Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wenye Furaha Ni Yule Ambaye Mungu Wake Ni Yehova

Wenye Furaha Ni Yule Ambaye Mungu Wake Ni Yehova

Simulizi la Maisha

Wenye Furaha Ni Yule Ambaye Mungu Wake Ni Yehova

LIMESIMULIWA NA TOM DIDUR

Jumba la watu wote lilikuwa tayari limekodishwa. Karibu watu 300 walitarajiwa kuhudhuria kusanyiko katika mji wa Porcupine Plain, Saskatchewan, huko Kanada. Siku ya Jumatano theluji ilianza kuanguka, na kufikia Ijumaa kulikuwa dhoruba kali ya theluji na haikuwezekana kuona kabisa. Halijoto ilishuka na kufikia nyuzi -40° Selsiasi. Watu 28 walihudhuria, kutia ndani watoto wachache. Hilo ndilo kusanyiko la kwanza nililohudhuria nikiwa mwangalizi mpya wa mzunguko. Wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 25 na nilikuwa na wasiwasi. Kabla sijakueleza yaliyotukia, acha nikusimulie jinsi nilivyopata pendeleo hili la pekee la utumishi.

MIMI ni wa saba kati ya ndugu wa kiume wanane. Mzaliwa wa kwanza ni Bill, ambaye anafuatwa na Metro, John, Fred, Mike, na Alex. Nilizaliwa mwaka wa 1925, na Wally ndiye kitinda-mimba. Tuliishi karibu na mji wa Ukraina, Manitoba, ambapo wazazi wangu Michael na Anna Didur walikuwa na shamba dogo. Baba alifanya kazi ya kutunza reli. Tuliishi kwenye shamba letu kwa kuwa nyumba ndogo za reli zilizokuwa mbali hazikuwa mahali pazuri pa kulelea familia kubwa. Mara nyingi Baba hakuishi nyumbani, kwa hiyo Mama ndiye aliyetulea. Mara kwa mara Mama alienda kumtembelea Baba kwa juma moja au zaidi, lakini alihakikisha kwamba tunajua kupika, kuoka mikate, na kufanya kazi mbalimbali za nyumbani. Na kwa kuwa tulikuwa wafuasi wa Kanisa Katoliki la Ugiriki, tangu utotoni Mama alitufundisha kukariri sala na kushiriki desturi nyingine.

Napata Kweli ya Biblia

Tamaa yangu ya kuelewa Biblia ilichochewa nikiwa kijana. Jirani yetu ambaye alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alitembelea familia yetu kwa ukawaida na kutusomea sehemu za Biblia zinazohusu Ufalme wa Mungu, Har–Magedoni, na baraka za ulimwengu mpya. Mama hakupendezwa hata kidogo na ujumbe huo, lakini Mike na Alex walipendezwa nao. Kwa kweli mambo waliyojifunza yaliwachochea wakatae kutumikia jeshini wakati wa vita vya pili vya ulimwengu. Kwa sababu hiyo, Mike alifungwa jela kwa muda mfupi, naye Alex akapelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu huko Ontario. Baada ya muda, Fred na Wally pia walikubali ukweli. Hata hivyo, ndugu zangu wakubwa watatu hawakuukubali. Kwa miaka mingi, hata Mama alipinga ukweli, lakini sote tulishangaa alipochukua msimamo upande wa Yehova. Alibatizwa akiwa na umri wa miaka 83, akafa akiwa na umri wa miaka 96. Baba pia alipendezwa na ukweli kabla hajafa.

