Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kabla na Baadaye—Wakati Uliopita Wenye Mashaka, Wakati Ujao Mzuri Ajabu

Kabla na Baadaye—Wakati Uliopita Wenye Mashaka, Wakati Ujao Mzuri Ajabu

“Mkaribieni Mungu, Naye Atawakaribia”

Kabla na Baadaye—Wakati Uliopita Wenye Mashaka, Wakati Ujao Mzuri Ajabu

“NENO la Mungu liko hai na hukazia nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili . . . na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.” (Waebrania 4:12) Hivyo ndivyo mtume Paulo alivyosema kuhusu ujumbe wa Mungu wenye nguvu ambao unaweza kupenya katika moyo. Uwezo wake wa kupenya katika moyo ulidhihirika hasa katika karne ya kwanza W.K. Licha ya uvutano usiofaa wakati huo, wale waliopata kuwa Wakristo walivaa utu mpya.—Waroma 1:28, 29; Wakolosai 3:8-10.

Hata leo tunaona kwamba neno la Mungu lina nguvu za kubadili maisha ya watu kama inavyoonyeshwa katika Biblia. Kwa mfano, fikiria kisa cha mwanamume mmoja mrefu na mwenye nguvu aitwaye Richard. Kwa kuwa alikuwa mwenye hasira kali, Richard angepigana iwapo angechokozwa kidogo tu. Alikuwa mwenye jeuri sana na hata alijiunga na kilabu cha ndondi. Alifanya mazoezi kwa bidii sana na akawa bingwa wa taji la dondi za uzani wa juu huko Westphalia, Ujerumani. Richard pia alikunywa pombe kupindukia na mara nyingi alijiingiza katika mapigano. Katika mojawapo ya mapigano hayo mtu mmoja aliuawa, na kwa sababu hiyo karibu Richard atiwe gerezani.

Namna gani ndoa ya Richard? Richard anasema, “Kabla mimi na Heike tuanze kujifunza Biblia, kila mtu alifanya alivyotaka. Heike alitumia muda mwingi na marafiki wake wa kike huku mimi nikijishughulisha na mambo niliyopenda, yaani, ndondi, kuteleza juu ya mawimbi, na kupiga mbizi.”

Richard na Heike walipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, Richard aliona kama haingewezekana kufanya mabadiliko yaliyohitajiwa ili kuishi kupatana na viwango vya juu vya Neno la Mungu. Hata hivyo, alipopata kumjua Yehova Mungu vizuri zaidi, Richard alitamani sana kumpendeza. Richard alitambua kwamba Mungu hapendezwi na watu wanaopenda jeuri au wale wanaojitumbuiza kwa jeuri. Richard alijifunza kwamba ‘Yehova humchukia yeyote anayependa jeuri.’—Zaburi 11:5, NW.

Isitoshe, tumaini la kuishi milele katika dunia paradiso liliwavutia Richard na Heike. Walitaka kuishi huko pamoja! (Isaya 65:21-23) Richard aliguswa moyo sana na mwaliko huu: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” (Yakobo 4:8) Aliona umuhimu wa ushauri huu ulioongozwa kwa roho: “Usimhusudu mtu mwenye jeuri, wala usiichague mojawapo ya njia zake. Maana mtu mkaidi ni chukizo kwa BWANA, bali siri yake ni pamoja na wanyofu.”—Mithali 3:31, 32.

Licha ya kuwa na tamaa kubwa ya kubadili mwenendo wake, Richard alitambua kwamba hangeweza kufanya mabadiliko hayo kwa nguvu zake mwenyewe. Kwa hiyo akaona ni muhimu atafute msaada wa Mungu kupitia sala. Hivyo alitenda kupatana na maneno haya ya Yesu kwa mitume Wake: ‘Salini kwa kuendelea, ili msipate kuingia ndani ya jaribu. Bila shaka, roho ni yenye hamu, lakini mwili ni dhaifu.’—Mathayo 26:41.

Baada ya kujifunza jinsi Mungu anavyoona jeuri na hasira za ghafula, Richard alijua kabisa kwamba kupigana ndondi hakufai. Richard aliacha jeuri kwa msaada wa Yehova na kitia moyo alichopata kutoka kwa wale waliojifunza Biblia pamoja naye. Aliacha ndondi na mapigano na akaamua kuboresha maisha ya familia yake. Richard, ambaye sasa ni mzee mwenye upole katika mojawapo ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, anasema, “kujifunza kweli ya Biblia kumenisaidia niache kutenda bila kufikiri.” Anaendelea kusema: “Leo mimi ninaongozwa na kanuni za upendo na heshima katika uhusiano wangu na mke na watoto wangu. Kwa sababu hiyo, familia yetu imekuwa na ukaribu.”

Mara kwa mara watu ambao wameelezwa habari zisizo za kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova wamewashutumu kuwa wavunjaji wa familia. Hata hivyo, mfano kama wa Richard unaonyesha kwamba madai yao ni ya uwongo. Kwa kweli wale ambao zamani waliishi maisha yenye mashaka wanaweza kuwa na familia thabiti na kuwa na tumaini la wakati ujao mzuri kwa kujifunza kweli ya Biblia.—Yeremia 29:11.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Tumaini la kuishi milele katika dunia paradiso lilinichochea kubadilika”

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Kanuni za Biblia Zinazofanya Kazi

Biblia ina uwezo mkubwa wa kubadili maisha ya watu. Zifuatazo ni kanuni za Biblia ambazo zimewasaidia watu fulani wenye jeuri wabadilike:

“Asiye mwepesi wa hasira ni mwema kuliko shujaa; na mtu aitawalaye roho yake kuliko mtu atekaye mji.” (Mithali 16:32) Hasira isiyodhibitiwa ni ishara ya udhaifu wala si nguvu.

“Busara ya mtu huiahirisha hasira yake.” (Mithali 19:11) Kuwa na busara na kuelewa hali ilivyo humsaidia mtu afahamu kiini hasa cha ugomvi, na hiyo inaweza kuzuia hasira isilipuke.

‘Usifanye urafiki na mtu mwenye hasira nyingi usije ukajifunza njia zake.’ (Mithali 22:24, 25) Kwa hekima Wakristo huepuka kushirikiana na watu ambao wana mazoea ya kukasirika.