Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunapaswa Kuwaonaje Watu Siku ya Yehova Inapokaribia?

Tunapaswa Kuwaonaje Watu Siku ya Yehova Inapokaribia?

Tunapaswa Kuwaonaje Watu Siku ya Yehova Inapokaribia?

“Yehova si wa polepole kwa habari ya ahadi yake, . . . bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”—2 PETRO 3:9.

1, 2. (a) Yehova anawaonaje watu leo? (b) Tunaweza kujiuliza maswali gani?

WATUMISHI wa Yehova wana kazi ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mathayo 28:19) Tunapofanya kazi hiyo na kungojea “siku ya BWANA iliyo kuu,” tunapaswa kuwaona watu jinsi anavyowaona. (Sefania 1:14) Yehova huwaonaje watu? Mtume Petro anasema: “Yehova si wa polepole kwa habari ya ahadi yake, kama watu fulani waonavyo kuwa ni upolepole, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Mungu huona kwamba kila mtu anaweza kutubu. “Mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4) Yehova hufurahi wakati mtu ‘anapoghairi na kuiacha njia yake mbaya, akaishi.’—Ezekieli 33:11.

2 Je, sisi tuna maoni kama ya Yehova kuelekea watu? Kama yeye, je, tunaona kwamba watu wa kila jamii na taifa wanaweza kuwa “kondoo wa malisho yake”? (Zaburi 100:3; Matendo 10:34, 35) Acheni tuchunguze mifano miwili ambayo huonyesha umuhimu wa kuwa na maoni kama ya Mungu. Katika mifano hiyo, uharibifu ulikuwa unakaribia nao watumishi wa Yehova walijulishwa mapema kuhusu jambo hilo. Mifano hiyo ni ya maana hasa tunapongojea siku kuu ya Yehova.

Abrahamu Alikuwa na Maoni ya Yehova

3. Yehova aliwaonaje wakaaji wa Sodoma na Gomora?

3 Mfano wa kwanza unahusu mzee wa ukoo Abrahamu, aliyekuwa mwaminifu, na miji yenye uovu ya Sodoma na Gomora. Yehova aliposikia “malalamiko mengi dhidi ya watu wa Sodoma na Gomora,” hakuharibu miji hiyo na wakaaji wake mara moja. Kwanza alifanya uchunguzi. (Mwanzo 18:20, 21, Biblia Habari Njema) Malaika wawili walitumwa Sodoma, ambako waliishi katika nyumba ya Loti, mwanamume mwenye haki. Usiku ambao malaika hao walifika, ‘watu wa mji waliizunguka nyumba, vijana kwa wazee, watu wote waliotoka pande zote,’ wakitaka kufanya ngono za wanaume kwa wanaume pamoja na malaika hao. Ni wazi kwamba, hali iliyopotoka ya wakaaji wa miji hiyo ilionyesha kwamba ilistahili kuharibiwa. Hata hivyo, malaika hao walimwambia Loti hivi: “Je! unaye mtu hapa zaidi? Mkwe, wanao, na binti zako, na wo wote ulio nao katika mji, uwatoe katika mahali hapa.” Yehova alifungua njia ili awaokoe baadhi ya wakaaji wa mji huo, lakini mwishowe, Loti tu na binti zake wawili ndio waliokoka uharibifu.—Mwanzo 19:4, 5, 12, 16, 23-26.

4, 5. Kwa nini Abrahamu aliwaombea wakaaji wa Sodoma, na je, maoni yake kuhusu watu yalikuwa sawa na ya Yehova?

4 Sasa, na turudi nyuma hadi wakati ambapo Yehova alifunua kusudi lake la kuichunguza miji ya Sodoma na Gomora. Wakati huo Abrahamu aliomba hivi: “Huenda wakawapo wenye haki hamsini katika mji, utaharibu, wala hutauacha mji kwa ajili ya hao hamsini wenye haki waliomo? Hasha usifanye hivyo, ukamwue mwenye haki pamoja na mwovu, mwenye haki awe kama mwovu. Hasha; Mhukumu ulimwengu wote asitende haki?” Abrahamu alitumia neno “hasha” mara mbili. Kutokana na mambo aliyojionea, Abrahamu alijua kwamba Yehova hawezi kuharibu wenye haki pamoja na waovu. Yehova aliposema kwamba hangeharibu Sodoma kama kungekuwa na watu “wenye haki hamsini katika mji,” Abrahamu alipunguza hesabu hiyo hatua kwa hatua hadi ikafika watu kumi tu.—Mwanzo 18:22-33.

