Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kristo Azungumza na Makutaniko

Kristo Azungumza na Makutaniko

Kristo Azungumza na Makutaniko

“Haya ndiyo mambo asemayo yeye ashikaye zile nyota saba katika mkono wake wa kuume.”—UFUNUO 2:1.

1, 2. Kwa nini tupendezwe na yale ambayo Kristo aliyaambia makutaniko saba huko Asia Ndogo?

YESU KRISTO, Mwana-mzaliwa pekee wa Yehova, ndiye Kichwa cha kutaniko la Kikristo. Ili kutaniko la wafuasi wake watiwa-mafuta liendelee kuwa bila doa, Kristo analiongoza kwa kulipongeza na kulirekebisha. (Waefeso 5:21-27) Kwenye Ufunuo sura ya 2 na ya 3 tunaona jinsi Yesu alivyoyapongeza na kuyarekebisha makutaniko saba huko Asia Ndogo kupitia ujumbe wake wenye nguvu na upendo.

2 Mtume Yohana alipewa maono kuhusu “siku ya Bwana” kabla ya kusikia maneno ya Yesu kwa yale makutaniko saba. (Ufunuo 1:10) “Siku” hiyo ilianza wakati Ufalme wa Kimesiya uliposimamishwa mwaka wa 1914. Kwa hiyo, yale ambayo Kristo aliyaambia makutaniko hayo ni muhimu sana siku hizi za mwisho. Kitia-moyo na ushauri wake hutusaidia kukabiliana na nyakati hizi hatari.—2 Timotheo 3:1-5.

3. “Nyota,” “malaika,” na “vinara saba vya taa vya dhahabu” ambavyo mtume Yohana aliona, vinafananisha nini?

3 Yohana alimwona Yesu Kristo aliyetukuzwa ambaye ‘anashika zile nyota saba katika mkono wake wa kuume’ na ‘anayetembea katikati ya vile vinara saba vya taa vya dhahabu,’ au makutaniko. “Nyota” hizo ni “wale malaika wa makutaniko saba.” (Ufunuo 1:20; 2:1) Wakati mwingine, nyota hufananisha malaika ambao ni viumbe wa roho, lakini Kristo hangetumia mwanadamu kuwaandikia viumbe wa roho ujumbe. Hivyo, kwa kufaa “nyota” hizo zinawakilisha waangalizi na mabaraza ya wazee watiwa-mafuta. Neno “malaika” linahusiana na kazi yao wakiwa wajumbe. Kwa sababu ya ukuzi wa tengenezo la Mungu, “msimamizi-nyumba mwaminifu” pia amewaweka rasmi wanaume wanaostahili miongoni mwa “kondoo wengine” wa Yesu, kuwa waangalizi.—Luka 12:42-44; Yohana 10:16.

4. Wazee hunufaikaje kwa kusikiliza yale ambayo Kristo anayaambia makutaniko?

4 “Nyota” hizo ziko kwenye mkono wa kuume wa Yesu, yaani, anaziongoza na kuzidhibiti, na zinapata ulinzi na kibali chake. Kwa hiyo, zinawajibika kwake. Kwa kusikiliza maneno yake kwa kila mojawapo ya yale makutaniko saba, wazee wa siku hizi wanapata kujua namna ya kushughulika na hali kama hizo. Bila shaka, Wakristo wote wanapaswa kumsikiliza Mwana wa Mungu. (Marko 9:7) Kwa hiyo, tunaweza kujifunza nini kwa kumsikiliza Kristo anapozungumza na makutaniko?

Kwa Malaika Katika Efeso

5. Efeso lilikuwa jiji la aina gani?

5 Yesu alilipongeza na kulikaripia kutaniko la Efeso. (Soma Ufunuo 2:1-7.) Hekalu kubwa la mungu wa kike Artemi lilikuwa katika jiji hilo lililokuwa kituo cha dini na biashara yenye kusitawi, kwenye pwani ya magharibi ya Asia Ndogo. Ingawa ukosefu wa maadili, dini isiyo ya kweli, na uchawi ulienea sana katika jiji la Efeso, Mungu alibariki huduma ya mtume Paulo na wengine katika jiji hilo.—Matendo, sura ya 19.

