Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Dini Moja Tu ya Kweli ya Kikristo

Kuna Dini Moja Tu ya Kweli ya Kikristo

Kuna Dini Moja Tu ya Kweli ya Kikristo

YESU KRISTO alianzisha kanisa, au kutaniko moja tu. Kutaniko hilo lilikuwa mwili wa kiroho, familia ya kiroho. Kwa kusema hivyo, tunamaanisha kwamba lilikuwa mkusanyiko wa watu waliochaguliwa na roho takatifu ya Mungu—wote wakitambuliwa na Mungu kuwa “watoto” wake.—Waroma 8:16, 17; Wagalatia 3:26.

Yesu alifundisha kwamba Mungu alitumia njia moja tu kuelekeza watu kwenye ukweli na uhai. Ili kueleza ukweli huo muhimu, Yesu aliifananisha njia ya kwenda kwenye uhai wa milele na barabara. Alisema: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.”—Mathayo 7:13, 14; Yohana 14:6; Matendo 4:11, 12.

Kutaniko Lenye Umoja

Hatupaswi kufikiri kwamba kutaniko hilo la karne ya kwanza ni “jamii ya ulimwenguni pote yenye utaratibu kama ile tunayorejelea tunapozungumza kuhusu kanisa katoliki,” chasema kichapo The New Dictionary of Theology. Kwa nini? Kichapo hicho kinasema “ni kwa sababu jamii hiyo ya ulimwenguni pote yenye utaratibu haijawahi kuwepo.”

Hakuna anayeweza kupinga kwamba kutaniko la kwanza la Kikristo halikufanana hata kidogo na matengenezo ya makanisa yaliyopo leo ambayo hufuata utaratibu na desturi mbalimbali. Lakini kutaniko hilo lilikuwa limepangwa kitengenezo. Makutaniko mojamoja hayakujitegemea yenyewe. Yote yalitambua mamlaka ya baraza linaloongoza kule Yerusalemu. Baraza hilo—lililofanyizwa na mitume na wanaume wazee kutoka kutaniko la Yerusalemu—lilisaidia kudumisha umoja wa kutaniko likiwa “mwili mmoja” wa Kristo.—Waefeso 4:4, 11-16; Matendo 15:22-31; 16:4, 5.

Kutaniko hilo moja la kweli lilipatwa na nini? Je, lilikuja kuwa Kanisa Katoliki lenye nguvu? Je, lilikuja kuwa matengenezo ya makanisa ya Kiprotestanti yaliyogawanyika ambayo yapo leo? Au je, jambo jingine lilitendeka?

“Ngano” na “Magugu”

Ili kupata majibu, acheni tuchunguze kwa makini yale ambayo Yesu Kristo mwenyewe alisema yangetukia. Utashangaa kujua kwamba Yesu alitarajia kutaniko lake litoweke na angeruhusu hali hiyo yenye kusikitisha iendelee kwa miaka mingi.

Akihusianisha kutaniko lake na “ufalme wa mbingu,” yeye alisema: “Ufalme wa mbingu umekuwa kama mtu aliyepanda mbegu bora katika shamba lake. Watu wakiwa wamelala usingizi, adui yake alikuja na kupandilia magugu katikati ya ngano, naye akaondoka. Wakati jani lilipoota na kutokeza matunda, ndipo magugu yalipoonekana pia. Kwa hiyo watumwa wa mwenye nyumba wakaja na kumwambia, ‘Bwana-mkubwa, je, hukupanda mbegu bora katika shamba lako? Jinsi gani, basi, lapata kuwa na magugu?’ Yeye akawaambia, ‘Adui, mtu fulani, alifanya hilo.’ Wakamwambia, ‘Basi, je, wataka sisi tutoke kwenda na kuyakusanya?’ Yeye akasema, ‘La; ili isitukie kuwa, mnapoyakusanya magugu, mwing’oe ngano pamoja nayo. Acheni vyote viwili vikue pamoja mpaka mavuno; na katika majira ya mavuno hakika nitawaambia wavunaji, Kwanza kusanyeni magugu na kuyafunga matita-matita ili kuyachoma kabisa, ndipo nendeni mkusanye ngano ghalani mwangu.’”—Mathayo 13:24-30.

