Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Solomoni Hakupambwa Kama Moja la Haya’

‘Solomoni Hakupambwa Kama Moja la Haya’

‘Solomoni Hakupambwa Kama Moja la Haya’

MAUA ya mwituni kama haya hukua kwa wingi kandokando ya barabara za kusini mwa Afrika. Yanaitwa cosmos na asili yake ni maeneo ya kitropiki ya Amerika. Huenda maua hayo maridadi yakatukumbusha jambo ambalo Yesu alifundisha. Wasikilizaji wake wengi walikuwa maskini na walihangaikia sana mahitaji yao ya kimwili, chakula na mavazi.

“Katika lile jambo la mavazi,” Yesu aliwauliza, “kwa nini mwahangaika? Twaeni somo kutokana na mayungiyungi ya shamba, jinsi yanavyokua; hayamenyeki kwa kazi, wala hayasokoti; lakini nawaambia nyinyi kwamba hata Solomoni katika utukufu wake wote hakupambwa kama moja la haya.”—Mathayo 6:28, 29.

Watu wametoa maoni mbalimbali kuhusu ua-mwitu hususa ambalo Yesu alikuwa akizungumzia. Hata hivyo, Yesu alilifananisha na mimea ya kawaida aliposema hivi: “Basi, ikiwa Mungu huvisha hivyo mimea ya shambani, ambayo ipo hapa leo na kesho hutupwa ndani ya joko, je, si afadhali zaidi sana yeye atawavisha nyinyi, nyinyi wenye imani kidogo?”—Mathayo 6:30.

Ingawa maua haya hayapatikani Israeli, bila shaka yanathibitisha yale ambayo Yesu alifundisha. Ni maua maridadi sana yawe yanatazamwa kwa mbali au kwa ukaribu na yanapendwa sana na wapiga-picha na wasanii. Kwa kweli, Yesu hakutilia chumvi aliposema, “hata Solomoni katika utukufu wake wote hakupambwa kama moja la haya.”

Tunajifunza nini leo? Wale wanaomtumikia Mungu wana uhakika kwamba atawasaidia kupata mahitaji yao hata katika nyakati za magumu. Yesu alieleza hivi: “Tafuteni ufalme wake [wa Mungu] kwa kuendelea, na mambo haya [kama vile chakula na mavazi] mtaongezewa.” (Luka 12:31) Naam, manufaa halisi hutokana na kuutafuta Ufalme wa Mungu. Lakini je, unajua Ufalme wa Mungu ni nini na utawafanyia nini wanadamu? Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kupata majibu kutoka katika Biblia.