Nikiwa na umri wa miaka 17, nilisafiri hadi Winnipeg kutafuta kazi na kushirikiana na watu ambao wangenisaidia kujifunza Biblia. Wakati huo Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku lakini walifanya mikutano kwa ukawaida. Mkutano wa kwanza niliohudhuria ulifanywa katika nyumba ya mtu. Kwa kuwa nililelewa katika Kanisa Katoliki la Ugiriki, mambo niliyosikia hapo mwanzoni yalikuwa mageni. Hata hivyo, hatua kwa hatua nilielewa kwa nini ule mgawanyo kati ya makasisi na waumini haukupatana na Maandiko na pia kwa nini Mungu hakuunga mkono jitihada za makasisi za kubariki vita. (Isaya 2:4; Mathayo 23:8-10; Waroma 12:17, 18) Niliona kuishi katika Paradiso duniani kuwa jambo linalopatana na akili kuliko lile wazo la kuhamia mahali pengine mbali ili kuishi huko milele.

Kwa kuwa nilisadiki kwamba huo ndio ukweli, nilijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa mwaka wa 1942 huko Winnipeg. Kufikia mwaka wa 1943, marufuku juu ya Mashahidi wa Yehova huko Kanada iliondolewa, na kazi ya kuhubiri ikapamba moto. Ukweli wa Biblia ulikuwa pia unatia mizizi moyoni mwangu. Nilikuwa na pendeleo la kutumikia nikiwa mtumishi katika kutaniko na pia kushiriki katika kampeni za kutangaza hotuba za watu wote na kuhubiri katika maeneo yasiyogawiwa mtu. Nilifanya maendeleo makubwa ya kiroho kwa sababu ya kuhudhuria makusanyiko makubwa nchini Marekani.

Kupanua Utumishi Wangu kwa Yehova

Katika mwaka wa 1950, nilianza upainia, na mwezi wa Desemba mwaka huo nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko. Nilipata pendeleo la kuzoezwa kazi hiyo na Charlie Hepworth karibu na Toronto. Ndugu huyo alikuwa mwaminifu na mwenye uzoefu. Pia nilifurahi kutumia juma la mwisho la mazoezi yangu nikiwa na ndugu yangu Alex, ambaye tayari alikuwa mwangalizi wa mzunguko huko Winnipeg.

Ningali nakumbuka kusanyiko langu la kwanza la mzunguko ambalo limetajwa mwanzoni mwa makala hii. Nilikuwa na wasiwasi kuhusu kufanikiwa kwa kusanyiko hilo. Hata hivyo, mwangalizi wetu wa wilaya, Ndugu Jack Nathan, alitufurahisha na kutupatia kazi nyingi za kufanya. Wote waliohudhuria walifurahia programu ya kusanyiko tuliyofupisha. Tulichukua zamu ya kusimulia mambo yaliyoonwa, kufanya mazoezi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba, kufanya ziara za kurudia, na kuonyesha jinsi ya kuongoza mafunzo ya Biblia. Tuliimba nyimbo za Ufalme. Kulikuwa na chakula kingi. Tulikunywa kahawa na keki karibu kila baada ya saa mbili. Wengine walilala kwenye benchi, jukwaani, na wengine sakafuni. Kufikia Jumapili, dhoruba ilikuwa imetulia kidogo na watu 96 walihudhuria hotuba ya watu wote. Tukio hilo lilinifundisha kukabiliana na hali ngumu.

Mgawo wangu uliofuata ulikuwa kaskazini mwa Alberta, British Columbia, na Yukon Territory, eneo ambapo jua huwaka usiku. Kusafiri na kuhubiri kwenye Barabara Kuu ya Alaska yenye mawe-mawe kutoka Dawson Creek, British Columbia, hadi Whitehorse, Yukon (umbali wa kilometa 1,477) kulihitaji uvumilivu na tahadhari. Baadhi ya magumu niliyokabili ni maporomoko ya theluji, miteremko yenye kuteleza, na kutoweza kuona vizuri kwa sababu ya ukungu wa theluji.

