Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yehova aliwaruhusu watumishi wake wa kale, Waisraeli, wafunge ndoa na wake wengi, lakini haruhusu ndoa hizo sasa. Je, viwango vyake hubadilika-badilika?

Yehova hajabadili maoni yake kuhusu ndoa za wake wengi. (Zaburi 19:7; Malaki 3:6) Ndoa za wake wengi hazikuwa sehemu ya mpango wake kwa wanadamu tangu mwanzoni, na hata sasa si sehemu ya mpango wake. Yehova alipomwumba Hawa kuwa mke wa Adamu, alisema kwamba kulingana na kiwango chake, mume anapaswa kuwa na mke mmoja. “Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.”—Mwanzo 2:24.

Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani, alirudia kiwango hicho alipokuwa akiwajibu wale waliouliza kuhusu kutaliki na kufunga ndoa tena. Alisema: “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba wao kutoka mwanzo aliwafanya wa kiume na wa kike na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mtu ataacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja.” Yesu aliendelea kusema: “Yeyote yule atalikiye mke wake, ila kwa sababu ya uasherati, na kuoa mwingine afanya uzinzi.” (Mathayo 19:4-6, 9) Kutokana na hayo, ni wazi kwamba kuoa mke mwingine au wengine zaidi, ni uzinzi pia.

Basi kwa nini ndoa za wake wengi ziliruhusiwa zamani? Kumbuka kwamba Yehova hakuanzisha zoea hilo. Mtu wa kwanza anayetajwa katika Biblia ambaye alikuwa na mke zaidi ya mmoja ni Lameki, mzao wa Kaini. (Mwanzo 4:19-24) Yehova alipoleta Gharika ya siku za Noa, Noa na wanawe watatu walikuwa na mke mmoja kila mmoja. Watu wote waliokuwa na wake zaidi ya mmoja waliharibiwa katika Gharika hiyo.

Karne nyingi baadaye, Yehova alipowachagua Waisraeli kuwa watu wake, tayari wengine wao walikuwa na wake zaidi ya mmoja, ingawa yaonekana wengi wao walikuwa na mke mmoja tu. Mungu hakutaka familia zilizokuwa na mke zaidi ya mmoja zivunjwe. Badala yake, aliweka sheria thabiti za kuongoza familia za aina hiyo.—Kutoka 21:10, 11; Kumbukumbu la Torati 21:15-17.

Yale ambayo Yesu alisema kuhusu kiwango cha ndoa ambacho Mungu aliweka hapo awali, na pia yale ambayo mtume Paulo aliandika chini ya uongozi wa roho ya Mungu, yanaonyesha kwamba ndoa za wake wengi ziliruhusiwa kwa muda tu. Paulo alisema hivi: “Acheni kila mwanamume awe na mke wake mwenyewe na kila mwanamke awe na mume wake mwenyewe.” (1 Wakorintho 7:2) Yeye pia aliongozwa na roho kuandika kwamba mwanamume yeyote anayewekwa rasmi kuwa mwangalizi au mtumishi wa huduma katika kutaniko la Kikristo lazima awe “mume wa mke mmoja.”—1 Timotheo 3:2, 12; Tito 1:6.

Hivyo, Yehova hakuendelea kuruhusu tena ndoa za wake wengi baada ya kutaniko la Kikristo kuanzishwa miaka 2,000 hivi iliyopita. Wakati huo, Mungu alirudisha kiwango cha ndoa alichoweka hapo mwanzoni alipomwumba mwanamume na mwanamke, yaani mwanamume awe na mke mmoja tu. Kiwango hicho ndicho kinachofuatwa na watu wa Mungu leo ulimwenguni pote.—Marko 10:11, 12; 1 Wakorintho 6:9, 10.