsafa (Ugnostiki) ambayo ilichafua imani ya waamini fulani ilikuwa ikienea. Wagnostiki waliamini kwamba mambo ya kiroho ni mazuri na vitu vyote ni viovu. Walikataa kufunga ndoa na kuzaa kwa sababu walisema kwamba mwili wote ni mwovu na walidai kwamba Shetani ndiye aliyeanzisha mambo hayo. Baadhi yao waliamini kwamba mtu anaweza kuutumia mwili wake kwa njia yoyote atakayo kwa sababu ni roho tu iliyo nzuri. Maoni hayo yaliwafanya watu waponde raha kupindukia au wajinyime raha kabisa. Wagnostiki walidai kwamba wokovu ulitokana na mafumbo ya Kignostiki, au mtu kujijua mwenyewe, na hivyo walipuuza kabisa kweli ya Neno la Mungu.

Wale waliodai kuwa Wakristo walikuwa na maoni gani kuhusu hatari ya Ugnostiki? Watu fulani wenye elimu walipinga waziwazi mafundisho yake ya uwongo, lakini wengine waliyaamini. Kwa mfano, Irenaeus alipambana na mafundisho ya waasi-imani maisha yake yote. Alikuwa amefundishwa na Polycarp ambaye aliishi wakati wa mitume. Polycarp aliwahimiza watu wafuate kabisa mafundisho ya Yesu Kristo na mitume wake. Hata hivyo, rafiki ya Irenaeus, aitwaye Florinus, alifundishwa pia na Polycarp, lakini hatimaye alikubali mafundisho ya Valentinus, kiongozi mashuhuri zaidi wa harakati ya Wagnostiki. Mambo yalikuwa magumu kwelikweli.

Vitabu vya Tatian, mwandishi maarufu wa karne ya pili, vinaonyesha mawazo ya kidini yaliyokuwapo wakati huo. Tatian alikuwa mtu wa aina gani? Alipataje kuwa mmoja wa wale wanaodai kuwa Wakristo? Na Tatian aliathiriwaje na uasi wa Wagnostiki? Watu wanaotafuta kweli leo wanaweza kujifunza mambo mengi kutokana na mfano wake na majibu yake yenye kushangaza.

Alisoma ‘Maandishi Fulani ya Kigeni’

Tatian alikuwa mkazi wa Siria. Alikuwa na ujuzi mwingi kuhusu utamaduni wa Wagiriki na Waroma wa wakati huo kwa sababu ya kusafiri kotekote na kusoma sana. Tatian aliwasili Roma akiwa msemaji anayesafiri-safiri. Hata hivyo, alivutiwa na Ukristo akiwa Roma. Alianza kushirikiana na Justin Martyr, na labda akawa mwanafunzi wake.

Tatian asema hivi kuhusu kujiunga kwake na Ukristo wa wakati huo: “Nilifikiria jinsi ninavyoweza kupata kweli.” Anaeleza jinsi alivyohisi aliposoma Maandiko kwa mara ya kwanza: “Nilisoma maandishi fulani ya kigeni yaliyo ya kale zaidi kuliko maoni ya Wagiriki, na bora kuliko maoni yao yenye makosa; na nilishawishiwa kuamini maandishi hayo yenye lugha ya kawaida, na waandishi wake wasiotaka kujionyesha, utabiri wake wa matukio ya wakati ujao, sheria zake bora, na tangazo la kwamba ulimwengu mzima unatawaliwa na Mungu mmoja.”

Tatian aliwaalika wengi walioishi wakati huo wachunguze Ukristo wa wakati wake na kuona jinsi ulivyo rahisi na wenye kueleweka, tofauti na mafundisho yasiyoeleweka ya kipagani. Tunaweza kujifunza nini kutokana na vitabu vyake?

Vitabu Vyake Vinaonyesha Nini?

Vitabu vya Tatian vinaonyesha kwamba alikuwa mwandishi aliyetetea imani yake. Alichukia kabisa falsafa ya kipagani. Katika kitabu chake Address to the Greeks (Hotuba kwa Wagiriki), Tatian anakazia ubatili wa upagani na busara ya Ukristo aliofuata. Anashutumu vikali mazoea ya Wagiriki. Kwa mfano, alisema hivi kumhusu mwanafalsafa aitwaye Heracleitus: “Upumbavu wa mtu huyo ulionekana wakati alipokufa; alikuwa amejifunza matibabu na falsafa, lakini alipopata ugonjwa wa kuvimba mwili, alijipaka mavi ya ng’ombe mwili mzima, ngozi yake yote ikanyauka yalipokauka, akakatika vipande-vipande na hatimaye akafa.”