Nilishangaa kuona kwamba ukweli ulikuwa umefikia eneo la Far North. Pindi moja, mimi na Walter Lewkowicz tulitembelea kibanda kilichokuwa karibu na kijiji cha Lower Post, British Columbia, kando ya Barabara Kuu ya Alaska, karibu na mpaka wa Yukon Territory. Tulijua kwamba kuna mtu aliyeishi kwenye kibanda hicho kwa sababu tuliona mwangaza mdogo kupitia dirisha dogo. Ilikuwa karibu saa tatu usiku tulipogonga mlango huo. Tulisikia sauti ya mwanamume ikitukaribisha, kwa hiyo tukaingia ndani. Tulishangaa kama nini kumwona mwanamume mzee amejilaza kwenye kitanda chake cha ghorofa akisoma gazeti la Mnara wa Mlinzi! Lo! alikuwa na gazeti la karibuni zaidi kuliko lile tulilokuwa tunaonyesha watu! Alitueleza kwamba yeye hupokea magazeti yake kwa ndege. Kufikia wakati huu, hatukuwa na magazeti ya karibuni zaidi kwa kuwa hatukuwa tumehudhuria mikutano kwa siku nane. Mtu huyo alituambia kwamba anaitwa Fred Berg, na ingawa alikuwa ameandikisha magazeti kwa miaka kadhaa, hii ndiyo iliyokuwa mara ya kwanza kutembelewa na Mashahidi wa Yehova. Fred alitukaribisha tulale kwake usiku huo. Tulimweleza kweli nyingi za Kimaandiko na tukapanga Mashahidi wengine waliokuwa wakipitia eneo hilo kwa ukawaida, wamtembelee.

Kwa miaka mingi nilitembelea mizunguko midogo mitatu. Mizunguko hiyo ilianzia mashariki kwenye jiji la Grande Prairie huko Alberta, hadi magharibi huko Kodiak, Alaska, eneo la zaidi ya kilometa 3,500.

Nilifurahi kujua kwamba katika maeneo ya mbali, sawa na kwingineko, Yehova huonyesha watu wote fadhili zenye upendo na kwamba roho yake huchochea akili na mioyo ya wale walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uhai wa milele. Mtu mmoja mwenye mwelekeo huo alikuwa Henry Lepine kutoka Dawson City, Yukon, jiji ambalo sasa linaitwa Dawson. Henry aliishi katika eneo lililojitenga. Alikuwa hajawahi kuondoka kwenye eneo la migodi ya dhahabu kwa zaidi ya miaka 60. Hata hivyo, roho ya Yehova ilimchochea mzee huyo mwenye umri wa miaka 84 kusafiri umbali wa zaidi ya kilometa 1,600 hadi Anchorage kuhudhuria kusanyiko la mzunguko, hata ingawa hakuwa amewahi kuhudhuria mkutano wa kutaniko hata mmoja. Alifurahia sana programu na ushirika huo. Aliporudi Dawson City, Henry aliendelea kuwa mwaminifu hadi kifo chake. Wengi waliomjua Henry walishangaa ni nini kilichomchochea mzee huyo kufunga safari hiyo ndefu. Kisa hicho kiliwachochea wazee wengine kukubali ukweli. Kwa hiyo, Henry alitoa ushahidi mzuri kwa njia isiyo ya moja kwa moja.

Nilipokea Fadhili Zisizostahiliwa za Yehova

Katika mwaka wa 1955, nilifurahi kupokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 26 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Mazoezi hayo yaliimarisha imani yangu na kunisaidia kumkaribia Yehova zaidi. Nilipohitimu, nilipewa mgawo wa kuendelea kuwa mwangalizi wa mzunguko nchini Kanada.

Kwa mwaka moja hivi nilitumika katika mkoa wa Ontario. Kisha nikapewa tena mgawo wa kutumika katika eneo maridadi la Alaska. Bado ninakumbuka mandhari nzuri ya barabara kuu zilizopitia kandokando ya maziwa yenye kumetameta na kuendesha gari kupitia safu za milima yenye vilele vilivyofunikwa kwa theluji. Wakati wa kiangazi, mabonde na makonde huwa na maua yenye rangi mbalimbali zenye kupendeza. Hewa na maji ni safi. Dubu, mbwa-mwitu, kongoni, kuro, na wanyama wengine wa mwituni huranda-randa kwa uhuru katika mazingira yao ya asili.

