Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kilijaza Pengo Fulani Moyoni Mwangu”

“Kilijaza Pengo Fulani Moyoni Mwangu”

“Kilijaza Pengo Fulani Moyoni Mwangu”

“NAWASHUKURU kutoka moyoni kwa zawadi nzuri, Mkaribie Yehova. Kilijaza pengo fulani moyoni mwangu, yaani uhitaji wa kupendwa na kuthaminiwa na Yehova. Sasa ninahisi nikiwa karibu zaidi na Yehova na Mwana wake mpendwa. Ninataka kueleza kila mtu kuhusu kitabu hiki na kumpa kila mmoja wa wapendwa wangu nakala moja.” Hivyo ndivyo mmoja wa Mashahidi wa Yehova alivyohisi kuhusu kitabu kipya chenye kurasa 320 kilichotolewa kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii” lililofanywa mwaka wa 2002/2003. Hebu tuchunguze mambo fulani yaliyo katika kitabu hiki kipya na tuone ni kwa nini kilichapishwa.

Mambo Yaliyo Katika Kitabu Hiki Kipya

Kitabu hiki kipya kinazungumzia nini? Kina habari yote ambayo tumezungumzia katika makala mbili za funzo katika toleo hili na habari nyingine nyingi! Kitabu hiki kina sura 31, kila sura ina urefu kama wa makala ya funzo la Mnara wa Mlinzi. Baada ya utangulizi na sura tatu za kwanza, kitabu hiki kimegawanywa katika sehemu nne, kila sehemu inazungumzia sifa moja kuu ya Yehova. Kila sehemu inaanza kwa kutoa muhtasari kuhusu sifa inayozungumziwa. Sura kadhaa zinazofuata zinazungumzia jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hiyo kwa njia mbalimbali. Kila sehemu pia ina sura inayoonyesha jinsi Yesu alivyoonyesha sifa hiyo. Kwa nini? Kwa sababu Yesu alisema: “Yeye ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:9) Yesu anatuonyesha waziwazi sifa za Mungu kwa matendo kwa sababu alimwiga kikamilifu. Sura ya mwisho katika kila sehemu inatufundisha jinsi tunavyoweza kumwiga Yehova katika kuonyesha sifa inayozungumziwa. Kitabu hiki kipya kinataja maandiko kutoka katika vitabu vyote vya Biblia kinapozungumzia sifa za Yehova.

Kitabu Mkaribie Yehova kina mambo mengine ya pekee. Kuanzia sura ya 2 na kuendelea, kila sura ina sanduku lenye kichwa “Maswali ya Kutafakari.” Maandiko na maswali yaliyoonyeshwa hayakusudiwi kurudia sura iliyozungumziwa. Badala yake, yanakusudiwa kukusaidia utafakari habari hiyo kwa undani zaidi ukitumia Biblia. Inapendekezwa kwamba usome kila Andiko kwa makini sana. Kisha utafakari swali, na ujitahidi kuona jinsi unavyoweza kutumia habari hiyo maishani mwako. Kutafakari huko kunaweza kuchochea moyo wako na kukusaidia umkaribie Yehova zaidi.—Zaburi 19:14.

Picha zilizo katika kitabu Mkaribie Yehova zimefanyiwa utafiti na kutayarishwa kwa uangalifu ili kufundisha na kuchochea. Katika sura 17 za kitabu hicho kuna kurasa nzima zenye picha maridadi kuhusu masimulizi ya Biblia.

Kwa Nini Kilichapishwa?

Kwa nini kitabu Mkaribie Yehova kilichapishwa? Kitabu hiki kipya kinakusudiwa hasa kutusaidia kumjua Yehova vizuri zaidi ili tuweze kuimarisha zaidi uhusiano wetu pamoja na Mungu wetu.

Je, unajua yeyote anayeweza kufaidika na kitabu Mkaribie Yehova, labda mwanafunzi wa Biblia au hata ndugu au dada Mkristo asiyetenda? Namna gani wewe—je, umeanza kukisoma kitabu hiki kipya? Ikiwa hujaanza kwa nini usipange wakati wa kukisoma haraka iwezekanavyo? Tafakari mambo unayoyasoma. Kitabu hiki kipya na kikusaidie kumkaribia zaidi Yehova Mungu, ili uweze kutangaza habari njema za Ufalme wake kwa bidii zaidi na kwa shangwe nyingi zaidi!