Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Katika sehemu nyingi za ulimwengu, kuna desturi ya kutoa zawadi za arusi. Tunapaswa kufikiria kanuni gani za Biblia tunapotoa au kupokea zawadi hizo?

Biblia inakubali utoaji wa zawadi ikiwa utoaji huo unafanywa kwa nia nzuri na katika pindi inayofaa. Biblia inawatia moyo Wakristo wa kweli wamwige Yehova, Mpaji mwenye ukarimu wanapotoa zawadi. (Yakobo 1:17) Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wenzake hivi: “Msisahau kule kutenda mema na kule kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana kwa dhabihu za namna hiyo Mungu hupendezwa vema.” Kwa hiyo, Wakristo wanatiwa moyo wawe wakarimu.—Waebrania 13:16; Luka 6:38.

Namna gani kutumia orodha ya zawadi za arusi, zoea ambalo limeenea katika nchi fulani? Kulingana na zoea hilo, wale wanaotarajia kufunga ndoa hujiandikisha kwenye duka fulani kwa kukagua bidhaa zilizo katika duka hilo kisha huandika orodha ya vitu ambavyo wangependa kupewa kama zawadi. Watu wa jamaa na marafiki wa watu hao huelekezwa kwenye duka hilo ili kununua vitu ambavyo vimeandikwa katika orodha hiyo. Huenda orodha hiyo ikamsaidia mwenye kutoa zawadi asitumie muda mwingi kutafuta zawadi, na wale wanaozipokea hawatasumbuka kurudisha dukani zawadi ambazo hawataki.

Iwapo wale wanaotarajia kufunga ndoa wangependa kutumia orodha hiyo, huo ni uamuzi wa kibinafsi. Hata hivyo, itafaa Mkristo awe mwangalifu ili kuepuka mazoea yoyote ambayo huenda yakavunja kanuni za Biblia. Kwa mfano, namna gani ikiwa wale wanaotarajia kufunga ndoa wataandika orodha ya vitu ambavyo ni vya bei ghali sana? Ikiwa hivyo, huenda wale wasio na pesa za kutosha wakashindwa kutoa zawadi, au wakaona kwamba ni afadhali wakatae mwaliko wa kuhudhuria arusi hiyo ili wasiaibike kwa kuleta zawadi ya bei rahisi. Mwanamke mmoja Mkristo aliandika hivi: “Kutoa zawadi za arusi kumekuwa mzigo. Nimejaribu kuwa mkarimu, lakini siku hizi furaha yote niliyokuwa nikipata katika kutoa imepotea.” Lingekuwa jambo lenye kusikitisha kama nini ikiwa arusi ingekuwa chanzo cha kuvunja moyo!

Kwa kweli, wale wanaotoa zawadi hawapaswi kulazimishwa kuhisi kwamba ili zawadi yao ikubaliwe, ni lazima inunuliwe kwenye duka fulani au iwe ya bei fulani. Kwani, Yesu Kristo alionyesha kwamba jambo lililo la thamani zaidi machoni pa Mungu ni mtazamo wa moyoni wa mwenye kutoa, wala si bei ya zawadi yenyewe. (Luka 21:1-4) Vivyo hivyo, mtume Paulo alisema hivi kuhusu zawadi za rehema kwa maskini: “Acheni kila mmoja afanye kama vile ameazimia moyoni mwake, si kwa kinyongo au kwa shurutisho, kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.”—2 Wakorintho 9:7.

Kulingana na Biblia, si kosa kuonyesha au kuandika barua fupi ya kukutambulisha kuwa mtoaji wa zawadi fulani. Hata hivyo, katika maeneo fulani, ni desturi kumtambulisha mwenye kutoa zawadi kwa wale waliohudhuria. Desturi hiyo inaweza kuleta matatizo. Huenda wale wanaotoa zawadi wasitake kujulikana na kusifiwa isivyofaa. Watu hao hutenda kulingana na kanuni iliyo kwenye Mathayo 6:3, ambapo Yesu anasema: “Lakini wewe, unapotoa zawadi za rehema, usiache mkono wako wa kushoto ujue lile ambalo mkono wako wa kuume unafanya.” Huenda wengine wakawa na maoni ya kwamba kutoa zawadi ni jambo la kibinafsi linalopaswa kujulikana kati ya mtoaji na mpokeaji. Zaidi ya hayo, kuwatambulisha watoaji huenda kukafanya watu waanze kulinganisha zawadi, na hivyo ‘kuchochea mashindano.’ (Wagalatia 5:26) Hakika Wakristo hawangependa kumwaibisha mtu yeyote kwa kutangaza hadharani majina ya watoaji.—1 Petro 3:8.

Naam, kutoa zawadi kutaendelea kuleta furaha ikiwa tutatenda kupatana na kanuni za Neno la Mungu.—Matendo 20:35.