Yesu alieleza kwamba yeye ndiye “mpanzi.” “Mbegu iliyo bora” ilifananisha wanafunzi wake wa kweli. “Adui” yake alikuwa Shetani Ibilisi. “Magugu” yalikuwa Wakristo bandia ambao walijipenyeza kwenye kutaniko la kwanza la Kikristo. Alisema kwamba ataacha “ngano” na “magugu” yakue pamoja hadi wakati wa “mavuno,” ambao ungekuwa kwenye “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 13:37-43) Hayo yote yalimaanisha nini?

Kutaniko la Kikristo Lachafuliwa

Punde tu baada ya mitume kufa, walimu waasi-imani waliokuwa ndani ya kutaniko walianza kuliongoza. Walisema “mambo yaliyopotoka ili kuvuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Matendo 20:29, 30) Kwa sababu hiyo Wakristo wengi ‘walianguka kutoka kwenye imani.’ ‘Waligeuzwa kando kwenye hadithi zisizo za kweli.’—1 Timotheo 4:1-3; 2 Timotheo 4:3, 4.

Kichapo The New Dictionary of Theology kinasema kwamba kufikia karne ya nne W.K., ‘Ukristo wa Kikatoliki ulikuwa umekuwa dini rasmi ya Milki ya Roma.’ Kulikuwa na “ushirikiano kati ya dini na mamlaka za kiserikali”—muungano huo kati ya Kanisa na Serikali ulipingana kabisa na imani ya Wakristo wa kwanza. (Yohana 17:16; Yakobo 4:4) Kichapo hicho hicho kinasema kwamba baada ya muda, muundo wote wa kanisa, na vilevile imani yake ya msingi, ulibadilika kabisa “chini ya uvutano wa mchanganyiko wa ajabu na usiofaa wa mafundisho ya Agano la Kale na falsafa za Plato.” Kama alivyotabiri Yesu Kristo, wanafunzi wake wa kweli walifunikwa huku Wakristo bandia wakistawi.

Wale waliokuwa wakimsikiliza Yesu walijua jinsi ilivyokuwa vigumu kutofautisha ngano ya kweli na magugu kama vile manyasi yenye sumu, ambayo yanapokua hufanana sana na ngano. Kwa hiyo mfano huo wa Yesu ulikuwa ukionyesha kwamba kwa muda fulani, ingekuwa vigumu kutofautisha Wakristo wa kweli na wale bandia. Hiyo haimaanishi kwamba kutaniko la Kikristo lilikoma kuwapo, kwa kuwa Yesu aliahidi angeendelea kuwaongoza ndugu zake wa kiroho “siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:20) Yesu alisema kwamba ngano ingeendelea kukua. Hata hivyo, kwa muda wa karne nyingi, inaonekana kwamba Wakristo wa kweli—wakiwa mtu mmoja-mmoja au wakiwa vikundi—walijitahidi wawezavyo kushika mafundisho ya Kristo. Lakini hawakuweza kutambuliwa waziwazi wakiwa kundi au tengenezo. Bila shaka hawakufanana na yale matengenezo ya dini za uasi-imani yaliyotambuliwa waziwazi ambayo kwa karne nyingi hayakutimiza lolote ila kuliletea dharau na kulivunjia heshima jina la Yesu Kristo.—2 Petro 2:1, 2.