5 Je, Yehova angesikiliza maombi ya Abrahamu kama yangekuwa kinyume cha maoni yake? La, hangemsikiliza. Akiwa “rafiki ya Yehova,” yaonekana Abrahamu alijua na alikubaliana na maoni Yake. (Yakobo 2:23) Wakati Yehova alipoelekeza fikira zake juu ya Sodoma na Gomora, alikuwa tayari kusikiliza maombi ya Abrahamu. Kwa nini? Kwa sababu Baba yetu wa mbinguni “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”

Yona Aliwaona Watu kwa Njia Tofauti Kabisa

6. Watu wa Ninawi waliitikiaje tangazo la Yona?

6 Sasa fikiria mfano wa pili unaohusu Yona. Katika mfano huo, mji ambao ulikuwa uharibiwe ni Ninawi. Nabii Yona aliambiwa atangaze kwamba uovu wa mji huo ‘ulikuwa umepanda juu mbele za Yehova.’ (Yona 1:2) Ninawi, kutia ndani vitongoji vyake, ulikuwa mji mkubwa, na ingechukua “mwendo wa siku tatu” kutembea eneo lote. Mwishowe, Yona alipotii na kuingia katika mji wa Ninawi, aliendelea kutangaza hivi: “Baada ya siku arobaini Ninawi utaangamizwa.” Ndipo “watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia.” Hata mfalme wa Ninawi alitubu.—Yona 3:1-6.

7. Yehova alionaje mtazamo wa kutubu wa Waninawi?

7 Itikio la watu wa Ninawi lilikuwa tofauti sana na la watu wa Sodoma! Yehova aliwaonaje Waninawi waliotubu? Andiko la Yona 3:10 linasema: “Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda; asilitende.” Yehova ‘alighairi’ katika maana ya kwamba alibadili uamuzi wake wa kuwaangamiza Waninawi kwa kuwa walibadili mwenendo wao. Viwango vya Mungu havikubadilika, lakini Yehova alibadili uamuzi wake alipoona kwamba Waninawi wametubu.—Malaki 3:6.

8. Kwa nini Yona alichukizwa?

8 Yona alipotambua kwamba Ninawi halitaharibiwa, je, aliona mambo jinsi Yehova alivyoyaona? Hapana, kwa sababu tunaambiwa: “Lakini jambo hili lilimchukiza Yona sana, naye akakasirika.” Yona alifanya jambo gani lingine? Masimulizi hayo yanasema: ‘Alimwomba BWANA, akasema, Nakuomba, Ee BWANA; sivyo hivyo nilivyosema, hapo nilipokuwa katika nchi yangu? Hii ndiyo sababu nalifanya haraka kukimbilia Tarshishi; kwa maana nalijua ya kuwa wewe u Mungu mwenye neema, umejaa huruma, si mwepesi wa hasira, u mwingi wa rehema, nawe waghairi mabaya.’ (Yona 4:1, 2) Yona alijua sifa za Yehova. Hata hivyo, wakati huo nabii huyo alichukizwa naye hakuwaona wakaaji wa Ninawi waliotubu kama Mungu alivyowaona.

9, 10. (a) Yehova alimfunza Yona somo gani? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba mwishowe Yona alikuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu Waninawi?

9 Yona alienda nje ya mji wa Ninawi, akatengeneza kibanda na kuketi kwenye kivuli chake “hata aone mji ule utakuwaje.” Yehova alifanya mtango ukue ili uandae kivuli kwa ajili ya Yona. Lakini mtango huo ukanyauka siku iliyofuata. Yona alipokasirika kuhusu jambo hilo, Yehova alisema: “Wewe umeuhurumia mtango, . . . na mimi, je! Haikunipasa kuuhurumia Ninawi, mji ule mkubwa; ambao ndani yake wamo watu zaidi ya mia na ishirini elfu, wasioweza kupambanua katika mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto; tena wamo wanyama wa kufugwa wengi sana?” (Yona 4:5-11) Yona alijifunza somo lililoje kuhusu jinsi Yehova anavyowaona watu!

