Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shule ya Gileadi Miaka 60 ya Mazoezi ya Kimishonari

Shule ya Gileadi Miaka 60 ya Mazoezi ya Kimishonari

Shule ya Gileadi Miaka 60 ya Mazoezi ya Kimishonari

“KWA sababu ya kujifunza mambo mengi kutoka katika Biblia, tulimkaribia Yehova na kujifunza mengi zaidi kuhusu tengenezo lake. Hilo lilitutayarisha kwa ajili ya maisha katika mgawo katika nchi ya kigeni.” Hivyo ndivyo mwanafunzi aliyehitimu kutoka katika darasa la kwanza alivyofafanua mafunzo aliyopata katika Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Tangu ilipoanzishwa miaka 60 iliyopita, Shule ya Gileadi imekuwa ikiwatuma mishonari. Mnamo Machi 8, 2003, darasa la 114 lilihitimu katika Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York. Watu 6,404 waliokusanyika katika jumba na katika sehemu nyingine zilizounganishwa kupitia televisheni walisikiliza kwa makini programu iliyotia ndani hotuba, mahojiano, na mazungumzo ya vikundi.

Mwenyekiti alikuwa Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Kwenye utangulizi wake alitaja kwamba kati ya wahudhuriaji kulikuwa na wasikilizaji kutoka nchi mbalimbali. Kulikuwa na wageni kutoka Amerika ya Kati na ya Kusini, Asia, Karibea, na Ulaya. Akitumia andiko la 2 Timotheo 4:5, Ndugu Jaracz alikazia kazi muhimu ya mishonari waliozoezwa Gileadi, yaani, ‘kufanya kazi ya mweneza-evanjeli.’ Mishonari hao wanaishuhudia kweli kwa kuwafundisha watu Biblia.

Wanafunzi Wapokea Maagizo ya Mwisho

Msemaji wa kwanza katika mfululizo wa hotuba fupifupi, John Larson, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani, alitoa hotuba yenye kuimarisha imani yenye kichwa “Ikiwa Mungu Yuko Upande Wetu, Nani Atakayekuwa Dhidi Yetu?” (Waroma 8:31) Msemaji huyo alieleza msingi wa Biblia utakaowasaidia wanafunzi kuwa na uhakika kamili katika nguvu za Yehova za kuwasaidia kushinda vizuizi vyovyote vinavyoweza kuwakabili katika migawo yao. Akitumia Waroma 8:38, 39, Ndugu Larson aliwahimiza wanafunzi hivi: “Tua ufikirie nguvu ambayo Mungu anatumia kwa niaba yako, na ukumbuke kwamba hakuna chochote kinachoweza kuuzuia upendo wa Yehova kwako.”

Aliyefuata kwenye programu alikuwa Guy Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Alichagua hotuba yenye kichwa “Dumisheni Macho Yenu Yakiwa Yenye Furaha!” (Luka 10:23) Alieleza kwamba furaha ya kweli inatia ndani kumjua Yehova na kuelewa kusudi lake la milele na pia kuona utimizo wa unabii mbalimbali wa Biblia. Popote wanapoenda, wanafunzi wanaweza kuendelea kuwa na furaha ya kweli kwa kudumisha macho yao yakiwa yenye furaha. Ndugu Pierce aliwatia moyo wanafunzi watafakari kwa uzito kuhusu wema wa Yehova na kukaza akili zao na moyo wao katika kufanya mapenzi Yake. (Zaburi 77:12) Kwa kudumisha mtazamo unaofaa, wanafunzi wanaweza kushinda matatizo yoyote yanayoweza kuwapata.

