Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uthibitisho wa Kwamba Yesu Kristo Aliishi Duniani

Uthibitisho wa Kwamba Yesu Kristo Aliishi Duniani

Uthibitisho wa Kwamba Yesu Kristo Aliishi Duniani

WATU wengi hawajaonana uso kwa uso na mwanasayansi mashuhuri anayeitwa Albert Einstein. Katika nchi nyingi, watu hata hawamjui. Hata hivyo habari zenye kuaminika kuhusu uvumbuzi wake na matokeo ya uvumbuzi huo yanathibitisha kwamba aliishi. Kwa mfano, wengi hunufaika kwa umeme ambao mara nyingine huzalishwa kwa kutumia uvumbuzi wake.

Kwa njia hiyohiyo tunaweza kuthibitisha kwamba Yesu Kristo, anayejulikana kuwa mtu mashuhuri zaidi, aliishi duniani. Mambo ambayo yameandikwa kumhusu na matokeo ya mafundisho yake yanathibitisha kabisa kwamba aliishi. Ijapokuwa maandishi kwenye lile sanduku linalotaja jina la Yakobo yanayofafanuliwa katika makala ya kwanza yanapendeza sana, hata hivyo, hatuwezi kutegemea maandishi hayo pekee wala kitu kingine cha kale ili kuthibitisha kwamba Yesu aliishi duniani. Lakini, yale ambayo wanahistoria waliandika kumhusu yeye na wanafunzi wake yanathibitisha kwamba Yesu aliishi.

Wanayosema Wanahistoria

Kwa mfano, fikiria anayosema Flavius Josephus, mwanahistoria Myahudi wa karne ya kwanza aliyekuwa Farisayo. Alimtaja Yesu Kristo katika kitabu Jewish Antiquities. Profesa Louis Feldman wa Chuo Kikuu cha Yeshiva anasema kwamba ijapokuwa watu fulani wanatilia shaka kwamba Josephus ndiye aliyeandika marejeo ya kwanza yanayomtaja Yesu kuwa Mesiya, hata hivyo, si wengi wanaotilia shaka marejeo ya pili kumhusu. Katika marejeo ya pili Josephus alisema hivi: “[Kuhani mkuu Ana] aliwaita mahakimu wa Sanhedrini kwenye mkutano na kumleta mwanamume aliyeitwa Yakobo mbele yao. Mwanamume huyo alikuwa ndugu ya Yesu, aliyeitwa Kristo.” (Jewish Antiquities, XX, 200) Ndiyo, Farisayo huyo aliyekuwa mfuasi wa madhehebu ambayo wafuasi wake walimchukia Yesu sana, alikiri kwamba “Yakobo, ndugu ya Yesu” aliishi.

Matokeo ya mafundisho ya Yesu yanaonekana wazi kupitia yale ambayo wafuasi wake walitenda na yanathibitisha kwamba aliishi. Mtume Paulo alipokuwa gerezani huko Roma yapata mwaka wa 59 W.K., wakuu wa Wayahudi walimwambia hivi: “Kwa habari ya farakano hili yajulikana kwetu kwamba kila mahali huwa lasemwa vibaya.” (Matendo 28:17-22) Waliwaita wafuasi wa Yesu “farakano hili.” Ikiwa walisemwa vibaya kila mahali, yaelekea wanahistoria wangewataja, sivyo?

Tacitus, aliyezaliwa yapata mwaka wa 55 W.K., ambaye anaonwa kuwa mmoja wa wanahistoria mashuhuri zaidi ulimwenguni, aliwataja Wakristo katika kitabu chake Annals. Tacitus aliandika hivi aliposimulia jinsi Nero alivyowalaumu Wakristo kwa kuanzisha moto mkubwa uliotokea Roma mwaka wa 64 W.K.: “Nero aliwashtaki na kuwatesa kikatili watu walioitwa Wakristo ambao walichukiwa sana kwa sababu ya tabia zao. Jina hilo lilitokana na jina la Kristo, ambaye Pontio Pilato alimhukumia kifo, wakati wa utawala wa Tiberio.” Mambo mbalimbali katika masimulizi hayo yanalingana na yale ambayo Biblia inasema kumhusu Yesu.

