Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu wa Kawaida Waitafsiri Biblia

Watu wa Kawaida Waitafsiri Biblia

Watu wa Kawaida Waitafsiri Biblia

KATIKA mwaka wa 1835, Henry Nott, mjenzi Mwingereza, na John Davies kutoka Wales aliyekuwa akijifunza kazi ya kuuza kwenye duka la bidhaa ndogo-ndogo, walimaliza mradi mkubwa sana. Walimaliza kutafsiri Biblia katika Kitahiti baada ya kujitahidi kwa zaidi ya miaka 30. Watu hao wa kawaida walipata magumu na matokeo gani katika kazi hiyo ya kujitolea?

“Ule Mwamko Mkuu”

Katikati ya karne ya 18, washiriki wa kikundi cha Waprotestanti kilichoitwa Mwamko Mkuu au tu Mwamko, walihubiri vijijini, karibu na migodi, na viwandani huko Uingereza. Lengo lao lilikuwa kuwafikia watu walioajiriwa. Wahubiri hao waliunga mkono kusambazwa kwa Biblia.

Mwanzilishi wa kikundi hicho, Mbaptisti aliyeitwa William Carey, alisaidia kuanzishwa kwa Sosaiti ya Mishonari ya London (LMS) mwaka wa 1795. Sosaiti hiyo iliwazoeza watu waliokuwa tayari kujifunza lugha ya wenyeji na kutumikia wakiwa mishonari katika eneo la Pasifiki ya Kusini. Lengo la mishonari hao lilikuwa kuhubiri Injili katika lugha ya wenyeji.

Eneo la kwanza la mishonari hao wa LMS lilikuwa kisiwa cha Tahiti ambacho kilikuwa kimevumbuliwa karibuni. Kulingana na washiriki wa kikundi hicho, visiwa hivyo vilikuwa ‘maeneo ya giza’ ya wapagani yaliyokuwa tayari kuvunwa.

Watu wa Kawaida Wafanikiwa Katika Kazi Ngumu

Mishonari 30 hivi wasio na ujuzi walichaguliwa upesi wasafiri kwa meli ya Duff iliyonunuliwa na LMS ili kuwahubiria watu wa Tahiti. Kulingana na ripoti moja, watu hao walitia ndani “makasisi wanne waliokuwa wamewekwa rasmi [ambao hawakuwa na mazoezi maalumu], maseremala sita, mafundi wa viatu wawili, wajenzi wawili, wafumaji wawili, mafundi wa nguo wawili, mwenye duka, mtengeneza-matandiko ya farasi, mfanyakazi wa nyumbani, mtunza-bustani, daktari, mfua-chuma, mtengeneza-mapipa, mtengeneza-pamba, mchuuzi wa kofia za wanawake, mtengeneza-nguo, fundi wa kabati, wenzi wa ndoa watano, na watoto watatu.”

Vifaa ambavyo mishonari hao walikuwa navyo ili kujifunza lugha za zamani za Biblia ni kamusi ya Kigiriki na Kiingereza na Biblia yenye kamusi ya Kiebrania. Kwa muda wa miezi saba baharini, mishonari hao walikariri maneno fulani ya Kitahiti, yaliyoandikwa na watu waliokuwa wametembea huko kabla yao, hasa waasi wa meli ya Bounty. Mwishowe meli ya Duff ilifika Tahiti, na katika Machi 7, 1797, mishonari wakafika kwenye nchi kavu. Hata hivyo, mwaka mmoja baadaye wengi walikuwa wamevunjika moyo na kurudi. Mishonari saba tu ndio waliobaki.

Kati ya hao saba alikuwa Henry Nott mwenye umri wa miaka 23 tu, ambaye hapo awali alikuwa mjenzi. Barua za kwanza alizoandika, zinathibitisha kwamba alikuwa na elimu ya msingi tu. Hata hivyo, tangu mwanzo alikuwa na kipawa cha kujifunza Kitahiti. Alitajwa kuwa mtu mnyofu, mtulivu, na wa kupendeza.