Kisha wanafunzi wakapokea maneno ya mwisho ya kuwatia moyo kutoka kwa walimu wao wawili waliokuwa wakiwafundisha kila siku. “Je, Unatafuta Utukufu?” akauliza Lawrence Bowen katika kichwa cha hotuba yake. Watu wengi huhusianisha utukufu na sifa, heshima, na umashuhuri wao wenyewe. Hata hivyo, mtunga-zaburi Asafu, alipata kuelewa maana ya utukufu wa kweli, yaani hazina isiyo na kifani ya kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova. (Zaburi 73:24, 25) Wanafunzi waliohitimu walitiwa moyo kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kwa kuendelea kujifunza zaidi Biblia. Malaika “wanatamani kuchungulia” ndani ya mambo yanayohusu kutimizwa kwa kusudi la Yehova kupitia Kristo. (1 Petro 1:12) Wanataka kujifunza mambo mengi iwezekanavyo kumhusu Baba yao ili waweze kuuonyesha utukufu wake. Kisha msemaji akawahimiza wanafunzi wamtukuze Yehova katika migawo yao ya mishonari kwa kuwasaidia wengine kuipata hazina hiyo yenye thamani isiyo na kifani.

Mwandikishaji wa shule hiyo, Wallace Liverance, akamalizia mfululizo huo wa kwanza wa hotuba kwa kichwa “Sema Hekima ya Mungu Katika Siri Takatifu.” (1 Wakorintho 2:7) Hekima hiyo ya Mungu ambayo mtume Paulo alizungumza juu yake katika utumishi wake wa mishonari ni nini? Ni njia ya Yehova yenye hekima na nguvu ya kuleta amani na umoja ulimwenguni. Hekima hiyo inamhusu Yesu. Badala ya kuhubiri Injili ya kijamii, mtume Paulo aliwasaidia watu kujua jinsi Mungu atakavyoondoa madhara ya dhambi ya Adamu. (Waefeso 3:8, 9) Msemaji akawatia moyo wasikilizaji wake hivi: “Tumieni pendeleo lenu la utumishi kama alivyofanya Paulo ambaye aliuona mgawo wake wa mishonari kuwa nafasi ya kuwasaidia watu kuona jinsi ambavyo Yehova angetimiza kusudi lake.”

Kisha, Mark Noumair, mwalimu mwingine wa Gileadi, akaongoza mazungumzo yenye uchangamfu pamoja na baadhi ya wanafunzi. Kichwa “Funzo la Neno la Mungu Hutokeza Wahudumu Wenye Bidii” kilikazia maneno ya Paulo kwenye Waroma 10:10. Wanafunzi walisimulia mambo mbalimbali waliyojionea shambani walipokuwa shuleni. Mambo hayo yalionyesha kwamba tunapojifunza na kutafakari Neno la Mungu, mambo mazuri kumhusu Yehova Mungu na Ufalme wake yataujaza moyo wetu nasi tutawaambia wengine juu yake. Katika kipindi cha miezi mitano waliyokaa katika Kituo cha Elimu cha Watchtower, wanafunzi hao walianza kujifunza Biblia na watu zaidi ya 30 wenye kupendezwa katika maeneo ambayo yamehubiriwa sana ya makutaniko ya karibu.

Ndugu Wakomavu Watoa Mashauri

Shule ilipokuwa ikiendelea, wanafunzi walifaidika kwa kushirikiana na washiriki wa familia ya Betheli ya Marekani. Washiriki wa ofisi ya tawi Robert Ciranko na Robert P. Johnson waliwahoji watumishi kadhaa ambao wamemtumikia Yehova kwa muda mrefu kutia ndani waangalizi wasafirio waliokuwa wakipokea mazoezi ya pekee kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower. Wote waliohojiwa walikuwa wahitimu wa Gileadi ambao wakati fulani walikuwa mishonari. Lilikuwa jambo lenye kutia moyo kwa wanafunzi hao, pamoja na familia na rafiki zao kusikia maneno yenye hekima kutoka kwa wanaume hao wa kiroho wenye ujuzi.

