Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Imara, na Ushinde Shindano la Mbio la Kupata Uhai

Uwe Imara, na Ushinde Shindano la Mbio la Kupata Uhai

Uwe Imara, na Ushinde Shindano la Mbio la Kupata Uhai

IWAPO ungesafiri kwenye bahari yenye dhoruba, ungechagua chombo cha aina gani? Je, ungechagua mashua ndogo nyepesi au meli imara, iliyotengenezwa vizuri? Bila shaka ungechagua meli, kwa sababu inaweza kusafiri vema zaidi katika bahari yenye mawimbi makali.

Tunakabili magumu yenye kutufadhaisha katika mfumo huu wa mambo wenye misukosuko na hatari. Kwa mfano, huenda mara nyingine vijana wakahisi wamechanganyikiwa na wamekosa usalama katika ulimwengu huu wenye maoni na mitindo yenye kutatanisha. Nao watu ambao wamekuwa Wakristo hivi karibuni wanaweza kuwa na shaka ya kadiri fulani. Huenda hata wengine walio imara ambao wamemtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka mingi wakawa wanakabili jaribu kwa sababu mataraja yao hayajatimizwa kikamili.

Hisia kama hizo si mpya. Nyakati nyingine, watumishi waaminifu wa Yehova, kama vile Musa, Ayubu, na Daudi, walikuwa na mahangaiko. (Hesabu 11:14, 15; Ayubu 3:1-4; Zaburi 55:4) Hata hivyo, waliishi maisha yaliyoonyesha kwamba walijitoa kwa Yehova bila kuyumbayumba. Kielelezo chao kizuri kinatutia moyo tuwe imara, lakini Shetani Ibilisi anataka kutukengeusha tutoke katika shindano la mbio la kupata uhai wa milele. (Luka 22:31) Kwa hiyo tunawezaje kuendelea kuwa imara, ‘tukiwa thabiti katika imani’? (1 Petro 5:9) Na tunawezaje kuwaimarisha waamini wenzetu?

Yehova Anataka Tuwe Imara

Sikuzote Yehova atatusaidia tuendelee kuwa thabiti iwapo tutakuwa waaminifu kwake. Mtunga-zaburi Daudi alikabili magumu mengi, lakini alimtumaini Mungu na angeweza kuimba hivi: ‘Yehova alinipandisha toka shimo la uharibifu, toka udongo wa utelezi; akasimamisha miguu yangu mwambani, akaziimarisha hatua zangu.’—Zaburi 40:2.

Yehova hutuimarisha tupigane “pigano bora la imani” ili tuweze kuwa na “mshiko imara juu ya uhai udumuo milele.” (1 Timotheo 6:12) Pia anatusaidia tuendelee kuwa thabiti na tushinde vita vyetu vya kiroho. Mtume Paulo aliwasihi Wakristo wenzake ‘waendelee kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezaji wa nguvu yake’ na ‘wavae suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili wapate kuweza kusimama imara dhidi ya mbinu za Ibilisi.’ (Waefeso 6:10-17) Lakini ni nini kinachoweza kutuhangaisha? Na tunawezaje kujikinga na uvutano huo hatari?

Jihadhari na Mambo Yanayoweza Kufanya Usiwe Thabiti

Ni jambo la hekima kukumbuka jambo hili muhimu: Maamuzi tunayofanya yataathiri uimara wetu wa Kikristo kwa njia nzuri au mbaya hatimaye. Vijana wanakabili maamuzi kuhusu kazi, elimu ya juu, na ndoa. Huenda watu wazima nao wakalazimika kuamua kama watahamia sehemu nyingine au kama watatafuta kazi ya ziada. Tunafanya maamuzi kila siku kuhusu jinsi tunavyotumia wakati na kuhusu mambo mengine mengi. Ni nini kitakachotusaidia tufanye maamuzi kwa hekima ambayo yatatuimarisha zaidi tukiwa watumishi wa Mungu? Mkristo mmoja ambaye ametumikia kwa muda mrefu alisema: “Mimi humwomba Yehova msaada ninapofanya maamuzi. Ninaamini kwamba ni muhimu kukubali na kufuata ushauri unaotolewa kwenye Biblia, kwenye mikutano ya Kikristo, na unaotolewa pia na wazee na vichapo vinavyozungumzia Biblia.”

