Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Wanayaonaje Mashirika ya Kutoa Misaada?

Watu Wanayaonaje Mashirika ya Kutoa Misaada?

Watu Wanayaonaje Mashirika ya Kutoa Misaada?

BAADA ya mashambulizi ya Septemba 11, 2001, huko New York City na Washington, D.C., watu wengi walijitolea kuwasaidia watu walioathiriwa na msiba huo. Mashirika ya kutoa misaada yalipokea michango ya dola bilioni 2.7 za Marekani ili kusaidia familia zilizoathiriwa. Kila mahali watu walihuzunishwa sana na msiba huo na wakataka kutoa misaada.

Lakini, baadhi ya watu walikasirika sana waliposikia madai ya kwamba mashirika maarufu ya kutoa misaada yalikuwa yakitumia vibaya pesa hizo. Wengi waliudhika sana waliposikia kwamba shirika moja kubwa la kutoa misaada lilipanga kutumia kwa makusudi mengine, karibu nusu ya dola milioni 546 zilizokusanywa. Ijapokuwa shirika hilo lilibadili uamuzi huo na kuomba radhi, ripota mmoja alisema hivi: “Wachambuzi wanasema kwamba shirika hilo lilichelewa mno kubadili maoni na hivyo halingeweza kutumainiwa tena kama ilivyokuwa” kabla ya mashambulizi hayo. Vipi wewe? Je, umeanza kushuku mashirika ya kutoa misaada?

Kutoa Kunakusaidia au Kunakuletea Hasara?

Kwa kawaida kutoa misaada huonwa kuwa tendo jema. Hata hivyo, si kila mtu anayekubaliana na maoni hayo. Zaidi ya miaka 200 iliyopita, Samuel Johnson, mwandishi Mwingereza wa insha, aliandika hivi: “Unakuwa na uhakika kwamba unafanya mema unapowalipa watu wanaofanya kazi kuliko unapotoa misaada ya kifedha.” Baadhi ya watu leo wana maoni kama hayo, na ripoti kuhusu mashirika ya kutoa misaada ambayo yanatumia vibaya michango hiyo zinawavunja wengi moyo. Fikiria mifano hii miwili ya karibuni.

Mkurugenzi wa shirika moja la kidini la kutoa misaada huko San Francisco alifutwa kazi baada ya madai ya kwamba alitaka shirika hilo lilipe ada ya upasuaji wa kurekebisha sura yake na pia malipo yake ya hotelini ya dola 500 kila juma kwa zaidi ya miaka miwili. Huko Uingereza, waandalizi wa kipindi maarufu cha televisheni cha kuomba misaada waliaibika ilipogunduliwa kwamba dola zipatazo milioni 10 zilizokusanywa ili kujenga makao ya mayatima huko Rumania zilitumiwa kujenga nyumba 12 tu za hali ya chini sana, na mamia ya maelfu ya dola zilizosalia zilitoweka. Ripoti mbaya kama hizo zimewafanya watu fulani wanaotoa michango wawe waangalifu zaidi kuhusu kiasi wanachotoa na yule wanayempa.

Utoe au Usitoe?

Hata hivyo, inasikitisha iwapo tunaruhusu matendo ya watu au mashirika machache yatuzuie kuwajali na kuwahurumia wengine. Biblia yasema hivi: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyo na unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kutazama mayatima na wajane katika dhiki yao.” (Yakobo 1:27) Naam, kuwasaidia maskini na watu wa hali ya chini ni jambo muhimu katika Ukristo.

Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Je, niendelee kutoa michango kwa mashirika ya kutoa misaada, au nijaribu tu kuwasaidia watu kwa kuwapa zawadi kibinafsi?’ Mungu hupenda utoaji wa aina gani? Makala inayofuata itajibu maswali hayo.