Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sikia Yale Ambayo Roho Husema!

Sikia Yale Ambayo Roho Husema!

Sikia Yale Ambayo Roho Husema!

“Acheni yeye aliye na sikio asikie lile ambalo roho huyaambia makutaniko.”—UFUNUO 3:22.

1, 2. Ni ushauri gani unaorudiwa katika kila ujumbe ambao Yesu anatoa kwa makutaniko saba yanayotajwa katika Ufunuo?

NI LAZIMA watumishi wa Yehova wasikilize maneno ambayo Yesu Kristo aliongozwa na roho kuyaambia yale makutaniko saba yanayotajwa katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Kwa kweli, kila ujumbe una ushauri huu: “Acheni yeye aliye na sikio asikie lile ambalo roho huyaambia makutaniko.”—Ufunuo 2:7, 11, 17, 29; 3: 6, 13, 22.

2 Tayari tumezungumzia ujumbe wa Yesu kwa malaika, au waangalizi wa Efeso, Smirna, na Pergamamu. Tunawezaje kunufaika na yale ambayo Yesu aliongozwa na roho takatifu kuyaambia yale makutaniko mengine manne?

Kwa Malaika Katika Thiatira

3. Jiji la Thiatira lilikuwa wapi, na lilikuwa maarufu kwa kutengeneza nini?

3 “Mwana wa Mungu” analipongeza na kulikaripia kutaniko la Thiatira. (Soma Ufunuo 2:18-29.) Jiji la Thiatira (ambalo sasa ni Akhisari) lilikuwa limejengwa kwenye kijito cha Mto Gediz (Hermus la kale) magharibi mwa Asia Ndogo. Jiji hilo lilikuwa maarufu kwa utengenezaji wa vitu vya sanaa. Watengenezaji-rangi wa jiji hilo walitumia mizizi ya mmea fulani kutengeneza rangi nyekundu au ya zambarau iliyokuwa maarufu. Lidia, aliyegeuza imani na kuwa Mkristo wakati Paulo alipotembelea jiji la Filipi huko Ugiriki, alikuwa “muuzaji wa rangi ya zambarau wa jiji la Thiatira.”—Matendo 16:12-15.

4. Kutaniko la Thiatira lilipongezwa kwa jambo gani?

4 Yesu analipongeza kutaniko la Thiatira kwa matendo yake mema, upendo, imani, uvumilivu, na kwa huduma yake. Kwa kweli, ‘vitendo vyake vya juzijuzi vilizidi vile vya hapo zamani.’ Hata kama tumekuwa na sifa nzuri, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu maadili yetu.

5-7. (a) Ni nani yule “mwanamke Yezebeli,” na ni nini ambacho kingefanywa kuhusu ushawishi wake? (b) Ujumbe wa Kristo kwa kutaniko la Thiatira huwasaidia wanawake wanaomwogopa Mungu wafanye nini?

5 Kutaniko la Thiatira lilikuwa likivumilia ibada ya sanamu, mafundisho ya uwongo, na mwenendo mchafu kingono. Miongoni mwao mlikuwa na “mwanamke Yezebeli”—labda kikundi cha wanawake waliokuwa na tabia kama za Malkia Yezebeli mwovu wa Ufalme wa Israeli wa makabila kumi. Wasomi fulani wanadokeza kwamba ‘manabii wa kike’ wa Thiatira walijaribu kuwashawishi Wakristo waabudu miungu ya kiume na ya kike ya shirika fulani la wanabiashara, na pia washiriki katika sherehe zenye vyakula vilivyotolewa kwa sanamu. Tusiruhusu mwanamke yeyote anayejisingizia kuwa nabii awapotoshe wengine katika kutaniko la Kikristo leo!

