Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna ‘Kanisa Moja Tu la Kweli’?

Je, Kuna ‘Kanisa Moja Tu la Kweli’?

Je, Kuna ‘Kanisa Moja Tu la Kweli’?

“KAMA vile kulivyo na Kristo mmoja, ndivyo kulivyo na mwili mmoja wa Kristo, Bibi-arusi mmoja wa Kristo: ‘Kanisa moja la Katoliki la mitume.’”—Dominus Iesus.

Hivyo ndivyo kadinali Mkatoliki, Joseph Ratzinger, alivyoeleza fundisho la kanisa lake kwamba kuna kanisa moja tu la kweli. Alisema kwamba kanisa hilo ni “Kanisa moja tu la Kristo, ambalo ni Kanisa Katoliki.”

“Si Makanisa ya Kweli”

Ingawa Papa John Paul wa Pili alisisitiza kwamba hati hiyo ya Dominus Iesus “haikuzidharau au kuzivunjia heshima dini nyingine,” viongozi wa makanisa ya Kiprotestanti waliipinga vikali. Kwa mfano, katika mkutano wa Baraza Kuu la Kanisa la Presibiteri uliofanywa Juni 2001, huko Belfast, Ireland Kaskazini, kasisi mmoja alisema kwamba hati hiyo iliandikwa na “kikundi chenye nguvu cha Kanisa Katoliki . . . kilichoogopeshwa na ule msimamo wa kukubali maoni ya wengine ulioanzishwa na Baraza la Pili la Vatikani.”

Robin Eames, Askofu wa Kanisa la Ireland alisema kwamba “atakatishwa tamaa sana” ikiwa hati hiyo “ingekuwa inarudia ule msimamo wa Kanisa kabla ya Baraza la Pili la Vatikani.” Akitoa maoni yake kuhusu dai la Vatikani kwamba makanisa yanayokataa mafundisho fulani ya Katoliki “si Makanisa ya kweli,” Eames alisema: “Kwa maoni yangu, hayo ni matusi.”

Kwa nini hati ya Dominus Iesus iliandikwa? Yaonekana kwamba Baraza la Usimamizi la Kanisa Katoliki lilikuwa na wasiwasi kuhusu ile imani ya kwamba kweli za kidini zinategemea maoni ya mtu binafsi. Kulingana na gazeti The Irish Times, “kutokea kwa theolojia inayounga mkono kuwepo kwa dini mbalimbali, na lile wazo la kwamba dini zote zinafanana . . . liliendelea kumsumbua Kadinali Ratzinger.” Yaonekana kwamba maoni hayo ndiyo yaliyomchochea kutoa maelezo kuhusu kanisa moja la kweli.

Je, Ni Muhimu Kuchunguza Kanisa Lako?

Bila shaka, kwa watu fulani, lile wazo la kwamba kweli za kidini zinategemea maoni ya mtu binafsi, na ile theolojia inayounga mkono kuwepo kwa dini mbalimbali huvutia na hupatana na akili kuliko kusema kwamba kuna kanisa moja tu la kweli. Kwa maoni yao, dini inapaswa kuwa uchaguzi wa mtu binafsi. Wao husema kwamba ‘kwa kweli, haijalishi wewe ni wa kanisa gani.’

Huenda hayo yakaonekana kuwa maoni yaliyosawazika zaidi hata ingawa yamefanya dini igawanyike kuwa madhehebu mbalimbali. Watu wengi husema kwamba ‘migawanyiko hiyo ya kidini inaonyesha kwamba watu wana uhuru wa kuchagua.’ Hata hivyo, kulingana na mwandishi Steve Bruce, kwa kweli kuwepo kwa “dini mbalimbali” kunaonyesha kwamba “watu hawapendezwi na dini.”—A House Divided: Protestantism, Schism, and Secularization.

Basi, ni maoni gani yaliyo sawa? Je, kuna kanisa moja tu la kweli? Je, kanisa hilo ni Kanisa Katoliki tu? Je, makanisa mengine pia hukubaliwa na Mungu? Kwa kuwa maswali hayo yanahusu uhusiano wetu na Muumba wetu, kwa kweli ni muhimu tujue maoni yake kuhusu jambo hilo. Tunawezaje kujua maoni yake? Kwa kusoma Biblia, Neno la Mungu lililoandikwa chini ya uongozi wa roho yake. (Matendo 17:11; 2 Timotheo 3:16, 17) Acheni tuchunguze Biblia inasema nini kuhusu kanisa moja la kweli.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]

COVER: Mark Gibson/Index Stock Photography