10 Biblia haionyeshi jinsi Yona alivyoitikia wakati Mungu aliposema kwamba anawahurumia watu wa Ninawi. Lakini, ni wazi kwamba nabii huyo alibadili maoni yake kuhusu Waninawi waliotubu. Tunasema hivyo kwa sababu Yehova alimtumia kuandika masimulizi hayo.

Wewe Una Mtazamo Gani?

11. Yaelekea Abrahamu angewaonaje watu wanaoishi leo?

11 Leo, tunakaribia uharibifu mwingine wa mfumo huu mwovu wa mambo katika siku kuu ya Yehova. (Luka 17:26-30; Wagalatia 1:4; 2 Petro 3:10) Abrahamu angewaonaje watu wanaoishi katika ulimwengu huu ambao utaharibiwa karibuni? Yaelekea sana kwamba angewahangaikia watu ambao bado hawajasikia “habari njema hii ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Abrahamu alimsihi Mungu tena na tena kuhusu watu fulani wa Sodoma ambao huenda walikuwa wenye haki. Je, sisi tunawahangaikia watu ambao wanaweza kuacha mienendo ya ulimwengu huu unaoongozwa na Shetani kama wangepewa nafasi ya kutubu na kumtumikia Mungu?—1 Yohana 5:19; Ufunuo 18:2-4.

12. Kwa nini ni jambo rahisi kukuza mtazamo kama wa Yona kuelekea watu tunaowakuta katika huduma, na tunaweza kufanya nini kuhusu hilo?

12 Ni jambo linalofaa kutamani uovu uishe. (Habakuki 1:2, 3) Lakini ni jambo rahisi sana kukuza mtazamo kama wa Yona wa kutohangaikia hali njema ya watu ambao huenda wakatubu. Hiyo ni kweli hasa ikiwa tunaendelea kuwakuta watu wasiopendezwa, wenye kupinga au hata wenye ugomvi tunapowatembelea nyumbani kwao tukiwa na ujumbe wa Ufalme. Huenda tukapuuza watu ambao Yehova bado atawakusanya kutoka katika mfumo huu mwovu wa mambo. (Waroma 2:4) Ikiwa baada ya kujichunguza tunaona kwamba tumeiga hata kwa kadiri ndogo mtazamo ambao Yona alikuwa nao kuelekea Waninawi, tunaweza kusali ili Yehova atusaidie tuwe na maoni kama yake.

13. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova anawahangaikia watu leo?

13 Yehova anawahangaikia wale ambao bado hawamtumikii, naye husikiliza maombi ya watu wake waliojiweka wakfu. (Mathayo 10:11) Kwa mfano ‘atasababisha haki ifanywe’ ili kujibu sala zao. (Luka 18:7, 8) Zaidi ya hayo, Yehova atatimiza ahadi zake zote na makusudi yake yote katika wakati wake. (Habakuki 2:3) Mambo hayo yanatia ndani kuondoa uovu duniani, kama vile alivyoharibu Ninawi baada ya wakaaji wake kurudia uovu.—Nahumu 3:5-7.

14. Tunapaswa kuwa tukifanya nini tunapongojea siku kuu ya Yehova?

14 Je, tutaendelea kungojea kwa subira huku tukifanya mapenzi ya Yehova kwa bidii mpaka mfumo huu mwovu wa mambo utakapoondolewa wakati wa siku kuu ya Yehova? Hatujui kabisa ni kwa kadiri gani kazi ya kuhubiri itafanywa kabla ya kuja kwa siku ya Yehova, lakini tunajua kwamba habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu mpaka Mungu aridhike kabla ya mwisho kuja. Na bila shaka tunapaswa kuhangaikia “vitu vinavyotamaniwa” ambavyo bado vitakusanywa Yehova anapoendelea kujaza nyumba yake utukufu.—Hagai 2:7.