Tatian aliheshimu sana imani ya kwamba kuna Mungu mmoja ambaye ni Muumba wa vitu vyote. (Waebrania 3:4) Katika kitabu Address to the Greeks, anamtaja Mungu kuwa “Roho” halafu anasema: “Ndiye peke yake asiye na mwanzo, na Yeye Ndiye mwanzo wa vitu vyote.” (Yohana 4:24; 1 Timotheo 1:17) Tatian alipinga matumizi ya sanamu katika ibada na kuandika hivi: “Ningewezaje kusema vipande vya mbao na mawe ni miungu?” (1 Wakorintho 10:14) Aliamini kwamba Neno, au Logos, aliumbwa kwanza na Baba yake wa mbinguni na baadaye akatumiwa kuumba ulimwengu. (Yohana 1:1-3; Wakolosai 1:13-17) Tatian asema hivi kuhusu wakati rasmi wa ufufuo: “Tunaamini kwamba miili itafufuliwa siku ya mwisho itakapofika.” Tatian aandika hivi kuhusu kinachofanya tufe: “Hatukuumbwa tufe, lakini tunakufa kwa sababu ya makosa yetu. Uhuru wetu wa kuchagua umetuharibu; tulikuwa huru lakini tumekuwa watumwa; tumeuzwa kwa sababu ya dhambi.”

Tatian anatoa maelezo yasiyoeleweka kuhusu nafsi. Anasema: “Si kwamba nafsi haiwezi kufa, inaweza kufa, Enyi Wagiriki. Hata hivyo, huenda isife. Ikiwa kwa hakika haijui kweli, inakufa, na inaharibika pamoja na mwili; lakini hatimaye itafufuka tena pamoja na mwili mwisho wa ulimwengu utakapofika; nayo itakufa kwa kuhukumiwa katika kutokufa.” Maneno hayo ya Tatian hayaeleweki. Je, yawezekana kwamba alifuata mafundisho fulani ya Biblia huku akijaribu kuwafurahisha watu na hivyo kupotoa kweli za Maandiko kwa falsafa za kipagani?

Kitabu kingine maarufu cha Tatian kinaitwa Diatessaron, au Harmony of the Four Gospels (Upatano wa Injili Nne). Tatian ndiye aliyekuwa wa kwanza kulikabidhi kutaniko la Siria Injili katika lugha yao. Kitabu hicho kiliheshimiwa sana, kiliunganisha Injili zote nne katika simulizi moja. Kilitumiwa na Kanisa la Siria.

Alikuwa Mkristo au Mwasi?

Uchunguzi wa makini wa vitabu vya Tatian unaonyesha kwamba aliyajua Maandiko na aliyaheshimu sana. Anasema jinsi yalivyomsaidia: “Sitamani kuwa tajiri; sitaki cheo cha kijeshi; nachukia uasherati; sina hamu ya kuwa baharia kwa sababu ya pupa ya utajiri; . . . sina kichaa cha kuwa mashuhuri . . . Wote hufaidika kutokana na jua lilelile, na wote hufa, wawe matajiri au maskini.” Tatian ahimiza hivi: “Jitenge kabisa na ulimwengu, chukia kabisa upumbavu wake. Ishi maisha yanayomfurahisha Mungu, na uvue utu wa kale unapomfahamu.”—Mathayo 5:45; 1 Wakorintho 6:18; 1 Timotheo 6:10.

Hata hivyo, fikiria kitabu cha Tatian kinachoitwa On Perfection According to the Doctrine of the Savior (Ukamilifu Kulingana na Fundisho la Mwokozi). Katika kitabu hicho anasema kwamba ndoa ilianzishwa na Ibilisi. Tatian anashutumu vikali ndoa na kudai kwamba watu wanaofunga ndoa wanajifanya watumwa wa ulimwengu huu unaopita.

Inaonekana kwamba karibu mwaka wa 166 W.K., baada ya kifo cha Justin Martyr, Tatian alianzisha au alishirikiana na madhehebu yanaoitwa Encratites ambayo yalikazia maisha ya kujinyima raha. Wafuasi wa madhehebu hayo walikazia sana kujidhibiti na kuuweza kabisa mwili. Walijinyima kabisa divai, ndoa, na mali.

Mambo Tunayopaswa Kujifunza

Kwa nini Tatian alikengeuka sana kutoka kwenye Maandiko? Je, alikuwa “msikiaji msahaulifu”? (Yakobo 1:23-25) Je, Tatian alinaswa na falsafa za wanadamu kwa sababu hakukataa hadithi za uwongo? (Wakolosai 2:8; 1 Timotheo 4:7) Je, yawezekana kwamba alifanya makosa hayo makubwa sana kwa sababu ya ugonjwa fulani wa akili?

Vyovyote iwavyo, vitabu vya Tatian na mfano wake unaonyesha mawazo ya kidini yaliyokuwapo wakati huo. Vinathibitisha kwamba falsafa ya kilimwengu inaweza kuleta madhara makubwa sana. Na tutii onyo la mtume Paulo la kugeuka mbali “kutoka kwenye semi tupu ambazo huhalifu lililo takatifu na kutoka kwenye mapinganisho yenye kuitwa ‘ujuzi’ isivyo kweli.”—1 Timotheo 6:20.