6 Kristo alikuwa ‘karibu kumtupa mwanamke huyo Yezebeli aingie katika kitanda cha ugonjwa, na wale wanaofanya uzinzi pamoja naye katika dhiki kubwa, isipokuwa watubu vitendo vyake.’ Waangalizi wanapaswa kukataa kabisa mafundisho hayo maovu na ushawishi wake, na si lazima Mkristo afanye uasherati halisi au wa kiroho, au aabudu sanamu ili atambue kwamba “mambo yenye kina kirefu ya Shetani” ni maovu kabisa. Tukisikiliza onyo la Yesu, ‘tutashika sana lile tulilo nalo,’ na dhambi haitatutawala. Watiwa-mafuta waliofufuliwa wanapokea “mamlaka juu ya mataifa” kwa sababu wamekataa mazoea, uchu, na miradi isiyo ya kimungu, nao watajiunga na Kristo kuyavunja mataifa vipande-vipande. Makutaniko leo yana nyota za mfano, na watiwa-mafuta watapewa “nyota nyangavu ya asubuhi,” ambayo ni Bwana-arusi, Yesu Kristo, wanapofufuliwa kwenda mbinguni.—Ufunuo 22:16.

7 Kutaniko la Thiatira lilionywa lisivumilie ushawishi mwovu wa wanawake wenye kuasi imani. Ujumbe ambao Kristo aliongozwa na roho kutoa kwa kutaniko huwasaidia wanawake wanaomwogopa Mungu watosheke na mahali pao katika mpango wa Mungu leo. Hawajaribu kuwa na mamlaka juu ya wanaume wala kuwashawishi akina ndugu wafanye uasherati halisi au wa kiroho. (1 Timotheo 2:12) Badala yake, wanawake hao humletea Mungu sifa kwa kuweka kielelezo chema katika matendo na katika utumishi wao. (Zaburi 68:11; 1 Petro 3:1-6) Ikiwa kutaniko litalinda lilicho nacho—mafundisho na mwenendo safi, na pia utumishi wa Ufalme wanaouthamini sana—Kristo atakuja kulibariki wala si kuliangamiza.

Kwa Malaika Katika Sardisi

8. (a) Jiji la Sardisi lilikuwa wapi, na ni mambo gani yanayotajwa kulihusu? (b) Kwa nini kutaniko la Sardisi lilihitaji msaada?

8 Kutaniko la Sardisi lilihitaji msaada haraka kwa sababu lilikuwa limekufa kiroho. (Soma Ufunuo 3:1-6.) Jiji la Sardisi lenye usitawi lilikuwa umbali wa kilometa 50 kusini ya Thiatira. Jiji hilo lilikuwa na utajiri kwa sababu ya biashara, mazao mengi ya kilimo, na utengenezaji wa mavazi ya sufu na mazulia, na wakati mmoja lilikuwa na watu wapatao 50,000. Kulingana na mwanahistoria Josephus, jiji la Sardisi lilikuwa na wakazi wengi sana Wayahudi katika karne ya kwanza K.W.K. Kati ya magofu ya jiji hilo kuna sinagogi na hekalu la mungu wa kike Artemi wa Efeso.

9. Tunapaswa kufanya nini ikiwa utumishi wetu ni wa kidesturi tu?

9 Kristo alimwambia malaika wa kutaniko la Sardisi hivi: “Mimi navijua vitendo vyako, kwamba una jina kuwa uko hai, lakini wewe ni mfu.” Iwapo tunajulikana kuwa watu wa kiroho lakini hatujali sana mapendeleo ya Kikristo, basi utumishi wetu ni wa kidesturi tu na tuko “tayari kufa” kiroho. Kwa hiyo, tunahitaji ‘kuendelea kuzingatia akilini jinsi tunavyopokea na kusikia’ ujumbe wa Ufalme, na tunapaswa kuchochea tena jitihada zetu katika utumishi mtakatifu. Bila shaka tunapaswa kuanza kushiriki kwa moyo wote katika mikutano ya Kikristo. (Waebrania 10:24, 25) Kristo alionya kutaniko la Sardisi hivi: “Usipoamka, nitakuja kama mwizi, na hutajua hata kidogo ni saa gani nitakapokuja juu yako.” Namna gani leo? Hivi karibuni itatubidi tutoe hesabu kwa matendo yetu.