6. Ni katika njia gani Wakristo waaminifu-washikamanifu leo ni kama wale wa Efeso la kale?

6 Kristo alilipongeza kutaniko la Efeso kwa kusema: “Mimi navijua vitendo vyako, na kazi yako ya jasho na uvumilivu, na kwamba huwezi kuhimili watu wabaya, na kwamba uliwatia kwenye jaribu wale ambao husema wao ni mitume, lakini wao sio, nawe uliwapata kuwa waongo.” Leo, makutaniko ya wafuasi wa kweli wa Yesu yana sifa hizohizo za kutenda mema, kufanya kazi kwa bidii, na kuvumilia. Hayastahimili ndugu wasio wa kweli wanaojifanya kuwa “mitume.” (2 Wakorintho 11:13, 26) Kama Waefeso, Wakristo waaminifu-washikamanifu leo ‘hawawezi kuwahimili watu wabaya.’ Kwa hiyo, ili kudumisha ibada ya Yehova ikiwa safi na kulinda kutaniko, wao hawashirikiani na waasi-imani wasiotubu.—Wagalatia 2:4, 5; 2 Yohana 8-11.

7, 8. Kutaniko la Efeso lilikuwa na tatizo gani kubwa, nasi tunawezaje kushughulika na hali kama hiyo?

7 Hata hivyo, Wakristo huko Efeso walikuwa na tatizo kubwa. “Nashika hili dhidi yako,” akasema Yesu, “kwamba umeacha upendo uliokuwa nao hapo kwanza.” Washiriki wa kutaniko walihitaji kuchochea tena upendo waliokuwa nao kwa Yehova hapo kwanza. (Marko 12:28-30; Waefeso 2:4; 5:1, 2) Sote tunapaswa kuwa waangalifu tusipoteze upendo tuliokuwa nao kwa Mungu hapo kwanza. (3 Yohana 3) Namna gani ikiwa tunatanguliza tamaa ya kuwa matajiri au kufuatia anasa maishani? (1 Timotheo 4:8; 6:9, 10) Badala ya kuwa na tamaa kama hizo, tunapaswa kuomba msaada wa Mungu kwa bidii ili kusitawisha upendo mwingi kwa Yehova na kushukuru kwa yale ambayo yeye na Mwana wake wametufanyia.—1 Yohana 4:10, 16.

8 Kristo aliwahimiza Waefeso hivi: “Kumbuka ni kutoka katika nini umeanguka, nawe tubu na kufanya vitendo vya kwanza.” Namna gani kama hawangefanya hivyo? “Usipofanya hivyo,” akasema Yesu, “Mimi ninakuja kwako, nami hakika nitaondoa kinara chako cha taa kutoka mahali pacho.” Iwapo kondoo wote wangepoteza upendo waliokuwa nao hapo kwanza, kile ‘kinara cha taa,’ au kutaniko halingeendelea kuwapo. Kwa hiyo, tukiwa Wakristo wenye bidii na tujitahidi sana kuona kwamba kutaniko linaendelea kung’aa kiroho.—Mathayo 5:14-16.

9. Tunapaswa kuyaonaje mafarakano?

9 Waefeso walistahili kupongezwa kwa sababu walichukia “vitendo vya farakano la Nikolausi.” Mbali na yale yanayosemwa katika kitabu cha Ufunuo, hakuna habari hususa inayoonyesha chanzo, mafundisho, na mazoea ya farakano hilo. Hata hivyo, kwa kuwa Yesu alishutumu desturi ya kufuata wanadamu, tunapaswa kuendelea kuchukia mafarakano kama walivyofanya Wakristo wa Efeso.—Mathayo 23:10.

