Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasaidia Watu Wanaotumia Lugha ya Pekee Nchini Korea

Kuwasaidia Watu Wanaotumia Lugha ya Pekee Nchini Korea

Kuwasaidia Watu Wanaotumia Lugha ya Pekee Nchini Korea

WATU wenye shauku sana ijapokuwa wanyamavu walihudhuria kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova nchini Korea mwaka wa 1997. Hilo lilikuwa kusanyiko la kwanza lililofanywa katika nchi hiyo kwa ajili ya viziwi na watu wasioweza kusikia vizuri. Watu 1,174 walihudhuria kusanyiko hilo. Hotuba zote, mahojiano, na drama, zilitolewa katika Lugha ya Ishara ya Korea na kuonyeshwa kwenye ubao mkubwa wa maonyesho ulioonekana kotekote katika Jumba la Kusanyiko. Kusanyiko hilo lilikuwa kilele cha kazi ambayo watu wengi waliojitolea walikuwa wamefanya kwa miaka mingi.

“Masikio ya viziwi yatazibuliwa” katika paradiso ya kidunia itakayokuja. (Isaya 35:5) Ili kuishi katika Paradiso hiyo, ni lazima watu wote, hata viziwi, waingie kwanza katika paradiso ya kiroho, yaani, hali nzuri ya kiroho ya watu wa Mungu wenye furaha. Ni lazima wawe watu wanaofundishwa na Yehova na kuwa Mashahidi wake waliojiweka wakfu na kubatizwa.—Mika 4:1-4.

Wachache Waanza

Ijapokuwa viziwi walikuwa wamehubiriwa kwa kadiri fulani katika miaka ya 1960, ni katika miaka ya 1970 ambapo viziwi wachache walianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova huko Seoul, jiji kuu la Korea. Ndugu Mkristo aliyeweza kuandika haraka aliandika ubaoni mambo makuu ya hotuba na maandiko ya Biblia yaliyozungumziwa.

Katika jiji la Taejon, Shahidi mmoja alianza kumfundisha mwana wake kiziwi, na marafiki viziwi wa mwana huyo, ujumbe wa Ufalme mwaka wa 1971. Watu kadhaa wenye bidii wa kikundi hicho sasa wanategemeza makutaniko mengi ya lugha ya ishara.—Zekaria 4:10.

Vijana Wajitoa kwa Hiari

Ili viziwi wajifunze kumhusu Yehova na Yesu na hivyo kuwa na tumaini la kuishi milele, watu wengine wenye kujitolea wangehitaji kujitahidi sana. (Yohana 17:3) Kwa hiyo, baadhi ya Mashahidi wa Yehova wamejifunza lugha ya ishara, nao wamebarikiwa sana.

Kijana mmoja mwenye umri wa miaka 15 anayeitwa Park In-sun alijiwekea mradi wa kujifunza lugha ya ishara. Ili ajifunze lugha hiyo, akawa mwanafunzi katika kiwanda fulani, ambapo viziwi 20 walikuwa wakifanya kazi. Alifanya kazi pamoja nao kwa miezi minane ili ajifunze lugha ya ishara na ili aelewe jinsi wanavyofikiri. Mwaka uliofuata, akawa painia wa kawaida, au mhubiri wa wakati wote wa Ufalme, na akasaidia kikundi kimoja cha viziwi waliotaka kujua kweli za Biblia. Kikundi hicho kiliongezeka haraka, na punde si punde zaidi ya watu 35 walikuwa wakihudhuria mikutano ya Jumapili.—Zaburi 110:3.

Baadaye, mikutano ya Kikristo katika lugha ya ishara ilipangwa kwa mara ya kwanza jijini Seoul. Ndugu Park In-sun alitumikia akiwa painia wa pekee katika kikundi hicho kilichoendelea kuongezeka. Wakati huo alikuwa amejua lugha ya ishara kabisa. Katika miezi fulani aliongoza mafunzo ya Biblia 28 na viziwi. Wengi wa wanafunzi hao walifanya maendeleo nao wakawa Mashahidi wa Yehova.

Kwa sababu ya bidii yake katika kazi hiyo ya kujitolea, kutaniko la kwanza la lugha ya ishara lilianzishwa Oktoba, 1976, jijini Seoul. Kutaniko hilo jipya lilikuwa na wahubiri 40 na mapainia wa kawaida 2. Matokeo hayo mazuri yaliwatia wengine moyo kuwahubiria viziwi katika majiji mengine huko Korea. Viziwi wengi walitaka kusikia habari njema na walikuwa wakingoja kutembelewa.