10. Hata katika hali kama za Sardisi, huenda Wakristo wachache wamefaulu kufanya nini?

10 Hata katika hali kama za Sardisi, huenda kuna wachache ambao ‘hawayatii unajisi mavazi yao ya nje, nao wanaweza kutembea pamoja na Kristo wakiwa wamevaa mavazi meupe, kwa sababu yanastahili.’ Nyakati zote mwenendo wao huwatambulisha kuwa Wakristo nao hudumu wakiwa safi bila kutiwa doa la kiroho au la kiadili na ulimwengu huu. (Yakobo 1:27) Hivyo, Yesu ‘hakika hatayafuta kwa vyovyote majina yao kutoka katika kitabu cha uhai, bali hakika atayakiri majina yao mbele ya Baba yake na mbele ya malaika.’ Wakiwa wametangazwa kuwa wanastahili kutembea pamoja na Kristo, watiwa-mafuta ambao ni jamii ya bibi-arusi watavikwa kitani nyangavu, safi, na bora ambacho hufananisha matendo ya uadilifu ya watakatifu wa Mungu. (Ufunuo 19:8) Mapendeleo mazuri ya utumishi watakayopata huko mbinguni huwachochea kuushinda ulimwengu huu. Wale wanaotarajia kuishi milele duniani watabarikiwa pia. Majina yao pia yanaandikwa katika kitabu cha uhai.

11. Tufanyeje ikiwa tumeanza kusinzia kiroho?

11 Hakuna mmoja wetu ambaye angependa kuwa katika hali yenye kusikitisha kiroho kama ile ya kutaniko la Sardisi. Lakini namna gani tukitambua kwamba tumeanza kusinzia kiroho? Tunapaswa kuchukua hatua mara moja kwa manufaa yetu wenyewe. Namna gani ikiwa tunavutiwa na njia zisizo za kimungu au tumeanza kulegea katika uhudhuriaji wetu wa mikutano au huduma yetu? Acheni tusali kwa bidii kupata msaada wa Yehova. (Wafilipi 4:6, 7, 13) Kusoma na kujifunza Biblia kila siku pamoja na vichapo vya “msimamizi-nyumba mwaminifu” kutatusaidia kuendelea kuwa macho kiroho. (Luka 12:42-44) Kisha tutakuwa kama wale waliokuwa Sardisi ambao walipata kibali cha Kristo, na tutawatia moyo waamini wenzetu.

Kwa Malaika Katika Filadelfia

12. Unaweza kufafanuaje hali ya kiroho katika Filadelfia la kale?

12 Yesu alilipongeza kutaniko la Filadelfia. (Soma Ufunuo 3:7-13.) Jiji la Filadelfia (ambalo sasa ni Alasehiri) lilikuwa kituo chenye ufanisi katika eneo ambapo divai ilitengenezwa, huko magharibi mwa Asia Ndogo. Hata Dionisio, mungu mkuu wa jiji hilo, alikuwa mungu wa divai. Yaonekana Wayahudi wa Filadelfia walishindwa kuwashawishi Wakristo Wayahudi huko kudumisha au kurudia desturi fulani za Sheria ya Musa.

13. Kristo ametumiaje “ufunguo wa Daudi”?

13 Kristo ‘ana ufunguo wa Daudi,’ na hivyo amekabidhiwa mambo yote yanayohusiana na Ufalme na usimamizi wa nyumba ya imani. (Isaya 22:22; Luka 1:32) Yesu alitumia ufunguo huo kuwawezesha Wakristo wa Filadelfia la kale na kwingineko kupata mapendeleo na migawo inayohusiana na Ufalme. Tangu mwaka wa 1919, amemfungulia “mlango mkubwa” “msimamizi-nyumba mwaminifu” ambao unaongoza kwenye kazi ya kuhubiri Ufalme na hakuna mpinzani yeyote anayeweza kuufunga. (1 Wakorintho 16:9; Wakolosai 4:2-4) Bila shaka, mlango unaoongoza kwenye mapendeleo ya Ufalme umefungwa kwa wale wa “sinagogi la Shetani,” kwa kuwa wao si Waisraeli wa kiroho.

