Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mfanye Yehova Kuwa Tumaini Lako

Mfanye Yehova Kuwa Tumaini Lako

Mfanye Yehova Kuwa Tumaini Lako

“Ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU, tumaini langu tokea ujana wangu.”—ZABURI 71:5.

1. Daudi, mvulana mchungaji, alikabili mwito gani?

MTU huyo alikuwa na urefu wa karibu meta tatu. Basi haishangazi kwamba askari-jeshi wote wa vikosi vya Israeli waliogopa kupigana naye! Kwa majuma mengi, kila asubuhi na kila jioni, Goliathi, jitu la Wafilisti, aliyatukana majeshi ya Israeli na kuyatolea mwito yatume shujaa apigane naye. Hatimaye, mwito huo ulikubaliwa, si na askari-jeshi, bali na kijana tu. Daudi, mvulana huyo mchungaji alionekana mdogo sana akilinganishwa na mpinzani wake. Hata huenda Daudi alikuwa na uzani mdogo kuliko silaha za Goliathi! Hata hivyo, kijana huyo alikabiliana na jitu hilo na akawa mfano unaojulikana sana wa ujasiri.—1 Samweli 17:1-51.

2, 3. (a) Kwa nini Daudi aliweza kukabiliana na Goliathi akiwa na ujasiri mwingi? (b) Tutachunguza hatua gani mbili tunazopaswa kuchukua ili kumfanya Yehova kuwa tumaini letu?

2 Ni nini kilichompa Daudi ujasiri huo? Hebu fikiria maneno fulani ambayo huenda yaliandikwa na Daudi katika miaka yake ya baadaye: “Ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU, tumaini langu tokea ujana wangu.” (Zaburi 71:5) Naam, akiwa kijana, Daudi alimtumaini Yehova kabisa. Alimkabili Goliathi na kusema: “Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la BWANA wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.” (1 Samweli 17:45) Goliathi alitumaini nguvu zake nyingi na silaha zake, lakini Daudi alimtumaini Yehova. Kwa kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu alikuwa upande wake, Daudi hakupaswa kumwogopa mwanadamu hata kama mwanadamu huyo alikuwa mkubwa na mwenye silaha nyingi kadiri gani.

3 Unaposoma kumhusu Daudi, je, unatamani tumaini lako kwa Yehova liwe lenye nguvu kama lake? Yaelekea wengi wetu wanatamani hivyo. Basi acheni tuchunguze hatua mbili tunazoweza kuchukua ili kumfanya Yehova kuwa tumaini letu. Kwanza, tunahitaji kushinda kizuizi kimoja ambacho hufanya watu wasimtumaini Yehova. Pili, tunahitaji kujua kumtumaini Yehova kunahusisha nini hasa.

Kushinda Kizuizi Ambacho Hufanya Wengi Wasimtumaini Yehova

4, 5. Kwa nini watu wengi wanaona ni vigumu kumtumaini Mungu?

4 Ni nini huwazuia watu wasimtumaini Mungu? Mara nyingi, watu fulani hushindwa kuelewa ni kwa nini mambo mabaya hutukia. Wengi wanafundishwa kwamba Mungu ndiye husababisha kuteseka. Msiba unapotokea, huenda makasisi wakasema kwamba Mungu “amewachukua” watu hao wakaishi naye mbinguni. Zaidi ya hayo, viongozi wengi wa kidini hufundisha kwamba Mungu alipanga kimbele kila kitu—kutia ndani kila msiba na tendo baya—kinachotokea katika ulimwengu huu. Ingekuwa vigumu sana kumtumaini Mungu asiyejali kama huyo. Shetani, ambaye hupofusha akili za wasioamini, anatamani sana kuendeleza ‘mafundisho hayo yote ya roho waovu.’—1 Timotheo 4:1; 2 Wakorintho 4:4.

5 Shetani anataka watu waache kumtumaini Yehova. Adui huyo wa Mungu hataki tujue sababu za kweli zinazofanya wanadamu wateseke. Na ikiwa tumejifunza katika Maandiko sababu zinazofanya tuteseke, Shetani angependa tuzisahau. Kwa hiyo, inafaa tujikumbushe mara kwa mara sababu tatu za msingi zinazoonyesha kwa nini kuna kuteseka ulimwenguni. Kwa kufanya hivyo, tunaweza kuihakikishia mioyo yetu kwamba Yehova hasababishi matatizo tunayopata maishani.—Wafilipi 1:9, 10.