Hata hivyo, eneo la Alaska lina magumu yake—halihewa inayobadilika-badilika na pia safari ndefu-ndefu. Mzunguko wangu ulikuwa na umbali wa kilometa 3,200 kutoka mashariki hadi magharibi. Wakati huo, waangalizi wa mzunguko hawakuwa wakipewa magari. Akina ndugu walijitolea kunisafirisha kutoka kutaniko moja hadi lingine. Hata hivyo, nyakati nyingine nililazimika kuomba lifti kwa wenye malori au watalii.

Kisa kimoja kilitendeka kwenye Barabara Kuu ya Alaska kati ya Tok Junction, Alaska, na Mile 1202, au eneo la Scotty Creek. Ofisi za forodha kati ya maeneo hayo mawili zilikuwa umbali wa kilometa 160. Baada ya kupita ofisi ya forodha ya Marekani huko Tok, nilipewa lifti kwa umbali wa kilometa 50 hivi. Baada ya hapo, hakuna gari lililopita, hivyo nilitembea umbali wa kilometa 40 kwa muda wa saa kumi hivi. Baadaye nilipata habari kwamba muda mfupi baada ya mimi kuvuka ofisi ya forodha, magari yote yalizuiwa yasipite kwenye barabara hiyo kwa sababu ya maporomoko ya theluji karibu na kituo hicho cha forodha. Kufikia saa sita usiku, halijoto ilishuka hadi nyuzi -23° Selsiasi na bado nilikuwa umbali wa kilometa 80 kutoka mahali ambapo ningepata makao. Nilitamani sana kupata makao ili nipumzike.

Nilipoendelea kujikokota, niliona gari lililoachwa kando ya barabara likiwa limefunikwa kwa theluji. Niliwaza kwamba nikiingia ndani na nilale kwenye viti, ningejikinga na baridi ya usiku huo. Nilifaulu kuondoa theluji na kufungua mlango, lakini nikakuta vyuma tupu ndani ya gari hilo. Nilipoteremka kidogo barabarani, nilifurahi kuona kibanda ambacho hakikuwa na watu. Baada ya kung’ang’ana kukifungua na kuwasha moto, nilipumzika kwa saa chache. Asubuhi iliyofuata, nilipata lifti hadi kwenye hoteli nyingine ambapo nilipata chakula cha kutosha na kuosha na kufunga vidole vyangu vilivyokuwa na vidonda.

Yehova Aukuza Ukweli Huko Alaska

Ziara yangu ya kwanza huko Fairbanks ilikuwa yenye kutia moyo sana. Tulipata matokeo mazuri katika huduma, na karibu watu 50 walihudhuria hotuba ya watu wote Jumapili hiyo. Tulikutana katika makao madogo ya mishonari walikoishi Vernor na Lorraine Davis. Watu walikuwa wakichungulia kutoka jikoni, chumba cha kulala, na ukumbini ili kusikia hotuba. Kwa kuwa watu wengi walikuja kusikia hotuba hiyo, tulijua kwamba ikiwa Jumba la Ufalme lingejengwa mahali hapo, kazi ya kuhubiri ingeimarika huko Fairbanks. Kwa hiyo, kwa msaada wa Yehova, tulinunua nyumba kubwa kiasi iliyotumiwa kama ukumbi wa kuchezea dansi na kuihamisha hadi kwenye kiwanja kinachofaa. Tulichimba kisima, tukajenga vyoo, na kuweka mfumo wa kupasha jumba joto. Katika muda wa mwaka mmoja, Jumba la Ufalme lilianza kutumiwa huko Fairbanks. Baada ya kujenga jikoni, jumba hilo lilitumiwa kwa ajili ya kusanyiko la wilaya mwaka wa 1958, na watu 330 walihudhuria.