14. (a) Yesu aliliahidi nini kutaniko la Filadelfia? (b) Tunawezaje kuepuka kuanguka katika “saa ya jaribu”?

14 Yesu aliwaahidi Wakristo wa Filadelfia la kale hivi: “Kwa sababu ulitunza neno juu ya uvumilivu wangu, hakika mimi pia nitakutunza utoke katika saa ya jaribu, itakayokuja juu ya dunia nzima inayokaliwa, ili kutia jaribu juu ya wale wanaokaa juu ya dunia.” Tunapohubiri tunahitaji kuwa wavumilivu kama Yesu. Yeye hakukubali ashindwe na maadui bali aliendelea kufanya mapenzi ya Baba yake. Kwa hiyo, Kristo alifufuliwa na kupewa uhai usioweza kufa huko mbinguni. Tukishikamana sana na uamuzi wetu wa kumwabudu Yehova na kuunga mkono Ufalme kwa kuhubiri habari njema, hatutaanguka wakati huu wa jaribu, yaani, “saa ya jaribu.” ‘Tutafuliza kushika sana lile tulilo nalo’ kutoka kwa Kristo kwa kujitahidi kuendeleza mambo yanayohusu Ufalme. Watiwa-mafuta wakifanya hivyo watapata taji la kimbingu lenye thamani kubwa, nao waandamani wao washikamanifu watapata uhai wa milele duniani.

15. Wale watakaokuwa “nguzo katika hekalu la Mungu” wanapaswa kufanya nini?

15 Kristo aendelea kusema: “Yeye ashindaye—hakika mimi nitamfanya kuwa nguzo katika hekalu la Mungu wangu, . . . nami hakika nitaandika juu yake jina la Mungu wangu na jina la jiji la Mungu wangu, Yerusalemu jipya lishukalo kutoka mbinguni kwa Mungu wangu, na jina langu jipya.” Waangalizi watiwa-mafuta wanapaswa kutetea ibada ya kweli. Ni lazima wadumishe sifa zinazowastahilisha kuwa washiriki wa “Yerusalemu jipya” kwa kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu na kuendelea kuwa safi kiroho. Hilo ni muhimu ikiwa wanataka kuwa nguzo katika hekalu la kimbingu lililotukuka na kuwa na jina la jiji la Mungu wakiwa raia wa kimbingu na pia kuwa na jina la Kristo wakiwa bibi-arusi wake. Na bila shaka, lazima wawe na masikio ambayo ‘yanasikia lile ambalo roho huyaambia makutaniko.’

Kwa Malaika Katika Laodikia

16. Ni mambo gani yanayotajwa kuhusu Laodikia?

16 Kristo alilikaripia kutaniko la Laodikia lenye uvuguvugu. (Soma Ufunuo 3:14-22.) Jiji la Laodikia lilikuwa umbali wa kilometa 150 mashariki ya Efeso kwenye makutano ya njia kuu zilizotumiwa na wafanyabiashara katika bonde lenye rutuba la Mto Lycus. Jiji hilo lilikuwa limesitawi sana kiviwanda na lilikuwa na benki nyingi. Mavazi yaliyotengenezwa kwa sufu nyeusi iliyopatikana katika eneo hilo yalikuwa maarufu. Jiji la Laodikia lilikuwa na chuo mashuhuri cha tiba, na huenda dawa ya macho ya unga-unga ilitengenezwa huko. Asclepius, mungu wa dawa, alikuwa mmoja wa miungu mikuu ya jiji hilo. Yaelekea Wayahudi wengi waliishi Laodikia na yaonekana baadhi yao walikuwa matajiri sana.