Tunapofanya maamuzi, tunapaswa kujiuliza: ‘Miaka mitano au kumi ijayo je, nitafurahia maamuzi ninayofanya sasa au nitajuta? Je, ninajitahidi kuhakikisha kwamba maamuzi yangu hayatafanya nisiwe thabiti kiroho bali yatanisaidia kufanya maendeleo kiroho?’—Wafilipi 3:16.

Watu fulani waliobatizwa wameanza kuyumbayumba maishani kwa sababu ya kushindwa na vishawishi au kujiachilia wakaribie sana kuvunja sheria za Mungu. Wakristo kadhaa ambao wameondoshwa katika kutaniko kwa kuendelea kufanya dhambi bila kutubu wamejitahidi sana kurudishwa, kisha wanatengwa tena—muda mfupi baadaye—kwa kufanya dhambi iyo hiyo. Je, inawezekana kwamba hawajaomba msaada wa Mungu ili ‘kukirihi lililo ovu, na kuambatana na lililo jema’? (Waroma 12:9; Zaburi 97:10) Sote tunahitaji ‘kufuliza kufanyia miguu yetu mapito yaliyo manyoofu.’ (Waebrania 12:13) Kwa hiyo, na tuchunguze mambo fulani yanayoweza kutusaidia kuendelea kuwa thabiti kiroho.

Endeleeni Kuimarika Kupitia Utendaji wa Kikristo

Njia moja ya kuendelea kuwa imara katika shindano letu la mbio la kupata uhai ni kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya kuhubiri Ufalme. Naam, huduma yetu ya Kikristo hutusaidia sana kukaza akili na mioyo yetu juu ya kufanya mapenzi ya Mungu na juu ya zawadi ya uhai wa milele. Kuhusiana na hilo, Paulo aliwasihi Wakorintho hivi: “Ndugu zangu wapendwa, iweni imara, wasioondoleka, sikuzote mkiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.” (1 Wakorintho 15:58) Kuwa “imara” humaanisha ‘hali ya kuwa na nguvu na kutotikisika.’ Neno ‘kutoondoleka’ linaweza kumaanisha ‘kuwa thabiti na kutoyumbishwa,’ kuwa na mengi ya kufanya katika huduma kunaweza kutuimarisha katika maisha yetu ya Kikristo. Tunapata furaha na kusudi maishani kwa kuwasaidia wengine wamjue Yehova.—Matendo 20:35.

Pauline, Mkristo ambaye ametumikia kwa miaka 30 akiwa mishonari na katika utumishi mbalimbali wa wakati wote, anasema: “Huduma ni ulinzi kwa sababu ninapowahubiria wengine ninakuwa na hakika kwamba nina kweli.” Tunapata uhakika huohuo pia kwa kushiriki kwa ukawaida katika utendaji mbalimbali wa Kikristo kama vile kuhudhuria mikutano ya ibada na kujifunza Biblia kwa bidii.

Tunaimarishwa na Upendo wa Kidugu

Kuwa katika tengenezo la ulimwenguni pote la waabudu wa kweli kunaweza kutusaidia tuwe thabiti sana. Ni baraka iliyoje kushirikiana na ndugu wenye upendo wa ulimwenguni pote! (1 Petro 2:17) Nasi tunaweza kuwasaidia waamini wenzetu wawe thabiti.

Fikiria jinsi Ayubu mwadilifu alivyowasaidia wengine. Hata Elifazi mfariji bandia alilazimika kukiri hivi: “Maneno yako yamemtegemeza huyo aliyekuwa anaanguka, nawe umeyaimarisha magoti manyonge.” (Ayubu 4:4) Je, sisi huwasaidia wengine? Sote tuna daraka la kuwasaidia ndugu na dada zetu wa kiroho waendelee kumtumikia Mungu. Tunapokuwa pamoja na ndugu na dada zetu, tunaweza kutenda kulingana na maneno haya: “Itieni nguvu mikono iliyo dhaifu, yafanyeni imara magoti yaliyolegea.” (Isaya 35:3) Kwa hiyo, mbona usiazimie kuwaimarisha na kuwatia moyo Wakristo wenzako unapokutana nao? (Waebrania 10:24, 25) Kwa kuwatia moyo, kuwapongeza, na kuwashukuru kwa jitihada zao za kumpendeza Yehova, unaweza kuwasaidia sana waendelee kuwa imara, wakiwa na taraja la kushinda shindano la mbio la kupata uhai.