Kuwasaidia Viziwi

Viziwi walipatikanaje? Mara nyingi wahubiri waliwaomba viziwi waliojifunza wawajulishe kwa marafiki wao. Wahubiri waliwaendea pia wenye maduka ya mchele, nao waliwajulisha majina na anwani za wateja wao viziwi. Ofisi fulani za serikali ziliwasaidia pia kupata majina na anwani za viziwi. Kuwatafuta na kuwahubiria viziwi kwa bidii kulifanikiwa sana hivi kwamba muda si muda makutaniko manne ya lugha ya ishara yalianzishwa. Vijana wengi Wakristo walitiwa moyo wajifunze lugha ya ishara.

Mapainia wa pekee waliokuwa wamejifunza lugha ya ishara walitumwa na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova kusaidia makutaniko hayo. Hivi majuzi, wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Huduma wametumwa kusaidia makutaniko hayo, na wameyaimarisha kiroho.

Hata hivyo, kuna magumu pia. Inawabidi wale wanaowahubiria viziwi kujitahidi kuelewa desturi na tabia za viziwi. Watu hao wanasema waziwazi na kutenda kwa njia ya moja kwa moja. Jambo hilo linawashangaza watu nyakati nyingine, na kwa hiyo kutoelewana kunaweza kutokea. Isitoshe, mbali na kuwafundisha Biblia, Mashahidi wanaoongoza mafunzo ya Biblia wanahitaji kuwasaidia viziwi kujua lugha yao ya ishara vizuri zaidi na kuwatia moyo wasome na wajifunze zaidi.

Viziwi hukabili matatizo katika shughuli fulani za kawaida maishani. Kwa mfano, kuongea na watu wenye mamlaka katika ofisi za serikali au hospitalini, na katika shughuli za kibiashara kunaweza kuwatatiza sana. Viziwi wamepata udugu wa kweli katika kutaniko la Kikristo kwa sababu Mashahidi katika makutaniko mengine wamejitolea kuwasaidia.—Yohana 13:34, 35.

Kutoa Ushahidi Katika Kila Fursa Huleta Matokeo

Shahidi mmoja alikutana na viziwi wawili katika jiji kubwa la bandari kusini mwa Korea, yaani, Pusan. Wao waliandika hivi kwenye karatasi: “Tunapenda Paradiso. Tunataka kuyajua maandiko yanayotaja uzima wa milele.” Ndugu huyo aliandika anwani yao na kupanga kuwatembelea. Alipowatembelea, aliwapata viziwi wengi katika chumba kimoja wakingoja kusikia ujumbe wa Ufalme. Jambo hilo lilimsukuma kuanza kujifunza lugha ya ishara. Punde kutaniko la lugha ya ishara likaanzishwa jijini Pusan.

Ndugu mmoja wa kutaniko hilo aliwaona viziwi wawili waliokuwa wakiwasiliana kwa kutumia ishara, naye akawaendea. Alipojulishwa kwamba wametoka tu kuhudhuria mkutano fulani wa kidini, aliwaalika kwenye Jumba la Ufalme saa nane alasiri hiyo. Walihudhuria mkutano, na funzo la Biblia likaanzishwa. Muda mfupi baadaye, viziwi hao 2 walihudhuria kusanyiko la wilaya pamoja na marafiki viziwi 20. Wengine kadhaa kutoka katika kikundi hicho wamejiweka wakfu kwa Yehova. Wawili sasa ni wazee katika makutaniko ya lugha ya ishara, na mmoja ni mtumishi wa huduma.

Jitihada Huleta Matokeo

Kwa sababu viziwi fulani wanaishi mbali na makutaniko ya lugha ya ishara, mara nyingi inawabidi ndugu kujitahidi sana kuwaandalia kwa ukawaida chakula cha kiroho kutoka katika Biblia. Kwa mfano, mwanamume mmoja mwenye umri wa miaka 31 alifanya kazi ya uvuvi kwenye kisiwa fulani. Ndugu yake mdogo aliyekuwa ametembelewa na Mashahidi wa Yehova alimweleza ujumbe wa Biblia. Ili kuridhisha njaa yake ya kiroho, mvuvi huyo kiziwi alisafiri kilometa 16 kwa mashua hadi Tongyoung City kwenye pwani ya kusini mwa Korea. Alifunga safari hiyo ili aonane na painia wa pekee wa kutaniko la lugha ya ishara la Masan City. Painia huyo alisafiri kilometa 65 kila Jumatatu ili aongoze funzo la Biblia pamoja na mvuvi huyo kiziwi.