17. Kwa nini watu wa Laodikia walikaripiwa?

17 Akizungumza na kutaniko la Laodikia kupitia “malaika,” Yesu anasema kwa mamlaka akiwa “shahidi mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Wakolosai 1:13-16) Watu wa Laodikia walikaripiwa kwa kuwa walikuwa “si baridi wala moto” kiroho. Kristo angewatapika kutoka kinywani mwake kwa sababu walikuwa vuguvugu. Haikuwa vigumu kwao kuelewa maneno ya Kristo. Eneo la Hierapolisi lililokuwa karibu lilikuwa na chemchemi za maji moto, na Kolosai lilikuwa na maji baridi. Kwa kuwa ilikuwa lazima kutumia mabomba ili kupeleka maji huko Laodikia, jiji lililokuwa mbali, yaelekea maji hayo yalifika huko yakiwa vuguvugu. Lakini katika sehemu nyingine maji hayo yalipita kwenye mfereji. Yalipokaribia Laodikia, yalipita kwenye mawe yaliyotobolewa ambayo yalikuwa yameunganishwa kwa saruji.

18, 19. Leo Wakristo walio kama wa Laodikia wanaweza kusaidiwaje?

18 Leo watu walio kama watu wa Laodikia hawana joto lenye kuchochea wala baridi yenye kuburudisha. Kama maji yenye uvuguvugu, watatapikwa kutoka kinywani! Yesu hataki wawe wasemaji wake wakiwa ‘mabalozi watiwa-mafuta walio badala ya Kristo.’ (2 Wakorintho 5:20) Wasipotubu watapoteza pendeleo lao la kuwa watangazaji wa Ufalme. Watu wa Laodikia walitafuta utajiri wa kimwili na ‘hawakujua walikuwa wenye taabu na wa kusikitikiwa na maskini na vipofu na uchi.’ Ili kumaliza umaskini wao wa kiroho, upofu, na uchi, leo watu wowote walio kama wale wa Laodikia, wanahitaji kununua kutoka kwa Kristo “dhahabu iliyosafishwa” ambayo ni imani iliyojaribiwa. Wanahitaji pia kununua “mavazi meupe ya nje” ya uadilifu na “dawa ya macho” ambayo huboresha uwezo wa kuona mambo kwa njia ya kiroho. Waangalizi Wakristo hufurahi kuwasaidia kuona uhitaji wao wa kiroho ili wawe “matajiri katika imani.” (Yakobo 2:5; Mathayo 5:3) Isitoshe, waangalizi wanahitaji kuwasaidia watumie ‘dawa ya kiroho ya macho,’ yaani, wakubali na kufuata mafundisho, ushauri, kielelezo, na mtazamo wa akili wa Yesu. Hiyo ni dawa ya kuponya “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho wa mtu wa kujivunia njia yake ya kutegemeza maisha.”—1 Yohana 2:15-17.

19 Yesu huwakaripia na kuwatia nidhamu wote anaowapenda. Waangalizi wanaotumikia chini yake wanapaswa kufanya vivyo hivyo kwa upole. (Matendo 20:28, 29) Watu wa Laodikia walihitaji ‘kuwa wenye bidii na kutubu,’ na kurekebisha maoni na maisha yao. Je, baadhi yetu tumeanza kutotilia maanani sana utumishi wetu mtakatifu kwa Mungu maishani? Basi na ‘tununue dawa ya macho kutoka kwa Yesu’ ili tuweze kutambua umuhimu wa kuwa wenye bidii katika kuutafuta kwanza Ufalme.—Mathayo 6:33.

20, 21. Ni nani wanaokubali kumfungulia Yesu ‘anapobisha’ mlango leo, nao wana matarajio gani?

