Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 2002, fungu la 7, ukurasa wa 11, lilisema kwamba waamini wapya Wayahudi waliobatizwa siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. walionyesha “wakfu wao kwa Mungu kupitia Kristo,” ijapokuwa maoni ya zamani yalikuwa kwamba Wayahudi waliobatizwa kuanzia mwaka wa 33 W.K. hadi 36 W.K. hawakuhitaji kujiweka wakfu?

Mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova Mungu aliwapa Waisraeli nafasi ya kuwa taifa takatifu kwake kama ‘wangetii sauti yake kweli kweli.’ Walijibu hivi: “Maneno yote aliyoyanena BWANA tutayatenda.”—Kutoka 19:3-8; 24:1-8.

Waisraeli walijiweka wakfu kwa Mungu kwa kukubali kutimiza matakwa ya agano la Sheria la Musa. Wayahudi waliozaliwa baada ya hapo walikuwa sehemu ya taifa hilo lililokuwa limewekwa wakfu. Hata hivyo, ubatizo wa Wayahudi waliokubali kuwa wafuasi wa Yesu Kristo kuanzia siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. haukumaanisha kwamba walijitoa kwa Mungu wakiwa watu wa taifa lililokuwa limewekwa wakfu. Ubatizo wao ulionyesha kwamba walikuwa wamejiweka wakfu kwa Yehova Mungu wakiwa na uhusiano mpya naye kupitia Yesu Kristo. Kwa nini?

Baada ya wanafunzi 120, waliokuwa wamekusanyika katika chumba cha juu huko Yerusalemu siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., kupokea roho takatifu, mtume Petro alisimama na akaanza kuhubiria umati wa Wayahudi na watu wa mataifa waliogeuzwa imani waliokuwa wamekusanyika kuona kile kilichokuwa kimetukia. Baada ya kutoa ushahidi kamili, aliwaambia hivi hao Wayahudi waliochomwa na dhamiri zao: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo kwa msamaha wa dhambi zenu.” Petro aliendelea kuwasihi, na “wale waliokubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo wakabatizwa, na katika siku hiyo nafsi karibu elfu tatu zikaongezwa.”—Matendo 2:1-41.

Wayahudi hao waliofuata ushauri wa Petro na kubatizwa, je, walikuwa watu wa taifa lililokuwa limewekwa wakfu? Je, walikuwa na uhusiano wa pekee na Mungu kwa sababu walikuwa watu wa taifa lililokuwa limewekwa wakfu kwa Mungu? La. Mtume Paulo aliandika kwamba ‘Mungu ameiondoa Sheria njiani kwa kuipigilia misumari kwenye mti wa mateso.’ (Wakolosai 2:14) Yehova Mungu alikomesha agano la Sheria kupitia kifo cha Kristo mwaka wa 33 W.K. Hapo awali, Waisraeli walikuwa na uhusiano wa pekee na Yehova Mungu kwa sababu walikubali agano hilo. Lakini sasa Mungu alilitupilia mbali taifa hilo lililokataa Mwana wake. ‘Israeli la kimwili,’ halikuwa tena taifa lililowekwa wakfu kwa Mungu.—1 Wakorintho 10:18; Mathayo 21:43.

Agano la Sheria lilikomeshwa mwaka wa 33 W.K., lakini Wayahudi bado waliendelea kuwa na pendeleo la pekee na uangalifu kutoka kwa Mungu kwa pindi fulani. * Pindi hiyo ingeendelea hadi mwaka wa 36 W.K., wakati Petro alipomhubiria Mwitalia aitwaye Kornelio, aliyemcha Mungu, na nyumba yake, na vilevile watu wengine wasiokuwa Wayahudi. (Matendo 10:1-48) Kwa nini Wayahudi walipewa pendeleo hilo la ziada?

Andiko la Danieli 9:27 linasema kwamba “[Mesiya] atafanya agano thabiti na watu wengi kwa muda wa juma moja.” Agano lililoendelea kuwapo kwa miaka saba, au “juma moja,” tangu ubatizo wa Yesu na mwanzo wa huduma ya Mesiya mwaka wa 29 W.K., lilikuwa agano la Abrahamu. Ili kuwa katika agano hilo mtu alihitaji tu kuwa mzao Mwebrania wa Abrahamu. Agano hilo lenye masharti ya upande mmoja tu halikumfanya mtu mmoja-mmoja awe na uhusiano wa pekee na Yehova uliotegemea kuwekwa wakfu. Kwa hiyo, ijapokuwa Wayahudi waamini waliobatizwa baada ya hotuba ya Petro siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. walipewa pendeleo la pekee kwa sababu walikuwa Wayahudi wa asili, hawakuwa watu waliowekwa wakfu kwa Mungu baada ya agano la Sheria kuondolewa. Kila mmoja wao alihitaji kujiweka wakfu kwa Mungu.

Wayahudi na watu wa mataifa waliogeuzwa imani ambao walibatizwa siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. walipaswa kujiweka wakfu kwa sababu nyingine muhimu pia. Mtume Petro aliwasihi wasikilizaji wake watubu na wabatizwe katika jina la Yesu. Walipaswa kuacha maisha ya ulimwengu na kumkubali Yesu kuwa Bwana, Mesiya, Kuhani Mkuu, na pia yule anayeketi upande wa kulia wa Mungu mbinguni. Walipaswa kuliitia jina la Yehova Mungu ili wapate wokovu kupitia Kristo Yesu. Hilo lilimaanisha kudhihirisha imani katika Kristo na kumkubali kuwa Kiongozi wao. Msingi wa kuwa na uhusiano pamoja na Mungu na kupata msamaha wa dhambi ulikuwa umebadilika kabisa. Kila Myahudi mwamini alihitaji kukubali mpango huo mpya. Jinsi gani? Kwa kujiweka wakfu kwa Mungu na kuonyesha peupe kwamba wamefanya hivyo kwa kubatizwa majini katika jina la Yesu Kristo. Ubatizo wa maji ulionyesha kwamba walikuwa wamejiweka wakfu kwa Mungu, na hivyo walikuwa na uhusiano mpya na Mungu kupitia Yesu Kristo.—Matendo 2:21, 33-36; 3:19-23.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Agano la Musa liliondolewa, na msingi wa “agano jipya” uliwekwa wakati Yesu Kristo alipopaa mbinguni na kumtolea Yehova Mungu thamani ya uhai wake wa kibinadamu ambao aliutoa kama dhabihu.—Yeremia 31:31-34.