Pliny Mchanga, ambaye alikuwa mtawala wa Bithinia, ni mwandishi mwingine aliyewataja wafuasi wa Yesu. Pliny alimwandikia Maliki Trajan yapata mwaka wa 111 W.K. kwa sababu alitaka kujua jinsi ya kuwashughulikia Wakristo. Pliny aliandika kwamba watu walioshtakiwa kwa uwongo kuwa Wakristo, walitoa sala kwa miungu na kuiabudu sanamu ya Trajan, ili tu wathibitishe kwamba wao si Wakristo. Pliny aliongezea: “Haiwezekani kuwalazimisha Wakristo wa kweli kufuata desturi hizo.” Wafuasi wa Kristo hawakufuata desturi hizo, badala yake walikuwa tayari kufa kwa sababu walimwamini. Jambo hilo linathibitisha kwamba Yesu aliishi.

Baada ya kuzungumzia marejeo ya wanahistoria wa karne mbili za kwanza kumhusu Yesu Kristo na wafuasi wake, kitabu The Encyclopædia Britannica (chapa ya 2002) kinasema hivi: “Masimulizi hayo mbalimbali yanathibitisha kwamba zamani za kale hata wapinzani wa Ukristo hawakutilia shaka kwamba Yesu alikuwa ameishi. Watu walianza kubishania jambo hilo kwa mara ya kwanza bila sababu nzuri mwishoni mwa karne ya 18, katika karne ya 19, na mwanzoni mwa karne ya 20.”

Wanayosema Wafuasi wa Yesu

Kitabu The Encyclopedia Americana kinasema: “Katika Agano Jipya kuna karibu uthibitisho wote unaohitajika ili tuelewe maisha na kifo cha Yesu na maoni ya Wakristo wa kwanza kuhusu umuhimu wake.” Huenda watu wenye kutilia shaka wasikubali Biblia kuwa uthibitisho wa kwamba Yesu aliishi. Maandiko yanaweza kutusaidia kwa njia mbili kuthibitisha kwamba Yesu aliishi duniani.

Kama tulivyoona, nadharia muhimu sana za Einstein zinathibitisha kwamba yeye aliishi. Vivyo hivyo, mafundisho ya Yesu yanathibitisha kwamba yeye aliishi. Fikiria kwa mfano, Mahubiri ya Mlimani yanayojulikana sana, ambayo Yesu alitoa. (Mathayo, sura ya 5-7) Mtume Mathayo aliandika hivi kuhusu matokeo ya mahubiri hayo: “Umati ulishangaa juu ya njia yake ya kufundisha; kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka.” (Mathayo 7:28, 29) Profesa Hans Dieter Betz alisema hivi kuhusu matokeo ya mahubiri hayo juu ya watu kwa karne nyingi: “Si Wayahudi na Wakristo tu wanaovutiwa na Mahubiri ya Mlimani, wala watu katika nchi za Magharibi.” Aliongeza kwamba mahubiri hayo “huwavutia watu ulimwenguni pote.”

Fikiria semi fupi za hekima zifuatazo zinazotusaidia maishani, ambazo zinapatikana katika Mahubiri ya Mlimani: “Yeyote akupigaye kofi kwenye shavu lako la kuume, mgeuzie lile jingine pia.” “Angalieni vizuri kwamba msidhihirishe uadilifu wenu mbele ya watu.” “Msihangaike kamwe juu ya siku ifuatayo, kwa maana siku ifuatayo itakuwa na mahangaiko yayo yenyewe.” “Msitupe lulu . . . mbele ya nguruwe.” “Fulizeni kuomba, nanyi mtapewa.” “Mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.” “Ingieni kupitia lango jembamba.” “Kwa matunda yao mtawatambua.” “Kila mti mwema hutokeza matunda bora.”—Mathayo 5:39; 6:1, 34; 7:6, 7, 12, 13, 16, 17.

Bila shaka umesikia baadhi ya semi hizo au huenda unajua kiini cha semi hizo. Huenda semi hizo hutumiwa kama methali katika lugha yako. Semi hizo zote zinatokana na Mahubiri ya Mlimani. Mahubiri hayo yamekuwa na matokeo katika tamaduni nyingi na juu ya watu wengi, na hiyo inaonyesha wazi kwamba yule “mwalimu mkuu” aliishi duniani.

Tuseme kwamba mtu fulani alibuni hadithi ya mtu anayeitwa Yesu Kristo, na kwamba mtu huyo alikuwa na akili ya kutosha kutunga mambo ambayo Biblia inasema Yesu aliyafundisha. Bila shaka mtu huyo angejitahidi kubuni hadithi ya Yesu na mafundisho yake kwa njia ya kuvutia sana. Hata hivyo, mtume Paulo alisema hivi: “Wayahudi waomba ishara nyingi na pia Wagiriki watafuta hekima; lakini sisi twahubiri Kristo aliyetundikwa mtini, kwa Wayahudi ni sababu ya kukwaza lakini kwa mataifa upumbavu.” (1 Wakorintho 1:22, 23) Ujumbe kumhusu Kristo aliyetundikwa mtini haukuwavutia Wayahudi wala watu wa mataifa. Hata hivyo, huyo ndiye Kristo aliyehubiriwa na Wakristo katika karne ya kwanza. Kwa nini walihubiri Kristo aliyetundikwa mtini? Hakuna sababu nyingine inayoridhisha isipokuwa kwamba waandishi wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo walisema kweli kuhusu maisha na kifo cha Yesu.