20 Kristo anasema, “Tazama! Mimi nimesimama mlangoni na kubisha. Ikiwa yeyote asikia sauti yangu na kuufungua mlango, hakika mimi nitakuja ndani ya nyumba yake na kula mlo wa jioni pamoja naye na yeye pamoja nami.” Mara nyingi Yesu alitoa maagizo ya kiroho alipokuwa akila. (Luka 5:29-39; 7:36-50; 14:1-24) Sasa anabisha mlango wa kutaniko lililo kama lile la Laodikia. Je, washiriki wake watamfungulia, wachochee tena upendo wao kwake, wamkaribishe katikati yao, na kumruhusu awafundishe? Wakifanya hivyo, Kristo atakula pamoja nao, nao watanufaika sana kiroho.

21 “Kondoo wengine” leo wanamkaribisha Yesu kwa njia ya mfano, na kwa kufanya hivyo watapata uhai wa milele. (Yohana 10:16; Mathayo 25:34-40, 46) Kristo atampa kila mtiwa-mafuta anayeshinda pendeleo la ‘kuketi pamoja naye katika kiti chake cha ufalme, kama vile yeye alivyoshinda na kuketi pamoja na Baba yake katika kiti Chake cha ufalme.’ Naam, Yesu anawaahidi watiwa-mafuta wanaoshinda thawabu tukufu ya kuketi pamoja naye katika kiti cha Ufalme, upande wa kuume wa Baba yake huko mbinguni. Nao kondoo wengine wanaoshinda wanatarajia kuishi katika dunia nzuri sana chini ya utawala wa Ufalme.

Mambo Ambayo Sote Tunajifunza

22, 23. (a) Wakristo wote wanawezaje kunufaika na yale ambayo Yesu aliyaambia makutaniko saba? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

22 Bila shaka Wakristo wote wanaweza kunufaika sana na yale ambayo Yesu aliyaambia yale makutaniko saba huko Asia Ndogo. Kwa mfano, kwa kutambua kwamba Kristo alitoa pongezi ilipohitajika, wazee Wakristo wenye upendo huchochewa kupongeza mtu mmojammoja na makutaniko ambayo yanaendelea vizuri kiroho. Wazee huwasaidia waamini wenzao walio na udhaifu mbalimbali watumie Maandiko kuboresha hali hizo. Sote tunaweza kuendelea kunufaika na ushauri mbalimbali ambao Kristo aliyapa yale makutaniko saba, mradi tunaufuata bila kukawia huku tukisali kwa bidii. *

23 Siku hizi za mwisho si wakati wa kujikalia tu, kufuatia vitu vya kimwili, au kitu chochote kinachoweza kufanya tumtolee Mungu utumishi wa kijuujuu tu. Kwa hiyo, makutaniko yote na yaendelee kung’aa kama vinara vya taa ambavyo Yesu ataviacha mahali pake. Tukiwa Wakristo waaminifu, na tuazimie sikuzote kumsikiliza Kristo anaposema na pia kusikiliza yale ambayo roho inasema. Hivyo, tutapata shangwe ya kudumu na kumtukuza Yehova tukiwa wachukuaji wa nuru.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 22 Andiko la Ufunuo 2:1–3:22 linazungumziwa pia katika sura ya 7 hadi ya 13 ya kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Ungejibuje?

• “Mwanamke Yezebeli” alikuwa nani, na kwa nini wanawake wanaomwogopa Mungu hawamwigi?

• Ni hali gani zilizokuwa katika kutaniko la Sardisi, nasi tunaweza kufanya nini ili tusiwe kama Wakristo wengi walioishi huko?

• Yesu alitoa ahadi gani kwa kutaniko la Filadelfia, nazo zinatuhusuje leo?

• Kwa nini watu wa Laodikia walikaripiwa, lakini Wakristo wenye bidii wana matarajio gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Njia za uovu za “mwanamke Yezebeli” zapaswa kuepukwa

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yesu amewafungulia wafuasi wake “mlango mkubwa” wa kupata mapendeleo ya Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 20]

Je, wewe unamkaribisha Yesu na kumsikiliza?