Katika mwaka wa 1801, Nott alichaguliwa kuwafundisha Kitahiti mishonari tisa wapya waliokuwa wamewasili. Kati yao alikuwa John Davies kutoka Wales mwenye umri wa miaka 28, aliyekuwa mwanafunzi stadi na mfanyakazi mwenye bidii. Alikuwa pia mwenye fadhili na mkarimu. Muda mfupi baadaye, wanaume hao wawili waliamua kutafsiri Biblia katika Kitahiti.

Kazi Ngumu

Hata hivyo, ilikuwa kazi ngumu kutafsiri katika Kitahiti kwa sababu lugha hiyo haikuwa na mfumo wa maandishi. Mishonari walilazimika kujifunza kwa kusikiliza. Hawakuwa na kamusi wala kitabu cha sarufi. Mishonari hao walivunjika moyo kwa sababu lugha hiyo ilikuwa na konsonanti chache, vokali nyingi zinazofuatana (kama tano hivi kwa neno moja), na sauti nzito za kukoroma. Walilalamika kwamba, “maneno mengi yana vokali tu na kila vokali ina sauti yake.” Walikiri kwamba hawakuweza “kuelewa sauti za maneno kama zilivyo hasa.” Hata walifikiri kwamba walisikia sauti zisizojulikana!

Jambo la kusikitisha hata zaidi ni kwamba wakati mwingine maneno fulani yalipigwa marufuku au ilikuwa mwiko kuyatamka katika Kitahiti na hivyo yalibadilishwa. Maneno yenye maana sawa yaliwatatiza pia. Kulikuwa na maneno ya Kitahiti zaidi ya 70 yaliyomaanisha “sala.” Kizuizi kingine kilikuwa kwamba mpangilio wa maneno ya Kitahiti ulikuwa tofauti kabisa na ya Kiingereza. Ijapokuwa magumu hayo, hatua kwa hatua mishonari hao walikusanya orodha ya maneno ambayo miaka 50 baadaye, Davies aliyachapisha na kuyafanyiza kamusi yenye maneno 10,000.

Kisha kukawa na tatizo la kuandika Kitahiti. Mishonari walijaribu kukiandika wakitumia mpangilio wa herufi za Kiingereza. Hata hivyo, matumizi ya alfabeti za Kilatini katika Kiingereza hayakupatana na sauti za Kitahiti. Kwa hiyo, kila mara mishonari walizungumza kuhusu matamshi na mwendelezo wa maneno. Mara nyingi mishonari walianzisha matamshi mapya kwa kuwa wao ndio waliokuwa wa kwanza katika Bahari ya Kusini kuiweka lugha hiyo katika maandishi. Hawakujua kwamba baadaye kazi yao ingetumiwa kama kielelezo cha maandishi ya lugha nyingi za Pasifiki ya Kusini.

Vifaa Vichache Lakini Maarifa Mengi

Watafsiri hao walikuwa na vitabu vichache tu vya marejeo. LMS ilipendekeza kwamba watumie kitabu cha Kilatini Textus Receptus (Maandiko Yaliyopokewa) na tafsiri ya King James Version kama maandishi ya msingi. Nott aliomba LMS wamtumie kamusi na Biblia zaidi katika lugha ya Kiebrania na Kigiriki. Haijulikani kama aliwahi kupokea vitabu hivyo. Davies alipokea vitabu vya kitaalamu kutoka kwa marafiki wake huko Wales. Mambo yaliyoandikwa yanaonyesha kwamba alikuwa na angalau kamusi ya Kigiriki, Biblia ya Kiebrania, Agano Jipya katika Kigiriki, na tafsiri ya Septuagint.

