Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Watu Wawili Walipiga Hodi Mlangoni Petu”

“Watu Wawili Walipiga Hodi Mlangoni Petu”

“Watu Wawili Walipiga Hodi Mlangoni Petu”

“MIAKA miwili imepita tangu tupatwe na huzuni kubwa ya kufiwa na binti yetu mdogo.” Huo ulikuwa utangulizi wa barua moja iliyochapishwa katika gazeti Le Progrès, la huko Saint-Étienne, Ufaransa.

“Mélissa alikuwa na umri wa miezi mitatu na aliugua ugonjwa mbaya unaoitwa trisomy 18. Huzuni ya kufiwa na mtoto haiishi kamwe. Msiba wa aina hiyo huonekana si haki kabisa. Ingawa tulilelewa katika dini ya Katoliki, mara kwa mara tulijiuliza, ‘Mungu, ikiwa wewe uko, kwa nini unaruhusu mambo haya?’” Bila shaka, mama aliyeandika barua hiyo alikuwa na huzuni, na hakujua la kufanya. Barua yake inaendelea kusema hivi:

“Muda mfupi baada ya matukio hayo, watu wawili waligonga hodi mlangoni petu. Nilitambua mara moja kuwa wao ni Mashahidi wa Yehova. Nilikuwa karibu kuwaambia kwa upole waende zao, lakini nikaona broshua waliyokuwa nayo. Ilikuwa ikizungumzia sababu Mungu anaruhusu kuteseka. Kwa hiyo, nikaamua kuwakaribisha ndani nikiwa na kusudi la kuvunja-vunja hoja zao. Niliwaza kwamba familia yangu ilikuwa imeteseka sana, na nilikuwa nimechoka kusikia watu wakisema, ‘Mungu ametupa, na Mungu amemchukua.’ Mashahidi hao walikaa kwa muda wa saa moja hivi. Walinisikiliza kwa huruma, na walipokuwa wakiondoka, nilihisi nafuu, nikakubali wanitembelee tena. Hayo yalitendeka miaka miwili iliyopita. Bado mimi si mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Lakini nilianza kujifunza Biblia pamoja nao, nami huhudhuria mikutano yao kadiri ninavyoweza.”