Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ibada ya Kweli Huunganisha Familia

Ibada ya Kweli Huunganisha Familia

Ibada ya Kweli Huunganisha Familia

MARIA alikuwa na umri wa miaka 13 wakati yeye na dada yake mdogo, Lucy, walipoelezwa na mtu wa ukoo kumhusu Yehova na pia kuhusu tumaini la Paradiso duniani. Walivutiwa sana hivi kwamba walienda naye kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Maria alivutiwa sana na mafundisho yenye kueleweka yaliyofundishwa huko. Hali ilikuwa tofauti sana na ilivyokuwa katika kanisa lake, ambako mara nyingi hawakufanya jambo lingine ila kuimba tu! Muda si muda watoto hao walianza kujifunza Biblia na mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Ndugu yao mkubwa, Hugo, alipendezwa na falsafa na fundisho la mageuzi. Alidai kwamba haamini kuwapo kwa Mungu. Lakini alipokuwa akitumikia jeshini, alisoma kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?  * Alipata majibu kwa maswali ambayo hakuna dini nyingine yoyote ingeweza kumjibu. Alipomaliza utumishi wake jeshini, alianza kuimarisha imani yake mpya katika Mungu kwa kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano pamoja na dada zake. Maria na Lucy walibatizwa mwaka wa 1992, miaka miwili baada ya kuelezwa kweli mara ya kwanza, naye ndugu yao akabatizwa miaka miwili baadaye.

Wakati huo wazazi wao walioshikilia sana mafundisho ya Wakatoliki, hawakupendezwa na kweli. Waliwaona Mashahidi wa Yehova kuwa wenye kusumbua, ingawa walivutiwa na tabia nzuri na mavazi ya kiasi ya Mashahidi vijana walioalikwa nyumbani na watoto wao. Pia, wakati wa chakula watoto walizungumzia mambo waliyojifunza mikutanoni, na wazazi wao wakaanza kupendezwa.

Hata hivyo, wazazi hao bado walipendezwa na uchawi. Baba alikuwa mlevi na alikuwa akimpiga mama. Familia hiyo ilikuwa karibu kuvunjika. Ndipo baba huyo akatiwa gerezani kwa majuma mawili kwa sababu ya matendo ya fujo yanayotokana na ulevi. Akiwa gerezani, alianza kusoma Biblia. Alipokuwa akisoma, aliona maneno ya Yesu kuhusu ishara za siku za mwisho. Baba na mama huyo walishangazwa na maneno hayo, nao wakaenda kwenye Jumba la Ufalme na wakakubali funzo la Biblia la nyumbani. Baada ya kujifunza kweli, waliharibu vitabu vyao vyote vya uchawi nao roho waovu wakaacha kuwashambulia kwa kuwa waliliitia jina la Yehova. Walianza kufanya mabadiliko makubwa katika nyutu zao.

Je, unaweza kuwazia jinsi Maria na Lucy walivyoguswa moyo kuona wazazi wao wakibatizwa na Hugo kwenye mojawapo ya makusanyiko ya wilaya huko Bolivia mwaka wa 1999? Miaka tisa ilikuwa imepita tangu Maria na Lucy waelezwe mara ya kwanza kumhusu Yehova na ahadi zake. Sasa wao pamoja na Hugo, wako katika utumishi wa wakati wote. Wanafurahi kama nini kwamba ibada ya kweli iliunganisha familia yao!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.