10. Wale wanaosikiliza yale ambayo roho husema watapata nini?

10 Kristo alisema, “Acheni yeye aliye na sikio asikie lile ambalo roho huyaambia makutaniko.” Alipokuwa duniani, Yesu alizungumza kwa kuongozwa na roho ya Mungu. (Isaya 61:1; Luka 4:16-21) Kwa hiyo, tunapaswa kusikiliza yale ambayo Mungu anasema sasa kupitia Yesu akitumia roho takatifu. Yesu alitoa ahadi hii akiongozwa na roho: “Kwake ambaye hushinda hakika nitamruhusu kula kutoka katika mti wa uhai, ambao umo katika paradiso ya Mungu.” Kwa watiwa-mafuta wanaosikiliza yale ambayo roho inasema, hiyo inamaanisha kutoweza kufa katika “paradiso ya Mungu” ya kimbingu, au kuwa mbele za Yehova. “Umati mkubwa” ambao pia husikiliza yale ambayo roho inasema, watafurahia kuishi katika dunia paradiso ambapo watakunywa kutoka kwa “mto wa maji ya uhai” na kuponywa kwa ‘majani ya miti’ iliyo kandokando ya mto huo.—Ufunuo 7:9; 22:1, 2; Luka 23:43.

11. Tunaweza kuwachocheaje wengine wampende Yehova?

11 Waefeso walikuwa wamepoteza upendo waliokuwa nao hapo kwanza, lakini namna gani hali kama hiyo ikianza kutokea kutanikoni? Kila mmoja wetu na awachochee wengine wampende Yehova kwa kuzungumzia njia zake za upendo. Tunaweza kuonyesha shukrani zetu kwa upendo ambao Mungu alionyesha kwa kutoa fidia kupitia Mwana wake mpendwa. (Yohana 3:16; Waroma 5:8) Inapofaa, tunaweza kutaja upendo wa Mungu tunapotoa maelezo ama tunapokuwa na migawo kwenye mikutano. Tunaweza kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kwa kulisifu jina lake katika huduma ya Kikristo. (Zaburi 145:10-13) Naam, maneno na matendo yetu yanaweza kuchochea tena au kuimarisha sana upendo ambao kutaniko lilikuwa nao hapo kwanza.

Kwa Malaika Katika Smirna

12. Historia hufunua nini kuhusu Smirna na mazoea yake ya kidini?

12 Kutaniko la Smirna lilipongezwa na Kristo, aliye “‘Wa-Kwanza na Wa-Mwisho,’ aliyekuwa mfu akaja kwenye uhai tena” kupitia ufufuo. (Soma Ufunuo 2:8-11.) Jiji la Smirna (ambalo sasa ni Izmir, Uturuki) lilijengwa kwenye pwani ya magharibi ya Asia Ndogo. Wagiriki walihamia jiji hilo lakini likaharibiwa na Walidia wapata mwaka wa 580 K.W.K. Wale waliotawala baada ya Aleksanda Mkuu walilijenga tena jiji hilo katika sehemu tofauti. Hivyo jiji la Smirna likawa sehemu ya mkoa wa Asia wa milki ya Roma, na kituo cha biashara yenye kusitawi kilichokuwa maarufu kwa majengo yake ya umma yenye kuvutia. Hekalu la Tiberio Kaisaria lililokuwa katika jiji hilo lililifanya liwe kituo cha ibada ya maliki. Waabudu walipaswa kufukiza kiasi kidogo cha uvumba na kusema “Kaisari ni Bwana.” Wakristo hawangeweza kufanya hivyo kwa sababu ‘Yesu ndiye Bwana’ wao. Hivyo, walipatwa na dhiki.—Waroma 10:9.

13. Ingawa Wakristo wa Smirna walikuwa maskini kimwili, walikuwa matajiri katika maana gani?

13 Mbali na dhiki, Wakristo wa Smirna walistahimili umaskini na labda walipatwa na magumu ya kiuchumi kwa sababu hawangeshiriki katika ibada ya maliki. Watumishi wa Yehova leo hupatwa na majaribu kama hayo. (Ufunuo 13:16, 17) Ingawa wale walio kama Wakristo wa Smirna ni maskini kimwili, wao ni matajiri kiroho, na hilo ndilo jambo muhimu zaidi!—Mithali 10:22; 3 Yohana 2.

14, 15. Andiko la Ufunuo 2:10 linaweza kuwafariji watiwa-mafuta jinsi gani?