Maoni Yetu Huonekana Katika Matendo Yetu

15. Ni nini kinachoweza kufanya tuthamini zaidi kazi ya kuhubiri?

15 Labda tunaishi kati ya watu ambao hawapendezwi sana na kazi yetu ya kuhubiri, na hali zetu hazituruhusu kuhamia maeneo ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi wa watangazaji wa Ufalme. Tuseme watu kumi wanaweza kupatikana katika eneo letu kabla ya mwisho kuja. Je, tunahisi kwamba watu hao kumi wanastahili kutafutwa? Yesu “alihisi sikitiko” kwa ajili ya umati “kwa sababu ulikuwa umechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Kwa kujifunza Biblia na kusoma kwa makini makala za Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, tunaweza kupata ufahamu zaidi kuhusu matatizo ya ulimwengu huu. Ufahamu huo unaweza kufanya tuthamini zaidi uhitaji wa kuhubiri habari njema. Zaidi ya hayo, tunapotumia kwa uthamini habari inayotegemea Biblia ambayo huandaliwa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” tunaweza kusaidiwa kuwa wenye ushawishi zaidi tunapohubiri eneo linalohubiriwa mara nyingi.—Mathayo 24:45-47; 2 Timotheo 3:14-17.

16. Tunawezaje kufanya huduma yetu iwe yenye matokeo zaidi?

16 Hangaiko letu kuhusu wale ambao huenda wakaitikia ujumbe wa Biblia wenye kutoa uhai hutuchochea kufikiria wakati na njia mbalimbali za kuwafikia wenye-nyumba katika huduma yetu. Je, tunakuta kwamba wengi hawako nyumbani wakati tunapowatembelea? Ikiwa ndivyo, tunaweza kufanya huduma yetu iwe yenye matokeo zaidi kwa kubadili wakati na maeneo ya kuhubiri. Wavuvi huenda kuvua wakati wanapoweza kupata samaki. Je, tunaweza kuwaiga wavuvi tunapofanya kazi yetu ya kuvua kiroho? (Marko 1:16-18) Kwa nini tusijaribu kuhubiri jioni au kuhubiri sokoni, iwapo inakubalika kisheria? Wengine wamegundua kwamba maegesho ya magari, vituo vya malori, vituo vya petroli, na maduka ni ‘maeneo ya uvuvi’ yenye matokeo. Tunaonyesha pia tuna mtazamo kama wa Abrahamu kuelekea watu tunapotumia nafasi mbalimbali kushiriki katika mahubiri yasiyo rasmi.

17. Tunawezaje kuwatia moyo mishonari na wahudumu wengine wa wakati wote?

17 Kuna watu wengi sana ambao bado hawajasikia ujumbe wa Ufalme. Mbali na kuhubiri, je, tunaweza kuonyesha tunahangaikia watu hao hata bila kuondoka nyumbani? Je, tunajua mishonari wowote au wahudumu wengine wa wakati wote? Ikiwa ndivyo, tunaweza kuwatia moyo, labda kwa kuwaandikia barua zinazoonyesha kwamba tunathamini kazi yao. Jambo hilo linawezaje kuonyesha kwamba tunawahangaikia watu kwa ujumla? Barua zetu za kitia moyo na pongezi zinaweza kuwaimarisha mishonari na wahudumu hao waendelee na mgawo wao na hivyo kuwasaidia watu wengi zaidi waijue kweli. (Waamuzi 11:40) Tunaweza pia kusali kwa ajili yao na wale ambao wana njaa ya kuijua kweli. (Waefeso 6:18-20) Njia nyingine ya kuonyesha hangaiko letu ni kutoa michango ya kifedha ili kusaidia kazi ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova.—2 Wakorintho 8:13, 14; 9:6, 7.

Je, Unaweza Kuhamia Eneo Lingine?