Uthibitisho mwingine unaoonyesha kwamba Yesu aliishi ni kwamba wafuasi wake walihubiri bila kuchoka kuhusu yale aliyofundisha. Miaka 30 hivi baada ya Yesu kuanza huduma yake Paulo aliweza kusema kwamba habari njema ‘ilikuwa imehubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.’ (Wakolosai 1:23) Ndiyo, mafundisho ya Yesu yalienea kotekote katika ulimwengu wa kale licha ya upinzani. Paulo ambaye aliteswa kwa sababu alikuwa Mkristo aliandika hivi: “Ikiwa Kristo hajafufuliwa, kuhubiri kwetu ni bure hakika, na imani yetu ni bure.” (1 Wakorintho 15:12-17) Ikiwa kuhubiri juu ya Kristo ambaye hakuwa amefufuliwa kungekuwa bure, basi kuhubiri juu ya Kristo ambaye hakuwahi kuishi kungekuwa bure hata zaidi. Kama tulivyosoma katika maandishi ya Pliny Mchanga, Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa tayari kufa kwa sababu ya imani yao katika Kristo Yesu. Walihatarisha maisha yao kwa ajili ya Kristo kwa sababu walikuwa na hakika kwamba alikuwa ameishi duniani, na alikuwa ameishi jinsi masimulizi ya Injili yanavyosema.

Umeona Uthibitisho

Iliwabidi Wakristo kuwa na imani katika ufufuo wa Yesu Kristo ili waweze kuhubiri. Hata wewe unaweza kuona akilini mwako Yesu aliyefufuliwa kwa kujionea matokeo ya mafundisho yake leo.

Kabla tu ya kutundikwa mtini, Yesu alitoa unabii unaohusisha mambo mengi juu ya kuwapo kwake wakati ujao. Pia alionyesha kwamba angefufuliwa na kuketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu akingoja kuanza kuwaondoa adui zake. (Zaburi 110:1; Yohana 6:62; Matendo 2:34, 35; Waroma 8:34) Baadaye, Yesu angechukua hatua dhidi ya Shetani na kumtupa yeye na roho wake waovu kutoka mbinguni.—Ufunuo 12:7-9.

Hayo yote yangetokea wakati gani? Yesu aliwapa wanafunzi wake ‘ishara ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo wa mambo.’ Ishara ambayo ingetambulisha kuwapo kwake kusikoonekana ilitia ndani vita kuu, upungufu wa chakula, matetemeko ya ardhi, kutokea kwa manabii wa uwongo, ongezeko la uvunjaji wa sheria, na magonjwa hatari yanayoambukizwa. Misiba hiyo ingetazamiwa, kwa kuwa kutupwa kwa Shetani Ibilisi duniani kungeleta “ole wa dunia.” Ibilisi amekuja kwenye ujirani wa dunia “akiwa na hasira kubwa, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.” Zaidi ya hayo, ishara hiyo inatia ndani kuhubiriwa kwa habari njema ya Ufalme katika “dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.”—Mathayo 24:3-14; Ufunuo 12:12; Luka 21:7-19.

Mambo mengi ambayo Yesu alitabiri yametimia sasa. Tangu Vita ya Kwanza ya Ulimwengu izuke mwaka wa 1914, tumeona ishara yenye mambo mengi yanayothibitisha kuwapo kusikoonekana kwa Yesu Kristo. Yeye anatawala akiwa Mfalme katika Ufalme wa Mungu na tunayaona matokeo makubwa ya utawala wake leo. Wewe unaweza kusoma gazeti hili kwa sababu ya kazi ya kuhubiri Ufalme huo inayoendelea leo.

Ili kuelewa vizuri zaidi matokeo ya mafundisho ya Yesu unahitaji kujifunza Biblia. Mbona usiwaulize Mashahidi wa Yehova upate habari zaidi kuhusu kuwapo kwa Yesu.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Josephus, Tacitus, na Pliny Mchanga walimtaja Yesu Kristo na wafuasi wake

[Hisani]

All three images: © Bettmann/CORBIS

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wakristo wa kwanza walikuwa na hakika kwamba Yesu alikuwa ameishi duniani