14 Wayahudi wengi huko Smirna walikuwa “sinagogi la Shetani” kwa sababu walifuata mapokeo yaliyo kinyume cha Maandiko, wakamkataa Mwana wa Mungu, na kuwakufuru wafuasi wake waliozaliwa kwa roho. (Waroma 2:28, 29) Watiwa-mafuta wanaweza kufarijiwa sana na maneno haya ya Kristo: “Usiogope mambo uliyo karibu kuteseka. Tazama! Ibilisi atafuliza kutupa baadhi yenu ndani ya gereza ili mpate kutiwa kwenye jaribu kikamili, na kwamba mpate kuwa na dhiki siku kumi. Jithibitishe mwenyewe kuwa mwaminifu hata kufikia kifo, nami hakika nitakupa taji la uhai.”—Ufunuo 2:10.

15 Yesu hakuogopa kufa kwa kutetea enzi kuu ya Yehova. (Wafilipi 2:5-8) Ingawa sasa Shetani anapigana vita na mabaki ya watiwa-mafuta, wao hawaogopi mateso ambayo lazima yawapate wakiwa kikundi, ambayo ni dhiki, kufungwa gerezani, au kuuawa kikatili. (Ufunuo 12:17) Wataushinda ulimwengu. Na badala ya shada la maua linalonyauka ambalo lilivaliwa na washindi kama taji katika michezo ya wapagani, Kristo anawaahidi watiwa-mafuta watakaofufuliwa “taji la uhai” mbinguni wakiwa viumbe wa roho wasioweza kufa. Kwa kweli hiyo ni zawadi yenye thamani kubwa kama nini!

16. Tunapaswa kukazia fikira suala gani iwapo tunashirikiana na kutaniko kama la Smirna la kale?

16 Namna gani, ikiwa tunashirikiana na kutaniko kama la Smirna la kale, iwe sisi tuna tumaini la kuishi mbinguni au duniani? Basi na tuwasaidie waamini wenzetu wakazie fikira sababu kuu inayofanya Mungu aruhusu mnyanyaso—ambayo ni suala kuhusu ni nani aliye na haki ya kutawala ulimwengu. Kila Shahidi wa Yehova anayeendelea kushika uaminifu-maadili, huthibitisha Shetani kuwa mwongo na huonyesha kwamba hata mwanadamu anayenyanyaswa, anaweza kutetea kwa uimara haki ya Mungu ya kutawala akiwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu. (Mithali 27:11) Na tuwatie moyo Wakristo wengine wavumilie mateso na hivyo kuendelea kuwa na “pendeleo la kumtolea [Yehova] utumishi mtakatifu bila hofu kwa uaminifu-mshikamanifu na uadilifu mbele yake siku zetu zote”—hata milele.—Luka 1:68, 69, 74, 75.

Kwa Malaika Katika Pergamamu

17, 18. Pergamamu lilikuwa kituo cha ibada ya aina gani, na ni nini kingeweza kumpata mtu aliyekataa kushiriki ibada hiyo ya sanamu?

17 Kutaniko la Pergamamu lilipongezwa na kurekebishwa pia. (Soma Ufunuo 2:12-17.) Ibada ya sanamu ilikuwa imeenea sana katika jiji la Pergamamu, lililokuwa umbali wa kilometa 80 kaskazini ya Smirna. Inaonekana kwamba mamajusi (watabiri wanaotumia nyota) Wakaldayo walikimbilia huko kutoka Babiloni. Wagonjwa walimiminika katika hekalu maarufu la Asclepius, mungu bandia wa uponyaji huko Pergamamu. Jiji hilo lililokuwa na hekalu ambalo lilitumiwa kwa ajili ya ibada ya Kaisari Augusto, limetajwa kuwa “kituo kikuu cha madhehebu ya kifalme katika milki ya awali.”—Encyclopædia Britannica, 1959, Buku la 17, ukurasa wa 507.