Wakati huo, kazi ya kuhubiri ya mishonari hao ilikuwa bila matokeo. Ingawa mishonari hao walikuwa wameishi Tahiti kwa miaka 12, hakuna hata mtu mmoja aliyebatizwa. Hatimaye kwa sababu ya vita visivyokoma vya wenyewe kwa wenyewe, mishonari wote ila tu Nott walilazimika kukimbilia Australia. Kwa muda, ni yeye tu aliyekuwa amebaki katika Visiwa vya Windward vya kikundi cha Visiwa vya Society, lakini alilazimika kumfuata Mfalme Pomare wa Pili wakati mfalme huyo alipokimbilia kisiwa cha karibu cha Moorea.

Hata hivyo, kuhama kwa Nott hakukukomesha kazi ya kutafsiri, na baada ya Davies kuishi Australia kwa miaka miwili, alijiunga naye tena. Wakati huo, Nott alikuwa amejifunza na kukijua vizuri sana Kigiriki na Kiebrania. Hivyo akaanza kutafsiri sehemu fulani za Maandiko ya Kiebrania katika Kitahiti. Alichagua mafungu ya maneno ya Biblia yenye habari ambayo wenyeji wangeelewa kwa urahisi.

Akishirikiana na Davies, Nott alianza kutafsiri Injili ya Luka iliyokamilika Septemba 1814. Aliandika maandishi ya Kitahiti cha kawaida, naye Davies akayakagua kwa kuyalinganisha na maandishi ya zamani. Katika mwaka wa 1817, Mfalme Pomare wa Pili aliomba achapishe ukurasa wa kwanza wa Injili ya Luka. Aliuchapisha akitumia mashine ndogo ya kupigia chapa iliyoendeshwa kwa mkono ambayo ilikuwa imepelekwa Moorea na mishonari fulani. Habari kuhusu kutafsiriwa kwa Biblia katika Kitahiti inapotajwa, Tuahine aliyekuwa Mtahiti mwaminifu anakumbukwa kwa kuwa aliishi na mishonari hao kwa miaka yote hiyo na kuwasaidia kuelewa tofauti ndogo-ndogo za maneno ya Kitahiti.

Kazi ya Kutafsiri Yakamilika

Kutafsiriwa kwa vitabu vya Injili, Matendo ya Mitume na Zaburi kulikamilika mwaka wa 1819 baada ya miaka sita ya kazi ngumu. Mishonari wapya walipofika walileta mashine ya kupigia chapa iliyorahisisha kazi ya uchapaji na ugawaji wa vitabu hivyo vya Biblia.

Kipindi cha kazi nyingi ya kutafsiri, kutoa makosa, na kurekebisha kilifuata. Baada ya kuishi Tahiti kwa miaka 28 Nott alishikwa na ugonjwa mwaka 1825 na LMS ikamruhusu arudi Uingereza. Inapendeza kwamba kufikia wakati huo kutafsiriwa kwa Maandiko ya Kigiriki kulikuwa kunakaribia kukamilika. Aliendelea kutafsiri vitabu vingine vya Biblia akiwa safarini kuelekea Uingereza na wakati alipokuwa huko. Katika mwaka wa 1827 Nott alirudi Tahiti. Miaka minane baadaye, mnamo Desemba 1835, Nott alikamilisha kutafsiri Biblia nzima. Kazi hiyo ngumu ilichukua zaidi ya miaka 30.

Mnamo 1836, Nott alirudi tena Uingereza ili kuchapisha Biblia nzima ya Kitahiti huko London. Mnamo Juni 8, 1838 Nott alifurahi kumpa Malkia Viktoria tafsiri ya kwanza ya Biblia iliyochapishwa katika Kitahiti. Ni kweli kwamba huo ulikuwa wakati wenye kusisimua sana kwa mjenzi huyo ambaye miaka 40 iliyopita alisafiri kwa meli ya Duff na kujifunza tamaduni za watu wa Tahiti ili kumaliza kazi hiyo kubwa iliyochukua muda mrefu.