Wazee Wakristo wanaweza kutimiza mengi kwa kuwatia moyo wapya. Wanaweza kufanya hivyo kwa kutoa madokezo na ushauri wa Kimaandiko unaofaa na kwa kuhubiri pamoja nao. Kila mara mtume Paulo alitumia fursa mbalimbali kuwaimarisha wengine. Alitamani kuwaona Wakristo huko Roma ili aweze kuwaimarisha kiroho. (Waroma 1:11) Aliwaona ndugu na dada zake wapendwa huko Filipi kuwa ‘shangwe na taji’ lake na kuwahimiza ‘wasimame imara katika njia hii katika Bwana.’ (Wafilipi 4:1) Aliposikia magumu yaliyowapata ndugu zake huko Thesalonike, Paulo alimtuma Timotheo ‘akawafanye imara na kuwafariji kwamba yeyote asipate kuyumbishwa na dhiki.’—1 Wathesalonike 3:1-3.

Mtume Paulo na Petro walishukuru na kuthamini jitihada za uaminifu za waabudu wenzao. (Wakolosai 2:5; 1 Wathesalonike 3:7, 8; 2 Petro 1:12) Vivyo hivyo, badala ya kuzingatia udhaifu wa ndugu zetu, na tuzingatie sifa zao nzuri na jinsi wanavyofanikiwa katika pambano lao la kuendelea kuwa imara na kumtukuza Yehova.

Huenda bila kujua tukafanya iwe vigumu kwa ndugu zetu kuendelea kuwa imara katika imani iwapo tuna maoni yasiyofaa au tunawachambua. Inafaa kama nini kukumbuka kwamba ndugu zetu ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku’ katika mfumo huu wa mambo! (Mathayo 9:36) Katika kutaniko la Kikristo, wanatarajia kupata faraja na burudiko. Kwa hiyo, sote na tufanye yote tuwezayo kuwajenga waamini wenzetu na kuwasaidia waendelee kuwa imara.

Huenda mara kwa mara wengine wakatutendea kwa njia inayoweza kudhoofisha uimara wetu. Je, tutapunguza bidii yetu katika utumishi wa Yehova kwa sababu ya maneno yasiyo ya huruma au tendo lisilo la fadhili? Na tusiruhusu mtu yeyote kamwe atupotoshe na kufanya tuache uimara wetu!—2 Petro 3:17.

Ahadi za Mungu Hufanya Tuwe Thabiti

Ahadi ya Yehova ya wakati ujao ulio mzuri chini ya utawala wa Ufalme hutupatia tumaini linalotusaidia kuendelea kuwa imara. (Waebrania 6:19) Na uhakika kwamba sikuzote Mungu hutimiza ahadi zake hutuchochea ‘kukaa macho na kusimama imara katika imani.’ (1 Wakorintho 16:13; Waebrania 3:6) Huenda imani yetu ikajaribiwa tunapoona kana kwamba ahadi fulani za Mungu zinakawia kutimizwa. Kwa hiyo ni muhimu tujilinde dhidi ya kupotoshwa na mafundisho ya uwongo na kuacha tumaini letu.—Wakolosai 1:23; Waebrania 13:9.

Tunapata onyo kutokana na kielelezo kibaya cha Waisraeli waliokufa kwa sababu ya kutokuwa na imani katika ahadi za Yehova. (Zaburi 78:37) Badala ya kuwa kama wao, na tuendelee kuwa imara, tukimtumikia Mungu huku tukitambua umuhimu wa nyakati tunamoishi katika siku hizi za mwisho. Mzee mmoja mwenye uzoefu alisema, “kila siku ninaishi kana kwamba siku ya Yehova itakuja kesho.”—Yoeli 1:15.

Naam, siku kuu ya Yehova inakaribia. Hata hivyo, hatupaswi kuogopa chochote mradi tunakuwa karibu na Mungu. Tukishika viwango vyake vya uadilifu bila kuyumbayumba na kuendelea kuwa imara, tunaweza kukimbia na kushinda shindano la mbio la kupata uhai wa milele!—Mithali 11:19; 1 Timotheo 6:12, 17-19.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Je, unafanya yote uwezayo ili kuwasaidia Wakristo wenzako waendelee kuwa imara?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 21]

The Complete Encyclopedia of Illustration/J. G. Heck