6. Andiko la 1 Petro 5:8 linaonyeshaje sababu moja ya kuteseka kwa wanadamu?

6 Sababu moja ya kuteseka kwa wanadamu ni kwamba Shetani anataka kuvunja uaminifu wa watu waaminifu wa Yehova. Alijaribu kuvunja uaminifu wa Ayubu. Shetani hakufaulu wakati huo, lakini bado anaendelea kujaribu. Akiwa mtawala wa ulimwengu huu, anajaribu “kunyafua” watumishi waaminifu wa Yehova. (1 Petro 5:8) Hiyo inatia ndani kila mmoja wetu! Shetani anataka kutufanya tuache kumtumikia Yehova. Kwa hiyo, mara nyingi yeye huchochea mnyanyaso. Ingawa mateso hayo huwa makali, tuna sababu nzuri ya kuvumilia. Kwa kuvumilia, tunachangia kumthibitisha Shetani kuwa mwongo na kumfurahisha Yehova. (Ayubu 2:4; Mithali 27:11) Tumaini letu kwa Yehova huimarika, anapotupatia nguvu za kuvumilia mnyanyaso.—Zaburi 9:9, 10.

7. Andiko la Wagalatia 6:7 hutusaidia kutambua sababu gani ya kuteseka kwa wanadamu?

7 Sababu ya pili ya kuteseka kwa wanadamu inaonyeshwa na kanuni hii: “Lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia.” (Wagalatia 6:7) Wakati mwingine watu hupanda kwa kufanya maamuzi mabaya, nao huvuna kuteseka. Wanaweza kuamua kuendesha gari vibaya na kupata aksidenti. Wengi huamua kuvuta sigara, na hivyo wanapatwa na ugonjwa wa moyo au kansa ya mapafu. Huenda wale ambao huamua kujihusisha katika matendo yasiyo ya kiadili kingono, wakateseka kwa sababu ya kuvunjika kwa familia, kujishushia heshima, kupatwa na magonjwa yanayoambukizwa kingono, na mimba zisizotakiwa. Huenda watu wakamlaumu Mungu kwa mateso hayo, lakini kwa kweli wanateseka kwa sababu ya maamuzi yao wenyewe yaliyo mabaya.—Mithali 19:3.

8. Kulingana na Mhubiri 9:11, kwa nini watu huteseka?

8 Sababu ya tatu ya kuteseka kwa wanadamu inatajwa kwenye Mhubiri 9:11: “Nikarudi, na kuona chini ya jua, ya kwamba si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” NW] huwapata wote.” Nyakati nyingine, watu huwa mahali pasipofaa, wakati usiofaa. Bila kuzingatia nguvu zetu au udhaifu wetu, huenda yeyote kati yetu akapatwa na kuteseka na kifo wakati wowote bila kutarajia. Kwa mfano, katika siku za Yesu mnara mmoja huko Yerusalemu ulianguka na kuwaua watu 18. Yesu alionyesha kwamba Mungu hakuwa akiwaadhibu watu hao kwa dhambi walizotenda hapo awali. (Luka 13:4) Yehova hapaswi kulaumiwa kwa mateso hayo.

9. Ni jambo gani ambalo watu wengi hawaelewi kuhusu kuteseka?

9 Ni muhimu kuelewa baadhi ya sababu za kuteseka kwa wanadamu. Hata hivyo, kuna jambo fulani kuhusu kuteseka ambalo watu wengi huona ni vigumu kulielewa. Hilo ni: Kwa nini Yehova Mungu anaruhusu kuteseka?

Kwa Nini Yehova Anaruhusu Kuteseka?

10, 11. (a) Kulingana na Waroma 8:19-22, “viumbe vyote” vilipatwa na nini? (b) Tunaweza kujuaje yule aliyevitiisha viumbe chini ya ubatili?

