Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, ni kosa kumuua mnyama-kipenzi aliye mgonjwa sana au aliyezeeka?

Watu wengi hufurahia sana kuwa na wanyama mbalimbali. Wanyama fulani wa kufugwa huwa wanyama-vipenzi wazuri. Kwa mfano, mbwa wanajulikana kwa sababu ya kuwatii kabisa na kuwapenda wamiliki wao. Kwa hiyo, inaeleweka kwa nini watu huwapenda wanyama-vipenzi kama hao, hasa wale ambao wamekuwa nao kwa miaka mingi.

Hata hivyo, wanyama-vipenzi wengi huishi kwa muda mfupi tu. Mbwa na paka wanaweza kuishi kati ya miaka 10 na 15 hivi, ikitegemea jamii yao. Huenda wanyama-vipenzi wakawa wagonjwa na kulemaa wanapozeeka na hilo laweza kuwahangaisha wamiliki wao wanapokumbuka jinsi wanyama hao walivyokuwa walipokuwa wachanga na wenye nguvu. Je, ni kosa kukomesha mateso ya wanyama hao kwa kuwaua?

Mkristo anapaswa kuzingatia mapenzi ya Mungu anaposhughulika na wanyama. Bila shaka kuwatendea wanyama kikatili ni kinyume cha mapenzi ya Mungu, kwa kuwa Neno lake lasema: “Mwenye haki huufikiri uhai wa mnyama wake.” (Mithali 12:10) Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba Mungu huwaona wanyama kama anavyowaona wanadamu. Mungu alipowaumba wanadamu, alionyesha wazi kwamba kuna tofauti kubwa kati yao na wanyama. Kwa mfano, aliwapa wanadamu tumaini la kuishi milele, lakini si wanyama. (Waroma 6:23; 2 Petro 2:12) Kwa kuwa yeye ni Muumba, ana haki ya kuamua uhusiano unaofaa kati ya wanadamu na wanyama.

Andiko la Mwanzo 1:28 hutuambia kuhusu uhusiano huo. Mungu aliwaambia wanadamu wa kwanza hivi: “Mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.” Vivyo hivyo, Zaburi 8:6-8 inasema: “[Mungu] umevitia vitu vyote chini ya miguu yake [mwanadamu]. Kondoo, na ng’ombe wote pia; naam, na wanyama wa kondeni; ndege wa angani, na samaki wa baharini.”

Mungu alisema wazi kwamba wanadamu wangeweza kuwatumia wanyama na kuwaua ifaavyo. Kwa mfano, ngozi yao ingeweza kutumiwa kama mavazi. Pia, Mungu aliwaruhusu wanadamu kula nyama ya wanyama baada ya Gharika ya siku za Noa, kuongezea mlo wa mboga waliopewa hapo awali.—Mwanzo 3:21; 4:4; 9:3.

Hiyo haiwapi wanadamu ruhusa ya kuwaua wanyama ovyoovyo katika michezo. Kwenye Mwanzo 10:9, Biblia inamtaja Nimrodi kuwa “hodari wa kuwinda wanyama.” Lakini mstari huohuo unasema pia kwamba hilo lilimfanya kuwa ‘mpinzani wa Yehova,’ NW.

Kwa hiyo, mwanadamu ana mamlaka juu ya wanyama, lakini hapaswi kuyatumia vibaya, anapaswa kuyatumia kulingana na kanuni za Neno la Mungu. Hilo linaweza kutia ndani kutomwacha mnyama-kipenzi ateseke isivyo lazima kwa sababu ya kuzeeka, jeraha baya, au ugonjwa hatari. Katika hali kama hizo, ni jukumu la Mkristo kuamua atakalofanya. Akiona kwamba ni jambo la rehema kumuua mnyama-kipenzi badala ya kumwacha tu ateseke bila tumaini la kupona, basi ni uamuzi wake.