Waliwashauri hivi: “Endeleeni kuwa na shughuli nyingi iwezekanavyo katika huduma na kutanikoni.” “Msijione kuwa watu bora sana. Kazieni fikira kusudi lenu la kuwa mishonari na kuufanya mgawo wenu kuwa nyumbani kwenu.” Maelezo mengine yalionyesha jinsi ambavyo mazoezi ya Gileadi humwezesha mhudumu kufanya kazi nzuri hata mgawo wake uwe wapi. Baadhi yake ni: “Tulijifunza kushirikiana na kufanya kazi pamoja.” “Shule ilitusaidia kukubali tamaduni mpya.” “Tulifundishwa kutumia Maandiko kwa njia mpya.”

John E. Barr, mshiriki wa muda mrefu wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya msingi ya programu. Kichwa chake cha kimaandiko kilikuwa “Mvumo Wao Ulitoka Ukaenda Kuingia Katika Dunia Yote.” (Waroma 10:18) Akauliza, Je, watu wa Mungu wameweza kutimiza hilo leo? Bila shaka, ndiyo! Tangu mwaka wa 1881, wasomaji wa gazeti Mnara wa Mlinzi waliulizwa hivi: “Je, unahubiri?” Kisha msemaji akawakumbusha wasikilizaji wote ule mwito wa kihistoria kwenye kusanyiko la mwaka wa 1922 huko Cedar Point, Ohio, Marekani: “Tangazeni Mfalme na Ufalme wake!” Kadiri ambavyo wakati umepita, bidii ya watumishi waaminifu wa Mungu imewachochea kutangaza kweli nzuri za Ufalme kwa mataifa yote. Kwa vichapo na kwa mahubiri, habari njema imewafikia watu duniani pote—ikimletea Yehova utukufu na sifa. Katika hotuba ya mwisho yenye kusisimua, Ndugu Barr aliwahimiza wanafunzi wanaohitimu wafikirie baraka walizo nazo, akisema: “Siku baada ya siku, unaposali kwa Yehova ukiwa katika mgawo wako, mshukuru kutoka moyoni kwa sehemu ambayo umeshiriki katika kutimiza maneno haya, ‘Mvumo wao ulitoka ukaenda kuingia katika dunia yote.’”

Baada ya hotuba hiyo, salamu zilisomwa, naye mwenyekiti akampa diploma kila mwanafunzi anayehitimu. Kisha, kukiwa na hisia zilizotofautiana, za furaha pamoja na huzuni kwa kuondoka katika shule hiyo waliyoipenda sana, ndugu mmoja akiliwakilisha darasa alisoma azimio la kutoka moyoni ambalo liliandikiwa Baraza Linaloongoza na familia ya Betheli, likionyesha kwamba wanafunzi wameazimia kumsifu Yehova “tangu sasa na hata milele.”—Zaburi 115:18.

Tunasali kwamba wanafunzi hao watauzoea mgawo wao mpya na kuchangia ukuzi wa kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri, kama tu vile ambavyo wale waliowatungulia wamefanya kwa miaka ipatayo 60.

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi zilizowakilishwa: 12

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 16

Idadi ya wanafunzi: 48

Wastani wa umri: 34.4

Wastani wa miaka katika kweli: 17.6

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 13.5

[Picha katika ukurasa wa 24]

Darasa la 114 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Rosa, D.; Garrigolas, J.; Lindström, R.; Pavanello, P.; Tait, N. (2) Van Hout, M.; Donabauer, C.; Martínez, L.; Millar, D.; Festré, Y.; Nutter, S. (3) Martínez, P.; Clarke, L.; Maughan, B.; Fischer, L.; Romo, G. (4) Romo, R.; Eadie, S.; Tuynman, C.; Campbell, P.; Millar, D.; Rosa, W. (5) Lindström, C.; Garrigolas, J.; Markevich, N.; Lindala, K.; van den Heuvel, J.; Tait, S.; Nutter, P. (6) Maughan, P.; Pavanello, V.; Eadie, N.; West, A.; Clarke, D.; Markevich, J. (7) Fischer, D.; Donabauer, R.; Curry, P.; Curry, Y.; Carfagno, W.; West, M.; Tuynman, A. (8) Van Hout, M.; Campbell, C.; Festré, Y.; Carfagno, C.; van den Heuvel, K.; Lindala, D.