‘Mtu wa Uasi-Sheria Afunuliwa’

Mtume Paulo alitabiri jambo jingine ambalo lingetambulisha matengenezo hayo ya dini bandia. Aliandika: “Msiache mtu yeyote awashawishi nyinyi katika namna yoyote, kwa sababu [siku ya Yehova] haitakuja isipokuwa uasi-imani uje kwanza na mtu wa uasi-sheria apate kufunuliwa.” (2 Wathesalonike 2:2-4) ‘Mtu huyo wa uasi-sheria’ si mwingine ila ni jamii ya makasisi iliyojikweza na kutawala kutaniko la “Kikristo.” *

Uasi-imani huo ulianza katika siku za mtume Paulo. Baada ya mitume kufa na uvutano wao wa kuuzuia kutoweka, uasi-imani ulizidi. Paulo alisema kwamba uasi-imani huo ungetambuliwa kwa “utendaji wa Shetani pamoja na kila kazi yenye nguvu na ishara za uwongo na mambo ya ajabu na pamoja na kila udanganyo usio wa uadilifu.” (2 Wathesalonike 2:6-12) Maneno hayo yanaeleza vizuri sana yale ambayo viongozi wengi wa kidini wamefanya kwa muda wa karne nyingi.

Ili kuunga mkono dai lao kwamba Ukatoliki ndio kanisa moja la kweli, viongozi Wakatoliki husema kwamba maaskofu wao “wamerithi utume wao kutoka kwa mitume kupitia mfuatano wa mitume wa kwanza.” Kwa kweli dai hilo halina msingi wa kihistoria au Kimaandiko. Hakuna ushuhuda thabiti unaoonyesha kwamba matengenezo ya makanisa yaliyotokea baada ya mitume wa Yesu kufa yaliongozwa na roho takatifu ya Mungu.—Waroma 8:9; Wagalatia 5:19-21.

Namna gani makanisa mengine ambayo yalitokea baada ya yale Marekebisho Makubwa ya Kidini? Je, yalirudia kile kielelezo cha kutaniko la kwanza la Kikristo? Je, yalirudisha usafi wa kutaniko la kwanza la Kikristo? Ni kweli kwamba baada ya yale Marekebisho Makubwa ya Kidini, watu wengi wa kawaida walipata Biblia katika lugha zao wenyewe. Hata hivyo, historia inaonyesha kwamba makanisa hayo yaliendelea kufundisha mafundisho yasiyo ya kweli. *Mathayo 15:7-9.

Hata hivyo, kumbuka kwamba Yesu Kristo alitabiri waziwazi kuwa kutaniko moja la kweli lingerudishwa wakati wa kipindi alichokiita umalizio wa mfumo wa mambo. (Mathayo 13:30, 39) Utimizo wa unabii wa Biblia unaonyesha kwamba tunaishi katika kipindi hicho sasa. (Mathayo 24:3-35) Kwa hiyo, kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Kanisa hilo moja la kweli liko wapi?’ Linapaswa kutambuliwa waziwazi leo.

Huenda ukahisi kwamba tayari umepata kanisa, au kutaniko hilo. Ni muhimu uhakikishe jambo hilo. Kwa nini? Kwa sababu kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, kuna kanisa moja tu la kweli. Je, umejitahidi kuhakikisha ikiwa kanisa lako linafuata kwa ukaribu kielelezo kilichowekwa na kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, na kwamba linashikamana kwa uaminifu na mafundisho ya Yesu Kristo? Kwa nini usichunguze jambo hilo sasa? Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kufanya hivyo.—Matendo 17:11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Habari zaidi kuhusu jinsi ya kumtambua “mtu wa uasi-sheria” inapatikana katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 1990, ukurasa 10-14.

^ fu. 20 Ona sura “Yale Mapinduzi Makubwa ya Kidini—Jitihada ya Kutafuta Ilichukua Mgeuko Mpya” katika kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, ukurasa wa 306-328, kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mfano wa Yesu wa ngano na magugu unatufundisha nini kuhusu kutaniko la kweli?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, kanisa lako linafuata kielelezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza cha kuhubiri na kufundisha?