Katika mwaka wa 1960, nilifunga safari ndefu kwa gari hadi kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko New York ili kuhudhuria mazoezi ya kuboresha stadi za waangalizi wote wa mzunguko nchini Marekani na Kanada. Nikiwa huko, Ndugu Nathan Knorr na ndugu wengine wenye madaraka waliniuliza kuhusu uwezekano wa kuanzisha ofisi ya tawi huko Alaska. Miezi michache baadaye, tulifurahi kusikia kwamba kuanzia Septemba 1, 1961, Alaska ingekuwa na ofisi ya tawi. Ndugu Andrew K. Wagner alipewa mgawo wa kusimamia kazi katika ofisi hiyo ya tawi. Yeye na mke wake Vera walikuwa wametumikia huko Brooklyn kwa miaka 20 na pia walikuwa na uzoefu wa kazi ya kusafiri. Kuanzishwa kwa ofisi ya tawi huko Alaska kulithaminiwa sana kwa kuwa kulipunguza safari za mwangalizi wa mzunguko na kumwezesha kukaza fikira zaidi kwenye mahitaji hususa ya makutaniko na maeneo ya mbali.

Mwaka wa 1962 ulikuwa pindi yenye shangwe huko Alaska. Ofisi ya tawi ya Alaska iliwekwa wakfu, na kusanyiko la wilaya lilifanywa huko Juneau, Alaska. Majumba mapya ya Ufalme yalijengwa huko Juneau na Whitehorse, Yukon, na vikundi vipya kadhaa vilivyojitenga vikaanzishwa.

Narudi Kanada

Kwa miaka kadhaa nilikuwa nikimwandikia barua Margareta Petras kutoka Kanada. Reta, kama dada huyo alivyoitwa, alianza upainia mwaka wa 1947, akahitimu kutoka Gileadi mwaka wa 1955, na alikuwa akifanya upainia mashariki mwa Kanada. Nilimwomba tufunge ndoa, naye akakubali. Tulifunga ndoa Februari 1963 huko Whitehorse. Mnamo mwaka huo, nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko magharibi mwa Kanada na tulifurahi kutumikia huko kwa miaka 25.

Kwa sababu afya yetu ilikuwa inadhoofika, mwaka wa 1988 tulipewa mgawo wa kuwa mapainia wa pekee huko Winnipeg, Manitoba. Mgawo wetu ulitia ndani kutunza Jumba la Kusanyiko na tulifanya hivyo kwa miaka mitano. Tungali tunajitahidi kadiri tuwezavyo kushiriki katika kazi inayofurahisha ya kufanya wanafunzi. Tulipokuwa katika kazi ya mzunguko, tulianzisha mafunzo mengi ya Biblia na kuwaachia wengine wayaongoze. Sasa, kwa fadhili zisizostahiliwa za Yehova, sisi huanzisha mafunzo na hufurahi wanapofanya maendeleo kufikia kujiweka wakfu na kubatizwa.

Nasadiki kwamba kumtumikia Yehova ndiyo njia bora zaidi ya maisha kwa kuwa inatupa kusudi, inaridhisha, na huongeza upendo wetu kwa Yehova kila siku. Kufanya hivyo huleta furaha ya kweli. Iwe tumepewa mgawo gani, au iwe tunatumikia wapi, tunakubaliana na mtunga-zaburi aliyesema: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!”—Zaburi 144:15, NW.

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Nikifanya kazi ya mzunguko

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikimtembelea Henry Lepine huko Dawson City. Niko upande wa kushoto

[Picha katika ukurasa wa 26]

Jumba la Ufalme la kwanza huko Anchorage

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mimi na Reta, mwaka wa 1998