Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Unawathamini Waamini Wenzako Waliozeeka?

Je, Wewe Unawathamini Waamini Wenzako Waliozeeka?

Je, Wewe Unawathamini Waamini Wenzako Waliozeeka?

WATU wa Israeli la kale walipokuwa katika uhusiano wa agano pamoja na Mungu, waliamriwa hivi: “Mwondokeeni mtu mwenye mvi; heshimuni uso wa mtu mzee; nawe mche Mungu wako.” (Mambo ya Walawi 19:32) Kwa hiyo, kuwaheshimu waliozeeka kulikuwa wajibu mtakatifu na kulihusiana na ujitiisho kwa Mungu. Ingawa Wakristo leo hawapo tena chini ya Sheria ya Musa, sheria hiyo hutukumbusha kwamba Yehova huwathamini wazee-wazee wanaomtumikia. (Mithali 16:31; Waebrania 7:18) Je, tuna maoni kama ya Yehova? Je, tunawathamini ndugu na dada zetu Wakristo waliozeeka?

Alimthamini Rafiki Yake Mzee

Simulizi moja la Biblia linaloonyesha umuhimu wa kuwaheshimu wazee-wazee linapatikana katika Kitabu cha Pili cha Wafalme. Simulizi hilo linaeleza jinsi nabii mchanga Elisha alivyochukua mahali pa nabii Eliya. Fikiria mambo yaliyotendeka siku ya mwisho ya Eliya akiwa nabii katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi.

Siku hiyo, nabii huyo mzee alielekezwa na Yehova asafiri kutoka Gilgali hadi Betheli, kutoka Betheli hadi Yeriko, na kutoka Yeriko hadi kwenye Mto Yordani. (2 Wafalme 2:1, 2, 4, 6) Wakati wa safari hiyo yenye umbali wa karibu kilometa 50, Eliya alimsihi Elisha mara tatu aache kumfuata. Hata hivyo, Elisha alikataa kumwacha nabii Eliya mzee kama vile miaka mingi mapema mwanamke mchanga Ruthu alivyokataa kabisa kumwacha Naomi. (Ruthu 1:16, 17) Elisha alisema hivi mara tatu: “Kama BWANA aishivyo, na roho yako iishivyo, sitakuacha.” (2 Wafalme 2:2, 4, 6) Kufikia wakati huo, Elisha alikuwa tayari amemsaidia Eliya kwa miaka sita hivi. Ingawa hivyo, alitamani kufanya kazi pamoja na Eliya kwa muda mrefu iwezekanavyo. Kwa kweli, simulizi hilo linaongeza kusema hivi: “Ikawa, walipokuwa wakiendelea mbele na kuongea, tazama! . . . Eliya akapanda mbinguni.” (Mstari wa 11) Eliya na Elisha walikuwa wakiongea hadi kufikia mwisho kabisa wa huduma ya Eliya huko Israeli. Inaonekana yule nabii mchanga alikuwa na hamu ya kupata maagizo mengi iwezekanavyo na kitia-moyo kutoka kwa yule nabii mzee na mwenye uzoefu zaidi. Ni wazi kwamba alimthamini rafiki yake mzee.

‘Kama Baba na Kama Mama’

Si vigumu kuelewa kwa nini Elisha alimpenda yule nabii mzee aliyekuwa kama baba wa kiroho na rafiki yake. (2 Wafalme 2:12) Muda mfupi tu kabla ya mgawo wake kumalizika huko Israeli, Eliya alimwambia Elisha hivi: “Omba kwangu lolote utakalo nikutendee, kabla sijaondolewa kwako.” (Mstari wa 9) Kwa hiyo, hadi kufikia mwisho kabisa, Eliya alihangaikia hali ya kiroho ya mwandamizi wake na kuendelezwa kwa kazi ya Mungu.

Leo, inachangamsha moyo kuona jinsi Wakristo waliozeeka ambao ni kama baba na mama wanavyowahangaikia vijana na walivyo tayari kuwagawia ujuzi na hekima waliyo nayo. Kwa mfano, wajitoleaji wa muda mrefu wanaotumikia kwenye ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova huwasaidia kwa utayari Wanabetheli wapya wajipatie ustadi wanaohitaji ili kutimiza kazi zao. Vivyo hivyo, waangalizi wasafirio na wake zao ambao wamekuwa wakiyatembelea makutaniko kwa miaka mingi hufurahi kutumia ujuzi wao mwingi pamoja na wale wanaozoezwa watumikie wakiwa wahudumu wasafirio. Zaidi ya hayo, katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, kuna ndugu na dada wazee ambao wamekuwa wakimtumikia Yehova kwa uaminifu kwa makumi ya miaka na ambao hushiriki hekima na uzoefu wao kwa shangwe pamoja na washiriki wapya wa kutaniko.—Mithali 2:7; Wafilipi 3:17; Tito 2:3-5.

Hangaiko la kutoka moyoni linaloonyeshwa na Wakristo hao wapendwa waliozeeka hufanya tufurahie kweli kuwaheshimu. Kwa hiyo, tunataka kuiga mfano wa Elisha kwa kuwathamini kabisa waamini wenzetu waliozeeka. Kama mtume Paulo anavyotukumbusha, acheni tuendelee kutendea “mwanamume mzee . . . kama baba” na “wanawake wazee zaidi kama mama.” (1 Timotheo 5:1, 2) Kwa kufanya hivyo, tunasaidia sana kutaniko la Kikristo ulimwenguni pote liendelee kufanya kazi vizuri na kufanya maendeleo.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Elisha alitamani kufanya kazi pamoja na Eliya muda mrefu iwezekanavyo

[Picha katika ukurasa wa 31]

Vijana hunufaika sana kwa kushirikiana na Wakristo wazee-wazee