10 Fungu fulani katika barua ya mtume Paulo kwa Waroma hutusaidia kuelewa habari hii muhimu. Paulo aliandika hivi: “Taraja lenye hamu la viumbe linangoja kufunuliwa kwa wana wa Mungu. Kwa maana viumbe vilitiishwa chini ya ubatili, si kwa mapenzi yavyo vyenyewe bali kupitia yeye aliyevitiisha hivyo, juu ya msingi wa tumaini kwamba viumbe vyenyewe pia vitawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu. Kwa maana twajua kwamba viumbe vyote vinafuliza kupiga kite pamoja na kuwa katika maumivu pamoja hadi sasa.”—Waroma 8:19-22.

11 Ili kufahamu maana ya mistari hiyo, kwanza tunahitaji kupata majibu kwa maswali fulani muhimu. Kwa mfano, Ni nani aliyevitiisha viumbe chini ya ubatili? Wengine wanasema ni Shetani; wengine ni Adamu. Lakini wala Shetani wala Adamu hangeweza kuvitiisha viumbe chini ya ubatili. Kwa sababu gani? Kwa sababu yule anayevitiisha viumbe chini ya ubatili, anafanya hivyo “juu ya msingi wa tumaini.” Naam, anatoa tumaini kwamba hatimaye watu waaminifu ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu.’ Wala Adamu wala Shetani hangeweza kutoa tumaini hilo. Ni Yehova tu ndiye ambaye angeweza kufanya hivyo. Basi, ni wazi kwamba yeye ndiye aliyevitiisha viumbe chini ya ubatili.

12. Watu wameshindwa kuelewa nini kuhusu “viumbe vyote,” na swali hilo linaweza kujibiwaje?

12 Hata hivyo, “viumbe vyote” vinavyotajwa katika fungu hilo ni nini? Wengine husema kwamba “viumbe vyote” ni vitu vyote vilivyo hai, kutia ndani wanyama na mimea yote. Lakini, je, mimea na wanyama wana tumaini la kupata “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu”? La. (2 Petro 2:12) Kwa hiyo, “viumbe vyote” ni wanadamu peke yao. Hao ndio viumbe ambao hupatwa na dhambi na kifo kwa sababu ya uasi uliotokea Edeni na hivyo wanahitaji sana tumaini.—Waroma 5:12.

13. Uasi wa Edeni ulikuwa na matokeo gani kwa wanadamu?

13 Uasi huo ulikuwa na matokeo gani kwa wanadamu? Paulo anafafanua matokeo hayo kwa neno moja: ubatili. Kulingana na kichapo kimoja cha marejeo, neno hilo hufafanua “ubatili wa kitu ambacho hakifanyi kazi kama kilivyokusudiwa.” Wanadamu walikusudiwa waishi milele, wakifanya kazi ya kutunza dunia paradiso wakiwa familia kamilifu, yenye umoja. Badala yake, wanaishi maisha mafupi, yenye maumivu na yenye kukatisha tamaa. Kama Ayubu anavyosema, “mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu.” (Ayubu 14:1) Huo ni ubatili kweli!

14, 15. (a) Kuna uthibitisho gani kwamba ile hukumu ya Yehova juu ya wanadamu ilikuwa ya haki? (b) Kwa nini Paulo alisema kwamba haikuwa ‘mapenzi ya viumbe vyenyewe’ kutiishwa chini ya ubatili?

14 Sasa tunakuja kwa swali muhimu: Kwa nini “Mhukumu ulimwengu wote” alitiisha wanadamu chini ya maisha hayo yenye maumivu na yenye kukatisha tamaa? (Mwanzo 18:25) Je, alikuwa na haki ya kufanya hivyo? Kumbuka yale ambayo wazazi wetu wa kwanza walifanya. Kwa kumwasi Mungu, walimuunga mkono Shetani ambaye alianzisha upinzani mkubwa kwa enzi kuu ya Yehova. Kwa matendo yao, waliunga mkono dai la kwamba mwanadamu anaweza kufanikiwa kujitawala mwenyewe chini ya uongozi wa kiumbe-roho mwasi badala ya kumtegemea Yehova. Alipowahukumu waasi hao, Yehova aliwapa kile walichotaka. Alimruhusu mwanadamu ajitawale mwenyewe chini ya uongozi wa Shetani. Chini ya hali hizo, kwa haki Yehova alitiisha wanadamu chini ya ubatili lakini juu ya msingi wa tumaini.