Ili kuhudhuria mkutano wa Jumapili huko Masan City, ilimbidi mwanafunzi huyo wa Biblia kusafiri kilometa 16 kwa mashua kisha kusafiri kilometa 65 kwa basi. Lakini jitihada hizo zilikuwa na matokeo mazuri. Baada ya miezi michache alijua lugha ya ishara vizuri zaidi, herufi nyingi zaidi za Kikorea, na jambo muhimu zaidi ni kwamba alijua jinsi ya kujenga uhusiano wa karibu na Yehova. Alipotambua umuhimu wa mikutano na kazi ya kuhubiri, alihamia karibu na kutaniko la lugha ya ishara. Haikuwa rahisi kufanya uamuzi huo. Ilimbidi kuacha kazi yake ya uvuvi iliyomletea mapato ya dola 3,800 za Marekani kila mwezi. Lakini uamuzi wake ulimletea uradhi. Baada ya kufanya maendeleo ya kiroho, alibatizwa na sasa anamtumikia Yehova kwa furaha pamoja na familia yake.

Kutafsiri kwa Ajili ya Viziwi

Habari njema za Ufalme huhubiriwa kwa mdomo mara nyingi. Hata hivyo, ili kueneza Neno la Mungu kwa usahihi, ni muhimu mafundisho ya Biblia yawasilishwe kwa njia yenye kudumu zaidi. Kwa hiyo, katika karne ya kwanza, barua na vitabu viliandikwa na wazee wenye ujuzi mwingi. (Matendo 15:22-31; Waefeso 3:4; Wakolosai 1:2; 4:16) Leo tunaandaliwa chakula kingi cha kiroho katika vitabu na magazeti ya Kikristo. Vitabu na magazeti hayo yametafsiriwa katika mamia ya lugha, kutia ndani lugha mbalimbali za ishara. Vitabu hivyo hutafsiriwa katika Lugha ya Ishara ya Korea kwenye idara ya tafsiri ya ofisi ya tawi ya Korea. Video za lugha ya ishara hutengenezwa pia katika idara ya video. Chakula cha kiroho hutayarishwa kwa njia hiyo kwa ajili ya wahubiri viziwi wa habari njema na watu wanaopendezwa kotekote nchini Korea.

Ijapokuwa wengi wamejua lugha ya ishara kabisa na wamesaidia kutengeneza video, watoto wa viziwi ndio watafsiri stadi zaidi. Wao wamejifunza lugha ya ishara tangu utotoni. Mbali na kutumia ishara sahihi, ishara zao za mkono na uso hukazia maana na huonyesha hisia za moyoni, na hivyo ujumbe hueleweka na kufikia moyo.

Kama tulivyotangulia kutaja, sasa makusanyiko ya lugha ya ishara hufanywa kwa ukawaida nchini Korea. Kazi nyingi imefanywa na pesa nyingi zimetumiwa ili kufikia lengo hilo. Hata hivyo, wale wanaohudhuria makusanyiko hayo huthamini mpango huo. Baada ya makusanyiko hayo wengi hukawia kuondoka kwa sababu wanataka kuendelea kufurahia ushirika mzuri na kuzungumza juu ya chakula kizuri cha kiroho kilichoandaliwa. Bila shaka nyakati nyingine inaweza kuwa vigumu kutumikia kikundi hicho cha pekee, lakini jambo hilo huleta baraka nyingi za kiroho pia.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Video za lugha ya ishara zilizotengenezwa nchini Korea: “Mungu Anataka Tufanye Nini?,” “Kuthamini Urithi Wetu wa Kiroho,” “Vielelezo vya Kuonya Leo,” na “Heshimu Mamlaka ya Yehova”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kuanzia chini kuelekea kulia: Video ya lugha ya ishara ikitengenezwa kwenye ofisi ya tawi nchini Korea; ishara za maneno ya kitheokrasi zinatayarishwa; watafsiri wa lugha ya ishara; ndugu anayetafsiri kwa kutumia ishara anaelekezwa, video inapotengenezwa