18 Huko Pergamamu kulikuwa na madhabahu yaliyotumiwa kwa ajili ya ibada ya Zeusi. Jiji hilo pia lilikuwa kituo cha ibada iliyochochewa na Ibilisi ya kuwaabudu wanadamu. Si ajabu kwamba kutaniko la Pergamamu lilisemekana kuwa mahali ambapo “kiti cha ufalme cha Shetani” kilikuwa! Mteteaji wa enzi kuu ya Yehova angeweza kuuawa kama angekataa kumwabudu maliki. Ulimwengu bado uko chini ya mamlaka ya Ibilisi, na sasa nembo za kitaifa zinaabudiwa. (1 Yohana 5:19) Tangu karne ya kwanza hadi sasa, Wakristo wengi waaminifu wamefia imani, kama yule ambaye Kristo alimwita “Antipasi, shahidi wangu, aliye mwaminifu, aliyeuawa kando yenu.” Bila shaka, Yehova Mungu na Yesu Kristo wanawakumbuka watumishi hao waaminifu-washikamanifu.—1 Yohana 5:21.

19. Balaamu alifanya nini, nao Wakristo wote wanapaswa kujihadhari na nini?

19 Kristo pia alizungumza kuhusu “ufundishaji wa Balaamu.” Balaamu, nabii asiye wa kweli, alijaribu kuwalaani Waisraeli kwa sababu ya pupa ya vitu vya kimwili. Mungu alipogeuza laana yake ikawa baraka, Balaamu alishirikiana na Mfalme Balaki wa Moabu na kuwashawishi Waisraeli wengi washiriki katika ibada ya sanamu na mwenendo mchafu kingono. Wazee Wakristo wanahitaji kuwa imara kwa ajili ya uadilifu kama Finehasi, ambaye alipinga mbinu za Balaamu. (Hesabu 22:1–25:15; 2 Petro 2:15, 16; Yuda 11) Kwa kweli, Wakristo wote wanapaswa kujihadhari na ibada ya sanamu na kupenya kwa mwenendo mchafu kingono kutanikoni.—Yuda 3, 4.

20. Ikiwa Mkristo yeyote anaanza kuwa na maoni ya uasi-imani, anapaswa kufanya nini?

20 Kutaniko la Pergamamu lilikuwa katika hatari kubwa kwa sababu liliwaruhusu wale ‘walioshika sana ufundishaji wa farakano la Nikolausi’ waendelee kuwa miongoni mwake. Kristo aliliambia hivi kutaniko hilo: ‘Tubu. Usipofanya hivyo, mimi ninakuja kwako upesi, nami hakika nitapiga vita nawe kwa ule upanga mrefu wa kinywa changu.’ Wanaounga mkono mafarakano wanataka kuwadhuru Wakristo kiroho, nao wale walio na nia ya kuendeleza migawanyiko na mafarakano hawataurithi Ufalme wa Mungu. (Waroma 16:17, 18; 1 Wakorintho 1:10; Wagalatia 5:19-21) Ikiwa Mkristo yeyote anaanza kuwa na maoni ya uasi-imani na anataka kuyaeneza, maneno ya Kristo yanapaswa kuwa onyo kwake! Ili asije akapatwa na msiba, anapaswa kutubu na kutafuta msaada wa kiroho kutoka kwa wazee wa kutaniko. (Yakobo 5:13-18) Ni muhimu kufanya hivyo bila kukawia, kwa kuwa Yesu anakuja upesi kutekeleza hukumu.

21, 22. Ni nani wanaokula “mana iliyofichwa,” nayo inawakilisha nini?

21 Wakristo watiwa-mafuta waaminifu na waandamani wao waaminifu-washikamanifu hawapaswi kuogopa hukumu inayokuja. Wote wanaosikiliza ushauri wa Yesu unaotolewa kwa mwongozo wa roho takatifu ya Mungu watabarikiwa. Kwa mfano, watiwa-mafuta wanaoshinda ulimwengu wataalikwa kula kiasi fulani cha “mana iliyofichwa” na watapewa “kijiwe cheupe cha mviringo” chenye “jina jipya.”