15 Bila shaka, hayo hayakuwa ‘mapenzi ya viumbe vyenyewe.’ Hayakuwa mapenzi yetu tuzaliwe chini ya utumwa wa dhambi na uharibifu. Lakini kwa rehema zake, Yehova aliwaruhusu Adamu na Hawa waendelee kuishi muda wote wa maisha yao na kuzaa watoto. Ingawa sisi, wazao wao, tumetiishwa chini ya ubatili wa dhambi na kifo, tuna nafasi ya kufanya yale ambayo Adamu na Hawa walishindwa kufanya. Tunaweza kumsikiliza Yehova na kujifunza kwamba enzi yake kuu ni adilifu na kamilifu lakini utawala wa mwanadamu pasipo kumtegemea Yehova huleta tu maumivu, kukata tamaa, na ubatili. (Yeremia 10:23; Ufunuo 4:11) Kuongezea hayo, uongozi wa Shetani hufanya hali iwe mbaya hata zaidi. Historia ya mwanadamu inathibitisha kweli hizo.—Mhubiri 8:9.

16. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba si Yehova anayesababisha mateso tunayoona ulimwenguni leo? (b) Kwa upendo, Yehova ametoa tumaini gani kwa watu waaminifu?

16 Ni wazi kwamba Yehova alikuwa na haki ya kutiisha wanadamu chini ya ubatili. Hata hivyo, je, hiyo inamaanisha kwamba Yehova ndiye anayesababisha ubatili na mateso ambayo hutupata sisi leo? Hebu fikiria hakimu anayemhukumu mhalifu kwa haki. Huenda mfungwa huyo akateseka sana anapotumikia kifungo chake, lakini je, anaweza kwa haki kumlaumu hakimu kuwa msababishaji wa mateso yake? La, hasha! Zaidi ya hayo, Yehova hawezi kuwa chanzo cha uovu. Andiko la Yakobo 1:13 linasema: “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” Pia tukumbuke kwamba Yehova alitoa hukumu hiyo “juu ya msingi wa tumaini.” Kwa upendo, amefanya mipango ili wazao waaminifu wa Adamu na Hawa wauone mwisho wa ubatili na wafurahie “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” Kwa umilele wote, wanadamu waaminifu hawatakuwa na wasiwasi kwamba huenda viumbe vyote vikatumbukia tena katika maumivu ya ubatili. Kwa kushughulikia kwa haki hali hiyo, Yehova atathibitisha kwamba ana haki ya kuwa mwenye enzi kuu milele.—Isaya 25:8.

17. Tunapaswa kuwa na maoni gani baada ya kuchunguza sababu za kuteseka ulimwenguni leo?

17 Tunapochunguza sababu za kuteseka kwa wanadamu, je, tunaweza kuwa na msingi wa kumlaumu Yehova kuwa ndiye anayesababisha uovu au tuache kumtumaini? La, badala yake kuchunguza sababu hizo kunatufanya tukubaliane na maneno haya ya Musa: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Na tujikumbushe mambo hayo mara kwa mara kwa kuyatafakari. Kwa hiyo, tunapokabili majaribu, tutakinza jitihada za Shetani za kupanda mbegu za shaka akilini mwetu. Hata hivyo, namna gani kuhusu hatua ya pili iliyotajwa hapo mwanzoni? Kumtumaini Yehova kunahusisha nini?

Maana ya Kumtumaini Yehova

18, 19. Biblia inatumia maneno gani kututia moyo tumtumaini Yehova, lakini watu fulani wana maoni gani yasiyofaa kuhusiana na hilo?

18 Neno la Mungu linatuhimiza hivi: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:5, 6) Maneno hayo mazuri yanatupa uhakika kama nini! Kwa kweli, hakuna mwingine katika ulimwengu wote ambaye anatumainika zaidi kuliko Baba yetu mpendwa wa mbinguni. Hata hivyo, ingawa ni rahisi kusoma maneno haya katika kitabu cha Mithali, huenda isiwe rahisi kuyatenda.