18. Wakristo fulani wamefanyaje ili kuendeleza mambo ya Ufalme katika nchi wanamoishi?

18 Watu ambao wamehamia maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa zaidi wa watangazaji wa Ufalme wamebarikiwa kwa sababu ya jitihada zao za kujidhabihu. Hata hivyo, Mashahidi wengine wa Yehova wamejifunza lugha nyingine wakiwa bado nchini mwao ili kuwasaidia kiroho wahamiaji. Jitihada hizo zimebarikiwa kwelikweli. Kwa mfano Mashahidi saba wanaowasaidia watu kutoka China katika jiji la Texas, Marekani, waliwakaribisha watu 114 kwenye mwadhimisho wa Mlo wa Jioni wa Bwana mwaka wa 2001. Wale wanaosaidia vikundi hivyo wameona kwamba mashamba yao yako tayari kuvunwa.—Mathayo 9:37, 38.

19. Inafaa kufanya nini ikiwa unafikiria kuhamia nchi ya kigeni ili kuendeleza kazi ya kuhubiri Ufalme?

19 Labda wewe na familia yako mnahisi kwamba mnaweza kuhamia eneo ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Bila shaka, ni jambo la hekima ‘kuketi na kupiga hesabu ya gharama’ kwanza. (Luka 14:28) Jambo hilo linafaa hasa mtu anapofikiria kuhamia nchi ya kigeni. Mtu yeyote anayefikiria uwezekano wa kufanya hivyo anapaswa kujiuliza maswali kama haya: ‘Je, nitaweza kuitegemeza familia yangu? Je, ninaweza kupata visa ifaayo? Je, tayari ninazungumza lugha ya nchi hiyo, au je, niko tayari kujifunza? Je, nimefikiria hali ya hewa na utamaduni wa nchi hiyo? Je, kweli ninaweza kuwa “msaada wenye kutia nguvu” wala si mzigo kwa waamini wenzangu katika nchi hiyo?’ (Wakolosai 4:10, 11) Ili kujua uhitaji wa nchi ambayo unataka kuhamia, inafaa kuandikia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ambayo inasimamia kazi ya kuhubiri katika eneo hilo. *

20. Kijana mmoja Mkristo amejitoleaje kwa faida ya waamini wenzake na wengine katika nchi za kigeni?

20 Mkristo mmoja ambaye alikuwa akijenga Majumba ya Ufalme huko Japani alipata habari kwamba kulikuwa na uhitaji wa wajenzi wenye ustadi wa kujenga mahali pa ibada huko Paraguay. Kwa kuwa alikuwa mseja na mwenye nguvu za ujana, alihamia nchi hiyo ambako alifanya kazi kwa miezi minane. Yeye ndiye aliyekuwa mfanyakazi pekee wa wakati wote kwenye mradi huo. Akiwa huko, alijifunza Kihispania na akaongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani. Aliona kwamba nchi hiyo ilihitaji watangazaji wa Ufalme. Ingawa alirudi Japani, alienda Paraguay tena baada ya muda mfupi naye alisaidia kukusanya watu kuja kwenye Jumba lilelile la Ufalme.

21. Tunapaswa kuwa na hangaiko na maoni gani hasa tunapongojea siku kuu ya Yehova?

21 Mungu atahakikisha kwamba kazi ya kuhubiri imetimizwa kikamili, kupatana na mapenzi yake. Leo, anaharakisha uvunaji wa mwisho wa kiroho. (Isaya 60:22) Basi, tunapongojea siku ya Yehova, acheni tushiriki kwa bidii kazi ya kuvuna na kuwaona watu jinsi Mungu wetu mwenye upendo anavyowaona.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Haifai sikuzote kuhamia nchi ambako kazi ya kuhubiri imepigwa marufuku au imezuiwa. Kufanya hivyo kunaweza kuwaletea madhara wahubiri wa Ufalme wanaohubiri kwa busara chini ya hali hizo.

Je, Unakumbuka?

Tunapaswa kuwaonaje watu tunapongojea siku ya Yehova?

Abrahamu aliwaonaje watu fulani wenye haki ambao huenda walikuwa wakiishi Sodoma?

Yona aliwaonaje watu wa Ninawi waliotubu?

Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawaona watu ambao bado hawajasikia habari njema kama Yehova anavyowaona?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Abrahamu aliwaona watu jinsi Yehova anavyowaona

[Picha katika ukurasa wa 17]

Yona alikuja kuwaona Waninawi waliotubu jinsi Yehova alivyowaona

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kuwajali watu hutuchochea kufikiria wakati na njia mbalimbali za kuhubiri habari njema