22 Waisraeli walipokuwa wakitangatanga nyikani kwa miaka 40, Mungu aliwapa mana kuwa chakula chao. Waliweka kiasi fulani cha “mkate” huo katika mtungi mdogo wa dhahabu uliokuwa ndani ya sanduku la agano na hivyo ukafichwa katika Patakatifu Zaidi pa tabenakulo, ambapo nuru ya kimuujiza iliwakilisha kuwapo kwa Yehova. (Kutoka 16:14, 15, 23, 26, 33; 26:34; Waebrania 9:3, 4) Hakuna aliyeruhusiwa kula mana hiyo iliyofichwa. Hata hivyo, wanapofufuliwa, wafuasi wa Yesu watiwa-mafuta huvaa hali ya kutoweza kufa inayowakilishwa na kula “mana iliyofichwa.”—1 Wakorintho 15:53-57.

23. “Kijiwe cheupe cha mviringo” na “jina jipya” humaanisha nini?

23 Katika mahakama za Roma, kijiwe cheusi cha mviringo kilimaanisha kifungo, ilhali kijiwe cheupe kilimaanisha kuachiliwa huru. Yesu anapowapa “kijiwe cheupe cha mviringo” Wakristo watiwa-mafuta wanaoshinda, hiyo inamaanisha kwamba anawaona kuwa wasio na hatia, waliotakata, na safi. Kwa kuwa Waroma pia walitumia vijiwe vya mviringo kama tiketi ya kuingia kwenye sherehe muhimu, huenda “kijiwe cheupe cha mviringo” kikamaanisha kualikwa kwa mtiwa-mafuta mbinguni wakati wa ndoa ya Mwana-kondoo. (Ufunuo 19:7-9) Yaelekea “jina jipya” linamaanisha pendeleo la kuungana na Yesu wakiwa warithi-washirika katika Ufalme wa mbinguni. Bila shaka, mambo hayo yote huwatia moyo watiwa-mafuta na pia wale wanaoshirikiana nao kumtumikia Yehova, ambao wana tumaini la kuishi katika paradiso duniani.

24. Tunapaswa kuchukua msimamo gani kuhusiana na uasi-imani?

24 Ni jambo la hekima kukumbuka kwamba waasi-imani walihatarisha kutaniko la Pergamamu. Iwapo hali kama hiyo inahatarisha hali njema ya kiroho ya kutaniko tunaloshirikiana nalo, na tukatae katakata uasi-imani na kuendelea kutembea katika kweli. (Yohana 8:32, 44; 3 Yohana 4) Kwa kuwa walimu wa uwongo au watu fulani wenye mwelekeo wa kuasi imani wanaweza kupotosha kutaniko zima, ni lazima tudumishe msimamo imara dhidi ya uasi-imani, na tusiruhusu kamwe ushawishi mwovu utuzuie kuitii kweli.—Wagalatia 5:7-12; 2 Yohana 8-11.

25. Makala inayofuata itazungumzia ujumbe wa Kristo kwa makutaniko gani?

25 Tumechochewa kama nini kuzungumzia maneno ya pongezi na ushauri ambao Yesu Kristo aliyetukuzwa alitoa kwa makutaniko matatu kati ya yale saba huko Asia Ndogo! Hata hivyo, Yesu akiongozwa na roho takatifu ana mengi pia ya kuyaambia yale makutaniko manne yaliyosalia. Ujumbe huo, kwa makutaniko ya Thiatira, Sardisi, Filadelfia, na Laodikia utazungumziwa katika makala inayofuata.

Ungejibuje?

• Kwa nini tunapaswa kusikiliza yale ambayo Kristo anasema kwa makutaniko?

• Tunawezaje kuchochea tena upendo ambao kutaniko lilikuwa nao hapo kwanza?

• Kwa nini tunaweza kusema kwamba Wakristo waliokuwa maskini kimwili huko Smirna la kale walikuwa matajiri?

• Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu uasi-imani kwa kutafakari hali ya kutaniko la Pergamamu?

[Maswali ya Funzo]

[Ramani katika ukurasa wa 10]

 

UGIRIKI

ASIA NDOGO

Efeso

Smirna

Pergamamu

Thiatira

Sardisi

Filadelfia

Laodikia

[Picha katika ukurasa wa 12]

“Umati mkubwa” utafurahia dunia paradiso

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wakristo wanaonyanyaswa wameushinda ulimwengu