19 Wengi wana maoni yasiyofaa kuhusu maana ya kumtumaini Yehova. Wengine hufikiri kwamba kumtumaini Yehova kunamaanisha kuwa na hisia fulani yenye kufurahisha ambayo huchemka moyoni mwao. Huenda wengine wakafikiri kumtumaini Mungu humaanisha kwamba tunaweza kutarajia atukinge na taabu zote, atatue matatizo yetu yote, na atuondolee majaribu yetu mara moja kama tunavyotaka! Lakini maoni hayo hayana msingi. Kuwa na tumaini kunahusisha mengi zaidi kuliko kuwa na hisia fulani, na si jambo la kuwaziwa tu. Kwa watu wazima, kuwa na tumaini kunahusisha kufanya maamuzi baada ya kuyafikiria kwa makini.

20, 21. Kumtumaini Yehova kunahusisha nini? Toa mfano.

20 Ona tena jinsi Mithali 3:5 inavyosema. Inatofautisha kumtumaini Yehova na kutegemea akili zetu wenyewe, ikionyesha kwamba hatuwezi kufanya yote mawili. Je, hiyo inamaanisha kwamba haturuhusiwi kutumia nguvu zetu za uelewevu? La, kwa kuwa Yehova ndiye aliyetupa nguvu hizo na anatarajia tuzitumie kumtumikia. (Waroma 12:1) Lakini sisi hutegemea nini? Ikiwa kufikiri kwetu hakupatani na kwa Yehova, je, sisi tunakubali kwamba hekima yake ni ya juu sana kuliko yetu? (Isaya 55:8, 9) Kumtumaini Yehova humaanisha kuacha kufikiri kwake kuongoze kufikiri kwetu.

21 Kwa mfano: Wazia mtoto mdogo akiwa ameketi kwenye kiti cha nyuma cha gari huku wazazi wake wakiwa mbele. Baba yake ndiye anayeendesha gari hilo. Matatizo yakitokea wakati wa safari, labda kuhusu barabara inayofaa au hali ya hewa au hali ya barabara, mtoto mtiifu na mwenye kutumaini wazazi atatendaje? Je, atawaamuru la kufanya, akimwambia baba yake jinsi ya kuendesha gari? Je, atatilia shaka uamuzi wa wazazi wake au akatae kusikiliza anapoambiwa aendelee kuketi akiwa amejifunga mkanda wa usalama? La, kwa kawaida yeye atawatumaini wazazi wake washughulikie mambo hayo hata ingawa wao si wakamilifu. Yehova ni Baba yetu mkamilifu. Je, hatupaswi kumtumaini kabisa, hasa tunapokabili hali ngumu?—Isaya 30:21.

22, 23. (a) Kwa nini tunapaswa kumtumaini Yehova tunapokabili matatizo, na tunawezaje kufanya hivyo? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

22 Hata hivyo, andiko la Mithali 3:6 linaonyesha kwamba tunapaswa ‘kumkiri Yehova katika njia zetu zote,’ si wakati tu tunapokabili hali ngumu. Kwa hiyo maamuzi tunayofanya kila siku yanapaswa kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova. Matatizo yanapotokea, hatupaswi kuvunjika moyo, kushtuka, au kukataa mwongozo wa Yehova kuhusu jinsi ya kushughulikia mambo kwa njia bora zaidi. Tunapaswa kuona matatizo kuwa nafasi ya kutetea enzi kuu ya Yehova, kuchangia kumthibitisha Shetani kuwa mwongo, na kusitawisha utii na sifa nyingine zinazompendeza Yehova.—Waebrania 5:7, 8.

23 Tunaweza kuonyesha tumaini letu kwa Yehova hata tukitishwa na vizuizi vyovyote vile. Tunaonyesha hivyo kwa sala zetu na jinsi tunavyotegemea mwongozo wa Neno la Yehova na tengenezo lake. Hata hivyo, tunawezaje kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova hasa tunapokabili matatizo ya ulimwengu huu? Habari hii itazungumziwa katika makala yetu inayofuata.

Ungejibuje?

• Daudi alionyeshaje kwamba alimfanya Yehova kuwa tumaini lake?

• Kuna sababu gani tatu za kuteseka kwa wanadamu leo, na kwa nini inafaa kuzichunguza mara kwa mara?

• Yehova alitoa hukumu gani juu ya wanadamu, na kwa nini hukumu hiyo ilikuwa ya haki?

• Kumtumaini Yehova kunahusisha nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Daudi alimfanya Yehova kuwa tumaini lake

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yesu alionyesha kwamba wakati mnara fulani ulipoanguka huko Yerusalemu, si Yehova aliyesababisha msiba huo