Miezi miwili baadaye, Nott alirudi Pasifiki ya Kusini akiwa na masanduku 27 yenye nakala 3,000 za Biblia nzima katika Kitahiti. Baada ya kufika Sydney alikuwa mgonjwa tena, lakini hakuyaacha masanduku hayo yenye thamani. Baada ya kupata nafuu, aliwasili Tahiti mnamo mwaka wa 1840, ambapo umati uling’ang’ania nakala za Biblia za Kitahiti. Nott alikufa huko Tahiti mnamo Mei 1844 akiwa mwenye umri wa miaka 70.

Msaada Mkubwa Sana

Hata hivyo, kazi ya Nott iliendelea. Tafsiri yake iliwasaidia sana Wapolinesia. Kwa kuandika Kitahiti, mishonari hao walihifadhi lugha hiyo. Mwandishi mmoja alisema: “Nott aliandika sarufi yenye kueleweka ya Kitahiti. Ili kujifunza Kitahiti asili ni lazima kuisoma Biblia.” Kazi ya watafsiri hao wenye bidii ilisaidia kuhifadhi maneno mengi ambayo yangesahauliwa kabisa. Karne moja baadaye, mwandishi mmoja alisema: “Tafsiri ya Biblia ya Kitahiti ya Nott ni kazi yenye ustadi wa pekee na kila mtu anakubaliana na hilo.”

Kazi hiyo muhimu iliwafaidi Watahiti na pia ikaweka msingi wa kazi ya utafsiri katika lugha nyingine za Pasifiki ya Kusini. Kwa mfano, watafsiri katika Visiwa vya Cook na Samoa waliitumia kama kielelezo. Mtafsiri mmoja alikiri hivi: “Nimechunguza kwa makini tafsiri ya Bw. Nott, nami kwa hakika ninafuata kielelezo chake.” Ilisemekana kwamba mtafsiri mwingine ‘alikuwa na kitabu cha Zaburi katika Kiebrania na tafsiri za Kiingereza na Kitahiti’ alipokuwa ‘akitafsiri mojawapo ya zaburi za Daudi katika lugha ya Kisamoa.’

Mishonari huko Tahiti walifuata kielelezo cha kile kikundi cha Mwamko cha Uingereza na hivyo walifurahia kuwafundisha watu kusoma na kuandika. Kwa kweli, Biblia peke yake ndiyo iliyokuwa kitabu cha watu wa Tahiti kwa zaidi ya karne moja. Hivyo ikawa muhimu katika utamaduni wa Kitahiti.

Jina la Mungu linapatikana mara nyingi sana katika Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki, jambo linalochangia ubora wa tafsiri ya Nott Version. Matokeo yamekuwa kwamba jina la Yehova limejulikana sana huko Tahiti na visiwa vyake. Hata linapatikana kwenye makanisa fulani ya Waprotestanti. Hata hivyo, jina la Mungu linahusianishwa na Mashahidi wa Yehova ambao wanahubiri kwa bidii wakitumia Biblia ya Kitahiti iliyotafsiriwa na Nott na wenzake. Jitihada hizo za watafsiri kama vile Henry Nott, zinatukumbusha jinsi tunavyopaswa kushukuru kwamba leo watu wengi wana Neno la Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Tafsiri ya kwanza katika Kitahiti ya mwaka wa 1815. Ina jina la Yehova

Henry Nott (1774-1844), mtafsiri mkuu wa Biblia ya Kitahiti

[Hisani]

Tahitian Bible: Copyright the British Library (3070.a.32); Henry Nott and letter: Collection du Musée de Tahiti et de ses Îles, Punaauia, Tahiti; catechism: With permission of the London Missionary Society Papers, Alexander Turnbull Library, Wellington, New Zealand

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kitabu cha katekisimu cha lugha ya Kitahiti na ya Welsh cha 1801, ambacho kina jina la Mungu

[Hisani]

With permission of the London Missionary Society Papers, Alexander Turnbull Library, Wellington, New Zealand

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kanisa la Kiprotestanti lenye jina Yehova upande wa mbele, kisiwa cha Huahine, Polinesia ya Ufaransa

[Hisani]

Avec la permission du Pasteur Teoroi Firipa